Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa—United States ya Amerika
BILA shaka tengenezo la Kikristo lenye nguvu lilihitajiwa siku hizo kwa sababu Mashahidi wa Yehova waliteswa vikali sana. Mateso mengi yalianza mwaka wa 1935. Kwa njia gani? Katika kusanyiko la Washington D.C., Jumatatu, Juni 3, Ndugu Rutherford alikubali kujibu ulizo juu ya kusalimu bendera kwa watoto shuleni. Aliwaambia wasikilizaji kwamba kusalimu mfano wa kidunia, kuuhesabu kama wenye kuleta wokovu, kulikuwa ni kutoaminika kwa Mungu. Rutherford alisema kwamba yeye asingefanya hivyo. Alipokuwa akijibu waandishi wa magazeti baadaye, Rutherford alionyesha kwamba ingawa Mashahidi wa Yehova wanaiheshimu bendera, wajibu wao wa Biblia na uhusiano wao kwa Mungu unakataza kabisa wasisalimu mfano wo wote. Hilo lingekuwa tendo la ibada kwa watumishi wa Yehova, lililo kinyume cha kanuni zilizoandikwa katika Amri Kumi. (Kut. 20:4-6) Jibu lake lilionyesha pia kwamba hasa wazazi wa Kikristo ndio wenye daraka la kufundisha watoto wao na kwamba lazima watoto wafundishwe kweli kulingana na ufahamu wa Maandiko Matakatifu ambao wazazi wao wanao.
Ingawa wakuu wengi wa shule na waalimu walikuwa wenye ufahamu, wengine walikuwa washupavu wakafukuza watoto wa Mashahidi wa Yehova shuleni kwa sababu ya kukataa kusalimu bendera.
Mahali pengi Wakristo waliteswa kwa sababu ya msimamo wao unaolingana na Biblia kuhusu kusalimu bendera. Kwa mfano, kundi lenye ghasia la watu pamoja na mapolisi lilishambulia Mashahidi wa Yehova wakati walipokuwa na mkutano wa Biblia Rockville, Maryland, Juni 20, 1940. Baada ya kuingia katika Jumba la Ufalme, kiongozi wa kundi hilo aliinua bendera akasema, “Nawapa ninyi dakika mbili za Kiamerika mwisalimu bendera hii ama sivyo damu itaruka hapa.” Sotir K. Vassil asema hivi: “Kukawa kimya karibu dakika moja, kisha mtu mmoja ambaye hiyo ndiyo iliyokuwa mara yake ya kwanza kuja mkutanoni akaogopa sana akainuka haraka, akaisalimu bendera na kutoka nje . . . Hakuna mwingine aliyeisalimu bendera. Dakika zile mbili zilipokwisha, kiongozi huyo alipiga vitu vyote nilivyokuwa nimeshika akaviangusha kisha akalipa kundi lile lenye ghasia maagizo ya “kuvunja kila kitu,” viti, na kadhalika, halafu vitu vikaanza kurushwa. Wale mapolisi wawili wenye bastola viunoni walikuwa ndani ya jumba nami niliwaendea nikawauliza kama wanaweza kuzuia mambo hayo. Hata hawakufungua midomo yao wala hawakuchukua hatua ya kulikomesha kundi hilo lenye ghasia.” Mambo yalizidi kuharibika. “Wakaanza kutenda kama kundi la mashetani,” asema Ndugu Vassil, wakitusukuma-sukuma nje ya jumba. Wakaendelea kupaza sauti wakisema: ‘Waueni! Waueni! Wao ni Wanazi.’ Watoto wengine waliokuwamo jumbani wakaanza kulia kisha wengine wa kundi hilo lenye ghasia wakapaza sauti kwamba ‘tu-watu huto tutupwe nje dirishani.’ Walituburuta kweli kweli wakitutoa jumbani na kutuelekeza barabarani halafu wakaanza kupiga makelele kusema: ‘Wafukuzeni mjini! Wafukuzeni mjini!’
Mara nyingi watumishi wa Yehova walishambuliwa na makundi ya watu wenye ghasia walipokuwa wakitoa ushuhuda barabarani kwa kutumia The Watchtower na Consolation.
Jumamosi moja karibu Mashahidi kumi na watano walifikiwa na watu fulani. “Tukajua lazima tumtegemee Yehova Mungu na kutumia uamuzi mzuri ndio tuweze kuokoa maisha zetu,” asema Ndugu McKee, kisha aendelea kusema hivi: “Wakatuingilia watatu kati yetu moja kwa moja wakitumia visu na marungu yao. . . . Sisi tuliwaendea madaktari wetu wanne mtaani tukiwa tumevunjika mikono, mafuvu yetu ya vichwa yakiwa yamevunjwa kidogo na tukiwa na madhara mengine, lakini wote walikataa kututibu. Ikatulazimu kwenda mtaa ulioko maili 50 kutoka hapo tukatibiwe na daktari mwenye huruma. Karibuni tukapona majeraha nasi tukarudi kwenye pembe ile ile ya barabara Jumamosi iliyofuata tukiwa na habari njema za Ufalme. Tuliendelea kuwa na roho iyo hiyo nyakati zote za taabu tulipokuwa tukiteswa sana.”
SIKU ZA MWISHO YA BROTHER RUTHERFORD BETH-SARIM
Kufika Novemba wa mwaka wa 1941 ugonjwa wa Ndugu Rutherford ulimzidia akalazimika kupasuliwa katika Elkart, Indiana. Baada ya hapo alisema alitaka kwenda California. Kwa hiyo akapelekwa San Diego mahali panapoitwa “Beth-Sarim.” Kwa kipindi fulani washirika wenzake waliona wazi pamoja na madaktari hodari kwamba asingeweza kupona.
Asubuhi moja karibu na katikati ya Desemba ndugu watatu, kutia na Ndugu Knorr, walifika kutoka Brooklyn. Dada Burford akumbuka hivi: “Walikaa siku kadha naye wakichunguza ripoti ya kila mwaka itakayoandikwa katika Yearbook na mambo mengine yaliyohusu tengenezo. Walipoondoka, Ndugu Rutherford aliendelea kudhoofika na, karibu juma tatu baadaye, Alhamisi, Januari 8, 1942, alimaliza mwendo wake wa kidunia kwa uaminifu akahitimu kuingia katika mapendeleo kamili ya utumishi katika nyua za Baba yake wa kimbinguni.” Alikuwa amekuwa msimamizi wa Watch Tower Society kwa miaka 25. Wakati msimamizi wa Sosaiti wa kwanza, Charles Taze Russell, alipokufa mwaka wa 1916 Wanafunzi wa Biblia walishtuka na wengi hawakujua namna wangeweza kuendelea kumtumikia Mungu. Zaidi ya hilo, watu wenye kufikiria yao tu walijaribu kuongoza Sosaiti wakaleta magumu kwa muda, ingawa upinzani wao na mipango yao Mshindwa kabisa kwa msaada wa kimungu. Walakini, J. F. Rutherford alipokufa mambo hayakuwa hivyo. Bila shaka, adui za watu wa Mungu walidhani kwamba kazi ya Mashahidi wa Yehova ingekoma kabisa, lakini walikuwa wakikosea. “Tengenezo la kitheokrasi lilisonga mbele bila kituo wala kikwazo,” asema Grant Suiter.
Januari 13, 1942, washiriki wote wa baraza ya mashirika ya Pennsylvania na New York yanayotumiwa na watu wa Mungu walikutana pamoja katika Betheli ya Brooklyn. Siku kadha kabla ya hapo, msimamizi mdogo wa Sosaiti, Nathan H. Knorr, alikuwa amewaomba watafute hekima ya kimungu kwa bidii kwa kusali na kutafakari. Walifungua mkutano wao kwa sala ya kuomba uongozi wa Yehova, na baada ya kufikiri kwa uangalifu Ndugu Knorr akatajwa na kuchaguliwa na wote kuwa msimamizi wa Sosaiti.
Nathan Homer Knorr, alizaliwa Bethlehem, Pennsylvania, mwaka wa 1905, na wazazi wazaliwa wa Amerika. Alipokuwa na umri wa miaka kumi na sita, akawa akishirikiana na kundi la Allentown la Wanafunzi wa Biblia, na mwaka wa 1922 akahudhuria kusanyiko la Cedar Point, ambako aliamua kutokuwa tena mshiriki wa Reformed Church. Alipata nafasi ya kuzamishwa majini kuonyesha wakf wa maisha yake kwa Yehova Mungu Julai 4, 1923, wakati Frederick W. Franz, wa Betheli ya Brooklyn, alipokuwa amelitembelea kundi la Allentown. Ndugu Fred Franz alitoa hotuba ya ubatizo, kisha Nathan H. Knorr mwenye umri wa miaka kumi na minane akawa mmoja wa watu waliobatizwa siku hiyo katika Mto Little Lehigh. Sikuzote imekuwa furaha kukumbuka siku hiyo, tena Ndugu Knorr amefurahi sana kuwa na pendeleo la kufanya kazi na Ndugu Fred Franz karibu karibu kwa zaidi ya miaka 52 sasa!
Karibu miezi miwili baadaye, Septemba 6, 1923, Ndugu Knorr akawa mshiriki wa jamaa ya Betheli ya Brooklyn. C. W. Barber akumbuka hivi: “Adhuhuri aliyofika, alipokuja nyumbani kula chakula cha mchana, sisi tuliona ndugu kijana akiwa na shughuli ya kuweka mavazi na vitu vyake katika mojawapo la makabati katika chumba namba A-9. Kwa kuwa hatukujua kwamba badiliko lilikuwa limefanywa na kwamba alikuwa akichukua mahali pa ndugu aliyekuwa amehamishwa kwenda kwenye kituo cha radio WBBR katika Staten Island, tulimgombeza kidogo. ‘Wafanya nini hapa?’ ‘Tuliomo chumbani humu tumetosha wala hatuna nafasi ya mtu mwingine.’ Tuliona kwamba mtu mmoja zaidi akiingia chumbani tungekuwa wengi kupita kiasi, lakini tukatulia, na kumbe ndugu kijana huyo hakuwa mwingine ila Ndugu N. H. Knorr. Huo haukuwa ukaribishaji mzuri, lakini tulifurahi mara nyingi tulipozungumza juu ya jambo hilo miaka mingi baadaye tukacheka sana. Tangu mwanzo ilikuwa wazi kwamba alikuja Betheli kufanya kazi kwa bidii. Alijitahidi sana katika idara ya kusafirisha vitabu akafanya maendeleo upesi katika kutimiza madaraka yake akifanya lo lote aliloagizwa.”
Baadaye alitumikia katika meza ya kuangalia barua zinazokwenda nje katika kiwanda cha Sosaiti cha uchapaji na Februari 8, 1928, akawekwa na Ndugu Rutherford kuwa msaidizi wa kuchapa gazeti Golden Age. Kwa habari ya nia ya Ndugu Knorr juu ya kazi, J. L. Cantwell asema hivi: “Mwaka wa 1940, kulipokuwa na mateso mengi, matawi yalikuwa yakifungwa na makundi ya watu yalifanya ghasia nyingi. Usiku mmoja tulikuwa tukifanya kazi ya ziada kiwandani. Tuliombwa tuje tusaidiane kazi naye Ndugu Knorr, aliyesimamia waliokuja, akasema: ‘Najua kwamba yaonekana hakuna matumaini mazuri kwa kazi hii. Lakini yatupasa sote tuliopo hapa tukumbuke kwamba: Har–Magedoni ikija kesho, twataka tuwe tumekwisha fanya kazi kiwandani usiku kucha.”
MTAALA WA HUDUMA YA KITHEOKRASI
“Mwezi mmoja hivi ulipopita baada ya Ndugu Knorr kuwa msimamizi wa Sosaiti,” asema Henry A. Cantwell, “mipango ilifanywa kutayarisha ulioitwa wakati huo Mtaala Wenye Maendeleo katika Huduma ya Kitheokrasi.” Hiyo ilikuwa nini? Ilikuwa shule iliyoanzwa Betheli ya Brooklyn Februari mwaka wa 1942. Je! waifahamu shule hiyo? Ikiwa wewe u mmoja wa Mashahidi wa Yehova, unajua kilichoanza zaidi ya makumi matatu ya miaka iliyopita katika Betheli ya Brooklyn, yaani, Shule ya Kitheokrasi.
YEHOVA ARUHUSU USHUHUDA UTOLEWE ULIMWENGUNI POTE
Makumi matatu ya miaka iliyopita wanadamu waliona Vita ya Ulimwengu ya Pili. Pengine wengine walidhani wakati huo kwamba haikufaa kupanga kuwe na mpanuko wa kuhubiri Ufalme katika mataifa yote. Lakini roho ya Yehova ilitia watumishi wake nguvu wasonge mbele. Kutoa elimu ya uzima kulikuwa kwa lazima kabisa.
Septemba wa mwaka wa 1942, Ndugu Knorr na wasimamizi wengine wa Watch Tower Society walikubali kwa umoja kuanzwa kwa shule iliyokusudiwa kuzoeza wamisionari waweze kuhudumu katika nchi zilizo duniani pote. Ingekuwa wapi? Katika viwanja vya Sosaiti katika eneo la Finger Lakes la wilaya ya juu ya New York—Kingdom Farm, karibu na South Lansing.
Huko kulikuwa na jengo la matofali lenye orofa tatu lililomalizwa kujengwa na Watchtower Society mwaka wa 1941. Lilikuwa limejengwa liwe kimbilio la Wanabetheli wa Brooklyn, mateso makali yakifanya iwe lazima wahamie huko. Lakini halikutimiza kusudi hilo. Yaelekea kwamba Yehova aliongoza mambo yote, akiwa na kusudi la pekee kwa jengo hilo. Sasa mipango ilifanywa kutayarisha shule nyingine mpya ya kitheokrasi. Shule hiyo yaitwa Watchtower Bible School of Gilead.
Uchunguzi wa Biblia, Huduma ya Kitheokrasi ya Shambani, Kuhutubu Hadharani juu ya Biblia, Sheria Iliyo Kuu Zaidi, Vichwa vya Habari za Biblia—ni baadhi ya habari ambazo wanafunzi wenye bidii walifundishwa wakati wa mtaala huo wa miezi mitano. Walifunzwa pia lugha mpya—darasa la kwanza lilifunzwa Kispania. Lakini wanafunzi wa Gilead walitumia wakati fulani kila siku ya masomo wakifanya kazi za shamba na za nyumbani. Kwanza, hiyo iliwasaidia kuondoa wasiwasi. Jioni za siku za katikati ya juma zilikuwa za funzo la kipekee. Miisho ya juma ilikuwa nyakati nzuri za kufanya kazi yenye kuokoa uhai ya kuuhubiri Ufalme. Wanafunzi na waalimu pia walifanya utumishi wa shambani.
Darasa la 35 la Shule ya Gilead lilihitimu katika Kingdom Farm Julai 24, 1960. Darasa la 36 lilianza katika majumba ya Watch Tower Society katika 107 Columbia Heights, Brooklyn, New York, Jumatatu, Februari 6, 1961. Ni jambo lenye faida sana kuwa na shule hiyo katika makao makuu ya Sosaiti! Sasa wanafunzi wana pendeleo la kusikia hotuba zikitolewa na ndugu wengi zaidi wa Sosaiti, kutia na washiriki wa baraza inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova.
Makumi matatu ya miaka yamepita tangu Watchtower Bible School of Gilead ilipoanzwa. Mpaka sasa zaidi ya wanafunzi 5,500 wamehudhuria masomo hayo ya kitheokrasi. Kati yao, zaidi ya 2,500 wangali wakiendelea katika utumishi wa wakati wote, wakizihubiri habari njema za Ufalme ulimwenguni pote.
SHULE YA HUDUMA YA UFALME
Mkazo umeendelea kutiwa juu ya elimu ya kitheokrasi ya uzima miaka iliyopita. Mwaka wa 1958 matayarisho yalianza kufanywa juu ya mtaala wa shule mpya. Shule hiyo ilikuwa ya waangalizi. Inaitwa Shule ya Huduma ya Ufalme na hapo kwanza mtaala wake ulikuwa wa siku 24 za masomo, vipindi 96 vya masomo darasani na hotuba 20 za maagizo. Mambo yaliyofunzwa yalikuwa Mafundisho ya Ufalme, Huduma ya Shambani, Kuhutubu na Waangalizi. Shule ya Huduma ya Ufalme imesaidia sana kutayarisha waangalizi wa Kikristo watimize madaraka na mapendeleo yao.
Katika nchi nyingi tengenezo la watu wa Mungu limepanga kuwe na madarasa ya kufundisha watu hao; mengine yamesifiwa sana na wakuu wa serikali. Wanaume na wanawake wamejifunza kusoma na kuandika na wengi kati yao hata wamefurahia mapendeleo mengi ya utumishi wakamletea Yehova heshima na utukufu.
—Kutoka 1975 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.