Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 9/15 kur. 10-15
  • Lazima Wote Watoe Hesabu kwa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Lazima Wote Watoe Hesabu kwa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Malaika Wana Wajibu wa Kutoa Hesabu
  • Mwana wa Mungu Ana Wajibu wa Kutoa Hesabu
  • Wenye Wajibu wa Kutoa Hesabu Wakiwa Mataifa
  • Vielelezo vya Wajibu wa Kibinafsi wa Kutoa Hesabu
  • Wajibu wa Kutoa Hesabu Katika Kutaniko la Kikristo
  • Yehova na Apendezwe na Hesabu Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Roho Inayoendesha Taratibu ya Zamani Iliyopo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Wakristo Wanahitajiana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 9/15 kur. 10-15

Lazima Wote Watoe Hesabu kwa Mungu

“Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—WARUMI 14:12, NW.

1. Ni mipaka gani iliyowekewa uhuru wa Adamu na Hawa?

YEHOVA MUNGU aliwaumba wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, wakiwa viumbe walio huru kuchagua. Ingawa walikuwa wa hali ya chini kuliko malaika, walikuwa viumbe wenye akili waliokuwa na uwezo wa kufanya maamuzi yenye hekima. (Zaburi 8:4, 5) Hata hivyo, uhuru huo waliopewa na Mungu haukuwapa wanadamu ruhusa ya kujiamulia kibinafsi mema na mabaya. Walikuwa na wajibu wa kutoa hesabu kwa Muumba wao, na wajibu huo wa kutoa hesabu ulifikia wazao wao wote.

2. Yehova atafanyiza kutoa hesabu kupi karibuni, na kwa nini?

2 Sasa kwa sababu tunakaribia upeo wa mfumo huu mwovu wa mambo, Yehova atafanyiza kutoa hesabu duniani. (Linganisha Warumi 9:28.) Karibuni, watu wasiomwogopa Mungu watalazimika kutoa hesabu kwa Yehova Mungu kwa sababu ya uangamizi wa mali za dunia, uharibifu wa uhai wa kibinadamu, na hasa mnyanyaso wa watumishi wake.—Ufunuo 6:10; 11:18.

3. Ni maswali gani tutakayofikiria?

3 Kwa sababu tunakabili taraja hilo linalotufanya tufikiri, ni faida kwetu kukumbuka shughuli zenye uadilifu za Yehova pamoja na viumbe wake katika nyakati zilizopita. Maandiko yanaweza kutusaidiaje, kibinafsi, kutoa hesabu yenye kukubalika kwa Muumba wetu? Ni vielelezo vipi ambavyo huenda vikawa vyenye kusaidia, na ni vipi tuepuke kuiga?

Malaika Wana Wajibu wa Kutoa Hesabu

4. Twajuaje kwamba Mungu huwapasisha malaika kutoa hesabu kwa ajili ya vitendo vyao?

4 Viumbe wa kimalaika wa Yehova walio mbinguni wana wajibu uleule tulio nao wa kutoa hesabu kwake. Kabla ya Furiko la siku ya Noa, malaika fulani kwa kutotii walijitwalia miili ya kibinadamu ili wafanye ngono pamoja na wanawake. Wakiwa viumbe hai walio huru kuchagua, viumbe hao wa roho waliweza kufanya uamuzi huo, lakini Mungu aliwatoza hesabu. Wale malaika wasiotii waliporudi kwenye makao ya roho, Yehova hakuwaruhusu warudie cheo chao cha awali. Mwanafunzi Yuda atuambia kwamba “amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu.”—Yuda 6.

5. Shetani na roho zake waovu wamepatwa na anguko gani, na hesabu ya uasi wao itatozwaje?

5 Mtawala wa malaika hao wasiotii, au roho waovu, ni Shetani Ibilisi. (Mathayo 12:24-26) Malaika huyo mwovu aliasi dhidi ya Muumba wake akapinga uhaki wa enzi kuu ya Yehova. Shetani aliongoza wazazi wetu wa kwanza kwenye dhambi, na tokeo likawa kufa kwao hatimaye. (Mwanzo 3:1-7, 17-19) Ingawa Yehova alimruhusu Shetani afikie makao ya kimbingu kwa kipindi fulani baada ya tukio hilo, kitabu cha Biblia cha Ufunuo kilitabiri kwamba wakati wa Mungu uwadiapo, mwovu huyo angetupwa chini hadi ujirani wa dunia. Uthibitisho waonyesha kwamba hilo lilitendeka muda mfupi baada ya Yesu Kristo kupokea mamlaka ya Ufalme mwaka wa 1914. Hatimaye, Ibilisi na roho zake waovu wataingia katika uharibifu udumuo milele. Suala la enzi kuu likiwa limesuluhishwa hatimaye, ndipo hesabu ya uasi itakapokuwa imetozwa kwa haki.—Ayubu 1:6-12; 2:1-7; Ufunuo 12:7-9; 20:10.

Mwana wa Mungu Ana Wajibu wa Kutoa Hesabu

6. Yesu huonaje wajibu wake mwenyewe wa kutoa hesabu kwa Baba yake?

6 Ni kielelezo chema kama nini ambacho kimewekwa na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo! Akiwa binadamu mkamilifu aliyekuwa sawa na Adamu, Yesu alifurahia kufanya mapenzi ya kimungu. Aliterema pia kutozwa hesabu kwa ajili ya kufuata sheria ya Yehova. Kumhusu yeye, mtunga-zaburi alitoa unabii huu kwa kufaa: “Kuyafanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; naam, sheria yako imo moyoni mwangu.”—Zaburi 40:8; Waebrania 10:6-9.

7. Alipokuwa akisali katika siku ya kuamkia kifo chake, kwa nini Yesu aliweza kusema maneno yaliyorekodiwa kwenye Yohana 17:4, 5?

7 Ujapokuwa upinzani wenye chuki ambao Yesu alipatwa nao, alifanya mapenzi ya Mungu na alidumisha uaminifu-maadili hadi kifo kwenye mti wa mateso. Kwa njia hiyo alilipa bei ya fidia ili kuwakomboa wanadamu kutoka katika matokeo yenye kufisha ya dhambi ya Adamu. (Mathayo 20:28) Kwa sababu hiyo, katika siku ya kuamkia kifo chake, Yesu aliweza kusali hivi kwa uhakika: “Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye. Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:4, 5) Yesu aliweza kumwambia Baba yake wa kimbingu maneno hayo kwa sababu alikuwa akiupita kwa mafanikio ule mtihani wa kutoa hesabu na alikubalika kwa Mungu.

8. (a) Paulo alionyeshaje kwamba ni lazima tutoe hesabu kwa Yehova Mungu kujihusu wenyewe? (b) Ni nini kitakachotusaidia kupata kukubaliwa na Mungu?

8 Tofauti na yule mtu mkamilifu Yesu Kristo, sisi si wakamilifu. Hata hivyo, tuna wajibu wa kutoa hesabu kwa Mungu. Mtume Paulo alisema hivi: “Lakini kwa nini wewe wahukumu ndugu yako? Au kwa nini wewe pia wadharau ndugu yako? Kwa maana sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu; kwa maana imeandikwa: “‘Kama niishivyo,’ asema Yehova, ‘kwangu kila goti litakunjwa, na kila ulimi utakiri waziwazi kwa Mungu.’” Hivyo, basi kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Warumi 14:10-12, NW) Ili tuweze kufanya hivyo na kupata kukubaliwa na Yehova, ametupatia kwa upendo, dhamiri na pia Neno lake lililopuliziwa, Biblia, kutuongoza katika yale tusemayo na tufanyayo. (Warumi 2:14, 15; 2 Timotheo 3:16, 17) Kutumia kwa faida kamili maandalizi ya Yehova ya kiroho na kufuata dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia kutatusaidia kupata kukubaliwa na Mungu. (Mathayo 24:45-47) Roho takatifu, au kani ya utendaji ya Yehova, ni chanzo cha ziada cha kupata nguvu na mwongozo. Tukitenda kwa kupatana na mwelekezo wa roho na miongozo ya dhamiri yetu iliyozoezwa kwa Biblia, twaonyesha kwamba ‘hatumkatai Mungu,’ ambaye ni lazima tutoe hesabu kwake kwa ajili ya vitendo vyetu vyote.—1 Wathesalonike 4:3-8; 1 Petro 3:16, 21.

Wenye Wajibu wa Kutoa Hesabu Wakiwa Mataifa

9. Waedomu walikuwa nani, na ni jambo gani lililowapata kwa sababu ya jinsi walivyotenda kuelekea Israeli?

9 Yehova huyapasisha mataifa kutoa hesabu. (Yeremia 25:12-14; Sefania 3:6, 7) Fikiria ufalme wa kale wa Edomu, uliokuwa kusini mwa Bahari Iliyokufa na kaskazini ya Ghuba ya Akaba. Waedomu walikuwa Wasemiti, wenye ukoo wa karibu sana na Waisraeli. Ingawa babu wa kale wa Waedomu alikuwa Esau, mjukuu wa Abrahamu, Waisraeli hawakuruhusiwa kusafiri kupitia Edomu katika “njia kuu ya mfalme” walipokuwa njiani kwenda Bara Lililoahidiwa. (Hesabu 20:14-21) Karne zilipopita uhasama wa Edomu uliongezeka ukawa chuki isiyo na huruma kwa Israeli. Hatimaye, Waedomu walilazimika kutoa hesabu kwa ajili ya kusihi kwao Wababiloni sana waharibu Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. (Zaburi 137:7) Katika karne ya sita K.W.K., vikosi vya Babiloni chini ya uongozi wa Mfalme Nabonido vilishinda Edomu, nao ukawa ukiwa, sawa na alivyoamuru Yehova.—Yeremia 49:20; Obadia 9-11.

10. Wamoabi walitendaje kuelekea Waisraeli, na Mungu aliupasishaje Moabu kutoa hesabu?

10 Moabu ulipatwa na tokeo lilo hilo. Ufalme wa Moabu ulikuwa kaskazini ya Edomu na mashariki ya Bahari Iliyokufa. Kabla ya Waisraeli kuingia Bara Lililoahidiwa, Wamoabi hawakuwatendea kwa ukaribishaji-wageni, ikiwa dhahiri kwamba walikuwa wakiwapa mkate na maji ili tu kufaidika kifedha. (Kumbukumbu la Torati 23:3, 4) Mfalme Balaki wa Moabu alimwajiri nabii Balaamu awalaani Waisraeli, na wanawake Wamoabi walitumiwa ili kuwavuta wanaume Waisraeli katika ukosefu wa adili na ibada ya sanamu. (Hesabu 22:2-8; 25:1-9) Hata hivyo, Yehova hakupuuza chuki ya Moabu kwa Israeli. Kama ilivyotolewa unabii, Moabu ulipatwa na uharibifu mikononi mwa Wababiloni. (Yeremia 9:25, 26; Sefania 2:8-11) Ndiyo, Mungu aliupasisha Moabu kutoa hesabu.

11. Moabu na Amoni zilipata kuwa kama majiji gani, na unabii mbalimbali wa Biblia huonyesha nini kuhusu mfumo mwovu wa mambo uliopo?

11 Si Moabu tu bali Amoni pia ililazimika kutoa hesabu kwa Mungu. Yehova alikuwa ametabiri hivi: “Hakika Moabu atakuwa kama Sodoma, na wana wa Amoni kama Gomora, yaani, milki ya upupu, na mashimo ya chumvi, ukiwa wa daima.” (Sefania 2:9) Nchi za Moabu na Amoni ziliangamizwa, sawa na vile Mungu alikuwa ameharibu majiji ya Sodoma na Gomora. Kulingana na Shirika la Kijiolojia la London, watafiti hudai kwamba wamepata mahali pa magofu ya Sodoma na Gomora katika pwani ya mashariki ya Bahari Iliyokufa. Uthibitisho wowote wenye kutegemeka ambao huenda ukavumbuliwa kwa habari hii waweza tu kuunga mkono unabii mbalimbali wa Biblia unaoonyesha kwamba Yehova Mungu ataupasisha mfumo mwovu wa mambo uliopo kutoa hesabu.—2 Petro 3:6-12.

12. Ingawa Israeli lililazimika kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili ya dhambi zalo, ni jambo gani lililokuwa limetabiriwa kuhusu mabaki ya Wayahudi?

12 Ingawa Israeli lilikuwa limependelewa sana na Yehova, lililazimika kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili ya dhambi zalo. Yesu Kristo alipolijia taifa la Israeli, walio wengi walimkataa. Ni mabaki tu yaliyodhihirisha imani yakawa wafuasi wake. Paulo alitumia unabii fulani-fulani kuhusu mabaki hayo ya Wayahudi alipoandika hivi: “Isaya naye atoa sauti yake juu ya Israeli, kusema, Hesabu ya wana wa Israeli, ijapokuwa ni kama mchanga wa bahari, ni mabaki yao tu watakaookolewa. Kwa maana Bwana atalitekeleza neno lake [“atafanyiza kutoa hesabu,” NW] juu ya nchi, akilimaliza na kulikata. Tena kama Isaya alivyotangulia kunena, Kama Bwana wa majeshi asingalituachia uzao, tungalikuwa kama Sodoma, tungalifananishwa na Gomora.” (Warumi 9:27-29; Isaya 1:9; 10:22, 23) Mtume alitaja kielelezo cha wale 7,000 wakati wa Eliya ambao hawakuwa wameinamia Baali, kisha akasema: “Basi ni vivi hivi wakati huu wa sasa, yako mabaki waliochaguliwa kwa neema.” (Warumi 11:5) Mabaki yalitia ndani watu mmoja-mmoja waliokuwa na wajibu wa kibinafsi wa kutoa hesabu kwa Mungu.

Vielelezo vya Wajibu wa Kibinafsi wa Kutoa Hesabu

13. Ni jambo gani lililompata Kaini wakati Mungu alipompasisha kutoa hesabu kwa ajili ya kumuua kimakusudi ndugu yake Abeli?

13 Biblia hutaja visa vingi vya watu waliokuwa na wajibu wa kibinafsi wa kutoa hesabu kwa Yehova Mungu. Fikiria kielelezo cha Kaini, mzaliwa wa kwanza wa Adamu. Yeye na pia ndugu yake Abeli walimtolea Yehova dhabihu. Dhabihu ya Abeli ilikubalika kwa Mungu, lakini ya Kaini haikukubalika. Alipopasishwa kutoa hesabu kwa ajili ya kumuua kimakusudi ndugu yake, Kaini alimwambia Mungu hivi bila kuona huruma: “Mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?” Kwa sababu ya dhambi yake, Kaini alifukuziwa mbali hadi “nchi ya Nodi mbele ya Edeni.” Hakuonyesha toba yoyote yenye weupe wa moyo kwa ajili ya uhalifu wake, akijutia tu adhabu yake aliyostahili.—Mwanzo 4:3-16.

14. Wajibu wa kibinafsi wa kutoa hesabu kwa Mungu ulitolewaje kielezi katika kisa cha kuhani wa cheo cha juu Eli na wana wake?

14 Wajibu wa mtu wa kibinafsi wa kutoa hesabu kwa Mungu unaonyeshwa pia katika kisa cha kuhani wa cheo cha juu wa Israeli Eli. Wana wake, Hofni na Finehasi, walitumikia wakiwa makuhani rasmi lakini “walikuwa na hatia ya udhalimu kuelekea watu, na ya ukosefu wa heshima kuelekea Mungu, na hawakuepuka namna yoyote ya uovu,” asema mwanahistoria Yosefo. “Watu [hao] wasiofaa kitu” hawakumkiri Yehova, walishiriki katika mwenendo wa kukufuru, na walikuwa na hatia ya ukosefu mzito wa adili. (1 Samweli 1:3; 2:12-17, 22-25) Eli, akiwa baba yao na kuhani wa cheo cha juu wa Israeli, alikuwa na wajibu wa kuwatia nidhamu, lakini aliwakaripia kwa upole tu. Eli ‘aliendelea kuwaheshimu wana wake kuliko [“Yehova,” NW].’ (1 Samweli 2:29) Kisasi kikaja juu ya nyumba ya Eli. Wana wote wawili walikufa siku ileile ambayo baba yao alikufa, na nasaba yao ya ukuhani ilikomeshwa kabisa hatimaye. Kwa njia hiyo, ile hesabu ilitozwa.—1 Samweli 3:13, 14; 4:11, 17, 18.

15. Kwa nini Yonathani mwana wa Mfalme Sauli alithawabishwa?

15 Kielelezo kilicho tofauti kabisa kiliwekwa na Yonathani mwana wa Mfalme Sauli. Punde si punde baada ya Daudi kumuua Goliathi, “roho ya Yonathani ikaambatana na roho ya Daudi,” nao wakafanya agano la urafiki. (1 Samweli 18:1, 3) Yamkini, Yonathani alitambua kwamba roho ya Mungu ilikuwa imemwacha Sauli, lakini bidii yake mwenyewe kwa ajili ya ibada ya kweli iliendelea bila kupunguka. (1 Samweli 16:14) Uthamini wa Yonathani kwa mamlaka ya Daudi aliyopewa na Mungu haukupunguka kamwe. Yonathani aling’amua wajibu wake wa kutoa hesabu kwa Mungu, na Yehova alimthawabisha kwa sababu ya mwenendo wake wenye kuheshimika kwa kuhakikisha kwamba nasaba ya familia yake iliendelea kwa vizazi kadhaa.—1 Mambo ya Nyakati 8:33-40.

Wajibu wa Kutoa Hesabu Katika Kutaniko la Kikristo

16. Tito alikuwa nani, na kwa nini yaweza kusemwa kwamba alitoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu mwenyewe?

16 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo husema vema juu ya wanaume na wanawake wengi waliotoa hesabu njema kuhusu wao wenyewe. Mathalani, kulikuwa na yule Mkristo Mgiriki aliyeitwa Tito. Imedokezwa kwamba alikuwa Mkristo wakati wa safari ya kwanza ya mishonari ya Paulo hadi Kipro. Kwa kuwa Wayahudi na wageuzwa-imani kutoka Kipro huenda wakawa walikuwa Yerusalemu wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., huenda ikawa Ukristo ulifikia hicho kisiwa upesi baada ya tukio hilo. (Matendo 11:19) Hata hivyo, Tito alithibitika kuwa mmoja wa wafanyakazi wenzi waaminifu wa Paulo. Aliandamana na Paulo na Barnaba katika safari ya kwenda Yerusalemu karibu na mwaka wa 49 W.K., suala la tohara liliposuluhishwa. Jambo la kwamba Tito hakuwa ametahiriwa liliongezea umaana hoja ya Paulo ya kwamba wageuzwa-imani Wakristo hawapaswi kuwa chini ya Sheria ya Kimusa. (Wagalatia 2:1-3) Huduma nzuri ya Tito inashuhudiwa katika Maandiko, na hata Paulo alimwandikia barua yenye kupuliziwa kimungu. (2 Wakorintho 7:6; Tito 1:1-4) Ni wazi kwamba kufikia mwisho kabisa wa mwendo wake wa kidunia, Tito aliendelea kutoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu mwenyewe.

17. Timotheo alitoa hesabu gani, na kielelezo hicho chaweza kutuathirije?

17 Timotheo alikuwa mtu mwingine mwenye bidii aliyetoa hesabu yenye kukubalika kwa Yehova Mungu kujihusu mwenyewe. Ingawa Timotheo alikuwa na matatizo fulani ya afya, alionyesha ‘imani isiyo na unafiki’ na ‘alitumikia pamoja na Paulo kwa ajili ya habari njema.’ Kwa hiyo mtume aliweza kuwaambia Wakristo wenzake katika Filipi: ‘Sina mtu mwingine ambaye kama Timotheo, anawashughulikieni kwa moyo.’ (2 Timotheo 1:5; Wafilipi 2:20, 22; 1 Timotheo 5:23, Habari Njema kwa Watu Wote) Tukabilipo udhaifu mbalimbali wa kibinadamu na majaribu mengine, sisi pia twaweza kuwa na imani isiyo na unafiki na twaweza kutoa hesabu yenye kukubalika kwa Mungu kuhusu wao wenyewe.

18. Lidia alikuwa nani, naye alionyesha roho gani?

18 Lidia alikuwa mwanamke mwenye kumwogopa Mungu ambaye kwa wazi alitoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu mwenyewe. Yeye na watu wa nyumbani mwake walikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kukubali Ukristo katika Ulaya kwa sababu ya utendaji wa Paulo katika Filipi yapata mwaka wa 50 W.K. Akiwa mwenyeji wa Thiatira, labda Lidia alikuwa mgeuzwa-imani wa Dini ya Kiyahudi, lakini huenda ikawa kulikuwa na Wayahudi wachache na hakukuwa na sinagogi katika Filipi. Yeye na wanawake wengine wachaji walikuwa wakikutana kando ya mto, Paulo aliposema nao. Likiwa tokeo, Lidia akawa Mkristo na aliwashurutisha Paulo na washiriki wake wakae naye. (Matendo 16:12-15) Ukaribishaji-wageni ambao Lidia alionyesha ungali sifa inayowatambulisha Wakristo wa kweli.

19. Dorkasi alitoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu mwenyewe kwa matendo gani mema?

19 Dorkasi alikuwa mwanamke mwingine aliyetoa hesabu nzuri kwa Yehova Mungu kujihusu mwenyewe. Alipokufa, Petro alienda Yafa kwa kuitikia ombi kutoka kwa wanafunzi waliokuwa wakiishi huko. Wale wanaume wawili waliokutana na Petro “wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumwonyesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao.” Dorkasi alirudishwa kwenye uhai. Lakini je, yeye akumbukwe kwa sababu tu ya ukarimu wake wenye upendo? La. Alikuwa “mwanafunzi” na kwa hakika yeye mwenyewe alishiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. Leo vilevile wanawake Wakristo ‘wanajaa matendo mema na sadaka.’ Wanafurahia pia kushiriki kwa bidii katika kupiga mbiu ya habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi.—Matendo 9:36-42; Mathayo 24:14; 28:19, 20.

20. Ni maswali gani ambayo twaweza kujiuliza?

20 Biblia huonyesha kwa wazi kwamba ni lazima mataifa na watu mmoja-mmoja watoe hesabu kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu Jehovah. (Sefania 1:7) Ikiwa tumejiweka wakfu kwa Mungu, twaweza basi kujiuliza, ‘Mimi huonaje mapendeleo na madaraka niliyopewa na Mungu? Ninatoa hesabu ya aina gani kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo kujihusu mwenyewe?’

Majibu Yako Ni Nini?

◻ Ungethibitishaje kwamba malaika na Mwana wa Mungu wana wajibu wa kutoa hesabu kwa Yehova?

◻ Kuna vielelezo vipi vya Biblia kuonyesha kwamba Mungu huyapasisha mataifa kutoa hesabu?

◻ Biblia husema nini juu ya mtu kuwa na wajibu wa kibinafsi wa kutoa hesabu kwa Mungu?

◻ Ni nani baadhi ya watu mmoja-mmoja katika rekodi ya Biblia waliotoa hesabu nzuri kwa Yehova Mungu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu Kristo alitoa hesabu nzuri kwa Baba yake wa kimbingu kujihusu mwenyewe

[Picha katika ukurasa wa 15]

Sawa na Dorkasi, leo wanawake Wakristo hutoa hesabu njema kwa Yehova Mungu kuhusu wao wenyewe

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 13]

Kifo cha Abeli/The Doré Bible Illustrations/Dover Publications, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki