Lazima Mwe Watakatifu Kwa Sababu Yehova Ni Mtakatifu
“Iweni Watakatifu katika Mwenendo Wenu Wote.”—1 Pet. 1:15.
1. Huenda ukawa na mawazo gani unaposikia neno “-takatifu”?
UNAPOSIKIA mtu akilitaja neno “-takatifu,” wafikiria nini? Je! wadhani kwamba huwezi kuwa ‘“mtakatifu,” kwamba hiyo ni sifa usiyoweza kufikia? Au wadhani mtu “mtakatifu” ni kama yule anayeonyeshwa na Jumuiya ya Wakristo au waabudu wa miungu ya kishenzi, yaani, mtu mwenye kujionyesha kuwa mtawa, mwenye kuvaa vazi la pekee, mwenye kujionyesha kuwa mtakatifu kuliko watu wengine? Ikiwa hayo ndiyo yanayokuwa maoni yako neno “-takatifu” linapotajwa, basi yakupasa ufahamu Biblia humaanisha nini kwa kutumia neno hilo.
2. Maneno ya Kiebrania na Kigiriki ya “-takatifu” na “utakatifu” huwa na maana gani?
2 Maneno “-takatifu” na “utakatifu” yaliyomo katika Biblia yametafsiriwa kutokana na maneno ya Kiebrania yanayoelekea kuwa na maana ya asili ya “kuwa safi,” “kuwa -pya, -sio na taka.” Yanaweza kutumika kwa njia ya kimwili, lakini hasa yanatumika kwa njia ya kiroho au ya adili. Hivyo, maneno hayo yanahusu usafi wa adili hasa, kutakata kwa adili. Vilevile maneno hayo ya Kiebrania yamaanisha hali ya kujitenga, isiyohusu mambo mengine, au hali ya kutakaswa kwa matumizi ya Mungu. Katika Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki, maneno hayo mawili yamaanisha pia hali ya kujitenga kwa ajili ya matumizi ya Mungu, nayo yanahusu kutakata au kukamilika kwa mwenendo wa mtu bi nafsi.
3. Ni shauri gani linalohusu mambo mawili ambalo Petro alitoa katika 1 Petro 1:14-16, na ni nini kitakachotuongoza tuyatii maneno hayo?
3 Tunapokumbuka maana ya maneno hayo, twaweza kufahamu sababu ya mtume Petro kutoa shauri lililoandikwa katika 1 Petro 1:14-16: “Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza, za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.” Je! umeona kwamba agizo alilotoa Petro lahusu mambo mawili? Kwanza, alitaja ‘kutojifananisha na tamaa zenu za kwanza,’ na pili, Petro ataja kwamba lazima tuwe “watakatifu.” Ni nini kitakachotuongoza tutii amri hiyo inayohusu mambo hayo mawili? Sababu kubwa ya kutaka kuwa “watakatifu” ni kwamba Yehova ni “mtakatifu.” Ni kama vile Petro alivyosema: “Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”
KUPATA UTAKATIFU
4. Utakatifu hupatikanaje, nayo kweli yasaidiaje?
4 Kwa kuwa hii ni sifa ya Mungu, nasi tu watu wasiokamilika, tutaupataje utakatifu? Andiko la Petro wa Kwanza 1:14, lililotajwa juu, laeleza kwamba lazima tuonyeshe utii kama wa watoto, kisha mstari wa 22 wasema hivi: “Mkiisha kujitakasa [nafsi] zenu kwa kuitii kweli.” Basi, ni wazi kwamba lazima tuonyeshe ‘utii kama wa watoto’ juu ya kweli, inayopatikana katika Neno la Mungu, ili tuupate utakatifu. Yesu alijua vile “kweli” inavyosaidia kupata uhusiano mtakatifu na Mungu kwa maana asema hivi katika Yohana 17:17: “Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli.” Kwa hiyo, mtu ‘husafishwa,’ ‘hutakaswa’ na ‘hutengwa’ kwa ajili ya matumizi ya Mungu kwa kuitii kweli na kuiacha itende kazi maishani mwake.
5. (a) Tukikosa kutii kweli tutakuwa tukifanya nini, nasi tuna mifano gani miwili juu ya jambo hilo? (b) Eleza maana ya dhambi, na vile tunavyoweza kuepuka kufanya dhambi juu ya Mungu.
5 Lazima tufahamu kwamba tunapoitii kweli tunamtii Muumba wetu. Tunapokosa kuitii kweli, kwa kurudia njia na tamaa chafu za zamani, tunafanya dhambi juu ya Yehova mwenyewe. Daudi aliona hivyo alipofikiria uzinzi aliofanya na Bathsheba. Baada ya kutubu, alisema maneno haya yenye mkazo: “Nimekutenda dhambi Wewe [Yehova] peke yako, na kufanya maovu mbele za macho yako.” (Zab. 51:4) Mwana mpotevu alisema vivyo hivyo alipoacha kufuata mwendo wa umalaya, usio mtakatifu. Alinena hivi: “Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako.” (Luka 15:18) Kwa kuwa dhambi yaelezwa kuwa ni kukosa kufanya jambo la adili, kukosa shabaha ya ukamilifu, yamfanya Mkristo awe mchafu, mwenye taka, asiye safi kiroho na kwa adili. Kwa hiyo, lazima Mkristo ajitahidi aendelee kuwa mwaminifu na mtiifu kwa kweli badala ya kutokutii na kutenda dhambi juu ya Yehova, ili aonyeshe anathamini yote ambayo amemfanyia.
6. Kwa kuwa Waisraeli walipaswa kuwa watakatifu, je! utakatifu ulihusu matendo ya kidini tu? Kwa sababu gani sivyo?
6 Karne zote, Yehova ametaka watu wake wawe watakatifu, waendelee kuwa kama yeye hatua kwa hatua. Ili tulifahamu jambo hilo vizuri zaidi, acheni tuangalie kwa ufupi matendo ya Mungu pamoja na watu wake chini ya sheria ya Musa. Aliliambia hivi taifa hilo la Kiyahudi: “Mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi [Yehova], Mungu wenu, ni mtakatifu.” (Law. 19:2) Sasa, ni pande gani za matendo ya wanadamu ambazo Yehova alikuwa akizungumza hapa? Je! alikuwa akitaja matendo ya kidini tu? Sivyo. Maneno yanayofuata ile mistari 35 inayobaki katika sura hiyo, yaonyesha kwamba Mungu alikuwa akimaanisha kila upande wa maisha ya Wayahudi. Mambo kama wivi, kutopendelea katika hukumu, matumizi ya mizani na vipimo, namna ya kutenda juu ya vizuizi kama uziwi na upofu, na hata mambo ya ngono yanatajwa waziwazi. Kwa hiyo, utakatifu ulipaswa kuonyeshwa katika matendo yote ya maisha. Kwa kushikamana na kanuni za Mungu za utakatifu wakati huo, taifa hilo lingeweza kuwa watu “watakatifu,” au safi, waliotengwa na mataifa ya kilimwengu kama watu waliojitoa kwa Yehova peke yake. Sheria za ulaji, za afya na za adili ambazo Mungu aliwapa zilikuwa zikiwakumbusha sikuzote kwamba wamejitenga wakawa watakatifu kwa matumizi Yake.—Law. 22:31, 32.
MAANA YA UTAKATIFU YAELEZWA WAZI
7. (a) Kwa kuwa Waisraeli wangeweza kufanywa “watakatifu” kwa kiasi fulani tu, ilikuwa lazima Mungu afanye nini? (b) Ujumbe wa Yesu ulisaidiaje watu siku zake?
7 Walakini, Waisraeli wangeweza kusafishwa na kutengwa na ulimwengu wa kale na kufanywa “watakatifu” kwa kiasi fulani tu. Ndiyo sababu ilikuwa lazima Mungu amtume Yesu duniani, afunulie wanadamu habari zilizomhusu Baba yake na sifa Zake za ajabu, za haki, usafi na utakatifu. Mafundisho ya Yesu Kristo yangeweza kufanya watu wenye kuitikia wawe watakatifu hata zaidi kuliko wale waliokuwa chini ya Torati. Mafundisho yake yalifikia mioyo ya wenye kutaka kutii ujumbe wa Mungu. Yangeweza kuwasaidia wajipatanishe zaidi na Yehova. Wangeweza kumjua Mungu zaidi kuliko wale walioishi kabla ya Yesu kuja duniani.—Yohana 1:18.
8. Baada ya kuitaja Torati, Yesu alitoaje maelezo zaidi, na ni mifano gani miwili inayoonyesha hivyo?
8 Yesu alipokuwa akifanya utumishi wake aliopewa na Mungu aliitaja Torati mara nyingi kisha akaieleza wazi zaidi. Kwa njia gani? Alizungumza juu ya makusudi na sababu za kufanya mambo. Yesu alitaka kujua yaliyokuwa ndani ya moyo wa mtu. Alionyesha hivyo wakati mmoja alipokuwa akisema habari za Torati na uuaji na uzinzi. Alieleza hivi: “Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue; na mtu akiua, itampasa hukumu. Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanum ya moto.” (Mt. 5:21, 22) Baadaye, wakati Yesu alipokuwa akisema habari ya uzinzi, alieleza hivi: “Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.”—Mt. 5:27, 28.
9. (a) Onyesha tofauti kati ya Torati na Ukristo. (b) Yesu alikazia nini katika mafundisho yake?
9 Katika mifano hiyo miwili, twaweza kuona vile mafundisho ya Kristo yalivyo bora kuliko yale ya Torati juu ya kufanya mtu awe mtakatifu. Chini ya Torati matendo halisi ya uuaji na uzinzi ndiyo yaliyomfanya Mwisraeli ahukumiwe kufa. Lakini kwa habari ya Mkristo, hata mawazo na makusudi yake yangeweza kumfanya ahukumiwe na Yehova. Ilimpasa kuwa na moyo safi. (Marko 7:18-23) Mkristo asingeweza kusitawisha mawazo wala tamaa mbaya akatazamia kuwa na “utakatifu” wenye kuonyesha utukufu wa Yehova. (Flp. 4:8; 2 Kor. 3:18) Kwa hiyo Yesu alikazia kanuni zilizokuwa katika Torati. Alikazia roho ya Torati, ambayo ilikuwa imepuzwa sana na wenye kufundisha Torati.
10. Wafuasi wa Yesu walifaidikaje, naye Petro alisema nini juu ya Wakristo hao waliojitenga?
10 Mitume na wafuasi wengine wa Yesu walithamini shauri hilo kwa kujitahidi kuzitumia kanuni hizo na kufuata roho ya Torati katika maisha zao. Hiyo iliwasaidia wapate “utakatifu” waliotazamiwa kuwa nao. Walipokea “utakatifu” huo kwa kuuamini ubora wenye kulipia dhambi wa dhabihu ya Yesu Kristo. Alipokuwa akieleza kundi la Kikristo lilivyo, Petro aliongozwa kulisema kuwa “taifa takatifu,” taifa ambalo lilikuwa limetengwa kabisa na ulimwengu lipate kumtumikia Mungu wake. (1 Pet. 2:9) Watu hao, ingawa walikuwa wasiokamilika, walikuwa “watakatifu” au safi na wenye kung’aa machoni pa Yehova.
11. Malaki alisema nini juu ya kazi ya kusafisha, nayo kazi hiyo ilianza lini?
11 Kabla Yesu hajaja duniani, Malaki, mtu wa Mungu, alikuwa ametabiri kwamba Yehova angefanya kazi ya kusafisha wakati wa mwisho wa taratibu hii ya mambo. Aliieleza kazi hiyo kwa kusema hivi: “Lakini ni nani atakayestahimili siku ya kuja kwake? au ni nani atakayesimama atakapoonekana yeye? Kwa maana yeye ni mfano wa moto wa mtu asafishaye fedha, ni mfano wa sabuni ya mtu afuaye nguo; naye ataketi kama asafishaye fedha na kuitakasa.” (Mal. 3:2, 3) Orodha ya tarehe na mambo yanayoonekana yakitimiza unabii wa Biblia yaonyesha kwamba kazi hii ya kusafisha imefanywa tangu kipindi kifupi kilichofuata kusimamishwa kwa ufalme wa Mungu mwaka wa 1914. Kama vile Yehova alivyokuwa amesafisha watu wake zamani, ilikuwa lazima asafishe watu wake wa kisasa wenye jina lake hatua kwa hatua, ili awafanye watu watakatifu.
KUSAFISHWA HATUA KWA HATUA
12-16. Kazi ya kusafisha ilipokuwa ikiendelea, kulikuwa na matokeo gani juu ya (a) mafundisho mabaya, (b) uchafu wa adili, na (c) mazoea ya kutumia dawa za kulevya na tumbako?
12 Mengine ya mabadiliko ya polepole ambayo yamefanywa kidogo kidogo na kundi la kisasa la Kikristo ulimwenguni pote pamoja na watu mmoja mmoja waliomo ni nini? Kazi hii ya kusafisha ambayo Malaki alitabiri ni nini? Acheni tuanze kupata jibu letu kwa kurudi nyuma siku za C. T. Russell na J. F. Rutherford, waliofuatana wakiwa wasimamizi wa Watch Tower Society kutoka miaka ya 1880 mpaka ya 1940. Ilikuwa lazima mafundisho mabaya kama moto wa mateso (Mhu. 9:5, 10) na Utatu (Yohana 14:28; 1 Kor. 11:3) yaondolewe mbali. Baadaye, Wakristo wa kweli walitakaswa wakati mwadhimisho wa siku za kuzaliwa ulipoondolewa. (Mhu. 7:1) Halafu ukaja wakati wa Wakristo wa kweli kuonyeshwa lazima ya kujitenga na ulimwengu na mapigano yake, nayo mambo hayo yalielezwa wazi.—Yohana 15:19; 17:16.
13 Miaka iliyofuata Vita ya Ulimwengu ya Pili ufisadi wa ulimwengu uliongezeka kwa njia ya kuogofya. Kulikuwa na uwezekano wa kuchafuliwa kwa tengenezo safi la Mungu. Lakini Yehova alipendezwa na watu wake, kama zamani, na kwa hiyo alitoa habari kupitia kwa njia yake kuzuia uchafu ambao ungetia madoa juu ya watu wake na kuwachafua wasiwe watakatifu. (Mt. 24:45-47) Hasa kuanzia mwaka wa 1946, watu wa Bwana walihangaikia sana usafi wa adili wa mtu bi nafsi. (2 Kor. 7:1) Kuanzia mwaka wa 1952, mpango wa kawaida unaolingana na Maandiko wa kutenga watenda mabaya na ushirika ulianzwa. Wenye kutenda dhambi nzito kama uzinzi na uasherati walifukuzwa kundini, ikiwa hawakutubu. (1 Kor. 5:11-13) Tengenezo la Mungu lisingevumilia watu waliokataa kuwa bila madoa, kuwa safi na wenye kutakata machoni pa Yehova.
14 Miaka ya 1960 matembezi ya wavulana na wasichana yalikuwa ya kawaida na yenye kufuatwa sana na watu wengi ulimwenguni. Wengi ulimwenguni walipenda sana kugusana-gusana na kukumbatiana. Je! vijana wetu walikuwa katika hatari ya kuchafuliwa na kuharibiwa na “mwenendo mpotovu” na mazoea machafu? (Efe. 4:19, NW) Naam, walikuwa hatarini! Kwa hiyo, kwa mara nyingine, Yehova alitumia tengenezo lake kuonyesha kwamba mazoea hayo hayawafai watu “watakatifu.” Uchumba ulionyeshwa kuwa wa watu wazima wanaotaka kuoana. Matembezi ya wavulana na wasichana hayakuwa mchezo, bali jambo zito. Yapaswa yaongoze Wakristo waoane kwa njia ya heshima.—Ebr. 13:4.
15 Miaka ya karibuni, kulalana kwa wanaume na wenzao na wanawake na wenzao kumeenea sana ulimwenguni. Wanaume na wanawake hao wanadai kwamba wanafichua mambo yaliyokuwa yakitendwa kwa siri nao wanajigamba kwa kusema hivi, ‘Sisi twaona fahari kuwa watu wa namna hiyo.’ Ilikuwa wazi kwamba kuharibika kwa kanuni za adili kwa njia hiyo kungeweza kuletea watu watakatifu wa Mungu hatari, kwa hiyo makundi yalionywa na watenda mabaya wakaondolewa mbali. Vilevile, mazoea machafu, kama vile kupiga punyeto (kusugua-sugua viungo vya uzazi ili kuwasha tamaa), ambako kwaweza kuwa hatua moja ya kulalana kwa wanaume na wanaume na wanawake na wanawake, yameshughulikiwa kwa uzito lakini kwa ufahamu, ili kusaidia watu mmoja mmoja waendelee kuwa safi na kutakata machoni pa Yehova. Baadaye, jambo jingine lilipaswa kukaziwa fikira. Mazoea yasiyo ya asili ya ngono katika ndoa kama kutia uume ndani ya mdomo au mkundu wa mwenzi wa ndoa, yamefanya wengine wa watu wa Mungu wawe wachafu machoni pake. Lakini Mnara wa Mlinzi uliondoa matope hayo ya uchafu kwa kuonya waume na wake wafuate mawazo ya Mungu juu ya jambo hilo. Vilevile, uasherati (por·neiʹa, Kigiriki), ulionyeshwa kuwa unatia ndani namna zote za ngono za ufisadi. (1 Kor. 6:9, 10) Habari hizo zilithaminiwa, na wale walioacha mazoea hayo machafu walipatana kabisa na Daudi, aliyemwomba hivi Baba yake wa kimbinguni, “Unitakase na mambo [“dhambi,” NW] ya siri.”—Zab. 19:12.
16 Hivi karibuni, Yehova ameonyesha watu wake “watakatifu” uhitaji wa kutenga na ushirika Wakristo walio wakf na waliobatizwa wanaokataa kuvunja na kuacha mazoea ya kutumia dawa za kulevya na tumbako. Wazo la kwamba tumbako inachafua “mwili na roho” halikuwa jipya. Miaka mingi watu wa Mungu wameonyeshwa vile uvutaji wa sigara ulivyo kinyume cha Maandiko Matakatifu, katika mamia ya mitajo mbalimbali iliyokuwa katika vitabu vya Watch Tower Society. Kwa hiyo wakati ulikuwa umefika watu wa Mungu waondoe wenye kukataa kuona uhitaji wa kujisafisha na kila uchafu wa mwili na roho. Mei 1974, katika United States peke yake, zaidi ya watu 2,000 walikuwa wametengwa na ushirika kwa kukataa kuacha mazoea hayo machafu. Wao hawakuwa ‘wakitimiza utakatifu katika kumcha Mungu,” kama Paulo alivyotia watu moyo wafanye.—2 Kor. 7:1.
17. Mungu amelindaje watu wake kama jamii, na yapasa kila mmoja ajiulize ulizo gani la makini?
17 Ni wazi kutokana na mifano hii na mingine ya kusafisha kwamba Yehova anajitahidi ‘kutimiliza’ watu wake katika utakatifu. Kama vile baba anavyomshika mtoto wake mdogo mkono wanapotembea msituni amsaidie kuepuka mitego na vipingamizi vyo vyote, ndivyo Baba yetu wa kimbinguni ameongoza watu wake miaka yote hiyo. Kila hatua ambayo ametupitisha imekuwa ya lazima. Mambo yalipotokea ambayo yangeweza kututia madoa, Yehova aliyaondoa. Makundi yalipashwa habari na watu wa Mungu wakatayarishwa kwa mabadiliko ya wakati wake kabisa. Kwa hiyo ‘tunasafishwa’ na ‘kutakaswa’ tupate kuwa katika hali bora ya kumwakilisha Mungu kwa njia takatifu zaidi. Walakini, ulizo la makini ni hili, Sisi tunafanya nini kama watu mmoja mmoja? Je! tumefuatana na mabadiliko haya yote makubwa ya hatua kwa hatua? Yampasa kila mmoja wetu achunguze moyo wake apate jibu.
KUENDELEA KUFANYWA WATAKATIFU
18. Kwa sababu gani Yehova anatufahamisha kanuni zake takatifu, naye hufanya nini tunapotenda kosa?
18 Lazima tutambue kwamba kanuni za Mungu za utakatifu hazibadiliki. Sikuzote zimekuwa ndani ya Biblia. Wakati anapotujulisha mambo hayo, anatutaka tuzielewe zaidi kanuni na sheria za Neno lake. Anatutaka tujue mengi zaidi juu ya nia zake ili tuweze kujipatanisha zaidi na utakatifu wake. Tunapofanya kosa na kuanguka, yeye anatusubiri. Yeye ana huruma kwa sababu anaelewa hali zetu, “na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zab. 103:14) Hatutishi kwa kusema atatuondoa kundini kwa sababu ya kila kosa tunalofanya, bali yeye hutupa nafasi ya kuzidi kuthamini njia na sifa zake.
19. Ni kwa njia gani tunaweza kuzikubali fadhili zisizostahilika za Mungu na bado tukose kusudi lake?
19 Lakini sisi hatutaki kuzikubali fadhili zisizostahilika za Mungu kisha tukose, kusudi au sababu ya kuingizwa katika tengenezo safi la Mungu. (2 Kor. 6:1) Hatupaswi kuwa na ubaridi. Si hekima kuona mambo vivi hivi tu. Haitupasi kusimama mahali pamoja tu bila maendeleo. Lazima tuthamini yanayosemwa na Neno lake na yanayofunuliwa na tengenezo lake. Lazima tuthamini habari mpya tunazopokea na kujaribu kwa unyofu wa moyo kuzitumia katika maisha zetu. Tumeingia katika tengenezo safi la Mungu kwa kusudi la kumletea Yeye heshima na sifa. Tusipofanya hivyo, tunalikosa kusudi la kusafishwa na kufanywa “watakatifu.” Kwa kweli, je! tungeweza kutazamia baraka na msaada wa Mungu kwa kulikosa kusudi hilo?
20. (a) Mungu hutawalaje? (b) Kukosa kuitikia uongozi Wake kungeonyesha nini?
20 Mungu hutawala kwa upendo. (1 Yohana 4:16) Yeye ataka tufanye mambo kwa sababu ni ya haki. Huenda wakati fulani ujao tukapatwa na jaribu la kukubali habari fulani ambazo Mungu atatueleza. Huenda habari zenyewe zikapinga jambo tunalopenda kweli kweli. Tutafanya nini? Je! tutasita-sita kufuata mashauri tutakayopewa, pengine tukifikiri sana juu ya uamuzi ambao sisi tunataka kufuata? Tukifanya hivyo, hatutakuwa tukijiuliza wenyewe ulizo hili, ‘Sisi twataka kweli utawala wa Mungu?’ Je! kukataa kuitikia uongozi wa Mungu kupitia kwa tengenezo lake kusingeonyesha kweli kwamba twaukataa utawala wa kimungu?
21. Ni kwa njia gani leo Mungu anafanya watu wake wawe watakatifu zaidi?
21 Tunapopokea kila kitabu kipya kupitia kwa jamii ya “mtumwa” mwaminifu wa Yehova, tuwe “watiwa mafuta” au tuwe kati ya “mkutano mkubwa,” twaona tukielezwa mambo mapya yanayohusu kanuni takatifu za Yehova. Hivyo ndivyo tunavyosafishwa, wala si kwa kuongezewa sababu nyingi zaidi za kutenga watu na ushirika siku zijazo. Tunatakaswa tunapoitii kweli kama alivyosema Petro: “Mkiisha kujitakasa [nafsi] zenu kwa kuitii kweli.” (1 Pet. 1:22) Ni wazi kwamba watu wa Yehova kama jamii wanafanya hivyo, lakini ni lazima mmoja mmoja tuitikie anayotufanyia Yehova wakati huu. Yeye anatufanya “watakatifu” sawa na vile Yeye alivyo “mtakatifu.”
22. Badala ya kujipa udhuru kwa udhaifu wetu, yatupasa tufanye nini?
22 Twataka tuwe na mfano wa Baba yetu wa kimbinguni. Kwa hiyo, lazima tujitahidi kuendelea kuwa safi, hasa ulimwengu huu unapoendelea kuchafuka zaidi. Huu sio wakati wa kujipa udhuru kwa makosa ya kutokamilika tunayofanya. Lazima tujitahidi kufanya maendeleo. Lazima tujitahidi sana tuzidi kuwa kama Yehova. Ikiwa mzigo nyakati nyingine unaelekea kutulemea, yatupasa tufuate ombi la Mungu: “Umtwike [Yehova] mzigo wako naye atakutegemeza.”—Zab. 55:22; 68:19.
23. Ni mambo gani ambayo lazima tufanye sasa ndiyo tupate uzima katika taratibu mpya iliyo takatifu?
23 Ni jambo la maana pia tukaze fikira zetu kwenye Taratibu Mpya iliyo takatifu itakayojawa na watu watakatifu. Yakupasa sikuzote ufikirie wakati ambao wewe utakuwa safi na mtakatifu milele, kimwili, katika akili, kwa adili na kiroho. Walakini, yakupasa ushirikiane SASA na watu safi waliomo katika makundi ya Mungu ndiyo uzipate baraka hizo. Kufanya hivyo kutakuchochea utake kuuiga mfano mwema wao wanapojitahidi kuwa watakatifu. (Ebr. 10:24, 25) Acheni tuendelee kujisafisha sasa kwa kulitii Neno la Mungu la kweli. Tunataka kufuata maongozi ya kundi la Kikristo na kuitikia uongozi wa roho takatifu ambayo Yehova anamimina kutusaidia tuwe na utakatifu wake. Acheni tuonyeshe utakatifu wetu wa kweli kwa kupenda watu wengine bila unafiki na kumwitikia Mungu wetu mtakatifu, Yehova, kwa upendo wenye kuongezeka sikuzote.—Mt. 22:37-40.
24. Tunaweza kuona tukitimiziwa tumaini gani la ajabu, nayo sifa yote yaweza kumwendea nani?
24 Sote tuna tumaini la ajabu leo. Tunaweza kuwa na “utakatifu” ule ambao wengi walidhani usingeweza kupatikana. Litakuwa jambo zuri sana kufikiria sifa bora za Mungu katika umilele wote tukiwa watu “watakatifu” kweli kweli. Sifa na heshima yote yamwendea Yeye! Loo! tutamshukuruje Yehova milele kwa nafasi tuliyopewa ya kuitikia amri yake: “Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu”!—1 Pet. 1:16.
—Kutoka The Watchtower, Feb. 15, 1976.