Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 11/1 kur. 3-6
  • Faraja kwa Walioonewa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Faraja kwa Walioonewa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mchunguzi wa Kale wa Uonevu
  • Uonevu Utaisha Karibuni
  • Mtu Fulani Anajali Kikweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Wafariji Wale Wanaohuzunika
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Faraja ya Kweli Inaweza Kupatikana Wapi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Ni Nani Anayeweza Kuwakomboa Wale Wanaolilia Msaada?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 11/1 kur. 3-6

Faraja kwa Walioonewa

JE, UMEONA kwamba maishani mwako mwote maneno fulani yamerudiwa tena na tena katika vichwa vya habari? Je, umechoka kusoma maneno kama vita, uhalifu, msiba, njaa, na kuteseka? Ingawa hivyo, neno moja limekosekana kwa wazi katika ripoti za habari. Hata hivyo, ni neno linalowakilisha kitu ambacho wanadamu wanahitaji sana. Neno hilo ni “faraja.”

“Kufariji” kwamaanisha “kutolea nguvu na tumaini” na “kupunguza huzuni au taabu za” mtu. Kukiwa na msukosuko wote huo ambao ulimwengu umepitia katika karne ya 20, tumaini na kupunguzwa kwa huzuni kwahitajiwa sana. Ni kweli kwamba, wengine wetu leo hufurahia starehe ambazo wazazi wetu wa kale hata hawakuwazia zingewezekana. Kwa kiasi kikubwa hilo ni kwa sababu ya maendeleo ya kisayansi. Lakini sayansi na tekinolojia hazitufariji katika maana ya kuondolea wanadamu visababishi vyote vya kuteseka. Visababishi hivyo ni vipi?

Karne nyingi zilizopita mwanadamu mwenye hekima Sulemani alisema juu ya kisababishi kimoja cha msingi cha kuteseka aliposema hivi: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Mhubiri 8:9, Union Version ya Kiswahili, chapa ya 1952) Sayansi na tekinolojia haziwezi kubadili mwelekeo wa mwanadamu wa kutaka kuwa na mamlaka juu ya mwenziwe. Katika karne ya 20, hilo limeongoza kwenye udikteta mbalimbali wenye kuonea katika nchi mbalimbali na pia kwenye vita vyenye kuogofya kati ya nchi mbalimbali.

Tangu 1914 watu zaidi ya milioni mia moja wameuawa likiwa tokeo la vita. Fikiria maumivu makali ya kibinadamu ambayo tarakimu hii yawakilisha—mamilioni ya familia zenye kuomboleza zikihitaji faraja. Vita navyo huongoza kwenye aina nyingine za kuteseka zaidi ya kifo chenye jeuri. Mwishoni mwa vita ya ulimwengu ya pili, katika Ulaya kulikuwa na wakimbizi zaidi ya milioni 12. Katika miaka ya juzijuzi, watu zaidi ya milioni moja na nusu walikimbia maeneo ya vita katika Asia Kusini-Mashariki. Vita katika Balkani vimewalazimu watu zaidi ya milioni mbili kutoroka nyumbani kwao—katika visa vingi ili kuepuka “utakasaji wa kikabila.”

Kwa hakika wakimbizi wanahitaji faraja, hasa wale wanaolazimika kuhama nyumbani kwao wakiwa tu na vitu wawezavyo kubeba, bila kujua pa kwenda wala yatakayowapata wao na familia zao wakati ujao. Watu hao wamo miongoni mwa wahasiriwa wa uonevu wastahilio kusikitikiwa zaidi sana; wanahitaji faraja.

Katika sehemu zenye amani zaidi za dunia, mamilioni ya watu wanaishi katika hali inayokaribia ile ya utumwa kwa mfumo wa kiuchumi wa ulimwengu. Ni kweli kwamba watu fulani wana vitu vingi vya kimwili. Ingawa hivyo, walio wengi hukabili jitihada za kila siku za kujiruzuku. Wengi wanatafuta nyumba zinazofaa. Idadi inayoongezeka ya watu hawana kazi za kuajiriwa. “Ulimwengu,” latabiri gazeti la Kiafrika, “unaelekea kwenye tatizo la ukosefu wa kazi ya kuajiriwa usio na kifani, kukiwa na watu wanaozidi bilioni 1.3 wakitafuta kazi kufikia mwaka wa 2020.” Kwa hakika walioonewa kiuchumi wanahitaji “nguvu na tumaini”—faraja.

Kwa sababu ya hali zenye kutamausha, watu fulani hugeukia maisha ya uhalifu. Bila shaka, hilo hutokeza ugumu tu kwa wahasiriwa wao, na viwango vya juu vya uhalifu huongezea ule uonevu. Kichwa cha habari cha juzijuzi katika The Star, gazeti la habari la Johannesburg, Afrika Kusini, chasomeka hivi: “Siku moja katika ‘nchi yenye uuaji-kimakusudi mwingi zaidi ulimwenguni.’” Makala hiyo ilifafanua siku halisi katika na kuzunguka Johannesburg. Katika siku hiyo moja, watu wanne waliuawa kimakusudi na magari ya watu wanane yakaibiwa. Visa 17 vya wizi vya kuvunja nyumba viliripotiwa katika kiunga kimoja. Zaidi ya hayo, kulikuwa na visa kadhaa vya wizi vya kutumia silaha. Kulingana na gazeti hilo la habari, polisi walifafanua siku hiyo kuwa “yenye utulivu kwa kulinganishwa.” Kwa kueleweka, wale watu wa jamaa ya wahasiriwa wa uuaji-kimakusudi na wale waliovunjiwa nyumba zao na ambao magari yao yaliibiwa wahisi wameonewa sana. Wanahitaji uhakikishio na tumaini—faraja.

Katika nchi fulani, kuna wazazi wanaowauza watoto wao katika umalaya. Nchi moja ya Asia ambako watalii wanamiminikia “utalii wa kutafuta wenzi wa ngono,” yaripotiwa kwamba ina makahaba milioni mbili, ambao wengi wao walinunuliwa au kutoroshwa wakiwa watoto. Je, kuna wowote walioonewa kuliko wahasiriwa hao wastahilio kusikitikiwa? Likizungumzia biashara hiyo mbovu, gazeti Time liliripoti juu ya mkutano wa 1991 wa mashirika ya wanawake wa Asia Kusini-Mashariki. Humo, ilikadiriwa kwamba “wanawake milioni 30 walikuwa wameuzwa ulimwenguni pote tangu miaka ya katikati ya 1970.”

Bila shaka, si lazima watoto wauzwe katika umalaya ili wahasiriwe. Idadi inayoongezeka ya watoto wanatendwa vibaya au hata kubakwa na wazazi na watu wa ukoo wakiwa nyumbani mwao wenyewe. Huenda watoto hao wakawa na makovu ya kihisia-moyo kwa muda mrefu. Bila shaka, wakiwa wahasiriwa wa uonevu kwa njia yenye kuhuzunisha, wao wanahitaji faraja.

Mchunguzi wa Kale wa Uonevu

Mfalme Sulemani alichukizwa na kiwango cha uonevu wa kibinadamu. Yeye aliandika hivi: “Kisha nikarudi na kuona madhalimu yote yanayotendeka chini ya jua; na tazama, machozi yao waliodhulumiwa, ambao walikuwa hawana mfariji; na upande wa wale waliowadhulumu kulikuwa na uwezo, walakini wale walikuwa hawana mfariji.”—Mhubiri 4:1.

Ikiwa mfalme huyo mwenye hekima alitambua miaka 3,000 iliyopita kwamba walioonewa walihitaji sana mfariji, yeye angesema nini leo? Hata hivyo, Sulemani alijua kwamba hakuna mwanadamu asiye mkamilifu, kutia ndani yeye, angeweza kuandaa faraja inayohitajiwa na wanadamu. Mtu mkuu zaidi alihitajiwa ili kufutilia mbali nguvu za waonevu. Je, kuna mtu kama huyo?

Katika Biblia, Zaburi 72 husema juu ya mfariji mtukufu wa watu wote. Zaburi hiyo iliandikwa na baba ya Sulemani, Mfalme Daudi. Maandishi yayo ya utangulizi yasomeka hivi: “Kuhusu Sulemani.” (NW) Yaonekana, iliandikwa na Mfalme Daudi aliyezeeka kuhusu Yule ambaye angekirithi kiti chake cha ufalme. Huyo, kulingana na hiyo zaburi, angeleta kitulizo cha kudumu kutoka katika uonevu. “Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma. Na awe na enzi toka bahari hata bahari, . . . hata miisho ya dunia.”—Zaburi 72:7, 8.

