Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 3/15 kur. 8-9
  • Kutii Maneno ya Yesu ya Kuaga

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutii Maneno ya Yesu ya Kuaga
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Fulizeni Kufanya Hili Katika Ukumbuko Wangu”
  • “Amri Mpya Nawapa”
  • ‘Fanyeni Hivi kwa Kunikumbuka Mimi’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Nisani 14—Siku ya Kukumbukwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Mlo wa Jioni wa Bwana—Maadhimisho Yanayomletea Mungu Heshima
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Kwa Nini Tuadhimishe Mlo wa Jioni wa Bwana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 3/15 kur. 8-9

Walifanya Mapenzi ya Yehova

Kutii Maneno ya Yesu ya Kuaga

KWENYE jioni ya Nisani 14, 33 W.K., Yesu Kristo na mitume wake waaminifu 11 waliegama kwenye meza katika chumba kimoja cha juu huko Yerusalemu. Akitambua kwamba kifo chake kilikuwa karibu, yeye aliwaambia hivi: “Bado kitambo kidogo nipo pamoja nanyi.” (Yohana 13:33) Kwa hakika, Yuda Iskariote tayari alikuwa njiani kwenda kufanya hila na watu waovu waliotaka Yesu auawe.

Hakuna yeyote katika chumba hicho cha juu aliyehisi umuhimu wa hiyo hali kuliko Yesu. Yeye alijua vyema kwamba alikuwa anakaribia kuteseka. Yesu alijua pia kwamba mitume wake wangemwacha usiku uo huo. (Mathayo 26:31; Zekaria 13:7) Kwa kuwa hii ilikuwa fursa ya mwisho ya Yesu ya kuongea na mitume wake kabla ya kifo chake, twaweza kuwa na hakika kwamba maneno yake ya kuaga yalikaza fikira kwenye mambo ya umaana mkubwa.

“Fulizeni Kufanya Hili Katika Ukumbuko Wangu”

Akiwa na mitume wake waaminifu, Yesu alianzisha mwadhimisho mpya ambao ungechukua mahali pa Sikukuu ya Kupitwa ya Kiyahudi. Mtume Paulo aliuita “mlo wa jioni wa Bwana.” (1 Wakorintho 11:20, NW) Akichukua mkate usiotiwa chachu, Yesu alitoa sala. Kisha akaumega na kuwapa mitume wake mkate huo. “Chukueni, kuleni. Huu wamaanisha mwili wangu,” yeye akasema. Kisha akachukua kikombe cha divai, akatoa sala ya shukrani na kuwapa mitume wake, akisema: “Nyweni kutoka hicho, nyinyi nyote; kwa maana hii yamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo hakika itamwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.”—Mathayo 26:26-28, NW.

Umaana wa tukio hili ulikuwa nini? Kama alivyoonyesha Yesu, mkate uliwakilisha mwili wake usio na dhambi. (Waebrania 7:26; 1 Petro 2:22, 24) Divai ilifananisha damu ya Yesu iliyomwagwa, ambayo ingefanya msamaha wa dhambi uwezekane. Damu yake ya kidhabihu ingehalalisha pia agano jipya kati ya Yehova Mungu na wanadamu 144,000, ambao hatimaye wangetawala pamoja na Yesu mbinguni. (Waebrania 9:14; 12:22-24; Ufunuo 14:1) Kwa kualika mitume wake washiriki mlo huu, Yesu alionyesha kwamba wangeshiriki pamoja naye katika Ufalme wa kimbingu.

Kuhusu mlo huu wa uadhimisho, Yesu aliamuru hivi: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.” (Luka 22:19, NW) Ndiyo, Mlo wa Jioni wa Bwana ungekuwa tukio la kila mwaka, sawa tu na vile Sikukuu ya Kupitwa ilivyokuwa. Ingawa Sikukuu ya Kupitwa iliadhimisha kuokolewa kwa Waisraeli kutoka utumwa katika Misri, Mlo wa Jioni wa Bwana ungekaza fikira kwenye wokovu mkuu zaidi—ule wa wanadamu wawezao kukombolewa kutokana na dhambi na kifo. (1 Wakorintho 5:7; Waefeso 1:7) Na zaidi, wale wenye kushiriki mkate na divai ya ufananisho wangekumbushwa juu ya mapendeleo yao ya wakati ujao wakiwa wafalme na makuhani katika Ufalme wa Mungu wa kimbingu.—Ufunuo 20:6.

Kifo cha Yesu Kristo kwa kweli kilikuwa tukio la maana kupita yote katika historia ya binadamu. Wale wanaothamini kile alichofanya Yesu hutii amri yake kuhusiana na Mlo wa Jioni wa Bwana: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.” Mashahidi wa Yehova huadhimisha kifo cha Yesu kila mwaka katika tarehe inayolingana na Nisani 14. Katika 1996 tarehe hii yaangukia Aprili 2, baada ya mshuko jua. Unakaribishwa kwa uchangamfu kuhudhuria kwenye Jumba la Ufalme katika eneo lenu.

“Amri Mpya Nawapa”

Kando na kuanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana, Yesu alikuwa na shauri la kuaga mitume wake. Licha ya kuzoezwa kwao kuzuri, wanaume hawa walikuwa na mengi ya kujifunza. Hawakutambua kikamili kusudi la Mungu kwa Yesu, kwao, au kwa wakati ujao. Lakini Yesu hakujaribu kurekebisha mambo yote haya kwa wakati huu. (Yohana 14:26; 16:12, 13) Badala ya hivyo, yeye alisema juu ya jambo lenye umaana mkubwa. “Amri mpya nawapa,” yeye akasema, “Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo.” Kisha Yesu akaongeza: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”—Yohana 13:34, 35.

Ni kwa njia gani hii ilikuwa “amri mpya”? Sheria ya Kimusa iliamuru hivi: “Umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mambo ya Walawi 19:18) Hata hivyo, Yesu alitia moyo wafuasi wake waonyeshe upendo wa kujidhabihu ambao ungefikia kiwango cha mtu kutoa uhai wake kwa niaba ya Wakristo wenzake. Bila shaka, ‘sheria ya upendo’ ingetumika pia katika hali zisizo hatari sana. Katika hali zote mfuasi wa Yesu Kristo angechukua hatua ya kwanza kuonyesha upendo kwa kusaidia wengine kiroho na kwa njia nyinginezo.—Wagalatia 6:10.

Kwenye usiku huu wa mwisho wa maisha ya Yesu ya kidunia, upendo ulimsukuma Yesu kusali kwa Yehova Mungu kwa niaba ya wanafunzi wake. Yeye alisali hivi kwa sehemu: “Hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako. Baba mtakatifu, kwa jina lako ulilonipa uwalinde hawa, ili wawe na umoja kama sisi tulivyo.” (Yohana 17:11) Ni jambo la maana kwamba katika ombi lake kwa Baba yake, Yesu aliomba muungano wa wafuasi wake. (Yohana 17:20-23) Wao walihitaji ‘kupendana kama Yesu alivyowapenda.’—Yohana 15:12.

Mitume waaminifu walitii maneno ya Yesu ya kuaga. Sisi pia twapaswa kukubali amri zake. Katika hizi “siku za mwisho” zilizo hatari, upendo na muungano miongoni mwa waabudu wa kweli ni wa maana zaidi kuliko wakati mwingineo wote. (2 Timotheo 3:1) Kwa kweli, Wakristo wa kweli hutii amri za Yesu nao huonyesha upendo wa kidugu. Hili hutia ndani kutii amri yake ya kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki