Je, Mungu Hukubali Kila Namna ya Ibada?
MUNGU alimuumba mwanadamu akiwa na uhitaji wa kiroho—uhitaji wa kuabudu. Si jambo lililotokana na mageuzi. Huo ulikuwa sehemu ya mwanadamu tangu mwanzoni.
Hata hivyo, kwa kuhuzunisha, wanadamu wamesitawisha namna nyingi tofauti-tofauti za ibada, na kwa ujumla, hizi hazijatokeza familia ya kibinadamu yenye furaha, iliyounganika. Badala ya hivyo, vita vyenye umwagikaji wa damu vingali vinapiganwa katika jina la dini. Hilo latokeza swali hili la maana: Je, ni jambo la maana jinsi mtu anavyomwabudu Mungu?
Ibada Yenye Kutilika Shaka Katika Nyakati za Kale
Mataifa ya kale yaliyokaa Mashariki ya Kati yaandaa kielelezo cha kihistoria kinachotusaidia kujibu swali hilo. Wengi walimwabudu mungu aliyeitwa Baali. Pia waliwaabudu waandamani wa kike wa Baali, kama Ashera. Ibada ya Ashera ilihusisha utumizi wa nguzo takatifu iliyoaminiwa kuwa ufananisho wa kingono. Wachimbuzi wa vitu vya kale wakifanya kazi katika eneo hilo wamechimbua mifano mingi ya wanawake walio uchi. Mifano hii, yataarifu The Encyclopedia of Religion, “huonyesha mungu wa kike mwenye viungo vya uzazi vilivyo vikubwa, akiwa ameinua matiti yake,” na “labda huwakilisha . . . Ashera.” Jambo moja ni hakika, mara nyingi ibada ya Baali ilikuwa yenye kukosa adili sana.
Kwa hiyo, haishangazi kwamba ibada ya Baali ilihusisha sherehe za kingono. (Hesabu 25:1-3) Shekemu, Mkaanani, alimbaka yule bikira mchanga Dina. Licha ya hilo alionwa kuwa mwanamume mwenye kuheshimika sana katika familia yake. (Mwanzo 34:1, 2, 19) Ngono ya maharimu (watu wa ukoo), ugoni-jinsia-moja, na ngono na wanyama ilikuwa ya kawaida. (Mambo ya Walawi 18:6, 22-24, 27) Neno “usodoma” lenyewe, zoea la wagoni-jinsia-moja, hutokana na jina la jiji ambalo wakati mmoja lilikuwamo katika sehemu hiyo ya ulimwengu. (Mwanzo 19:4, 5, 28) Ibada ya Baali ilihusisha pia umwagikaji wa damu. Kwani, waabudu wa Baali walikuwa wakiwatupa watoto wao wakiwa hai ndani ya mioto yenye kuwaka sana wawe dhabihu kwa miungu yao! (Yeremia 19:5) Mazoea haya yote yalihusiana na mafundisho ya kidini. Jinsi gani?
“Ule unyama, ashiki, na kule kutojizuia kwa dhana za kingano za Kikanaani,” aeleza Dakt. Merrill Unger katika kitabu chake Archaeology and the Old Testament, “ni kubaya zaidi kuliko kwingineko katika Mashariki ya Karibu wakati ule. Na sifa yenye kutokeza ya miungu ya Kikanaani, kwamba haikuwa na sifa yoyote ya kiadili, lazima iwe ilitokeza tabia mbaya zaidi katika waabudu wayo na kutia ndani mengi ya mazoea yenye kupotosha zaidi ya wakati huo, kama umalaya mtakatifu, [na] kudhabihu watoto.”
Je, Mungu alikubali ibada ya Wakanaani? Bila shaka la. Yeye alifundisha Waisraeli jinsi ya kumwabudu katika njia safi. Kuhusu mazoea yaliyotajwa hapo juu, yeye alionya hivi: “Msijitie unajisi katika mambo hayo hata mojawapo; kwa maana hizo taifa nitakazozitoa mbele zenu zimekuwa najisi kwa mambo hayo yote; na hiyo nchi imekuwa najisi; kwa ajili ya hayo naipatiliza uovu wake juu yake, na hiyo nchi yatapika wenyeji wake na kuwatoa.”—Mambo ya Walawi 18:24, 25.
Ibada Safi Yachafuliwa
Waisraeli wengi hawakukubali maoni ya Mungu juu ya ibada safi. Badala ya hivyo, waliruhusu ibada ya Baali iendelee katika nchi yao. Upesi Waisraeli wakashawishwa kujaribu kuchanganya ibada ya Yehova na ile ya Baali. Je, Mungu alikubali namna hii ya ibada iliyochanganywa? Fikiria kilichotukia wakati wa utawala wa Mfalme Manase. Yeye alijenga madhabahu ya Baali, akamchoma mwanae mwenyewe kuwa dhabihu, na kuzoea mizungu. “Akaiweka sanamu ya kuchongwa [“nguzo takatifu,” NW] [ʼashe·rahʹ katika Kiebrania] ya Ashera aliyoifanya ndani ya nyumba, ambayo BWANA [alisema juu yayo] . . . Katika nyumba hii . . . nitaliweka jina langu milele.”—2 Wafalme 21:3-7.
Raia wa Manase walifuata kielelezo cha mfalme wao. Kwa kweli, yeye “a[li]wakosesha wafanye mabaya, kuliko mataifa BWANA aliowaharibu mbele za wana wa Israeli.” (2 Wafalme 21:9) Badala ya kutii maonyo yaliyorudiwa kutoka kwa manabii wa Mungu, Manase aliua kimakusudi kwa kiwango cha kulijaza Yerusalemu damu isiyo na hatia. Ingawa hatimaye Manase alijirekebisha, mwanae na mwandamizi wake, Mfalme Amoni, alianzisha upya ibada ya Baali.—2 Wafalme 21:16, 19, 20.
Hatimaye, malaya wa kiume wakaanza kujiendesha vibaya hekaluni. Mungu alionaje wonyesho huu wa ibada ya Baali? Yeye alikuwa ameonya hivi kupitia Musa: “Usilete ujira wa kahaba, wala mshahara wa mbwa [yaelekea mwanamume afiraye mvulana], katika nyumba ya BWANA, Mungu wako, kwa ajili ya nadhiri yo yote; kwani haya ni machukizo kwa BWANA, Mungu wako, yote mawili.”—Kumbukumbu la Torati 23:17, 18, NW, kielezi-chini.
Mjukuu wa Manase, Mfalme Yosia, alisafisha hekalu na kuondoa ibada ya Baali yenye kukosa adili. (2 Wafalme 23:6, 7) Lakini hali ilikuwa imepita kiasi. Punde si punde baada ya kifo cha Yosia, ibada ya sanamu ilikuwa ikiendelea tena katika hekalu la Yehova. (Ezekieli 8:3, 5-17) Kwa hiyo Yehova akasababisha mfalme wa Babiloni kuliharibu Yerusalemu na hekalu lalo. Jambo hili la hakika lenye kuhuzunisha ni ithibati kwamba namna fulani za ibada hazikubaliki kwa Mungu. Namna gani siku yetu?