Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 4/1 kur. 23-27
  • Kutafuta Paradiso

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutafuta Paradiso
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kurudi Mashambani
  • Imani Katika Mungu Yachochewa
  • Jibu kwa Sala Zangu
  • Kufanya Maendeleo ya Kiroho
  • Msaada Nikiwa Katika Taabu
  • Kujitahidi Kupata Kitu Kilicho Bora Zaidi
  • Betheli—Paradiso ya Kiroho Yenye Kutokeza
  • Je, Waweza Kujitolea?
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • Je, Hii Yaweza Kuwa Kazi-Maisha Inayokufaa Zaidi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Sijaacha Kamwe Kujifunza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Watu Wote Wanaalikwa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 4/1 kur. 23-27

Kutafuta Paradiso

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA PASCAL STISI

Ilikuwa usiku sana, nazo barabara za mji wa Béziers, kusini mwa Ufaransa, zilikuwa hazina watu. Tulipopata ukuta wa duka la vitabu vya dini ambao ulikuwa umepakwa rangi karibuni, mimi na rafiki yangu tuliandika juu yake, kwa kutumia herufi kubwa nyeusi, maneno haya ya Nietzsche, mwana-falsafa Mjerumani: ‘Miungu wamekufa. Na aishi kwa muda mrefu yule Mtu Bora Kupita Wote!’ Hata hivyo, ni nini kilichoniongoza kufanya hayo yote?

NILIZALIWA Ufaransa mwaka wa 1951 katika familia ya Wakatoliki iliyotoka Italia. Nilipokuwa mtoto, tulikuwa tukienda likizo huko kusini mwa Italia. Huko, kila kijiji kilikuwa na sanamu yake ya Bikira Maria. Huku nikitembea pamoja na babu yangu, nilifuata misululu isiyo na mwisho ya sanamu hizi kubwa zilizokuwa zimevikwa mavazi—lakini sikusadikishwa jambo lolote. Nilimaliza elimu yangu ya msingi katika shule ya kidini iliyosimamiwa na Wayesuiti. Hata hivyo, siwezi kukumbuka ikiwa nilisikia lolote ambalo kwa kweli lilisitawisha imani yangu katika Mungu.

Nilianza kufikiri juu ya kusudi la uhai wakati nilipojiunga na chuo kikuu huko Montpellier kusomea udaktari. Baba yangu alikuwa amejeruhiwa wakati wa vita na sikuzote madaktari walikuwa kando ya kitanda chake. Je, haingefaa zaidi kumaliza vita badala ya kutumia wakati na jitihada nyingi kuponya watu kutokana na madhara yake? Hata hivyo, Vita ya Vietnam ilikuwa imepamba moto. Kwa mfano, kwa maoni yangu, njia iliyopatana na akili ya kutibu kansa ya mapafu ilikuwa kuondoa kabisa kisababishi kikuu cha kansa hiyo, yaani, tumbaku. Na vipi kuhusu magonjwa yaliyotokana na utapiamlo katika nchi zinazositawi na yale yanayotokana na kula kupita kiasi katika nchi zenye utajiri? Je, haingefaa kuondoa visababishi badala ya kujaribu kurekebisha matokeo yenye kuhuzunisha? Kwa nini kulikuwa na kuteseka kwingi sana duniani? Nilihisi kwamba kulikuwa na kasoro kubwa kuhusiana na jamii hii yenye kujiua, nami nilizilaumu serikali.

Kitabu nilichokipenda zaidi kiliandikwa na mwasi-mamlaka fulani, nami nilikuwa nikinakili mistari yake juu ya kuta. Hatua kwa hatua, mimi pia nikawa mwasi-mamlaka, asiye na imani wala sheria za kiadili, ambaye hakutaka Mungu wala bwana-mkubwa. Kwa maoni yangu, Mungu na dini zilikuwa ubuni wa matajiri na wale wenye uwezo, ili waweze kututawala na kujinufaisha wenyewe. Ni kana kwamba walikuwa wakisema ‘Tufanyieni kazi kwa bidii duniani, nayo thawabu yenu itakuwa kubwa katika paradiso mbinguni.’ Lakini mamlaka ya miungu yalikuwa yamekwisha. Watu walihitaji kuambiwa. Njia moja ya kuwaambia ilikuwa kuandika juu ya kuta.

Tokeo ni kwamba masomo yangu yaliwekwa mahali pa pili. Wakati huohuo, nilikuwa nimejiunga na chuo kikuu kingine huko Montpellier ili kusomea jiografia na ikolojia, ambapo uasi dhidi ya mamlaka ulikuwa umeenea sana. Kadiri nilivyozidi kujifunza ikolojia, ndivyo nilivyozidi kuchukizwa kuona kuchafuliwa kwa sayari yetu nzuri.

Kila mwaka wakati wa likizo ya kiangazi, nilisafiri maelfu ya kilometa kotekote Ulaya kwa kuomba lifti. Nilipokuwa nikisafiri na kuzungumza na mamia ya madereva, nilijionea maovu na uharibifu unaoikumba jamii ya kibinadamu. Wakati mmoja, nilipokuwa nikitafuta paradiso, niliona fuo nzuri sana kwenye kisiwa kizuri cha Krete lakini zilikuwa zimefunikwa kwa mafuta. Nilihuzunika sana. Je, kulikuwa na sehemu ya paradiso ambayo ilikuwa imebaki popote duniani?

Kurudi Mashambani

Huko Ufaransa wanaikolojia walikuwa wakitetea kurudi mashambani kuwa utatuzi wa matatizo ya jamii. Nilitaka kufanya kazi kwa mikono yangu. Kwa hiyo, nilinunua nyumba ya zamani iliyojengwa kwa mawe katika kijiji kidogo kwenye vilima vilivyoko chini ya Milima ya Cévennes, kusini mwa Ufaransa. Kwenye mlango, niliandika “Paradiso Sasa,” maneno ya shime ya waasi-mila wa Marekani. Msichana kijana kutoka Ujerumani aliyekuwa akisafiri kupitia eneo letu akawa mwandamani wangu. Singeweza kwa vyovyote kukubali kuhalalisha ndoa yangu mbele ya meya, ambaye ni mwakilishi wa serikali. Vipi kuihalalishia kanisani? Sahau kabisa!

Mara nyingi tulitembea bila viatu, nami nilikuwa na nywele ndefu na ndevu za timtimu. Kilimo cha matunda na mboga kulinivutia sana. Wakati wa kiangazi, anga lilikuwa bluu nao nyenje waliimba. Maua ya pori yalikuwa yenye harufu nzuri sana, nayo matunda ya Bahari ya Mediterania tuliyokuza—zabibu na tini—yalikuwa matamu sana! Ilionekana kana kwamba tulikuwa tumepata mahali palipotufaa kabisa katika paradiso.

Imani Katika Mungu Yachochewa

Kwenye chuo kikuu, nilikuwa nimesomea biolojia ya chembe, taaluma ya maisha ya kiinitete, na elimu ya muundo wa mwili, nami nilivutiwa sana na utata na upatano wa vitu hivyo vyote. Kwa vile sasa ningeweza kufikiri kwa makini na kuchunguza uumbaji moja kwa moja kila siku, nilistaajabishwa na uzuri wake na nguvu zake zisizodhihirika. Kitabu cha uumbaji kilikuwa wazi mbele yangu, siku baada ya siku. Siku moja, nilipokuwa nikitembea vilimani, baada ya kufikiria sana maisha, nilifikia mkataa kwamba ni lazima kuwe na Muumba. Niliamua moyoni mwangu kuamini katika Mungu. Hapo awali, nilihisi utupu fulani moyoni mwangu, upweke wenye kusumbua. Siku ile nilipoanza kuamini katika Mungu, niliwaza, ‘Pascal, hutakuwa peke yako tena.’ Ulikuwa msisimko wa ajabu.

Baadaye kidogo, mimi na mwandamani wangu tulipata msichana mdogo—Amandine. Nilimpenda sana. Kwa kuwa sasa niliamini katika Mungu, nilianza kustahi sheria chache za adili nilizojua. Niliacha kuiba na kusema uwongo, na punde si punde nikang’amua kwamba kufanya hivyo kulinisaidia kuepuka kuwa na matatizo mengi na wale waliokuwa karibu nami. Naam, tulikuwa na matatizo yetu, na paradiso yangu haikuwa kwa vyovyote vile nilivyotarajia. Wakulima wa mizabibu wa mahali hapo walitumia viua-wadudu na viua-magugu ambavyo vilichafua mimea yangu. Swali langu kuhusu chanzo cha uovu lilikuwa bado halijajibiwa. Isitoshe, ingawa nilikuwa nimesoma sana juu ya maisha ya familia, jambo hilo halikuzuia mabishano makali kati yangu na mwandamani wangu. Tulikuwa na rafiki wachache, nao hawakuwa wa kweli; baadhi yao hata walimshawishi mwandamani wangu asiwe mwaminifu kwangu kingono. Lazima kulikuwa na paradiso nzuri zaidi.

Jibu kwa Sala Zangu

Nilisali kivyangu ili nipate mwongozo kutoka kwa Mungu. Jumapili moja asubuhi, mwanamke mwenye urafiki aliyeitwa Irène Lopez na mvulana wake mdogo walitutembelea nyumbani kwetu. Alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilisikiliza aliyosema na kukubali dokezo la kutembelewa tena. Wanaume wawili walikuja kuniona. Nilikumbuka mambo mawili kutokana na mazungumzo yetu—Paradiso na Ufalme wa Mungu. Nilizingatia mambo hayo, na kadiri miezi ilivyopita, nilielewa kwamba siku moja ingenibidi kupatanisha maisha yangu na viwango vya Mungu ikiwa nilitaka kuwa na dhamiri safi na kupata furaha ya kweli.

Mwanzoni, mwandamani wangu alikubali tuoane ili kupatanisha maisha yetu na Neno la Mungu. Kisha akaanza kushirikiana na watu waliomdharau Mungu na sheria zake. Nilishtuka sana niliporudi nyumbani jioni moja wakati wa masika. Nyumba yetu ilikuwa haina mtu. Mwandamani wangu alikuwa ameondoka na kumchukua binti yetu mwenye umri wa miaka mitatu. Niliwangoja warudi kwa siku nyingi—lakini hawakurudi. Badala ya kumlaumu Mungu, nilisali ili anisaidie.

Muda mfupi baadaye, nilichukua Biblia, nikaketi chini ya mtini wangu, nikaanza kusoma. Kwa kweli, niliisoma kwa bidii. Ingawa nilikuwa nimesoma vitabu vya aina nyingi vilivyoandikwa na matabibu-nafsia na wanasaikolojia, sikuwa nimewahi kuona hekima kama hiyo. Ni lazima kitabu hicho kiwe kilipuliziwa na Mungu. Nilishangazwa na mafundisho ya Yesu na uelewevu wake wa asili ya kibinadamu. Zaburi zilinifariji, nayo hekima yenye kutumika ya Mithali ikanishangaza. Niling’amua upesi kwamba, ingawa elimu ya uumbaji ni bora kabisa ili mtu aweze kumkaribia Mungu, hiyo yaweza tu kufunua ‘viunga vya njia zake.’—Ayubu 26:14.

Mashahidi hao walikuwa pia wameniachia vitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele na Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha.a Nilifahamu mambo mengi kwa kuvisoma. Kitabu Kweli kilinisaidia kuelewa ni kwa nini mwanadamu anakabili uchafuzi wenye kuenea sana, vita, jeuri yenye kuongezeka, na tisho la mwanadamu kuangamizwa kwa silaha za nyuklia. Na kama vile anga jekundu nililoona nikiwa katika bustani yangu lilivyoashiria halihewa nzuri siku iliyofuata, ndivyo matukio hayo yanavyothibitisha kwamba Ufalme wa Mungu uko karibu. Kwa habari ya kitabu Maisha ya Familia, nilitamani kwamba ningeweza kumwonyesha mwandamani wangu na kumwambia kwamba tungeweza kuwa wenye furaha kwa kutumia shauri la Biblia. Lakini haikuwezekana kufanya hivyo.

Kufanya Maendeleo ya Kiroho

Nilitaka kujua zaidi, hivyo nikamwomba Robert, ambaye ni Shahidi, anitembelee. Alishangaa nilipomwambia kwamba nilitaka kubatizwa, hivyo funzo la Biblia likaanzishwa. Nilianza mara moja kuzungumza na wengine juu ya yale niliyokuwa nikijifunza na kuanza pia kugawa vichapo nilivyopata kwenye Jumba la Ufalme.

Ili kujiruzuku, nilijiandikisha katika kozi ya uashi. Nikifahamu manufaa ambazo mtu aweza kupata kutokana na Neno la Mungu, nilitumia kila fursa kuwahubiria kivivi hivi wanafunzi wenzangu na walimu. Jioni moja, nilikutana na Serge ushorobani. Alikuwa na magazeti fulani mikononi mwake. “Ninaona kwamba unapenda kusoma,” nikamwambia. “Ndiyo, lakini nimechoka kusoma haya.” Je, unataka kitu ambacho kwa kweli ni kizuri kusoma?” Nikamwuliza. Tulikuwa na mazungumzo mazuri sana juu ya Ufalme wa Mungu, kisha akakubali fasihi ya Biblia. Juma lililofuata, aliandamana nami kwenda kwenye Jumba la Ufalme, kisha funzo la Biblia likaanzishwa.

Siku moja nilimwuliza Robert ikiwa ningeweza kuhubiri nyumba hadi nyumba. Alienda kwenye kabati yake ya nguo na kunitolea suti. Jumapili iliyofuata, nilishiriki mara ya kwanza katika huduma pamoja naye. Hatimaye, Machi 7, 1981, nilionyesha hadharani wakfu wangu kwa Yehova Mungu kwa kubatizwa.

Msaada Nikiwa Katika Taabu

Wakati huohuo nilikuwa nimegundua mahali Amandine na mama yake walikuwa wakiishi ng’ambo. Lo, mama yake—kihalali kabisa, kulingana na sheria za nchi alimokuwa akiishi—alinikataza nisimwone binti yangu. Nikakata tamaa. Mama ya Amandine aliolewa, na hali yangu ya kukata tamaa ikawa mbaya hata zaidi nilipopata taarifa rasmi kwamba mume wake alikuwa amemwasilisha binti yangu—bila hata kibali changu. Sikuwa na haki zozote tena kwa habari ya mtoto wangu. Licha ya kuchukua hatua ya kisheria, sikuweza kupata haki ya kumtembelea. Nilihisi kana kwamba nilikuwa nikibeba kilogramu 50 mgongoni mwangu, nilihuzunika sana.

Lakini Neno la Yehova lilinitegemeza katika njia kadhaa. Siku moja nilipokuwa nimehuzunika kabisa, nilirudia tena na tena maneno ya Mithali 24:10: “Ukizimia siku ya taabu, nguvu zako ni chache.” Mstari huo ulinisaidia nisikate tamaa kabisa. Pindi nyingine, baada ya jitihada zangu za kumwona binti yangu zilipokosa kufaulu, nilienda katika huduma huku nikishika kwa nguvu zangu zote kipete cha mfuko wangu wa vitabu. Katika nyakati hizo ngumu, nilipata kujua ukweli wa andiko la Zaburi 126:6, linalosema: “Ingawa mtu anakwenda zake akilia, azichukuapo mbegu za kupanda. Hakika atarudi kwa kelele za furaha, aichukuapo miganda yake.” Somo muhimu nililojifunza ni kwamba unapopatwa na majaribu makali, maadamu umefanya yote uwezayo kuyatatua, inakupasa uyasahau na kusonga mbele kwa bidii katika utumishi wa Yehova. Hiyo ndiyo njia pekee ya kudumisha shangwe yako.

Kujitahidi Kupata Kitu Kilicho Bora Zaidi

Walipoona mabadiliko niliyokuwa nimefanya, wazazi wangu wapendwa walijitolea kunisaidia kuendelea na masomo yangu kwenye chuo kikuu. Niliwashukuru, lakini sasa nilikuwa na mradi mwingine. Kweli ilikuwa imeniweka huru na falsafa, mafumbo, na unajimu wa kibinadamu. Sasa nilikuwa na rafiki wa kweli ambao hawangeweza kamwe kuuana vitani. Mwishowe nilipata jibu kwa swali langu juu ya ni kwa nini kuna kuteseka kwingi duniani. Kwa kumshukuru, nilitaka kumtumikia Mungu kwa nguvu zangu zote. Yesu alikuwa amejitoa kabisa katika huduma yake, nami nilitaka kufuata kielelezo chake.

Katika mwaka wa 1983, niliacha biashara yangu ya uashi, nikawa mhudumu wa wakati wote. Sala zangu zilijibiwa kwa kupata kazi isiyo ya wakati wote ili kujitegemeza. Ilikuwa shangwe iliyoje kuhudhuria shule ya mapainia pamoja na Serge, yule mwanamume kijana ambaye nilimtolea ushahidi katika shule ya uashi! Baada ya miaka mitatu nikiwa painia wa kawaida, nilitamani kumtumikia Yehova hata zaidi. Hivyo, katika mwaka wa 1986, niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee katika mji wenye kupendeza wa Provins, karibu na Paris. Mara nyingi, niliporudi nyumbani jioni, nilipiga magoti kumshukuru Yehova kwa siku nzuri sana niliyokuwa nimetumia nikizungumza na wengine kumhusu. Kwa kweli, mambo mawili ambayo mimi hupendezwa nayo zaidi maishani ni kuzungumza na Mungu na kuzungumza na wengine kumhusu.

Jambo jingine lililonifurahisha zaidi ni ubatizo wa mama yangu mwenye umri wa miaka 68 ambaye aliishi Cébazan, kijiji kidogo kilichoko kusini mwa Ufaransa. Mama yangu alipoanza kusoma Biblia, nilimpelekea maandikisho ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Alikuwa mtu mwenye kusababu, na upesi sana akaitambua kweli katika yale aliyosoma.

Betheli—Paradiso ya Kiroho Yenye Kutokeza

Wakati Watch Tower Society ilipoamua kupunguza idadi ya mapainia wa pekee, nilipeleka maombi ya kujiunga na Shule ya Mazoezi ya Kihuduma na pia Betheli, yaani, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa. Nilitaka Yehova aamue jinsi ambavyo ningeweza kumtumikia vyema zaidi. Miezi michache baadaye, Desemba 1989, nilialikwa Betheli ya Louviers, kaskazini-magharibi mwa Ufaransa. Hayo yalithibitika kuwa matokeo bora kabisa, kwa kuwa mahali hapo paliniwezesha kusaidia ndugu yangu na shemeji yangu kuwatunza wazazi wangu walipokuwa wagonjwa sana. Nisingeliweza kufanya hivyo kama ningelikuwa umbali wa maelfu ya kilometa katika utumishi wa mishonari.

Mama yangu alikuja kunitembelea Betheli mara kadhaa. Ingawa ilikuwa ni kujinyima kuishi mbali nami, mara nyingi aliniambia hivi: “Kaa Betheli, Mwanangu. Ninafurahi unamtumikia Yehova kwa njia hiyo.” Kwa kusikitisha, wazazi wangu sasa wamekufa. Ninatazamia kwa hamu kama nini kuwaona katika dunia iliyobadilishwa kuwa paradiso halisi!

Ninaamini kwelikweli kwamba Betheli, yaani, “Nyumba ya Mungu,” ndiyo pekee inayostahili kufafanuliwa kuwa “Paradiso Sasa” kwa kuwa, zaidi ya yote, paradiso halisi ni ya kiroho, na hali ya kiroho iko juu Betheli. Tuna fursa ya kusitawisha matunda ya roho. (Wagalatia 5:22, 23) Chakula kingi cha kiroho ambacho sisi hupata wakati wa mazungumzo ya andiko la Biblia la kila siku na pia funzo la Mnara wa Mlinzi la familia ya Betheli, husaidia kuniimarisha kwa ajili ya utumishi wa Betheli. Isitoshe, kuweza kushirikiana na ndugu na dada wenye maoni ya kiroho ambao wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miongo mingi, hufanya Betheli kuwa mahali pa pekee pa kukulia kiroho. Ingawa nimetenganishwa na binti yangu kwa miaka 17 sasa, kwenye Betheli nimekuta vijana wengi wenye bidii, ambao mimi huwaona kuwa watoto wangu, nami hupendezwa na maendeleo yao ya kiroho. Kwa miaka minane iliyopita, nimepata migawo saba tofauti-tofauti. Ingawa mabadiliko haya hayakuwa rahisi siku zote, kuzoezwa huko hunufaisha baadaye.

Nilikuwa nikikuza aina ya maharagwe ambayo huzaa mara mia. Vivyo hivyo, nimepata kujua kwamba unapopanda kitu kibaya, unavuna ubaya mara mia zaidi—wala si mara moja tu. Kujua jambo kupitia tu kupatwa nalo ni kama shule ambapo masomo ni ya gharama kubwa, kusema kitamathali. Ingelikuwa afadhali kama ningelilelewa katika njia za Yehova, kuliko kujiandikisha kwa vyovyote katika shule hiyo. Wana pendeleo lililoje wale vijana ambao wanalelewa na wazazi Wakristo! Bila shaka, ni vema zaidi kupanda kilicho chema katika utumishi wa Yehova na kuvuna amani zaidi na uradhi mara mia zaidi.—Wagalatia 6:7, 8.

Nilipokuwa painia, nyakati nyingine nilikuwa nikipita karibu na lile duka la vitabu vya dini ambalo kwenye ukuta wake tuliandika yale maneno ya shime ya mwasi-mamlaka. Hata niliingia ndani na kuzungumza na mwenye duka hilo juu ya Mungu aliye hai na kusudi lake. Naam, Mungu yu hai! Isitoshe, Yehova, Mungu wa pekee wa kweli, ni Baba mwaminifu, ambaye haachi watoto wake kamwe. (Ufunuo 15:4) Umati kutoka katika mataifa yote na upate kuiona paradiso ya kiroho sasa—na Paradiso itakayorudishwa—kwa kumtumikia na kumsifu Mungu aliye hai, Yehova!

[Maelezo ya Chini]

a Vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa nimechochewa na maajabu ya uumbaji, niliamua moyoni mwangu kuamini katika Mungu (Kulia) Katika utumishi wa Betheli leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki