Ibada ya Baali—Pambano la Kupata Mioyo ya Waisraeli
Kwa karibu miaka elfu moja,pambano liliendelea kwa ajili ya kupata mioyo ya taifa la Israeli. Woga wa kishirikina na sherehe za kingono kwa upande mmoja zilipambana na imani na uaminifu-mshikamanifu kwa upande mwingine. Pambano hilo la kufa na kupona lilitokeza shindano kali kati ya ibada ya Baali na ibada ya Yehova.
JE, TAIFA la Israeli lingeshikamana kwa uaminifu na Mungu wa kweli, aliyewatoa Misri? (Kutoka 20:2, 3) Au je, wangemgeukia Baali, mungu aliyependwa na Wakanaani, ambaye aliahidi kufanya nchi izae?
Pambano hilo la kiroho, lililopiganwa maelfu ya miaka iliyopita, latuhusu. Kwa nini? “Mambo hayo,” akaandika mtume Paulo, “yaliandikwa kuwa onyo kwetu sisi ambao juu yetu miisho ya mifumo ya mambo imewasili.” (1 Wakorintho 10:11) Onyo la kimsingi la pambano hilo la kihistoria litakuwa na umaana zaidi ikiwa twaelewa Baali alikuwa nani, na kile ambacho ibada ya Baali ilihusisha.
Baali Alikuwa Nani?
Waisraeli walijua kuhusu Baali walipowasili Kanaani, karibu mwaka wa 1473 K.W.K. Walikuta kwamba Wakanaani waliabudu miungu mingi ambayo haikutofautiana na miungu ya Misri, ingawa ilikuwa na majina tofauti na tabia fulani tofauti. Hata hivyo, Biblia hutaja Baali kihususa kuwa ndiye mungu mkuu wa Wakanaani, na uvumbuzi wa kiakiolojia wathibitisha sifa yake. (Waamuzi 2:11) Ingawa Baali hakuwa mungu mkuu wa miungu yao yote, yeye ndiye aliyekuwa wa muhimu sana kwa Wakanaani. Waliamini kwamba alidhibiti mvua, upepo, na mawingu na kwamba yeye pekee angeweza kuwaokoa watu—na vilevile mifugo yao na mimea yao—kutokana na kutozaa na hata kifo. Pasipo ulinzi wa Baali, Mot, mungu wa Wakanaani mwenye kulipiza kisasi, kwa kweli angeleta misiba juu yao.
Ibada ya Baali iliongozwa na sherehe za kingono. Hata vifaa vya kidini vilivyohusu Baali, kama vile nguzo takatifu, vilikuwa vitu vilivyodokeza ngono. Kwa wazi, nguzo takatifu—miamba au mawe yaliyochongwa kwa mfano wa uume—ziliwakilisha Baali, sehemu ya kiume ya mwungano wa kingono. Kwa upande mwingine, nguzo takatifu za mbao au miti ziliwakilisha Ashera, mke wa Baali na sehemu ya uke.—1 Wafalme 18:19.
Ukahaba wa hekaluni na kudhabihu watoto vilikuwa sehemu nyingine kuu za ibada ya Baali. (1 Wafalme 14:23, 24; 2 Mambo ya Nyakati 28:2, 3) Kitabu The Bible and Archaeology chasema hivi: “Katika mahekalu ya Wakanaani kulikuwepo makahaba wa kiume na wa kike (wanaume na wanawake ‘watakatifu’) na walifanya kila aina ya ngono yenye kupita kiasi. [Wakanaani] waliamini kwamba katika njia fulani hizi sherehe zilisababisha mimea na mifugo kusitawi.” Kwa vyovyote, hiyo ndiyo iliyokuwa sababu ya kidini iliyotolewa, ingawa ukosefu wa adili wa jinsi hiyo bila shaka ulivutia tamaa za kimwili za waabudu. Ni jinsi gani, basi, Baali alishawishi mioyo ya Waisraeli?
Kwa Nini Ilivutia Sana?
Labda Waisraeli wengi walipendelea kufuata dini ambayo haikuwataka wafanye mengi. Kwa kuabudu Baali hawangehitajika kushika Sheria, kama vile Sabato na vizuizi vingi vya kiadili. (Mambo ya Walawi 18:2-30; Kumbukumbu la Torati 5:1-3) Yawezekana mafanikio ya mali za kimwili ya Wakanaani yaliwashawishi wengine kwamba Baali alihitaji kuridhishwa.
Madhabahu za Wakanaani, zilizoitwa mahali pa juu na zilizokuwa katika vijisitu vya miti ubavuni mwa milima, huenda zilifanyiza mandhari ya sherehe za uzazi zilizofanyiwa hapo. Punde si punde, Waisraeli hawakutosheka na kwenda mara kwa mara kwenye maeneo matakatifu ya Wakanaani; wao hata walijenga yao wenyewe. “Hao pia wakajijengea mahali pa juu, na nguzo, na maashera, juu ya kila kilima kirefu, na chini ya kila mti wenye majani mabichi.”—1 Wafalme 14:23; Hosea 4:13.
Lakini kwanza kabisa, ibada ya Baali ilichochea tamaa ya mwili. (Wagalatia 5:19-21) Mazoea ya kiashiki yalizidi tamaa ya kupata mazao mengi na mifugo wengi. Ngono ilitukuzwa. Hilo lathibitishwa na sanamu nyingi ndogo ambazo zimefukuliwa, zikiwa na sehemu za siri zenye kutokeza sana, zikionyesha hamu ya kingono. Karamu, kucheza dansi, na muziki viliwatayarisha kwa ajili ya mwenendo mpotovu kiadili.
Twaweza kuwazia juu ya mandhari ya mfano wakati wa majira ya mvua. Katika hali halisi yenye kutokeza, wakiwa wamekula kwa pupa na kuchangamshwa kwa divai, hao waabudu wacheza. Dansi yao ya ashiki imekusudiwa kumwamsha Baali kutoka katika kutotenda kwake wakati wa kiangazi ili nchi ipate mvua. Wanacheza kuzunguka nguzo za uume na nguzo za Ashera. Miendo, hasa ile ya makahaba wa hekaluni, inaamsha nyege na ashiki. Muziki na watazamaji vyawatia ari. Na yaelekea, kwenye upeo wa dansi hiyo, wacheza dansi wanaenda kwenye vyumba vya nyumba ya Baali ili kufanya ngono zisizo za adili.—Hesabu 25:1, 2; linganisha Kutoka 32:6, 17-19; Amosi 2:8.
Walitembea kwa Kuona, Si kwa Imani
Ingawa aina hiyo ya ibada yenye ashiki iliwavutia wengi, woga pia uliwaingiza Waisraeli katika kuabudu Baali. Waisraeli walipopoteza imani yao katika Yehova, kuogopa wafu, kuogopa wakati ujao, na kupendezwa na mafumbo viliwaingiza katika zoea la uwasiliani-roho, ambao kwa upande mwingine ulihusisha sherehe zenye upotovu mkubwa sana. The International Standard Bible Encyclopedia yafafanua jinsi ambavyo Wakanaani waliheshimu roho za wafu ikiwa sehemu ya kuabudu wazazi wa kale waliokufa: “Karamu . . . zilisherehekewa kwenye kaburi la familia au mahali pa kuzikia kukiwa na ulevi wa kisherehe na kufanya ngono (labda ikihusisha ngono ya maharimu), na ilidhaniwa kwamba wafu walishiriki.” Kushiriki mazoea ya uwasiliani-roho yenye upotovu kama huo kuliwatenganisha Waisraeli hatua kwa hatua kutoka kwa Mungu wao, Yehova.—Kumbukumbu la Torati 18:9-12.
Sanamu—na sherehe zilizoambatana nazo—pia ziliwavutia Waisraeli ambao walipendelea kutembea kwa kuona badala ya kutembea kwa imani. (2 Wakorintho 5:7) Hata baada ya kuona miujiza yenye kutokeza kupitia mkono usioonekana wa Yehova, Waisraeli wengi waliotoka Misri waliona uhitaji wa kitu kilichoonekana, chenye kuwakumbusha kuhusu Yehova. (Kutoka 32:1-4) Baadhi ya wazao wao vilevile walitaka kuabudu kitu kinachoonekana, kama vile sanamu za Baali.—1 Wafalme 12:25-30.
Nani Alipata Ushindi?
Pambano la kupata mioyo ya Waisraeli liliendelea kwa karne nyingi, kutoka wakati walipowasili kwenye nyanda za Moabu punde tu kabla ya kuingia Bara Lililoahidiwa hadi wakati wa kuhamishiwa Babiloni. Ushindi ulionekana kugeuka-geuka. Nyakati nyingine, Waisraeli walio wengi walibaki waaminifu kwa Yehova, lakini mara kwa mara walimgeukia Baali. Sababu kuu ya kufanya hivyo ilikuwa ushirikiano wao na watu wapagani waliowazunguka.
Baada ya kushindwa katika vita ya kijeshi, Wakanaani walipigana kwa mbinu zenye ujanja zaidi. Waliishi pamoja na Waisraeli na kuwatia moyo washindi wao kufanya miungu ya nchi hiyo kuwa yao wenyewe. Waamuzi wenye ujasiri kama Gideoni na Samweli walipinga mwelekeo huo. Samweli aliwahimiza watu hivi: “Iondoleeni mbali miungu migeni . . . , mkamtengenezee BWANA mioyo yenu, mkamtumikie yeye peke yake.” Kwa muda fulani Waisraeli walitii himizo la Samweli, na “wakayaondoa Mabaali na Maashtorethi, wakamtumikia BWANA peke yake.”—1 Samweli 7:3, 4; Waamuzi 6:25-27.
Baada ya utawala wa Sauli na Daudi, Solomoni alianza kutoa dhabihu kwa miungu ya kigeni katika miaka yake ya baadaye. (1 Wafalme 11:4-8) Wafalme wengine wa Waisraeli na Yuda walifanya vivyo hivyo na wakamgeukia Baali. Hata hivyo, manabii na wafalme waaminifu, kama vile Eliya, Elisha, na Yosia, waliongoza katika kupigana dhidi ya ibada ya Baali. (2 Mambo ya Nyakati 34:1-5) Zaidi ya hayo, kwa kipindi hicho chote cha historia ya Israeli, kulikuwako watu mmoja-mmoja waliobaki waaminifu kwa Yehova. Hata wakati wa Ahabu na Yezebeli, wakati ambapo ibada ya Baali ilifikia upeo, watu elfu saba walikataa ‘kumwinamia Baali.’—1 Wafalme 19:18.
Hatimaye, baada ya Wayahudi kurudi kutoka uhamishoni Babiloni, hakuna mtajo wowote tena kuhusu ibada ya Baali. Kama wale wanaorejezewa kwenye Ezra 6:21, wote ‘walijitenga’ kutoka uchafu wa mataifa, ili kumtaka BWANA, Mungu wa Israeli.’
Maonyo Kutoka kwa Ibada ya Baali
Ingawa ibada ya Baali ilitoweka kitambo, dini ya Wakanaani na jamii ya leo vina kitu kimoja kinachofanana—utukuzo wa ngono. Vitu vya kutushawishi tuingie katika ukosefu wa adili vyaonekana kuwa vimo katika hewa tunayopumua. (Waefeso 2:2) “Tunapigana dhidi ya nguvu isiyoonekana ambayo inaudhibiti ulimwengu huu wenye giza, na waakilishi wa kiroho kutoka makao makuu hasa ya uovu,” Paulo aonya.—Waefeso 6:12, Phillips.
“Nguvu [hiyo] isiyoonekana” ya Shetani huendeleza ukosefu wa adili katika ngono ili kuwatumikisha watu kiroho. (Yohana 8:34) Katika jamii ya siku hizi yenye uendekevu, kujiingiza mno katika ngono hakuzoewi kama sherehe ya uzazi bali, kama njia ya kujipa uradhi au ya mtu kufanya mambo yake mwenyewe. Nayo propaganda hiyo inashawishi vivyo hivyo. Kupitia vitumbuizo, muziki, na matangazo ya biashara, jumbe za kingono hujaa akili za watu. Watumishi wa Mungu wanaweza kudhuriwa na shambulio hilo. Kwa hakika, wengi wa wale waliotengwa kutoka kutaniko la Kikristo ni watu ambao walijiingiza katika mazoea ya jinsi hiyo. Ni kwa kukataa katakata mielekeo hiyo ya ukosefu wa adili ndipo tu Mkristo atabaki akiwa safi kiadili.—Waroma 12:9.
Mashahidi wachanga hasa wanakabili hatari, kwa kuwa vitu vingi ambavyo huenda wakaona kuwa vinavutia vimejaa mambo ya kingono. Kufanya mambo kuwa magumu zaidi, wanapaswa kukinza msongo wa vijana wengine wanaowahimiza wajiingize katika mambo hayo. (Linganisha Mithali 1:10-15.) Kwa mfano, wengi wametumbukia katika matatizo, wakiwa katika vikusanyiko vikubwa. Kama ilivyokuwa katika ibada ya Baali nyakati za kale, muziki, kucheza dansi, na uvutio wa kingono hutokeza mchanganyiko wenye kulevya.—2 Timotheo 2:22.
“Jinsi gani kijana aisafishe njia yake?” mtunga-zaburi akauliza. “Kwa kutii, akilifuata neno [la Yehova],” akajibu. (Zaburi 119:9) Kama vile tu Sheria ya Mungu ilivyowaamuru Waisraeli wakatae ushirikiano wa karibu na Wakanaani, vivyo hivyo Biblia hutuweka macho kuhusu hatari za mashirika mabaya. (1 Wakorintho 15:32, 33) Kijana Mkristo huonyesha ukomavu wake anapokataa kitu ambacho huenda kikawa chenye kuvutia kiashiki lakini ambacho yeye ajua ni chenye madhara kiadili. Kama Eliya mwaminifu, hatupaswi kuruhusu wimbi la maoni ya watu wengi litufanyie maamuzi.—1 Wafalme 18:21; linganisha Mathayo 7:13, 14.
Onyo jingine lahusu kupoteza imani, “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.” (Waebrania 12:1) Yaonekana kuwa Waisraeli wengi bado walimwamini Yehova, lakini walimtegemea Baali akiwa mungu ambaye angelinda mimea yao na kuwaandalia mahitaji yao ya kila siku. Labda walihisi kwamba hekalu la Yehova lililokuwa Yerusalemu lilikuwa mbali sana na kwamba haikuwezekana kushika sheria zake. Ibada ya Baali haikuwataka wafanye mengi na iliwafaa sana —hata wangeweza kutoa uvumba kwa Baali wakiwa juu ya paa za nyumba zao. (Yeremia 32:29) Yawezekana waliingia katika ibada ya Baali kupitia kushiriki tu katika sherehe kadhaa au hata kwa kutoa matoleo kwa Baali katika jina la Yehova.
Twaweza kupotezaje imani na tutoke kwa Mungu aliye hai hatua kwa hatua? (Waebrania 3:12) Twaweza kupoteza uthamini tuliokuwa nao kwa mikutano na makusanyiko hatua kwa hatua. Mtazamo wa jinsi hiyo hudhihirisha ukosefu wa uhakika katika uandalizi wa Yehova wa ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao.’ (Mathayo 24:45-47) Tukiwa tumedhoofishwa hivyo, huenda tukalegeza “kushika kwa mkazo neno la uhai” au hata kukuza moyo uliogawanyika, labda tukijiachilia tuingilie ufuatiaji wa vitu vya kimwili au ukosefu wa adili.—Wafilipi 2:16; linganisha Zaburi 119:113.
Kushika Sana Uaminifu-Maadili Wetu
Hakuna shaka kwamba leo pambano linaendelea kwa ajili ya moyo. Je, tutabaki waaminifu-washikamanifu kwa Yehova au tutakengeushwa na maisha mapotovu ya ulimwengu huu? Kwa kuhuzunisha, kama tu vile Waisraeli walivyovutiwa na mazoea yenye kuchukiza ya Wakanaani, baadhi ya Wakristo wanaume na wanawake leo wameshawishwa kutenda vitendo vya aibu.—Linganisha Mithali 7:7, 21-23.
Kushindwa huko kwa kiroho kwaweza kuepukwa ikiwa, kama Musa, twaendelea ‘tukiwa imara kama tunaona Yeye asiyeonekana.’ (Waebrania 11:27) Ni kweli, twahitaji ‘kufanya pigano kali kwa ajili ya imani.’ (Yuda 3) Lakini kwa kubaki waaminifu-washikamanifu kwa Mungu wetu na kwa kanuni zake, twaweza kutazamia kwa hamu wakati ambapo ibada isiyo ya kweli itapotelea mbali milele. Kama vile tu ibada ya Yehova ilivyopata ushindi dhidi ya ibada ya Baali, vivyo hivyo twaweza kuwa na uhakika kwamba karibuni “dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Magofu katika Gezer ya nguzo takatifu zilizotumiwa katika ibada ya Baali
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 28]
Musée du Louvre, Paris