Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 10/1 kur. 4-7
  • Je, Ndoto Zaweza Kutabiri Wakati Ujao?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Ndoto Zaweza Kutabiri Wakati Ujao?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ndoto Ambazo Hazitoki kwa Mungu
  • Yajaribu Madai
  • Je, Ndoto Ni Ujumbe Kutoka kwa Mungu?
    Amkeni!—2001
  • Ndoto
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Ndoto Kutoka kwa Mungu
    Amkeni!—2014
  • Ndoto Yenye Kusumbua Inayokuhusu Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 10/1 kur. 4-7

Je, Ndoto Zaweza Kutabiri Wakati Ujao?

TANGU nyakati za kale, wanadamu wamekuwa na upendezi mwingi katika ndoto. Wamisri walitayarisha vitabu vyenye maelezo mengi vya kufafanua ndoto, na Wababiloni walikuwa na wafafanuzi wao wa ndoto. Miongoni mwa Wagiriki desturi ilikuwa kuwafanya wagonjwa walale katika mahekalu ya Asclepius ili kupata maagizo juu ya afya katika ndoto zao. Katika karne ya pili ya Wakati wa Kawaida wetu, Artemidorus alitokeza kitabu ambacho katika hicho alitoa ufafanuzi wa mifano ya ndoto. Vitabu vingi vinavyofanana na hicho ambavyo vimetokezwa tangu wakati ule vimetegemea kitabu chake. Kufikia leo, jitihada zinafanywa ili kufafanua ndoto, lakini je, kweli zinatoa ufahamu wenye kina katika matukio ya wakati ujao?

Ili ziwe na umaana unaohusu wakati ujao, kani iliyo juu zaidi ingepaswa kuwa na uvutano juu yazo. Katika Biblia twapata visa vingi ambavyo katika hivyo Mungu aliandaa kani iyo hiyo. Aliwapa watumishi wake ndoto za kiunabii na pia watu fulani ambao hawakumwabudu. Kwa kweli, Ayubu 33:14-16 lasema hivi: “Mungu hunena . . . katika ndoto, katika maono ya usiku, usingizi mzito uwajiliapo watu, katika usingizi kitandani; ndipo huyafunua masikio ya watu.”

Mungu alifanya hivyo katika kisa cha Farao wa Misri katika siku za Yusufu, aliyeishi zaidi ya miaka 1,700 kabla ya Wakati wa Kawaida. Ndoto ya Farao inapatikana kwenye Mwanzo 41:1-7, na katika mstari wa 25 hadi wa 32, Yusufu aifafanua kuwa yenye kutabiri miaka saba ‘ya shibe katika nchi yote ya Misri’ ikifuatwa na miaka saba ya njaa kali. Yusufu alimwelezea Farao hivi: “Mungu amemwonyesha Farao atakayoyafanya.” (Mwanzo 41:28) Hiyo ndoto ilikuwa unabii wa yale yaliyotukia kikweli.

Mfalme mashuhuri wa Wababiloni alijionea jambo lilo hilo. Nebukadreza alikuwa na ndoto iliyomsumbua sana, lakini hakuweza kuikumbuka. Kwa hivyo aliwaita wachawi wake ili wamjulishe ile ndoto na ufafanuzi wayo. Hilo lilikuwa ombi wasiloweza kutimiza.—Danieli 2:1-11.

Kwa kuwa Mungu alikuwa amempa mfalme ile ndoto, Yeye alimwezesha nabii Danieli aifunue ndoto na ufafanuzi wayo. Danieli 2:19 lasema: “Ndipo Danieli alipofunuliwa siri hiyo katika njozi ya usiku.” Danieli alimpa Mungu sifa kwa ajili ya ndoto hiyo: “Ile siri aliyoiuliza mfalme, wenye hekima hawawezi kumfunulia mfalme; wala wachawi, wala waganga, wala wanajimu; lakini yuko Mungu mbinguni afunuaye siri, naye amemjulisha mfalme Nebukadreza mambo yatakayokuwa siku za mwisho.”—Danieli 2:27, 28.

Nyakati fulani Mungu aliwapa watu wake maagizo kupitia ndoto, na nyakati nyingine aliwapa uhakikishio wa upendeleo wa kimungu au aliwasaidia waelewe jinsi alivyokuwa akiwapa msaada. Katika kisa cha Yakobo, Mungu alifunua kibali chake kupitia ndoto.—Mwanzo 48:3, 4.

Yusufu, baba mlezi wa Yesu, alipogundua kwamba Mariamu alikuwa mja-mzito, aliamua kumtaliki. Ndipo akapata maagizo ndotoni asifanye hivyo. Mathayo 1:20 lasema: “Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu.” Baadaye akapokea onyo ndotoni: “Malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri.”—Mathayo 2:13.

Ndoto Ambazo Hazitoki kwa Mungu

Jambo la kwamba ufafanuzi wa ndoto ulikuwa wa kawaida miongoni mwa wale ambao hawakuwa watu wa Mungu laonyesha kwamba ndoto kwa ujumla haziwezi kuonwa kuwa funuo zenye kutegemeka za wakati ujao. Katika siku za Yeremia, nabii wa Mungu, manabii wasio wa kweli walikuwa wakisema: “Nimeota ndoto; nimeota ndoto.” (Yeremia 23:25) Walikuwa na nia ya kuwaongoza watu vibaya wakifikiri kwamba Mungu alikuwa akisema kupitia wao. Kuhusu waotaji-ndoto hao, Yeremia alipuliziwa kusema hivi: “BWANA wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Manabii walio kati yenu, na wabashiri wenu, wasiwadanganye ninyi, wala msisikilize ndoto zenu, mnazootesha. Kwa maana kwa jina langu hutabiri maneno ya uongo kwenu . . . asema BWANA.”—Yeremia 29:8, 9.

Kwa sababu manabii hao wasio wa kweli walikuwa “wabashiri [“wenye kuzoea uaguzi,” NW],” ndoto zao zingaliweza kuathiriwa na majeshi ya roho waovu kwa kusudi la kuwadanganya watu. Jambo lilo hilo laonyeshwa na yale yanayotaarifiwa kwenye Zekaria 10:2: “Vinyago vimenena maneno ya ubatili, nao waaguzi wameona uongo; nao wameleta habari za ndoto za uongo, wafariji bure.”

Ibilisi ndiye mdanganyi mkuu ambaye kwa maelfu ya miaka ametumia viongozi wa kidini kudai isivyo kweli kwamba Mungu amesema nao kupitia maono na ndoto, kama vile manabii wasio wa kweli walivyofanya katika siku za Yeremia na Zekaria. Kuhusu hao, Yuda, mwandikaji wa Biblia aliyepuliziwa, aliwaandikia Wakristo wa karne ya kwanza hivi: “Kuna watu waliojiingiza kwa siri, watu walioandikiwa tangu zamani hukumu hii, makafiri, wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi, nao humkana yeye aliye peke yake Mola, na Bwana wetu Yesu Kristo.” Alisema watu hao, walikuwa ‘wakiota,’ kwa kusema kitamathali.—Yuda 4, 8.

Yajaribu Madai

Huenda mtu akadai kwamba Mungu alisema naye katika ndoto au kwamba ndoto zake za matukio ya wakati ujao zilithibitika kuwa za kweli, hata hivyo hiyo si sababu ya kutosha ya kumwamini na kumfuata bila kufikiria kwanza. Ona maagizo walioandikiwa Waisraeli, yanayopatikana kwenye Kumbukumbu la Torati 13:1-3, 5: “Kukizuka katikati yako nabii, au mwotaji wa ndoto, akikutolea ishara au ajabu, ikatukia hiyo ishara au hiyo ajabu aliyokuambia akisema, Na tuifuate miungu mingine usiyoijua, tuitumikie hiyo; wewe usiyasikize maneno ya nabii yule, au yule mwotaji wa ndoto . . . Na yule nabii, au yule mwotaji wa ndoto, na auawe.” Mungu aliwaruhusu hao waseme isivyo kweli ukiwa mtihani wa uaminifu-mshikamanifu wa watu wake.

Badala ya kuamini bila kufikiria kwanza madai ya waotaji-ndoto wenye kuvutia watu, mwendo wenye hekima wa kufuatwa nasi ni kuyajaribu madai yao ili kuepuka kuongozwa vibaya na yule mdanganyi mkuu asiyeonekana, ‘anayeudanganya ulimwengu wote.’ (Ufunuo 12:9) Lakini yanaweza kujaribiwaje kwa njia ya kutegemeka?

Neno la Mungu lililoandikwa ndilo mwongozo tuliopewa kimungu wa kufikia kweli. Kuhusu hilo, Yesu Kristo alisema hivi: “Neno lako ndiyo kweli.” (Yohana 17:17) Kwa hiyo tunaonywa kwa upole hivi kwenye 1 Yohana 4:1: “Wapenzi, msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani.” Yanapolinganishwa kwa uangalifu na Biblia, madai yao, falsafa zao, na matendo yao yatapingana nalo. Neno la Mungu ndilo mamlaka kuhusu yaliyo kweli.

Je, mwotaji wa ndoto anayedai kuwa ana ujuzi wa pekee anatumia hasa uaguzi au mazoea mengine ya uasiliani-roho? Ikiwa ndivyo, analaumiwa na Neno la Mungu. “Asionekane kwako mtu . . . atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA.”—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

Akidai kuwa na nafsi isiyoweza kufa ndani yake, anapinga Neno la Mungu linalotaarifu hivi kwa wazi: “Roho [“nafsi,” NW] ile itendayo dhambi itakufa.” (Ezekieli 18:4) Je, anajitukuza na kuvuta wafuasi wa kibinafsi? Mathayo 23:12 huonya hivi: “Ye yote atakayejikweza, atadhiliwa.” Na Matendo 20:30 lawaonya Wakristo hivi: “Katika ninyi wenyewe watainuka watu wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.”

Je, yeye hushindania vitendo jeuri? Yakobo 3:17, 18 humlaumu: “Hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki. Na tunda la haki hupandwa katika amani na wale wafanyao amani.” Je, yeye hujaribu kupata mamlaka au uvutano wa kisiasa ulimwenguni? Neno la Mungu humshutumu kwa mkazo, likisema: “Kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu.” Hivyo Biblia hufunua yasiyo ya kweli.—Yakobo 4:4.

Mtu akiota ndoto juu ya kifo cha mshiriki wa familia au rafiki, labda ni kwa sababu amekuwa akimhangaikia mtu huyo. Jambo la kwamba huenda ikawa mtu huyo alikufa usiku uleule wa hiyo ndoto halithibitishi lenyewe kwamba ndoto hiyo ilikuwa ya kiunabii. Kwa kila ndoto ya aina hiyo inayoonekana kutimia, kuna mamia ambayo hayatimii.

Ingawa Mungu alitumia ndoto katika wakati uliopita ili kufunua matukio ya kiunabii na kutoa maagizo wakati ambapo Neno lake lililoandikwa lilikuwa likitokezwa, yeye hahitaji kufanya hivyo leo. Neno hilo lililoandikwa lina maagizo yote kutoka kwa Mungu ambayo wanadamu wanahitaji kwa wakati huu, na unabii walo mbalimbali huhusu matukio ya zaidi ya miaka elfu moja katika wakati ujao. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa hiyo twaweza kuwa na uhakika kwamba ndoto zetu si ishara kutoka kwa Mungu juu ya wakati ujao lakini ni utendaji mbalimbali wa lazima wa ubongo ili kudumisha hali njema yetu ya akilini.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Sawa na vile ndoto ya Farao ilivyoonyesha mambo yaliyotazamiwa kuja, Neno la Mungu huelimisha juu ya wakati ujao wetu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki