Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 8/1 uku. 10
  • Lazima Mwe Watakatifu kwa Kuwa Mimi ni Mtakatifu’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Lazima Mwe Watakatifu kwa Kuwa Mimi ni Mtakatifu’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi Israeli Lilivyohusiana na Chanzo cha Utakatifu
  • Sababu Yehova Alilikataa Israeli
  • Mioyo Safi Huongoza Kwenye Ibada Safi
  • Ule Ugumu—Kukabili Udhaifu Wetu Mbalimbali
  • Twaweza Kubakije Tukiwa Watakatifu?
  • Iweni Watakatifu Katika Mwenendo Wenu Wote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • “Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Ni Bwana”
    Mkaribie Yehova
  • Lazima Mwe Watakatifu Kwa Sababu Yehova Ni Mtakatifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • “Lazima Muwe Watakatifu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 8/1 uku. 10

Lazima Mwe Watakatifu kwa Kuwa Mimi ni Mtakatifu’

“Mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi BWANA, Mungu wenu, ni mtakatifu.”—MAMBO YA WALAWI 19:2.

1. Ni baadhi ya watu gani waonwao na ulimwengu kuwa watakatifu?

NYINGI za dini kubwa-kubwa za ulimwengu zina watu ziwaonao kuwa watakatifu. Mother Teresa, aliye maarufu kwa sababu ya kazi yake ya muda mrefu katika India mara nyingi huonwa kuwa mtakatifu kwa sababu ya kujitoa kwake kwa maskini. Papa huitwa “Baba Mtakatifu.” José María Escrivá, mwanzilishi wa ile harakati ya Katoliki ya kisasa, iitwayo Opus Dei, huonwa na Wakatoliki fulani kuwa “kigezo cha utakatifu.” Dini ya Hindu ina maswami, au watu watakatifu wayo. Gandhi alistahiwa sana kuwa mtu mtakatifu. Dini ya Buddha ina watawa wayo wa kiume, na Uislamu una nabii wao mtakatifu. Lakini kuwa mtakatifu humaanisha nini hasa?

2, 3. (a) Maneno “-takatifu” na “utakatifu” yamaanisha nini? (b) Ni baadhi ya maswali gani yahitajiyo kujibiwa?

2 Neno “-takatifu” limefasiliwa kuwa “1. . . . -enye kushirikiana na nguvu za kimungu; -takatifu. 2. -enye kuhusianishwa na au -enye kustahili ibada au kicho . . . 3. Kuishi kulingana na mfumo wa kidini au wa kiroho ulio imara au wa kiadili sana . . . 4. -enye kutajwa hususa au kuwekwa kando kwa ajili ya kusudi la kidini.” Katika muktadha wa Kibiblia, utakatifu humaanisha “usafi au utakato wa kidini; utakatifu.” Kulingana na mabuku ya marejezo ya Biblia Insight on the Scriptures, “[neno] la awali la Kiebrania qoʹdhesh hutoa wazo la kujitenga na, kuwa peke -ake, au utakaso kwa Mungu, . . . hali ya kuwekwa kando kwa ajili ya utumishi wa Mungu.”a

3 Taifa la Israeli liliamuriwa liwe takatifu. Sheria ya Mungu ilitaarifu hivi: “Mimi ni BWANA, Mungu wenu; takaseni nafsi zenu basi; iweni watakatifu, kwa kuwa mimi ni Mtakatifu.” Ni nani aliyekuwa Chanzo cha utakatifu? Waisraeli wasio wakamilifu wangewezaje kuwa watakatifu? Na ni masomo gani tuwezayo kujipatia wenyewe leo katika mwito wa Yehova wa kutaka utakatifu?—Mambo ya Walawi 11:44.

