Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 1/1 kur. 4-9
  • Mashariki na Magharibi, Yehova Huwaimarisha Watu Wake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mashariki na Magharibi, Yehova Huwaimarisha Watu Wake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ufanisi Chini ya Marufuku
  • Namna Gani Mabara ya Amerika?
  • Katika Afrika Iliyogawanywa na Ugomvi
  • Katika “Bara la Tai”
  • “Ongeza Urefu wa Kamba Zako”
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Mashahidi wa Yehova—Ripoti ya Kitabu-Mwaka 1994
    1994 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 1/1 kur. 4-9

Mashariki na Magharibi, Yehova Huwaimarisha Watu Wake

KATIKA maeneo ambamo kazi ya kuhubiri imepigwa marufuku, katika mabara yaliyogawanywa na jeuri, na katika nchi ambamo marufuku yameondolewa hivi karibuni—kwa kweli, kotekote katika shamba la ulimwenguni pote—Yehova huendelea kuwaandalia Mashahidi wake “nguvu inayozidi iliyo ya kawaida.”—2 Wakorintho 4:7.

Ufanisi Chini ya Marufuku

Katika kikundi kimoja cha visiwa vya Mashariki ya Mbali, kazi ya kuhubiri imekuwa chini ya marufuku kwa muda wa miaka 17 sasa. Je! Mashahidi wamevunjika moyo? Hasha! Katika mwezi wa Mei uliopita, walifikia kilele kipya cha wahubiri 10,756, ambao 1,297 kati yao walikuwa wakitumikia wakiwa wahudumu wa wakati wote. Hali za ulimwengu zizorotapo, watu wa visiwani wanaelekea zaidi kusikiliza kweli kuliko wakati mwingine wowote. Kwa hiyo wamekuwa wakiripoti mafunzo ya Biblia 15,654 yaongozwayo nyumbani mwa watu wenye kupendezwa. Mapema zaidi, 25,397 walihudhuria mikutano iliyofanywa kwa siri ili kuadhimisha kifo cha Yesu.

“Ufundishaji wa Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya ilipofanywa—kwa busara tena kulingana na hali za mahali hapo—ndugu walifurahia kupokea, katika lugha yao, nakala zao za vitolewa vilevile vilivyokuwa vimetolewa katika United States. Watafsiri, wasahihishaji, na wengine walikuwa wamejitolea kufanya kazi ya ziada ili waweze kutayarisha kile kitolewa kikuu, chenye mamia ya kurasa, kwa wakati ulioratibiwa. Na kiwanda cha kilimwengu cha uchapishaji chenye ushirikiano kilifurahi kufanya kazi nzuri ya kuchapa na kujalidi. Wakusanyikaji walifurahi sana kupokea kichapo hicho, chenye picha zacho zaidi ya elfu moja zenye rangi-rangi. Maofisa wengi wa serikali huwastahi Mashahidi wa Yehova, na mara nyingi upinzani hutoka kwa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo hasa. Inatazamiwa kwamba marufuku yataondolewa hivi karibuni.

Namna Gani Mabara ya Amerika?

Mashahidi wa Yehova katika nchi hizo za Magharibi wameunganika na ndugu zao wa Mashariki katika kutatua matatizo yao kwa moyo mkuu, na roho takatifu ya Yehova huwasaidia washinde hali ngumu. Kwa kielelezo, chukua ripoti ifuatayo kutoka bara la Amerika ya Latini ambako vikundi vya walanguzi wa madawa ya kulevya husafiri kwa ukawaida misituni.

Kikundi kimoja cha Mashahidi kilienda kwa basi hadi eneo la mbali. Waliposhuka basi hilo, waliona barabara ndogo ya kando iliyoelekea nje ya kijiji. Kwa hiyo wale ndugu watano walienda kuona ni wapi ambako njia hiyo ndogo isiyo na lami ilielekea, wakiwagawia dada na watoto wahubiri kijijini. Ndugu mmoja asimulia hivi:

“Ni nyumba chache zilizoonekana baada ya muda wa saa mbili tukitembea barabara hiyo. Kisha, wanaume wanne wenye silaha na vifuniko juu ya vichwa vyao walitoka msituni kwa ghafula. Wengine walikuwa na bunduki mimina-risasi, na wengine walikuwa na simi. Tulikuwa tumekabili nini? Tulianza kuwauliza walichotaka, lakini tuliambiwa tunyamaze na tusiongee—tuendelee mbele tu. Tulifanya hivyo! Muda mwingine wa saa mbili tukitembea katika msitu wenye vichaka vingi ulituleta kwenye sehemu iliyo wazi ambayo bila shaka ilikuwa kambi yenye silaha. Walinzi wenye bunduki walikuwa kila mahali. Katikati palikuwa nyumba iliyojengwa vizuri ambayo tulielekezwa kwayo.

