Jinsi Ambavyo Wachungaji Wakristo Hukutumikia
KATIKA sehemu nyingi inawezekana kuona jinsi ambavyo wachungaji huchunga kundi la mifugo. Wao huongoza, hulinda, na kuandalia kondoo. Hili hupendeza wazee Wakristo, kwa kuwa kazi yao hutia ndani utendaji mbalimbali wa uchungaji. Kwa kweli ni daraka lao “kulichunga kutaniko la Mungu” na ‘kukazia uangalifu kwa kundi lote.’—Matendo 20:28, NW.
Ikiwa wewe ni mshiriki wa kutaniko la Kikristo, wachungaji wa kiroho waweza kukutumikiaje? Na unapaswa kuitikiaje jitihada zao kwa niaba yako? Kwa nini kutaniko huhitaji msaada wao?
Ulinzi Dhidi ya Nini?
Katika nyakati za kale simba na wanyama wengine wakali walihatarisha mifugo na kuvizia kondoo mmoja-mmoja. Wachungaji walilazimika kuandaa ulinzi. (1 Samweli 17:34, 35) Shetani Ibilisi naye “huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.” (1 Petro 5:8) Yeye hapigi tu vita kwa ghadhabu nyingi dhidi ya tengenezo la kidunia la Yehova kwa ujumla bali pia dhidi ya kila mtumishi mmoja-mmoja wa Mungu. Lengo la Shetani ni nini? Anataka kuvunja moyo watu wa Yehova na hata kuwazuia ‘wasizishike amri za Mungu’ na ‘kushuhudia Yesu.’—Ufunuo 12:17.
Yehova aliwashutumu wachungaji wa kiserikali wa Israeli la kale kwa upuuzaji kwa sababu kondoo wake walikuwa wamekuwa “chakula cha wanyama-mwitu wote.” (Ezekieli 34:8) Hata hivyo, wazee Wakristo wana tamaa ya moyoni ya kulinda wale walio katika kutaniko ili kwamba hakuna mtu apotezwaye kupitia kupuuzwa au kwa sababu ya uvutano wa Shetani, ulimwengu, au waasi-imani walio kama “mbwa-mwitu.” (Matendo 20:29, 30) Wachungaji husaidiaje washiriki wote wa kundi kudumisha akili zao na kuwa macho? Njia moja ni kwa kutoa hotuba za Kimaandiko zilizotayarishwa vizuri katika jukwaa la Jumba la Ufalme. Njia nyingine ni kwa mazungumzo chanya yenye kutia moyo kabla ya na baada ya mikutano. Na bado njia nyingine yenye matokeo ni wao wenyewe kuzuru “kondoo” nyumbani. (Linganisha Zaburi 95:7.) Lakini ziara ya uchungaji ni nini? Ziara hiyo yapaswa kufanywaje? Na ni nani wapaswao kutembelewa?
Ziara ya Uchungaji Ni Nini?
Ziara ya uchungaji si ziara tu ya kirafiki ya mazungumzo juu ya mambo madogo-madogo. Mzee mmoja alieleza: “Watangazaji wengi hufurahia sana kusoma andiko au kuzungumzia mtu fulani wa Biblia. Bila shaka, huyo mzee hatawali mazungumzo. Mtangazaji wa Ufalme anayetembelewa hufurahia kueleza maoni yake juu ya Biblia, na kufanya hivyo huimarisha imani yake mwenyewe. Huyo mzee aweza kubeba gazeti la Mnara wa Mlinzi au Amkeni! ili azungumzie makala yenye kujenga. Labda ni mazungumzo hayo ya kiroho yanayotofautisha ziara ya uchungaji na ziara ya kirafiki.”
Mzee mwingine mwenye uzoefu alisema: “Kabla ya ziara, mzee hutumia wakati fulani akifikiria mahitaji ya mtangazaji atakayemzuru. Ni nini kingeweza kumjenga mtangazaji huyo? Pongezi yenye unyoofu ni sehemu muhimu ya ziara za uchungaji, kwa kuwa hiyo huimarisha mtu avumilie.” Ndiyo, ziara ya uchungaji si ziara ya kirafiki tu ambayo mtu yeyote aweza kufanya.
Kwa Nini Mchungaji Hukuzuru?
Mzee anapozuru nyumba fulani, yeye amejitayarisha kutia moyo waamini wenzake na kuwasaidia kuwa imara katika imani. (Warumi 1:11) Hivyo, mzee mmoja au wawili wanapotaka kukuzuru, wewe huitikiaje? Mwangalizi mmoja asafiriye alisema: “Ziara za uchungaji zinapofanywa tu wakati kuna tatizo, itikio la kwanza kwa ziara iliyopangwa laweza kuwa, ‘Nimefanya kosa gani?’” Wachungaji wa kiroho wenye upendo humwiga Yehova, aliyemchunga mtunga-zaburi na ‘kuburudisha nafsi yake,’ sikuzote hasa katika nyakati za taabu na uhitaji wa pekee.—Zaburi 23:1-4, NW.
Lengo la ziara ya uchungaji ni ‘kujenga, si kubomoa.’ (2 Wakorintho 13:10) Yenye kutia moyo sana ni maneno ya uthamini kwa ajili ya uvumilivu, bidii, na kazi yenye uaminifu ya yule anayetembelewa. Mzee mmoja alisema: “Katika ziara ya uchungaji, si vema kutoa wazo la kwamba umekuja kwa nia ya kugundua na kujadili matatizo. Bila shaka, mtangazaji mwenyewe huenda akataka kuzungumza juu ya tatizo fulani hususa. Na kondoo akichechemea au akijitenga kutoka kwenye kundi, mzee ahitaji kusaidia.”
Bila shaka wazee Wakristo watatunza watu wowote walio kama wale wanaofafanuliwa katika maneno haya: “Nami [Yehova] nitawatafuta waliopotea, nitawarudisha waliofukuzwa, nitawafunga waliovunjika, nitawatia nguvu wagonjwa.” (Ezekieli 34:16) Ndiyo, kondoo waweza kuhitaji kutafutwa, kurudishwa, au kuimarishwa. Wachungaji wa Israeli walipuuza madaraka hayo. Kutimiza kazi hizo huhitaji kwamba mchungaji awakaribie kondoo fulani na kutunza mahitaji yao. Hili hasa lapaswa kuwa jambo kuu la kila ziara ya uchungaji leo.
Kondoo Wenye Afya Wahitaji Kutunzwa
Je, tukate kauli kwamba wachungaji wa kiroho wa kisasa hawahitaji kuonyesha uangalifu hususa kwa kondoo wenye afya? Kondoo halisi anapopata matatizo, kumsaidia ni rahisi ikiwa ana uhakika na mchungaji. Kitabu kimoja chasema kwamba “kiasili kondoo huogopa wanadamu, na si rahisi sikuzote wapate kukutumaini.” Miongoni mwa mambo mengine, kitabu icho hicho chadokeza mwongozo huu wa msingi wa kufanya kondoo wakutumaini: “Sema na wanyama hao kwa ukawaida. Wao huzoea sauti hiyo, ambayo huwapa tumaini. Zuru kondoo malishoni mara nyingi.”—Alles für das Schaf. Handbuch für die artgerechte Haltung (Kila Kitu Kuhusu Kondoo. Kitabu cha Jinsi ya Kuwatunza Ifaavyo).
Basi, mawasiliano na kondoo binafsi ni ya lazima ikiwa uhusiano wenye kutumainiana utakuwapo kati ya mchungaji na kondoo. Ndivyo ilivyo kwa kutaniko la Kikristo. Mzee mmoja alisema: “Kujulikana kutanikoni kuwa mzee atembeleaye kondoo kwa ukawaida hufanya iwe rahisi kumtembelea mtu ambaye ana matatizo.” Hivyo, wachungaji wa kiroho hawapaswi kujaribu kulisha na kutunza kondoo kwenye Jumba la Ufalme pekee. Kadiri hali iruhusuvyo, wazee wapaswa kuwajua kondoo kwa kufanya ziara za uchungaji nyumbani kwao. Mkristo mmoja akumbuka kwamba alipokuwa ametoka kuwekwa rasmi kuwa mzee, mwangalizi-msimamizi alipiga simu na kumwomba azuru na kumfariji ndugu ambaye alikuwa ametoka kumpoteza binti yake katika aksidenti mbaya ya gari. Mzee huyo akiri hivi: “Nilisikitika kama nini, kwa kuwa sikuwa nimepata kumtembelea ndugu huyo na hata sikujua alikoishi! Nilipata kitulizo wakati mzee mkomavu alipojitolea kwenda nami.” Ndiyo, wazee husaidiana katika ziara za uchungaji.
Katika kutayarisha na kufanya ziara fulani za uchungaji, mzee aweza kwenda pamoja na mtumishi wa huduma anayefikia “kazi njema” ya kuwa mwangalizi. (1 Timotheo 3:1, 13) Mtumishi wa huduma huthamini kama nini kuona jinsi mzee atumikiavyo kondoo katika ziara za uchungaji! Hivyo, wazee na watumishi wa huduma hukaribiana na wote kutanikoni, wakiimarisha vifungo vya upendo na muungano wa Kikristo.—Wakolosai 3:14.
Kupanga Wakati wa Ziara za Uchungaji
Wakati baraza moja la wazee lilipoacha ziara za uchungaji zifanywe na viongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko, watangazaji wote katika vikundi fulani walitembelewa kwa muda wa miezi sita, na katika vikundi vingine hakuna yeyote aliyetembelewa. Hilo lilimfanya mzee mmoja aseme: “Inaonekana kwamba wazee fulani huchukua hatua na kufanya kazi nyingi za uchungaji, lakini wengine wahitaji kitia-moyo cha wazee wenzao wafanye hivyo.” Mabaraza fulani ya wazee hufanya mipango ya watangazaji wote kutembelewa na wachungaji katika muda fulani hususa wa wakati.
Bila shaka, mzee au mtangazaji yeyote aweza kumzuru mtu katika kutaniko bila kungoja mipango ya kipekee kufanywa. Kabla ya kufanya ziara ya uchungaji, mzee mmoja hupiga simu na kusema, “Mimi huzuru familia moja kila mwezi. Je, naweza kuwazuru kwa muda wa saa moja hivi wakati fulani mwezi ujao? Mngependelea nije wakati gani?”
Baraka za Ziara za Uchungaji
Kadiri mikazo kutoka kwa mfumo mwovu iongezekapo, ziara zenye kutia moyo zinazofanywa na wachungaji wenye uelewevu huzidi kuwa zenye mafaa. Wote kutanikoni watiwapo moyo na kusaidiwa kupitia ziara za uchungaji, kila kondoo huhisi salama salimini.
Kuhusu kutaniko ambamo watangazaji wote wa Ufalme walitembelewa na wachungaji kwa ukawaida, iliripotiwa hivi: “Watangazaji walikuwa chanya sana kuhusu ziara za uchungaji. Ilikuwa kawaida sana kwa mtangazaji kumwendea mmoja wa wazee kumwuliza atazuru lini tena, kwa kuwa huyo alifurahia mazungumzo yenye kujenga wakati wa ziara iliyopita. Ziara za uchungaji zilikuwa jambo moja lililosaidia kuboresha roho ya kutaniko.” Ripoti nyinginezo zaonyesha kwamba wachungaji wanapohudumu hivyo kwa upendo, kutaniko hukua katika upendo, muungano, na uchangamfu. Hiyo ni baraka iliyoje!
Wachungaji Wakristo huzuru ili kuendeleza hali-njema ya kiroho ya kondoo. Wazee wanataka kutia moyo na kuimarisha waamini wenzao. Tatizo zito linalohitaji shauri likifunuliwa wakati wa ziara hiyo, inaweza kuwa vema kufanya mipango kwa ajili ya mazungumzo wakati mwingine, hasa ikiwa mzee ameandamana na mtumishi wa huduma. Kwa vyovyote vile, inafaa kufunga ziara ya uchungaji kwa sala.
Je, mchungaji wa kiroho anataka kuzuru nyumba yako karibuni? Ikiwa ndivyo, furahi ukitazamia kitia-moyo kinachokungoja. Anakuja kukutumikia na kukuimarisha katika azimio lako la kubaki katika barabara iendayo kwenye uhai udumuo milele.—Mathayo 7:13, 14.
[Sanduku katika ukurasa wa 26]
Madokezo ya Kufanya Ziara za Uchungaji
◻ Fanya miadi: Kwa kawaida ni vizuri kufanya miadi. Mzee akipanga kushughulikia tatizo zito, ingefaa kumjulisha huyo mtangazaji jambo hili kabla ya wakati.
◻ Matayarisho: Fikiria utu na hali ya mtu huyo. Mpongeze kutoka moyoni. Uwe na lengo la kumpa ‘zawadi ya kiroho’ yenye kumtia moyo na kuimarisha imani yake.—Warumi 1:11, 12, NW.
◻ Mtu wa kwenda naye: Mzee mwingine au mtumishi wa huduma anayestahili.
◻ Wakati wa ziara: Huyo mzee apaswa kuwa mtulivu, mwenye upendo, chanya, na mwenye kubadilikana. Uliza hali ya familia, inavyoendelea, na kadhalika. Sikiliza kwa makini. Tatizo zito likitokea, inaweza kuwa bora kupanga kuwe na ziara ya uchungaji ya kipekee.
◻ Muda wa ziara: Dumisha wakati mliokubaliana, na uondoke wakati mwenye nyumba angali anafurahia ziara.
◻ Kumaliza ziara: Sala hufaa na huthaminiwa kikweli.—Wafilipi 4:6, 7.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Wachungaji wa Kikristo huandaa ulinzi wa kiroho
[Picha katika ukurasa wa 26]
Ziara za uchungaji huandaa fursa nzuri za kitia-moyo cha kiroho