Jinsi Israeli Lilivyohusiana na Chanzo cha Utakatifu

4. Utakatifu wa Yehova ulitolewaje kielelezo katika Israeli?

4 Kila kitu kilichohusiana na ibada ya Israeli kwa Yehova Mungu kilipaswa kuonwa kuwa kitakatifu na kutendewa hivyo. Kwa nini ilikuwa hivyo? Kwa kuwa Yehova mwenyewe ndiye chimbuko na chanzo cha utakatifu. Simulizi la Musa kuhusu matayarisho ya tabenakulo na yale mavazi na mapambo lamalizia kwa maneno: “Wakafanya hilo bamba la hiyo taji takatifu la dhahabu safi, na kuandika juu yake andiko, mfano wa kuchorwa kwa muhuri, MTAKATIFU KWA BWANA.” Hilo bamba la dhahabu safi lilibandikwa kwenye kilemba cha kuhani wa cheo cha juu, nalo lilimaanisha kwamba alikuwa amewekwa kando kwa utumishi wa utakatifu wa pekee. Walipoona maandishi hayo yaliyonakshiwa yakimetameta kwenye jua, Waisraeli walikumbushwa utakatifu wa Yehova kwa ukawaida.—Kutoka 28:36; 29:6; 39:30.

5. Waisraeli wasio wakamilifu wangewezaje kuonwa kuwa watakatifu?

5 Lakini Waisraeli wangewezaje kuwa watakatifu? Ni kupitia tu uhusiano wao wa karibu pamoja na Yehova na ibada yao safi kwake. Walihitaji ujuzi sahihi wa “Aliye Mtakatifu Zaidi Sana” ili wapate kumwabudu katika utakatifu, katika usafi wa kimwili na kiroho. (Mithali 2:1-6; 9:10) Kwa hiyo Waisraeli walipaswa kumwabudu Mungu wakiwa na nia safi na moyo safi. Aina yoyote ya ibada yenye unafiki ingemchukiza Yehova.—Mithali 21:27.

Sababu Yehova Alilikataa Israeli

6. Wayahudi katika siku ya Malaki waliitendeaje meza ya Yehova?

6 Chuki hiyo ilitolewa kielezi kwa wazi Waisraeli walipokuwa wakileta hekaluni kwa mioyo nusu-nusu dhabihu duni, zenye kasoro. Kupitia nabii wake Malaki, Yehova alishutumu matoleo yao hafifu: “Sina furaha kwenu, asema BWANA wa majeshi, wala sitakubali dhabihu yo yote mikononi mwenu. . . . Lakini ninyi mnalitia unajisi, kwa kuwa mwasema, Meza ya BWANA imetiwa unajisi; na matunda yake, yaani, nyama yake, hudharauliwa. Tena mwasema, Tazama, jambo hili linatuchokesha namna gani! nanyi mmelidharau, asema BWANA wa majeshi; nanyi mmeleta kitu kilichopatikana kwa udhalimu, na kilema, na kilicho kigonjwa; ndivyo mnavyoleta sadaka; je! niikubali hii mikononi mwenu? asema BWANA.”—Malaki 1:10, 12, 13.

7. Ni matendo gani yasiyo matakatifu ambayo Wayahudi walikuwa wakifanya katika karne ya tano K.W.K.?

7 Malaki alitumiwa na Mungu ili kushutumu mazoea yasiyo ya kweli ya Wayahudi, yaelekea katika karne ya tano K.W.K. Makuhani walikuwa wakiweka kielelezo kibaya, na mwenendo wao haukuwa mtakatifu kwa vyovyote. Watu, waliokuwa wakifuata mwongozo huo, hawakushika kanuni za kimungu, hata kufikia hatua ya kutaliki wake zao, labda ili waweze kuoa wake wachanga zaidi wapagani. Malaki aliandika: “BWANA amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana,b angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako. . . . Kwa hiyo jihadharini roho zenu; mtu awaye yote asimtende mke wa ujana wake mambo ya hiana. Maana mimi nakuchukia kuachana, asema BWANA.”—Malaki 2:14-16.