Yamkini, Daudi alipoandika maneno hayo, alikuwa akimfikiria mwana wake Sulemani. Lakini Sulemani alitambua kuwa asingeweza kuwatumikia wanadamu kwa njia iliyofafanuliwa katika hiyo zaburi. Angeweza kutimiza maneno ya hiyo zaburi kwa njia ndogo tu na kwa niaba ya taifa la Israeli, wala si kwa faida ya dunia nzima. Yaonekana, zaburi hiyo ya kiunabii iliyopuliziwa ilielekezea mtu mkubwa zaidi kuliko Sulemani. Huyo alikuwa nani? Angeweza tu kuwa Yesu Kristo.

Malaika alipotangaza kuzaliwa kwa Yesu, alisema hivi: “Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake.” (Luka 1:32) Tena, Yesu alijirejezea kuwa “mkubwa kuliko Sulemani.” (Luka 11:31) Tangu ufufuo wa Yesu kwenye mkono wa kuume wa Mungu, amekuwa mbinguni, mahali ambapo akiwa hapo aweza kutimiza maneno ya Zaburi 72. Zaidi, amepokea nguvu na mamlaka kutoka kwa Mungu ya kuvunja nira ya wanadamu waonevu. (Zaburi 2:7-9; Danieli 2:44) Kwa hiyo Yesu ndiye atakayetimiza maneno ya Zaburi 72.

Uonevu Utaisha Karibuni

Hilo lamaanisha nini? Lamaanisha kwamba uhuru huo kutoka katika aina zote za uonevu wa kibinadamu karibuni utakuwa uhalisi. Kuteseka na uonevu usio na kifani uonwao katika karne hii ya 20 ulitabiriwa na Yesu ukiwa sehemu ya ishara ambayo ingetia alama “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, NW) Miongoni mwa mambo mengine, alitabiriwa hivi: “Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Sehemu hiyo ya unabii ilianza utimizo wayo karibu na wakati ambapo vita ya ulimwengu ya kwanza ilipozuka katika 1914. “Kwa sababu ya kuongezeka maasi,” Yesu akaongeza, “upendo wa wengi utapoa.” (Mathayo 24:12) Maasi na ukosefu wa upendo umetokeza kizazi kiovu na chenye uonevu. Basi, wakati wa Yesu Kristo wa kuingilia mambo akiwa Mfalme mpya wa dunia lazima uwe ni karibu. (Mathayo 24:32-34) Hilo litamaanisha nini kwa wanadamu walioonewa ambao wana imani katika Yesu Kristo na wamtegemeao akiwa Mfariji wa wanadamu aliyewekwa rasmi kimungu?

Ili kupata jibu la swali hilo, acheni tusome maneno haya ya ziada ya Zaburi 72 ambayo yatatimizwa katika Kristo Yesu: “Atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.” (Zaburi 72:12-14) Hivyo Mfalme aliyewekwa rasmi wa Mungu, Yesu Kristo, atahakikisha kwamba hakuna atesekaye kwa sababu ya uonevu. Yeye ana nguvu za kumaliza aina zote za ukosefu wa haki.

‘Hilo lasikika kuwa lenye kupendeza,’ huenda mtu akasema, ‘lakini namna gani sasa? Kuna faraja gani kwa wale wanaoteseka sasa?’ Kwa kweli, kuna faraja kwa walioonewa. Makala mbili zifuatazo katika gazeti hili zitaonyesha jinsi mamilioni ya watu tayari wanapata faraja kupitia kukuza uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wa kweli, Yehova, na pamoja na Mwana wake mpendwa, Yesu Kristo. Uhusiano huo waweza kutufariji katika nyakati hizi zenye uonevu na waweza kumwongoza mtu kwenye uhai udumuo milele usio na uonevu. Yesu alisema hivi katika sala kwa Mungu: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Hakuna binadamu atakayemwonea mwingine katika ulimwengu mpya wa Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki