Kuenea kwa Maarifa Yatoayo Uzima
(Makala ya funzo la kitabu)
1, 2. Ni wapi penginepo katika kitabu cha Isaya tunapopata unabii unaolingana na ule wa Isaya 11:6-8, na ni mambo gani yanayoonyesha hapa juu ya wakati wa utimizo?
KATIKA toleo lililotangulia tulizungumza juu ya unabii wa Isaya 11:6-8. Unabii unaolingana na huo katika kitabu kilichoongozwa na Mungu cha Isaya unaonyesha wakati wa paradiso ya kiroho yenye amani na usalama. Ili tupate wakati wa utimizo wa unabii huu, yatupasa tuifikirie mistari inayotangulia unabii huu unaolingana na ule wa Isaya 11:6-8. Kwa sababu hiyo, twasoma hivi:
2 “Kwa kuwa taabu za kwanza zimesahauliwa, na kwa kuwa zimefichwa machoni pangu. Maana, tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha. Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza. . . . Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu; kwa sababu wao ni wazao wa hao waliobarikiwa na [Yehova], na watoto wao pamoja nao. Na itakuwa ya kwamba, kabla hawajaomba, nitajibu; na wakiwa katika kunena, nitasikia. Mbwa-mwitu na mwana-kondoo watalisha pamoja, na simba atakula majani kama ng’ombe; na mavumbi yatakuwa chakula cha nyoka. Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote, asema [Yehova].”—Isa. 65:16-25.
3. Unabii huu ulipata utimizo wake wa kwanza wakati gani, na wakati huo sababu ya “shangwe” ilikuwa nini?
3 Utimizo wa kwanza au mdogo wa unabii huu wa ajabu unatumika kama mfano wa unabii kufananisha utimizo wa mwisho, ulio mkubwa wa unabii huo. Utimizo mdogo wa unabii wa Isaya ulitukia baada ya kurudishwa kwa Wayahudi waliohamishwa kwenye nchi ya kwao, nchi ya Yuda, katika siku za mshindi wa Kiajemi Koreshi Mkuu. Mwishowe Yerusalemu ulijengwa katika makao yake ya zamani na mji huu mtakatifu ukawa “shangwe” wakati hekalu la Yehova lilipojengwa upya huko katika makao yake ya zamani na ibada yake iliyoanzishwa tena ikaendeshwa na makuhani na Walawi waliorudishwa. Masimulizi ya hili yameandikwa katika vitabu vya Ezra na Nehemia.
4. Ni wakati gani wa utimizo wa mwisho wa unabii huu, na wakati huo ni kazi gani ya kutokeza mgeuzo uliotabiriwa ingefanywa?
4 Kwa hiyo, utimizo mkubwa na wa mwisho huja katika muda wa kurudishwa kama huo. Ni wakati kuna kurudishwa kwa mabaki ya Israeli wa kiroho kutoka katika utumwa chini ya Babeli Mkuu wa kisasa kuletwa kwenye hali yao yenye haki ya kiroho katika kibali ya Yehova iliyoonyeshwa tena. Kulingana na historia ya karne ya 20, hili lilitukia katika mwaka uliofuata kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Kuanzishwa tena kwa uhodari kwa kutangazwa bure na waziwazi kwa “habari njema ya ufalme” ulimwenguni pote katika mwaka wa 1919 W.K. kulionyesha kwamba kulikuwa kumekuwako kurudishwa kwa mabaki yaliyokombolewa ya Israeli wa kiroho kwenye hali yao ya kiroho waliyopewa na Mungu duniani. Hali hii ya kiroho ya mabaki waliotiwa mafuta iligeuzwa kuwa paradiso ya kiroho kwa baraka na kwa utendaji wa roho takatifu ya Yehova. Katika hali hiyo ndimo uzuri wa kiroho wa waabudu Wake unamomtukuza Yehova Mungu na kuna amani, umoja wa kidugu na usalama.
5. Eleza Yerusalemu ambao ni “shangwe” ni nini katika utimizo huu wa mwisho wa unabii.
5 Yerusalemu ambao Yehova Mungu ameumba kama “shangwe” na ambao yeye mwenyewe anashangilia, si mji mkuu wa Jamhuri ya Kiyahudi ya Israeli bali ni Yerusalemu wa kimbinguni, wanaokaribia mabaki ya Israeli wa kiroho. (Ebr. 12:22-29) Ndiyo makao ya ufalme wa Kimasihi ulioanza kutawala katika mbingu mwishoni mwa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 W.K. (Ufu. 12:1-5) Mji huu uko katika Mlima Sayuni wa kimbinguni, ‘mlima mtakatifu’ wa Yehova, ambako Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo, amesimama katika mamlaka ya kifalme.—Zab. 2:6; Ufu. 14:1-5.
6. Ni kwa sababu gani kulikuwako kusahihishwa katika ufahamu wa malaki ya Israeli wa kiroho wa unabii wa Biblia tangu mwaka wa 1919?
6 Kwa hiyo wakati wa utimizo wa unabii wa Isaya juu ya kugeuzwa kwa tabia ya wanyama unaanza tangu mwaka uliofuata kumalizika vita wa 1919 W.K. Huu ulikuwa ndio mwanzo wa kipindi cha elimu katika Neno la Mungu lililoandikwa kulingana na maoni ya kwamba unabii wa Biblia unafahamika ukiisha kutimizwa. Hivyo kulikuwa na uhitaji wa kusahihisha maoni yetu ya zamani, na mabaki ya Israeli wa kiroho walioendelea kuishi walihitaji kurekebishwa upya kwa mambo ya hakika na nafasi za baada ya vita. Sasa kuhubiriwa kwa “habari njema ya ufalme” kulipaswa kuwe, si kwa serikali ya kimbinguni ijayo, bali kwa ufalme wa Kimasihi wa Mungu ambao sasa umesimamishwa katika mbingu tangu mwisho wa “majira ya Mataifa” katika mwaka wa 1914. Tangu wakati huo mabaki waliokombolewa walipaswa wawe mashahidi wa Bwana Mungu, Yeye aliyekuwa ametwaa uwezo wake mkuu ili atawale katika mwaka wa 1914 kwa njia ya ufalme wa Kristo wake. (Mt. 24:14; Luka 21:24; Ufu. 11:15-17) Programu hii iliyosahihishwa ya elimu ya Biblia ilikuwa na matokeo mengi juu ya mabaki. Ilielekeza kazi yao katika upande mzuri.
7. Matokeo ya kazi hii ya elimu yalitabiriwaje katika Isaya 11:9?
7 Kazi hii ya elimu pamoja na matokeo yake yenye kugeuza inatajwa katika sehemu nyingine ya unabii wa Isaya, katika maneno haya: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isa. 11:9) Maneno haya katika mstari huu yaweza kumaanisha wanyama-mwitu ambao wamekwisha kutajwa katika mistari mitatu iliyotangulia. Mistari hiyo ilisimulia mbwa-mwitu, chui, simba, dubu, fira, nyoka mwenye sumu kuwa hawadhuru wala wanyama wa kufugwa wala watoto wasio na hatia.
8. Hasa ni akina nani ambao, kwa sababu ya elimu hii hawadhuru wala kuharibu?
8 Walakini, bila shaka hawa wanaoweza kuwa wanyama wenye kudhuru wanatumiwa kama mifano katika unabii, kwa maana wanyama hao hawawezi kugeuzwa kiakili kwa kuijaza dunia maarifa ya Yehova. Hivyo maneno hayo kweli yahusu wakaaji wa paradiso ya kiroho ya Mungu kwa mabaki yake waliorudishwa wa Israeli wa kiroho duniani. Watu hawa wenye akili wenye kumwogopa Mungu ndio wangegeuzwa katika tabia zao na shughuli zao kwa kupokea “kumjua [Yehova].”
9-12. (a) Kupatana na unabii, vitabu vya Sosaiti vilitilia jina gani mkazo wenye kuongezeka? (b) Onyesha mfano wa hili kutokana na The Watch Tower, toleo la Agosti 1, 1919.
9 Kwa hiyo, katika vitabu vya Sosaiti, jina la Mungu, Yehova Aliye Juu Zaidi, lilianza kuonekana wazi, ili kumtambulisha zaidi sana Yeye aliyekuwa ametangulia kusemwa kwa jina la kawaida la cheo Bwana au Bwana Mungu. Kwa mfano, katika fungu la sita la makala kuu “Wabarikiwa Ni Wale Wasioogopa,” katika toleo la Agosti 1, 1919, la The Watch Tower, hali ya mabaki ya Israeli wa kiroho waliokombolewa ilifananishwa na ile ya Israeli wa kale walipokuwa karibu kuvuka Mto Yordani kuingia katika Nchi ya Ahadi chini ya uongozi wa Yoshua aliyemfuata Musa. Waisraeli walihitaji kutiwa moyo wasonge mbele, na fungu hilo likaendelea kusema:
10 “Kama Musa, Yoshua alikuwa mtu mpole, asiyezitumainia sana nguvu zake mwenyewe, lakini alikuwa na imani kuu katika Mungu na alionyesha imani hiyo kwa kuwatia watu moyo wasonge mbele wakamiliki kile ambacho Mungu alikuwa amewaahidi. Lakini Yoshua alihitaji kutiwa moyo na pia watu ambao angeongoza walihitaji kutiwa moyo wafanye matendo ambayo Yehova alikuwa ameweka mbele yao. Mungu alianza kuwatia moyo hivyo kwa kusema: ‘Basi, sasa, inukeni, mvuke Yordani huu, . . .’”
11 Fungu la nane (ukurasa wa 228) la makala ile ile lilisema juu ya ushindi aliopata Mwamuzi Gideoni hivi: “Waisraeli walikuwa wamelegea katika imani yao na utii wao kwa Mungu, nao Wamidiani wakaruhusiwa waje na kutaka kuitwaa sehemu kubwa zaidi ya nchi yao. Uaminifu wa Israeli ungalizuia kutaka kufanya shambulio hili. Wamidiani wakaja kwa jeshi kubwa, zaidi ya watu hodari 200,000 wakapiga kambi tayari kupigana na Waisraeli. Yehova alikusudia kupata ushindi juu ya adui hawa wa watu wake na kuwafukuza katika nchi ya ahadi. . . . Yehova alimpa Gideoni heshima kuu ya kutumiwa naye awakomboe Waisraeli. . . . Kwa uongozi wa Yehova, ndipo Gideoni alipoomba wenye kujitolea kutoka miongoni mwa Waisraeli wapigane na majeshi ya Midiani. . . . ”
12 Kusema juu ya kikosi kidogo cha Gideoni cha wenye kujitolea 300 kilichochaguliwa kwa njia ya pekee, fungu lifuatalo lasema hivi: “Kikosi hiki kidogo cha 300 kilikuwa na sifa zenyewe zenye kumpendeza Yehova.” Na kuendelea katika makala yote mpaka fungu la mwisho, lililosema kwa sehemu hivi: “Ni wale walio safi katika moyo peke yao ambao ni wakamilifu katika upendo, kwa hiyo kulingana na maneno ya Yesu, ni wale wasioogopa—wakamilifu katika upendo—walio Safi katika moyo, ndio watakaopokewa katika ufalme wamwone Yehova.”—Ukurasa wa 233.
13. (a) Ni “dunia” gani inayojawa na kumjua Yehova, kama ilivyotabiriwa katika Isaya 11:9? (b) Huku “kumjua [Yehova]” kunakoongezeka kwapatana na sehemu gani ya agano jipya?
13 Hivyo ndivyo “kumjua [maarifa ya Yehova]” kulivyoanza kuenea na kuijaa “dunia,” yaani, hali ya kiroho ya mabaki waliorudishwa wa Israeli wa kiroho, “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) Mabaki haya wamo katika agano lililopatanishwa na Yesu Kristo kati ya Mungu na “taifa takatifu” la Israeli wa kiroho. Mojawapo ya sehemu za agano hili bora imeandikwa katika maneno haya ya unabii: “Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue [Yehova]; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema [Yehova]; maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yer. 31:31-34; Ebr. 8:7-12) Kwa sababu hiyo, ilifaa sana kwamba hali ya kiroho ya mabaki ya “Israeli wa Mungu” wa Kikristo ijawe na “kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.”
14. (a) Mtu aliye na “kumjua [Yehova]” anageuzwaje nako? (b) Ni nini kinachowakilishwa na ‘mlima mtakatifu,’ unaotajwa katika Isaya 11:9, ambako hawadhuru wala kuharibu?
14 “Kumjua [Yehova] “kwamfanyia aliye nako jambo fulani. Kulingana na anayosema Yehova katika Isaya 11:9, kumjua Yehova kunasemwa kuwa ndiyo sababu “hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu.” Kwa kuwa ‘mlima mtakatifu’ ndiyo makao ya serikali na yalifananishwa na Mlima Sayuni, ambako Mfalme Daudi aliketi “katika kiti cha enzi cha [Yehova],” usemi huu “mlima wangu wote mtakatifu” watumiwa katika maana yenye kuwakilisha. Haumaanishi Mlima Sayuni wa kimbinguni peke yake, bali humaanisha makao yote ya Israeli wa kiroho hapa duniani. Maana yake ni hali ya sasa ya kiroho ya mabaki waliokombolewa na kurudishwa tangu mwaka wa 1919 W.K. Wanakiri na kutii yeye ambaye wakati mmoja alikuwa “chipukizi katika shina la Yese” kama Mfalme wa Kimasihi, ambaye Bwana Mungu ameweka katika Mlima Sayuni wa kimbinguni, ‘mlima mtakatifu’ Wake.—Isa. 11:1; Ebr. 12:22; Zab. 2:6.
15. Sababu gani “kumjua [Yehova]” kunageuza nyutu za wale walio nako?
15 Ni kwa sababu gani “kumjua [Yehova]” kunageuza wakaaji wa paradiso ya kiroho wawe wasiodhuru na wasioharibu? Kwa sababu inamaanisha zaidi ya kumjua tu. Kujua kunamaanisha kumkiri Yeye kwa kadiri ya kuishi kulingana na mapenzi Yake. Mtume wa Kikristo Yohana asema: “Na katika hili twajua ya kuwa tumemjua yeye, ikiwa tunashika amri zake. Yeye asemaye, Nimemjua, wala hazishiki amri zake, ni mwongo, wala kweli haimo ndani yake. Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo. Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake. Kwa maana huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito.”—1 Yohana 2:3, 4; 4:8, 16; 5:3.
MATOKEO YA KUTOKUMJUA YEHOVA
16. Yeremia alisema nini juu ya wale wasiomjua Yehova, tofauti na wale wanaomjua?
16 Matokeo yenye huzuni yanayofuata kwa sababu ya mtu kutokumjua Yehova, kutokumkiri, kutokumfahamu, yanatangazwa kwa kinywa cha manabii Wake. Kwa mfano, wakati wa miaka ya mwisho 40 kabla ya uharibifu wa Yerusalemu na hekalu lake na kuhamishwa kwa Wayahudi waliosalia kupelekwa Babeli, Yehova alitangaza kwa kinywa cha nabii wake Yeremia hivi: “Watu wangu ni wapumbavu, hawanijui, ni watoto waliopungukiwa na akili, wala hawana ufahamu; ni wenye akili katika kutenda mabaya, bali katika kutenda mema hawana maarifa.” (Yer. 4:22) “Ajisifuye na ajisifu kwa sababu hii, ya kwamba ananifahamu mimi, na kunijua, ya kuwa mimi ni [Yehova], nitendaye wema, na hukumu, na haki, katika nchi; maana mimi napendezwa na mambo hayo.”—Yer. 9:24; 1 Kor. 1:21.
17, 18. Wakati wa mapema, nabii Hosea alisema nini juu ya matokeo ya kukosa kumjua Mungu katika Israeli?
17 Pia, nabii Hosea aliongozwa na Mungu wakati fulani kabla ya kuharibiwa kwa ufalme wa Israeli wa kabila kumi kwa Mamlaka ya Ulimwengu ya Kiashuru katika mwaka wa 740 K.W.K. awaambie Waisraeli hivi: “Lisikieni neno la [Yehova] enyi wana wa Israeli; kwa maana [Yehova] ana mateto nao wakaao katika nchi, kwa sababu hapana kweli, wala fadhili, wala kumjua Mungu katika nchi. [Kwa matokeo gani?] Hapana neno ila kuapa kwa uongo, na kuvunja ahadi, na kuua, na kuiba, na kuzini; huruka mpaka, na damu hugusana na damu. Kwa ajili ya hayo nchi itaomboleza, na kila mtu akaaye ndani yake atadhoofika, pamoja na wanyama wa kondeni na ndege wa angani; naam, samaki wa baharini pia wataondolewa. Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, mimi nami nitawasahau watoto wako.”
18 “Kwa sababu hiyo nimewakata-kata kwa vinywa vya manabii; nimewaua kwa maneno ya kinywa changu; na hukumu yangu itatokea kama mwanga. Maana nataka fadhili wala si sadaka; na kumjua Mungu kuliko sadaka za kuteketezwa.” Hosea 4:13, 6; 6:5, 6.
19. Ni kwa sababu gani hali zilizomo katika paradiso ya kiroho ni tofauti sana na zile zilizokuwamo katika Israeli wa kale kama zinavyosimuliwa na nabii Hosea?
19 Kwa sababu ya kukataa “kumjua Mungu,” ufalme wa Israeli wa kabila kumi na ufalme wa Yuda zilipata matokeo mazito na yenye hatari. Tunapoona matokeo mabaya yaliyofuatana na kukataliwa huko kwa maarifa ambayo ni ya maana kuliko yote, twaweza kufahamu sababu yake nini hakuna kudhuru wala kuharibu ko kote miongoni mwa wale wanaokaa katika paradiso ya kiroho ya mabaki ya Israeli wa kiroho. Ni kwa sababu “kujua [Yehova]” kunajaa hali yao ya kiroho yenye baraka kama vile maji yanavyoifunika bahari. Maarifa haya ni yenye kina (mengi mno) kama bahari kuu, kama zile “bahari saba” kubwa zinazoienea dunia nzima.
20. Katika sala kwa Baba yake, Yesu alikazia nini kama takwa la kwanza ili kupata uzima wa milele?
20 Alipokuwa akitoa sala kwa ajili ya mitume wake waaminifu, kwa kufaa Yesu Kristo alisema kwa Yehova Baba yake wa kimbinguni hivi: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Katika paradiso ya kiroho ya leo, wakaaji wangali wakiyatwaa maarifa ya Yehova na ya Mfalme wake wa Kimasihi, Yesu Kristo, na kwa sababu hiyo maisha ya kiroho katika hali ya kiparadiso ya wale wanaomjua Yehova ni yenye amani na usalama.
—Kutoka kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand!, sura ya 11.