8. Watu fulani katika kutaniko la Kikristo wameathiriwaje na maoni ya kisasa juu ya talaka?

8 Katika nyakati za kisasa, katika nchi nyingi ambako talaka hupatikana kwa urahisi, kiwango cha talaka kimepanda upesi. Hata kutaniko la Kikristo limeathiriwa. Badala ya kutafuta msaada wa wazee ili kushinda vizuizi na kujaribu kufanya ndoa yao ifanikiwe, watu fulani wamewataliki wenzi wao upesi sana. Mara nyingi watoto huachwa wakiwa wameathiriwa sana kihisia-moyo.—Mathayo 19:8, 9.

9, 10. Tufikirieje kumwabudu kwetu Yehova?

9 Kama tulivyoona awali, kwa sababu ya ile hali mbaya ya kiroho katika siku ya Malaki, Yehova alilaumu waziwazi ibada ya kijuujuu ya Yuda naye akaonyesha kwamba angekubali ibada safi pekee. Je, hilo halipaswi kutufanya tufikirie ubora wa ibada yetu kwa Yehova Mungu, Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima, Chanzo cha utakatifu wa kweli? Je, kwa kweli twamtolea Mungu utumishi mtakatifu? Je, tunajiweka wenyewe katika hali iliyo safi kiroho?

10 Hilo halimaanishi kwamba twapaswa kuwa wakamilifu, jambo ambalo haliwezekani, au kwamba twapaswa kujilinganisha na wengine. Lakini hilo humaanisha kwamba kila Mkristo apaswa kuwa akimtolea Mungu ibada iliyo bora zaidi kulingana na hali zake. Hilo hurejezea ubora wa ibada yetu. Utumishi wetu mtakatifu wapaswa kuwa ulio bora zaidi—utumishi mtakatifu. Hilo hutimizwaje?—Luka 16:10; Wagalatia 6:3, 4.

Mioyo Safi Huongoza Kwenye Ibada Safi

11, 12. Mwenendo usio mtakatifu huanzia wapi?

11 Yesu alifundisha waziwazi kwamba yaliyomo moyoni yatadhihirika kwa yale mtu asemayo na atendayo. Yesu aliwaambia hivi Mafarisayo wenye kujihesabia uadilifu, na hata hivyo wasio watakatifu: “Enyi wazao wa nyoka, mwawezaje kunena mema, mkiwa wabaya? Maana, kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.” Baadaye alionyesha kwamba matendo maovu hutokana na mawazo maovu yaliyo moyoni, au katika mtu wa ndani. Yeye alisema hivi: “Vitokavyo kinywani vyatoka moyoni; navyo ndivyo vimtiavyo mtu unajisi. Kwa maana moyoni hutoka mawazo mabaya, uuaji, uzinzi, uasherati; wivi, ushuhuda wa uongo, na matukano; hayo ndiyo yamtiayo mtu unajisi.”—Mathayo 12:34; 15:18-20.

12 Hilo hutusaidia kuelewa kwamba matendo yasiyo matakatifu hayajitokezi ghafula tu wala kuwa bila msingi. Hayo ni matokeo ya mawazo yenye kutia unajisi ambayo yamekuwa yakijificha moyoni—tamaa za siri na labda hata mawazo tu. Hiyo ndiyo sababu Yesu alisema: “Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.” Yaani, uasherati na uzinzi tayari umetia mizizi moyoni kabla ya hatua yoyote kuchukuliwa. Kisha, fursa ikijitokeza katika hali fulani, yale mawazo yasiyo matakatifu yanakuwa mwenendo usio matakatifu. Mienendo kama uasherati, uzinzi, usodoma, wivi, makufuru, na uasi-imani inakuwa baadhi ya matokeo yenye kuonekana.—Mathayo 5:27, 28; Wagalatia 5:19-21.

13. Ni vipi baadhi ya vielelezo vya jinsi mawazo yasiyo matakatifu yawezavyo kuongoza kwenye matendo yasiyo matakatifu?

13 Hilo laweza kutolewa kielezi katika njia mbalimbali. Katika nchi fulani, vilinge vinaongezeka upesi sana, kwa njia hiyo vikiongeza fursa za kucheza kamari. Huenda mtu akashawishwa kujaribu kutatua matatizo yake ya kifedha kwa njia ionekanayo kuwa ndilo suluhisho. Kuwazawaza kwa njia ya udanganyifu kwaweza kumchochea ndugu akatae au apunguze uzito wa kanuni zake za Biblia.c Katika kisa kingine, ponografia ipatikanayo kwa urahisi iwe ni kupitia televisheni, video, kompyuta, au vitabu, yaweza kumwongoza Mkristo kwenye mwenendo usio mtakatifu. Anachohitaji kufanya tu ni kupuuza silaha zake za kiroho, na upesi ametumbukia ndani ya ukosefu wa adili. Lakini katika visa vingi ule mteremko kuelekea dhambi huanzia akilini. Ndiyo, katika visa hivyo, maneno ya Yakobo yanatimizwa: “Kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.”—Yakobo 1:14, 15; Waefeso 6:11-18.

14. Watu wengi wamerudiaje hali nzuri kutoka mwenendo wao usio mtakatifu?

14 Kwa furaha, Wakristo wengi wanaotenda dhambi katika udhaifu huonyesha toba ya kweli, na wazee wanaweza kurudisha hali yao nzuri ya kiroho. Hata wengi wanaotengwa kwa sababu ya kukosa toba hatimaye wanapata fahamu nao wanarudishwa tena kutanikoni. Wanapata kutambua jinsi Shetani alivyowashinda kwa urahisi waliporuhusu mawazo yasiyo matakatifu yatie mizizi moyoni.—Wagalatia 6:1; 2 Timotheo 2:24-26; 1 Petro 5:8, 9.

Ule Ugumu—Kukabili Udhaifu Wetu Mbalimbali

15. (a) Kwa nini ni lazima tukabili udhaifu wetu mbalimbali? (b) Ni nini kiwezacho kutusaidia kukiri udhaifu wetu mbalimbali?

15 Ni lazima tujitahidi kuujua moyo wetu wenyewe kwa unyoofu. Je, tuko tayari kukabili udhaifu wetu mbalimbali, kuukiri, kisha kufanya bidii ili kuushinda? Je, tuko tayari kuuliza rafiki mwenye haki jinsi tuwezavyo kufanya maendeleo, kisha kusikiliza shauri? Ili kubaki tukiwa watakatifu ni lazima tushinde mapungufu yetu. Kwa nini? Kwa kuwa Shetani aujua udhaifu wetu mbalimbali. Atatumia ufundi wake wenye hila ili kutuchochea tutende dhambi na kuwa na mwenendo usio mtakatifu. Kwa matendo yake ya ufundi, yeye hujaribu kututenganisha na upendo wa Mungu ili tusiwe tena wenye kutakaswa na wenye kustahili kumwabudu Yehova.—Yeremia 17:9; Waefeso 6:11; Yakobo 1:19.

16. Paulo alikuwa na pambano gani?

16 Mtume Paulo alikuwa na majaribu na mitihani yake mwenyewe, kama alivyoshuhudia katika barua yake kwa Waroma: “Najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema; kwa kuwa kutaka nataka, bali kutenda lililo jema sipati. Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. . . . Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani, lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.”—Warumi 7:18-23.

17. Paulo alishindaje vita yake dhidi ya udhaifu mbalimbali?

17 Sasa hoja ya maana katika kisa cha Paulo ni kwamba alikiri udhaifu wake mbalimbali. Licha yao, aliweza kusema: “Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu [mtu wa kiroho] wa ndani.” Paulo alipenda lililokuwa jema na kuchukia lililokuwa ovu. Lakini bado alikuwa na mashindano ya kukabiliana nayo, mashindano yaleyale ambayo sisi sote tunayo—dhidi ya Shetani, ulimwengu, na mwili. Kwa hiyo twaweza kushindaje ile vita ya kubaki tukiwa watakatifu, tukiwa tumejitenga na ulimwengu huu na kufikiri kwao?—2 Wakorintho 4:4; Waefeso 6:12.

Twaweza Kubakije Tukiwa Watakatifu?

18. Twaweza kubakije tukiwa watakatifu?

18 Utakatifu haupatikani kwa kufuata mwendo wa starehe au kwa kufurahia anasa za kibinafsi. Mtu wa aina hiyo sikuzote atatoa udhuru kwa ajili ya mwenendo wake na kujaribu kuweka lawama kwingineko. Huenda twahitaji kujifunza kuwa wenye kuchukua madaraka kwa ajili ya matendo yetu na kutokuwa kama wengine wanaodai kwamba wanafanya mambo kwa sababu ya malezi na tabia za urithi. Mizizi ya jambo hilo imo katika moyo wa mtu mmoja-mmoja. Je, yeye anapenda uadilifu? anatamani utakatifu? na kutamani baraka ya Mungu? Mtunga-zaburi alieleza wazi uhitaji wa utakatifu aliposema hivi: “Uache mabaya ukatende mema, utafute amani ukaifuatie.” Mtume Paulo aliandika hivi: “Pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema.”—Zaburi 34:14; 97:10; Warumi 12:9.

19, 20. (a) Twaweza kujengaje akili yetu? (b) Funzo la kibinafsi lenye matokeo lahusisha nini?

19 Twaweza ‘kuambatana na lililo jema’ tukiyaona mambo jinsi Yehova huyaona na tukiwa na akili ya Kristo. (1 Wakorintho 2:16) Hilo hutimizwaje? Kwa funzo la kawaida na kutafakari juu ya Neno la Mungu. Shauri hilo limetolewa mara nyingi kama nini! Lakini je, sisi twalichukua kwa uzito vya kutosha? Kwa kielelezo, je, wewe hujifunza gazeti hili kwelikweli, ukichunguza maandiko ya Biblia, kabla ya kuja mikutanoni? Tusemapo kujifunza hatumaanishi kupiga mistari tu mafungu machache ya maneno katika kila fungu. Makala ya funzo yaweza kupitiwa na kupigwa mistari kwa dakika 15 hivi. Je, hilo lamaanisha kwamba tumejifunza makala hiyo? Kwa kweli, huenda ikachukua muda wa saa moja au mbili kujifunza na kupata manufaa ya kiroho ambayo kila makala hutoa.

20 Labda twahitaji kujitia nidhamu ili kuondoka kwenye televisheni kwa saa chache kila juma na kukazia fikira kwelikweli utakatifu wetu wa kibinafsi. Funzo letu la kawaida hutujenga kiroho, likiitendesha akili ili ifanye maamuzi yanayofaa—maamuzi yaongozayo kwenye “mwenendo mtakatifu.”—2 Petro 3:11; Waefeso 4:23; 5:15, 16.

21. Ni swali gani linalobaki kujibiwa?

21 Swali sasa ni, Ni katika nyanja gani nyingine za utendaji na mwenendo tuwezazo kuwa watakatifu tukiwa Wakristo, kama Yehova alivyo mtakatifu? Makala ifuatayo itatoa habari istahiliyo kuchunguzwa kwa uangalifu.

[Maelezo ya Chini]

a Mabuku hayo mawili ya marejezo yanatangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Ili kupata mazungumzo kamili zaidi juu ya kinachomaanishwa na “kwa hiana,” ona Amkeni! la Februari 8, 1994, ukurasa 21, “Mungu Huchukia Talaka ya Aina Gani?”

c Ili kupata habari zaidi juu ya kwa nini kucheza kamari ni mwenendo usio mtakatifu, ona Amkeni! la Agosti 8, 1994, kurasa 14-15, lililotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

Je, Wakumbuka?

◻ Chanzo cha utakatifu kilitambulishwaje katika Israeli?

◻ Katika siku ya Malaki ibada ya Israeli ilikuwa isiyo takatifu katika njia zipi?

◻ Mwenendo usio mtakatifu huanzia wapi?

◻ Ili tuwe watakatifu, ni lazima tutambue nini?

◻ Twaweza kubakije tukiwa watakatifu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki