Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
“Maagizo Yako Yote Ni Kweli”
MUDA mfupi kabla ya kifo chake, Musa aliwahimiza watu wa Israeli watii kila amri ya Yehova. Alisema: “Yawekeni mioyoni mwenu maneno yote ambayo nashuhudia kwenu hivi leo; nayo waamuruni watoto wenu, wayatunze na kuyafanya maneno yote ya torati hii. Kwa maana si jambo lisilofaa kwenu; maana, ni maisha yenu.”—Kumbukumbu la Torati 32:46, 47.
Mamia ya miaka baadaye, mtunga-zaburi alionyesha umuhimu wa mafundisho yote ya Mungu aliposema: “Ee BWANA, wewe U karibu, na maagizo yako yote ni kweli.” (Zaburi 119:151) Katika karne ya kwanza, Yesu mwenyewe alirejezea thamani ya “kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” (Mathayo 4:4) Chini ya mwelekezo wa Mungu mtume Paulo aliandika kuwa “kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho.”—2 Timotheo 3:16.
Ni wazi kwamba Yehova Mungu huwatarajia waabudu wake watoe uangalifu mzito kwa ujumbe wote tuliopewa katika kurasa za Neno lake. Hakuna fungu la maneno hata moja katika Biblia lisilo na thamani. Hivyo ndivyo Mashahidi wa Yehova wanavyohisi juu ya Neno la Mungu, kama itolewavyo kielezi katika jambo lifuatalo lililoonwa kutoka Mauritius.
Bw. D—aliishi kwenye kijiji cha mbali, ambapo alikuwa mlinzi wa usiku. Kwa muda mrefu, alikuwa akitafuta kwa unyoofu njia ifaayo ya kumwabudu Mungu. Usiku, wakati alipokuwa akilinda, akaanza kuisoma Biblia. Baada ya muda akawa ameisoma jalada hadi jalada. Alijifunza kwamba jina la Mungu ni Yehova—jina lipatikanalo mara nyingi katika Biblia ya Kihindi. Alikiona kitabu cha Ufunuo kuwa chenye kushangaza sana.
Kisha alijiuliza ikiwa kuna dini itendayo kulingana na Biblia yote nzima. Alitambua kuwa dini alizofahamu zilikuwa zikifuata tu visehemu vya Biblia. Dini fulani zilikubali Maandiko ya Kiebrania na kukataa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Dini nyingine zilipuuza Maandiko ya Kiebrania, zikiyachukua Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo tu kuwa yenye mafaa.
Siku moja Bw. D—aliona wenzi wawili wa ndoa wakinyeshewa naye akawakaribisha ili wajikinge mvua nyumbani kwake. Walikuwa Mashahidi wa Yehova. Mke alikuwa akishika mkononi kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!a Mara moja Bw. D—akaomba hicho kitabu. Hao Mashahidi walihisi kuwa habari juu ya unabii wa Ufunuo ilikuwa nzito sana kwake, hivyo wakampa kichapo kingine badala yacho. Lakini Bw. D—akasisitiza apewe kitabu Ufunuo.
Alipopata nakala yake, alikisoma kitabu hicho upesi. Kisha akakubali funzo la Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Upesi alivutiwa na uhakika wa kwamba hao Mashahidi wanastahi sana Biblia nzima. Alianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, ambapo Maandiko ya Kiebrania na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanachunguzwa kwa uangalifu. Yeye sasa ni mpiga-mbiu wa Ufalme na mshiriki aliyebatizwa wa kutaniko la Kikristo.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.