“Tulipokuwa tumeketi tulizungumziwa na mmoja ambaye yaonekana alikuwa ndiye kiongozi wa kambi hiyo. Alikuwa amejivalia kinadhifu, mwenye elimu nzuri, na mwenye heshima sana. Alielekezea mmoja katika kikundi chetu cha ndugu akamwambia asimame. Kisha akamwuuliza: ‘Wafikirije juu ya kikundi [chetu]?’ Aking’amua kikamili tulikokuwa, ndugu huyo alijibu: ‘Twajua juu ya kikundi chenu, lakini hatupendezwi nacho hata kidogo wala na kikundi kingine chochote cha kisiasa. Sababu pekee ya sisi kuwa hapa ni kuhubiri juu ya Ufalme wa Yehova Mungu kupitia Kristo Yesu. Hivi karibuni huo utaharibu serikali zote za kisiasa za mfumo huu wa mambo na kuleta baraka nzuri ajabu kwa watu kwenye dunia hii chini ya hali za Paradiso—jambo ambalo hakuna mwanadamu wala kikundi cha wanadamu kiwezacho kufanya.’

“Mtazamo wa mtu huyo ulibadilika. Alianza kuuliza maswali. ‘Ulijifunza hayo yote kutoka wapi? Ulitayarishaje kuongea hivyo?’ Kwa muda wa saa moja na nusu, tuliweza kutoa ushahidi mzuri juu ya hali za ulimwengu na kuonyesha kwamba Biblia hutambulisha tumaini la pekee kwa ajili ya ainabinadamu. Tulieleza pia Warumi sura ya 13—kwamba sisi hutii mamlaka zinazotawala, lakini kunapokuwa hitilafiano kati ya Neno la Yehova na lazo, sisi humtii kwanza Mungu wetu, Yehova. Hatimaye, tulimtolea vitabu tulivyokuwa navyo. Alichukua vitatu kati yavyo na Biblia na, kwa mshangao wetu mkubwa, alitupa sisi mchango kwa ajili yavyo. Alisema kwamba angevisoma.

“Baadaye, kiongozi huyo alimwashiria mtu mmoja atupeleke nje ya kambi. Upesi tulikuwa njiani tukirudi, tukimshukuru Yehova kwa ajili ya ushindi tuliokuwa nao katika sehemu nyingi ya kutoa ushahidi.”

Katika Afrika Iliyogawanywa na Ugomvi

Katikati ya Mashariki ya Mbali na Magharibi ya mbali ni kontinenti ya Afrika. Vita vya kikabila vimegeuza nchi nyingine kuwa vimbunga vya ujeuri. Katika Liberia, mara nyingine tena watu wa Yehova wameathiriwa sana kwa sababu ya kuanza upya kwa vita ya wenyewe kwa wenyewe. Kwanza kulikuwa mapigano katika na karibu jiji kuu katika Oktoba na Novemba 1992. Kisha, vita hiyo ilipoenea mashambani, makutaniko mazima-mazima yalitawanyika ndugu wakitorokea vichakani pamoja na wakazi wale wengine. Hata hivyo, bidii yao imeendelea bila kupungua. Walipokuwa wakitoroka, walihubiri, na hilo limetokeza kutolewa kwa ushahidi mtukufu katika sehemu za mbali kabisa barani.

Kutaniko moja la ndugu waliolazimika kuacha makao yao lilijenga Jumba la Ufalme la muda tu katikati ya shamba kubwa la miti inayotoa mpira. Katika mji fulani karibu na sehemu ya mapigano, wakati wa usiku wakazi wasio wanajeshi walikuwa wakitorokea lile shamba kubwa la miti inayotoa mpira lililozunguka eneo hilo ili kukwepa makombora kutoka angani. Ndugu wa huko (kutia na wahubiri wengi wasio na makao kutoka jiji kuu, Monrovia) walipanga huduma ya shambani na waliweza kuonwa kwa ukawaida wakihubiri wale maelfu waliokuwa wakijificha chini ya miti hiyo inayotoa mpira! Wakati wowote ndege ilipokaribia, ndugu na dada walikuwa wakiruka ndani ya mtaro ulio karibu kisha, hatari ilipokuwa imepita, waliendelea na ziara zao.

Kwa kustaajabisha, wale wahubiri zaidi ya elfu moja wa kutaniko wawezao kutoa ripoti zao kwa Sosaiti wamekuwa na wastani wa muda wa saa 18.1 katika huduma ya shambani, na wanaongoza mafunzo ya Biblia 3,111 kwa mwezi, zijapokuwa hali hizo za vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Katika Afrika wakati wa ile miaka minne iliyopita, vizuizi dhidi ya kazi ya Mashahidi wa Yehova vimeondolewa katika nchi 18. Na ni shangwe iliyoje! Mnamo Agosti 12, marufuku juu ya Mashahidi katika Malawi iliyokuwa imewekwa katika Oktoba 1967, iliondolewa. Kazi ya kuhubiri habari njema kichini-chini ilikuwa imefanikiwa sikuzote, lakini sasa Mashahidi wanaweza kusonga mbele katika uhuru, ingawa watalazimika kungojea ufufuo ili kuwaamkua tena washiriki wao wapendwa wengi waliouawa kimakusudi na wapinzani.

Katika Msumbiji, mapatano ya amani yalianza kutenda mnamo Oktoba 4, 1992. Maeneo ambayo hayakufikika hapo kwanza kwa sababu ya ile vita yenye uharibifu ya miaka 16 iliyopita yanafikiwa. Katika eneo la Karioko, mawasiliano yalianzishwa upya na ndugu na dada 375 ambao hawakuweza kabisa kuwasiliana na tengenezo kwa muda wa miaka saba iliyopita. Siku ya kusanyiko la pekee ilifanywa katika Milange, jiji kuu la wilaya ambalo hapo kwanza lilikuwa mahali pa kambi ya mateso na kitovu kwa ajili ya “kuelimishwa upya” (kubadili maoni kwa lazima) kwa Mashahidi wa Yehova, wengi wao waliokuwa wakimbizi kutoka Malawi. Jumla ya kushangaza ya watu 2,915 walihudhuria, kutia na msimamizi wa mji, aliyewakaribisha Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo kile kilichokuwa kitovu kwa ajili ya “kuelimishwa upya” hapo kwanza kilikuwa kitovu kwa ajili ya ufundishaji wa kimungu kwa siku hiyo.

Mishonari mmoja katika Tete aandika: “Jambo lenye kupendeza lilionwa na mwakilishi mmoja wa UNHCR (Tume ya Wakimbizi ya Umoja wa Mataifa) kuhusu ndugu zetu waliojikuta katika kambi za wakimbizi katika Mkoa wa Tete. Alisema kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepanga kambi zao wenyewe, tofauti na vikundi vingine. ‘Kambi yao,’ akasema, ‘ilikuwa [kambi] pekee iliyosimamiwa ifaavyo,’ akiongeza, ‘Mashahidi wa Yehova ni safi, wenye utaratibu, na wenye elimu.’ Kisha akajitolea kunipeleka kwa ndege ng’ambo ya msitu ili nijionee mwenyewe. Kutoka angani, rubani alielekezea kambi mbili. Moja ilikuwa ya kizembe na chafu, ikiwa na nyumba za matope zilizojengwa karibukaribu bila mpango wowote. Ile nyingine ilikuwa imepangwa vizuri, nyumba zikiwa zimetenganishwa kwa barabara katika safu. Nyumba zilikuwa na sura nadhifu, zenye nyua zilizofagiliwa. Nyingine hata zilikuwa zimepakwa rangi iliyotengenezwa nyumbani. ‘Kisia ni ipi iliyo yenu?’ rubani akasema. Nilifurahi sana kukutana na ndugu katika kambi hiyo. Sasa kuna makutaniko manane katika kijiji hiki cha Mashahidi.”

Katika “Bara la Tai”

La, huyo si tai wa U.S.! Kati ya Mashariki na Magharibi kuna nchi moja ya Ulaya, Albania, jina layo katika lugha rasmi, Shqipëria, likimaanisha “Bara la Tai.” Hivi karibuni, marufuku yenye ukatili ya muda wa miaka 50 juu ya Mashahidi wa Yehova katika bara hilo yameondolewa, na wanaweza kuunganika na ndugu zao kutoka Mashariki na Magharibi katika furaha yao ya uhuru wa ibada. Kwa kweli ‘wanakomboa wakati.’ (Waefeso 5:16) Kusanyiko la kwanza katika historia ya Albania, kusanyiko la siku moja, lilifanywa kwenye Jumba la Michezo ya Kuigiza la Kitaifa, katika jiji kuu, Tiranë, mnamo Jumapili, Machi 21. Katika Jumamosi alasiri kikundi cha Mashahidi 75 waliojitolea walikuwa wamegeuza mahali pa kukutania palipoharibika pawe jumba la kusanyiko safi na jangavu. Wasimamizi walishangaa. Na yapaswa ijulikane kwamba kati ya wale 75 waliojitolea, ni 20 tu waliokuwa wamebatizwa!

Halihewa ilikuwa bora kabisa. Wahudhuriaji kutoka ng’ambo walipowasili, salamu—hasa kwa ishara za mwili na kwa kukumbatia—zilifanya ile siku ya kusanyiko la pekee iwe ya pekee sana. Ndugu Nasho Dori alitoa sala ya kufungua, viganja vyake vikiwa vimeelekezwa mbinguni. Alibatizwa katika 1930 na sasa yeye ni karibu kipofu. Programu ilitolewa katika Kialbania, sehemu kubwa zaidi ikifanywa na mapainia wa pekee wa kigeni. Wale 585 waliohudhuria waliimba ule wimbo “Wakfu wa Kikristo”—mmojawapo nyimbo sita zilizokuwa zimetafsiriwa katika Kialbania kwa ajili ya siku hiyo—ndugu na dada wapya 41 walipotembea kuelekea bwawa ambalo ndugu Wagiriki walikuwa wameweka kwa fadhili katika Jumba la Ufalme la huko. Lilikuwa badiliko lililoje! Zamani, kuwa na Biblia kulimaanisha kufungwa katika kambi za kazi ngumu, na mikutano ilifanywa tu katika vikundi vya watu wawili au watatu.

Siku iliyofuata ile ya kusanyiko, ofisi ya Watch Tower ilipokea simu kutoka kwa mkurugenzi wa jumba hilo. Kwa kawaida yeye hashughulikii sana matumizi ya jumba hilo. Hiyo ni kazi ya mkurugenzi msaidizi. Lakini alisema hivi: “Nililazimika tu kuwapigia simu na kutoa shukrani. Sijapata kamwe kuona mahali hapa pakiwa safi hivi. Ikiwa ningalipaswa kueleza juu yapo, ningalisema kwamba upepo kutoka mbinguni ulishuka juu ya jumba letu jana. Wakati wowote mngependa kutumia vifaa vyetu, tafadhali rudini, nasi tutawafikiria kwanza. Mwajua, kwa kweli twapaswa kuwaruhusu kulitumia kila miezi mitatu bila malipo.”

Mashahidi hao walirudi miji yao wakiwa wameimarishwa na wakiwa na shukrani na kuanza kutayarishia Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Siku 15 tu baadaye, mnamo Jumanne, Aprili 6, Ukumbusho wa kwanza wa waziwazi ulifanywa katika sehemu saba.

Katika mji wa Berat, hudhurio la mkutano limeongezeka hadi 170 hivi, na padri wa mahali hapo amekasirika sana. Kati ya wale wahubiri wa Ufalme 33 katika Berat, 21 walibatizwa kwenye kusanyiko. Berat uliripoti watu 472 waliohudhuria Ukumbusho. Mahudhurio mengine ya Ukumbusho yalikuwa yenye kutokeza pia, likiwa tokeo hasa la ule uongozi mzuri wa mapainia wa pekee.

Katika ule mji wa Albania wenye Wakatoliki wengi zaidi, Shkodër, ambako kuna basilika (kanisa kubwa), kanisa lilianza kuchapa gazeti dogo la habari la kila mwezi, na kila toleo limeshughulikia “Jinsi ya Kuwaepuka Mashahidi wa Yehova.” Toleo la mwisho lilisema: “Mashahidi wa Yehova wameshambulia Shkodër”! Lile jeshi kubwa la Mashahidi wawili huko lilikusanya watu 74 wenye mwenendo mzuri na wenye uzito kwenye Ukumbusho. Baada ya kusikia hotuba ya Ukumbusho, familia 15 ziliomba mafunzo ya Biblia nyumbani. Katika mji mwingine, Durres, ambako kuna jeshi la Mashahidi wanne, hudhurio lilikuwa bora sana la watu 79.

Kwa sababu ya upinzani wa vijana Wakatoliki, waliotisha kuwaondosha Mashahidi kwa mawe, mkutano wa Ukumbusho katika kijiji cha mlimani cha Kalmeti i Vogel ulihamishwa hadi nyumba ya ndugu mmoja wa hapo, ambako 22 walihudhuria kwa amani. Kuna wahubiri watano katika kikundi hicho, ambao watatu walibatizwa kwenye kusanyiko katika Tiranë.

Katika Vlorë vijana wawili walipokea nakala ya Mnara wa Mlinzi, wakaisoma, na kuandikia Sosaiti hivi: “Sasa sisi hujiita Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya kweli ambayo tumejifunza katika Mnara wa Mlinzi. Tafadhali tupelekeeni msaada.” Mapainia wa pekee wawili walipewa mgawo kwenda huko, na upesi mmoja wa vijana hao alistahili kuwa mhubiri. Alifurahi kuwa miongoni mwa wale 64 waliohudhuria Ukumbusho katika Vlorë.

Ndugu mmoja Mwalbania aliyejifunza kweli katika United States alirudi mji wa kwao wa Gjirokastër katika miaka ya 1950, ambako alitumikia kadiri alivyoweza hadi kifo chake. Alipanda mbegu za kweli moyoni mwa mwanae. Marufuku yalipoondolewa, mwana huyo aliomba msaada kutoka Watch Tower Society. Mtu mwingine mwenye kupendezwa aishiye katika kijiji kilicho kaskazini tu mwa hapo alikuwa pia ameandika akiomba msaada, kwa hiyo mapainia wa pekee wanne walitumwa huko. Jumatano asubuhi iliyofuata Ukumbusho, mmoja wao alipigia ofisi ya Sosaiti ya Tiranë na kusema hivi: “Nisingaliweza kujizuia nisiwaambie kiasi ambacho roho ya Yehova imefanya. Tumefurahi sana. Ukumbusho ulifanikiwa.” Hudhurio lilikuwa 106, kutia na kikundi chao cha wahubiri saba wa Ufalme.

Namna gani jumla ya hudhurio la Ukumbusho? Katika 1992, kulipokuwa wahubiri wa Ufalme 30 tu, hudhurio lilikuwa 325. Katika 1993, wale wahubiri 131 walikuwa wamekusanya wahudhuriaji 1,318. Katika miaka hiyo miwili, hudhurio limekuwa mara kumi zaidi ya idadi ya wahubiri. Yasisimua kama nini kuona “mdogo [akiwa] elfu” katika kipindi kifupi cha wakati jinsi hiyo!—Isaya 60:22.

“Ongeza Urefu wa Kamba Zako”

Kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova ipanukapo hadi kona zote za tufe, wito huu waenea: “Panua mahali pa hema yako, na wayatandaze mapazia ya maskani yako [tabenakulo lako tukufu, NW]; usiwakataze; ongeza urefu wa kamba zako; vikaze vigingi vya hema yako. Kwa maana utaenea upande wa kuume na upande wa kushoto.” (Isaya 54:2, 3) Kuenea huko katika ‘tabenakulo tukufu’ la Mungu—likiwakilishwa katika kutaniko la waabudu wake la ulimwenguni pote—kwa kweli kumeonekana wazi katika Ulaya ya Mashariki, hasa katika mabara yaliyokuwa Muungano wa Sovieti. Baada ya kuwategemeza watumishi wake katika miongo ya kuzuiwa, Yehova sasa anawaandalia Mashahidi wake nishati yenye kutendesha inayohitajiwa kupanua na kuimarisha tengenezo.

Katika Moscow, Urusi, kwenye Stediamu ya Locomotive, mnamo Julai 22-25, kilele cha watu 23,743 walihudhuria mkusanyiko wa kimataifa wenye kutokeza sana wa mwaka jana wa mfululizo wa “Ufundishaji wa Kimungu.” Ni nani angalifikiri hilo lingewezekana, hata miaka miwili iliyopita? Lakini walikuwa huko! Zaidi ya 1,000 walitoka Japani na Korea, karibu 4,000 walitoka United States na Kanada, na maelfu wengine walitoka mabara zaidi ya 30 katika Pasifiki Kusini, Afrika, Ulaya, na sehemu nyinginezo—kwa kweli kukutana kwa Mashariki na Magharibi. Yatia moyo kama nini kwa hao wote kuchangamana kwa uhuru pamoja na ndugu na dada zao Warusi zaidi ya 15,000! Kulikuwa na shangwe nyingi mno.

Jumla ya kustaajabisha ya Mashahidi wapya 1,489 walibatizwa. Ubatizo huo ulitangazwa sana na vyombo vya habari kotekote ulimwenguni, kutia na picha nzuri kwenye ukurasa wa mbele wa The New York Times. Ingawa makofi yalitoa mvumo mkubwa sana wakati wa ubatizo, mvumo huo ulikuwa mkubwa zaidi katika hotuba ya mwisho wakati ambapo, baada ya msemaji kuwashukuru wale 4,752 waliojitolea na maofisa waliokuwa wamesaidia kufanya mkusanyiko huo ufanikiwe jinsi hiyo, alisema: “Zaidi ya wote, twamshukuru Yehova!” Ndiyo, roho ya Yehova ilikuwa imezuia upinzani wenye nguvu kutoka kwa wanadini wa Orthodoksi na kuandaa nishati muhimu iliyofanya mkusanyiko uwe uhalisi wenye kusisimua.

Hata hivyo, mambo zaidi yangefuata katika jiji la Ukrainia la Kiev, Agosti 5-8. Tena, waliojitolea kwa hiari walitengeneza stediamu upya kabisa, na Jumba la Ufalme hilo kubwa mno lilitolea nafasi watu 64,714 kikiwa kilele cha hudhurio. Mara nyingine tena, Mashahidi walitoka Mashariki na Magharibi na sehemu zote za katikati. Hotuba kuu zilitafsiriwa katika lugha 12. Wahudhuriaji 53,000 hivi, waliowasili kwa usafiri wa umma, walihitaji kulakiwa kwenye vituo vya gari-moshi na viwanja vya ndege na kusafirishwa kwenye makao yao katika hoteli, shule, na nyumba za faragha, na pia kwenye meli. Hayo yote yalitimizwa kwa gharama ya chini kabisa kwa wororo na utaratibu wa kitengenezo ulioleta semi za kuonyesha mshangao na sifa kutoka kwa polisi wa jiji hilo.

Jambo kuu la programu ya mkusanyiko yenye kusisimua lilikuwa ubatizo, uliotumia nafasi yote ya muda wa saa mbili na nusu. Jumla ya ndugu na dada wapya 7,402 walifananisha wakfu wao kwa Yehova, huku makofi zikiendelea kuvuma kotekote katika stediamu hiyo kubwa mno. Hicho kilipita kile kilele cha ubatizo cha wakati wote cha 7,136 kilichorekodiwa wakati wakusanyaji 253,922 walipokusanyika katika New York City katika 1958.

Kipindi hiki cha hukumu kiendeleapo sasa kuelekea tamati yacho, watu wenye mfano wa kondoo kutoka Mashariki, Magharibi, na hata “miisho ya dunia” wanakusanywa katika muungano usio na kifani katika historia yote ya kibinadamu. Kwa kweli, “mkutano [umati, NW] mkubwa, . . . wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha” wanajiunga na Israeli la kiroho katika kutangaza imani yao katika dhabihu ya fidia ya Yesu yenye thamani kubwa, msingi wa yote yanayotimizwa katika kutetea utawala wa enzi kuu ya Yehova.—Matendo 1:8; Ufunuo 7:4, 9, 10.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Mashariki yakutana na Magharibi katika Moscow na Kiev

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki