Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Ripoti za miaka fulani zaonyesha kwamba idadi ya wanaoshiriki mifano ya ukumbusho iliongezeka kidogo. Je, hilo ladokeza kwamba wapya wengi wanatiwa mafuta kwa roho takatifu?
Kuna sababu nzuri kuamini kwamba idadi ya 144,000 ya Wakristo watiwa-mafuta ilitimia miongo iliyopita.
Katika Matendo 2:1-4, twasoma kuhusu wale wa kwanza wa kikundi hicho chenye idadi kamili: “Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka.”
Baada ya hayo, Yehova aliwachagua wengine, akawatia mafuta kwa roho yake takatifu. Maelfu yaliongezwa katika miaka ya mapema sana ya Ukristo. Kwenye sherehe ya Ukumbusho katika wakati wetu, mara nyingi msemaji huvuta uangalifu kwa maneno ya mtume Paulo kwenye Warumi 8:15-17, ambalo hutaja kwamba watiwa-mafuta ‘hupokea roho ya kufanywa wana.’ Paulo aliongeza kwamba roho takatifu waipokeayo ‘hushuhudia pamoja na roho zao, ya kuwa wao ni watoto wa Mungu; warithio pamoja na Kristo.’ Wale ambao kwa kweli wametiwa mafuta kwa roho, wanajua hilo kwa hakika. Si matamanio tu au wonyesho wa kihisia-moyo maoni yasiyo halisi ya kujifikiria wenyewe.
Twaelewa kwamba mwito huo wa kimbingu uliendelea kwa karne kadhaa, ingawa katika kile kipindi kiitwacho Enzi za Giza, kungeweza kuwapo nyakati ambapo idadi ya watiwa-mafuta ilikuwa ndogo sana.a Ukristo wa kweli uliporudishwa karibu na mwisho wa karne iliyopita, wengi waliitwa na kuchaguliwa. Lakini yaonekana kwamba katikati ya miaka ya 1930, idadi kamili ya 144,000 ilitimia. Hivyo kikundi cha Wakristo waaminifu-washikamanifu wenye matumaini ya kidunia kikaanza kuonekana. Yesu aliwaita hao “kondoo wengine,” ambao hujiunga na watiwa-mafuta katika ibada wakiwa kikundi kimoja kilichokubaliwa.—Yohana 10:14-16.
Mambo ya hakika kwa miongo kadhaa yaonyesha kutimia kwa mwito wa watiwa-mafuta na baraka ya Yehova juu ya “umati mkubwa” unaoongezeka ambao hutumainia kuokoka “dhiki kubwa.” (Ufunuo 7:9, 14, NW) Kwa kielelezo, kwenye sherehe ya Ukumbusho ya 1935, iliyohudhuriwa na 63,146, walioshiriki mifano wakithibitisha madai yao kuwa watiwa-mafuta, walikuwa 52,465. Miaka thelathini baadaye, au katika 1965, hudhurio lilikuwa 1,933,089, huku washiriki walipungua kufikia 11,550. Miaka 30 kuelekea nyakati zetu, katika 1995 hudhurio liliongezeka kufikia 13,147,201, lakini walioshiriki mkate na divai walikuwa 8,645 tu. (1 Wakorintho 11:23-26) Kwa wazi, kadiri miongo ilivyopita, idadi ya wale wanaodai kuwa mabaki ilipungua sana—karibu 52,400 katika 1935; 11,500 katika 1965; 8,600 katika 1995. Hata hivyo, wale wenye matumaini ya kidunia wamebarikiwa, na idadi yao imeongezeka kwa wingi.
Ripoti ya ukumbusho ya karibuni zaidi iliyochapishwa ni ya mwaka wa 1995, nayo huonyesha washiriki 28 zaidi ya mwaka uliotangulia ingawa kwa kweli uwiano wa walioshiriki ulishuka. Tufikiriapo yote hayo, ule uhakika wa kwamba wachache wengine walichagua kushiriki mifano haupasi kutuhangaisha. Kwa miaka kadhaa, hata waliobatizwa karibuni, kwa ghafula wameanza kushiriki. Katika visa kadhaa, baada ya muda fulani walikiri kwamba hilo lilikuwa kosa. Wengine walitambua kwamba walishiriki likiwa itikio la kihisia-moyo pengine kutokana na mkazo wa kimwili au wa kiakili. Lakini hatimaye wakatambua kwamba kwa kweli hawakuitwa kwa uhai wa kimbingu. Waliomba uelewevu wa Mungu wenye rehema. Na waliendelea kumtumikia wakiwa Wakristo wema, waaminifu-washikamanifu, wenye matumaini ya uhai udumuo milele juu ya dunia.
Hakuna uhitaji kwa yeyote wetu kuhangaishwa ikiwa mtu fulani anaanza kushiriki mifano au anaacha kufanya hivyo. Kwa kweli haituhusu ikiwa mtu fulani kwa hakika ametiwa mafuta kwa roho takatifu na ameitwa kwa uhai wa kimbingu au sivyo. Kumbuka hakikisho imara la Yesu: “Mimi ni mchungaji mwema, nami nawajua kondoo zangu.” (NW) Kwa hakika vivyo hivyo, Yehova awajua wale ambao amewachagua kuwa wana wa kiroho. Kuna kila sababu ya kuamini kwamba idadi ya watiwa-mafuta itaendelea kupungua kadiri uzee na matukio yasiyotazamiwa yamalizapo maisha yao ya kidunia. Hivyo, watiwa-mafuta hao wa kweli wathibitishapo uaminifu mpaka kifo, wakitazamia kupokea taji ya uhai, kondoo wengine, ambao wamefua mavazi yao katika damu ya Mwana-Kondoo, wanaweza kutumainia kuokoka dhiki kubwa iliyo karibu sana.—2 Timotheo 4:6-8; Ufunuo 2:10.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1965, kurasa 191-192, la Kiingereza.