Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 1/15 kur. 24-25
  • Musa na Aroni—Wapiga-Mbiu Wenye Moyo Mkuu wa Neno la Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Musa na Aroni—Wapiga-Mbiu Wenye Moyo Mkuu wa Neno la Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Muujiza Watokea
  • Masomo Kwetu
  • Musa na Haruni Wanamwona Farao
    Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Mapigo Matatu ya Kwanza
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
  • Kuzijua Njia za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 1/15 kur. 24-25

Walifanya Mapenzi ya Yehova

Musa na Aroni—Wapiga-Mbiu Wenye Moyo Mkuu wa Neno la Mungu

EBU wazia hii mandhari: Musa mwenye umri wa miaka 80 na ndugu yake, Aroni, wamesimama mbele ya mtu mwenye uwezo zaidi duniani—Farao wa Misri. Kwa Wamisri mtu huyo alikuwa zaidi ya kuwa tu mwakilishi wa miungu. Wao waamini kwamba yeye mwenyewe ni mungu. Aonwa kuwa mwili wa kibinadamu wa Horasi, mungu mwenye kichwa cha ndege-kipanga. Akiwa pamoja na Isisi na Osirisi, Horasi alifanyiza ule utatu mkuu miongoni mwa miungu ya kiume na ya kike ya Misri.

Mtu yeyote anayemwendea Farao bila shaka aliweza kuona mfano wenye kuogofya wa kichwa cha fira kikitokeza kutoka katikati ya taji lake. Ilisemekana kwamba nyoka huyo angeweza kutoa moto na uharibifu kutoka kinywani mwake juu ya maadui wowote wa Farao. Sasa Musa na Aroni wamekuja mbele ya mfalme huyo aliye mungu wakiwa na ombi lisilo na kifani—kwamba awaache Waisraeli waliowekwa utumwani waende zao ili waweze kumfanyia Mungu wao, Yehova, msherehekeo.—Kutoka 5:1.

Tayari Yehova alikuwa ametabiri kwamba moyo wa Farao ungekuwa mgumu. Kwa hiyo, Musa na Aroni hawakushangaa kusikia jibu lake lenye ukaidi: “BWANA [“Yehova,” NW] ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao? Mimi simjui BWANA [“Yehova,” NW], wala sitawapa Israeli ruhusa waende zao.” (Kutoka 4:21; 5:2) Hivyo basi mkabiliano wenye kutazamisha ukatayarishwa. Walipokutana tena, Musa na Aroni walimtolea Farao uthibitisho wa kushangaza kwamba wao walimwakilisha Mungu wa kweli aliye mweza yote.

Muujiza Watokea

Kama alivyoagizwa na Yehova, Aroni alifanya muujiza uliothibitisha ukuu wa Yehova uzidio wa miungu ya Misri. Aliangusha fimbo yake mbele ya Farao, na mara hiyo ikawa nyoka mkubwa! Akiwa amepigwa na bumbuazi kwa muujiza huo, Farao akawaita makuhani wake wenye kufanya mizungu.a Kwa msaada wa nguvu za roho waovu, watu hawa waliweza kufanya jambo kama hilo kwa fimbo zao wenyewe.

Ikiwa Farao na makuhani wake walifurahi, basi ilikuwa furaha ya muda tu. Ebu wazia nyuso zao wakati nyoka wa Aroni alipowameza nyoka zao, mmoja baada ya mwingine! Wote waliokuwapo waliweza kuona kwamba miungu ya Wamisri haingeweza kushindana na Mungu wa kweli, Yehova.—Kutoka 7:8-13.

Hata hivyo, hata baada ya hayo, moyo wa Farao ukabaki ukiwa mgumu. Ni baada tu ya Mungu kuleta mapigo kumi yenye kuharibu sana juu ya Misri ndipo hatimaye Farao alimwambia Musa na Aroni: “Ondokeni tokeni katika watu wangu, ninyi na wana wa Israeli; enendeni, kamtumikieni BWANA [“Yehova,” NW] kama mlivyosema.”—Kutoka 12:31.

Masomo Kwetu

Ni nini kilichowawezesha Musa na Aroni kumfikia Farao wa Misri mwenye uwezo sana? Kwanza, Musa alionyesha ukosefu wa uhakika katika uwezo wake, akidai kuwa “mimi si mwepesi wa kusema, na ulimi wangu ni mzito.” Hata baada ya kuhakikishiwa juu ya utegemezo wa Yehova, yeye alisihi hivi: “Nakuomba, tuma kwa mkono wake huyo utakayemtuma.” Kwa maneno mengine, Musa alisihi kwamba Mungu atume mtu mwingine. (Kutoka 4:10, 13) Hata hivyo, Yehova alimtumia Musa mwenye upole, akimpa hekima na nguvu alizohitaji ili atekeleze mgawo wake.—Hesabu 12:3.

Leo, watumishi wa Yehova Mungu na Yesu Kristo wanatekeleza ile amri ya ‘kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi.’ (Mathayo 28:19, 20) Ili tufanye sehemu yetu katika kutimiza utume huu, twapaswa kutumia kwa njia bora zaidi ujuzi wa Kimaandiko na uwezo wowote ule ambao twaweza kuwa nao. (1 Timotheo 4:13-16) Badala ya kukazia akili mapungukio yetu, na tukubali kwa imani mgawo wowote ambao Mungu ametupa. Anaweza kutufanya tustahili na kutuimarisha kufanya mapenzi yake.—2 Wakorintho 3:5, 6; Wafilipi 4:13.

Kwa kuwa Musa alishindana na upinzani wa kibinadamu na wa roho waovu, bila shaka alihitaji msaada upitao ule wa kibinadamu. Basi, Yehova akamhakikishia: “Nimekufanya wewe kuwa kama Mungu kwa Farao.” (Kutoka 7:1) Ndiyo, Musa alitegemezwa na pia akawa na mamlaka ya kimungu. Akiwa na roho ya Yehova, Musa hakuwa na sababu ya kumwogopa Farao au wenzi wa mtawala huyo mwenye kiburi.

Ni lazima sisi pia tuitegemee roho takatifu ya Yehova, au kani ya utendaji, ili tuitimize huduma yetu. (Yohana 14:26; 15:26, 27) Tukiwa na utegemezo wa kimungu sisi twaweza kuyarudia maneno ya Daudi, aliyeimba hivi: “Nimemtumaini Mungu, sitaogopa; mwanadamu atanitenda nini?”—Zaburi 56:11.

Kwa huruma yake nyororo Yehova hakumwacha Musa peke yake katika mgawo wake. Badala ya hivyo, Mungu alisema: “Ndugu yako Haruni atakuwa nabii wako. Utanena hayo yote nikuagizayo; na ndugu yako Haruni atanena na Farao.” (Kutoka 7:1, 2) Lilikuwa jambo la upendo kama nini kwa Yehova kutenda kwa kulingana na uwezo wa Musa!

Mungu huandaa ushirika wa Wakristo wenzetu wakubalio mwito wa kuwa Mashahidi wa Yehova, Aliye Juu Zaidi Sana. (1 Petro 5:9) Basi, tujapopata vizuizi, na tuwe kama Musa na Aroni—wapiga-mbiu wenye moyo-mkuu wa neno la Mungu.

[Maelezo ya Chini]

a Neno la Kiebrania lililotafsiriwa “makuhani wenye kufanya mizungu” larejezea kikundi cha wachawi waliodai kuwa na uwezo mwingi sana upitao ule wa roho waovu. Iliaminiwa kwamba watu hawa wangeweza kuwaomba roho waovu wawatii na kwamba roho waovu hawakuwa na uwezo juu ya hawa wachawi.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Musa na Aroni walimwakilisha Yehova mbele ya Farao kwa moyo mkuu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki