Mtu Fulani Anajali Kikweli
MAELFU ya watu huonyesha kwamba wanajali kikweli. Hawana maoni ya kutojali na ya kibinafsi kwamba matatizo ya wengine hayawahusu. Badala yake, wao hufanya yote wawezayo—wakati mwingine hata wakihatarisha maisha yao wenyewe—ili kupunguza kuteseka. Hiyo ni kazi kubwa mno, inayofanywa iwe ngumu na uvutano wenye nguvu wasioweza kuudhibiti.
Mambo kama pupa, njama za kisiasa, vita, na misiba ya kiasili yaweza kuzuia hata “jitihada za kitaalamu na za kudhamiria zaidi za kukomesha njaa,” asema mfanya-kazi mmoja wa kutoa misaada. Kukomesha njaa ni mojawapo tu ya matatizo mengi ambayo watu wanaojali wanapambana nayo. Wanapambana pia na matatizo kama maradhi, umaskini, ukosefu wa haki, na kuteseka kwingi mno kunakosababishwa na vita. Lakini je, wanafanikiwa?
Mkuu wa shirika moja la kutoa misaada alisema kwamba wale wanaofanya “jitihada [hizo] za kitaalamu na za kudhamiria” ili kupunguza njaa na kuteseka, ni kama yule Msamaria mwenye huruma aliyefafanuliwa na Yesu Kristo katika kielezi chake. (Luka 10:29-37) Hata wafanye nini, yeye akasema, idadi ya wahasiriwa inazidi kuongezeka. Hivyo akauliza: “Yule Msamaria mwema apaswa kufanya nini akisafiri barabara ileile kila siku kwa miaka kadhaa, na kila juma akuta mtu tofauti aliyepokonywa kando ya barabara?”
Ingekuwa rahisi kupatwa na kile ambacho kimefafanuliwa kuwa ‘hali mbaya ya uchovu wa wafadhili’ na kutosaidia kwa kuvunjika moyo. Ni jambo lenye kusifika kwamba wale wanaojali kikweli hawafi moyo kamwe. (Wagalatia 6:9, 10) Kwa mfano, mwanamume aliyeliandikia gazeti la Jewish Telegraph la Uingereza aliwasifu Mashahidi wa Yehova, ambao wakati wa Ujerumani ya Nazi “waliwasaidia maelfu ya Wayahudi kuokoka mateso ya Auschwitz.” “Chakula kilipokuwa haba,” mwandishi huyo akasema, “waligawana mikate yao na ndugu na dada zetu [Wayahudi]!” Mashahidi waliendelea kufanya waliyoweza kwa vitu walivyokuwa navyo.
Hata hivyo, ukweli ni kwamba hakuna kugawana kwokwote kwa mikate kuwezako kukomesha kabisa kuteseka kwa wanadamu. Hilo halikusudiwi kudunisha yale ambayo watu wenye huruma wamefanya. Tendo lolote ambalo hasa lapunguza kuteseka lafaa. Mashahidi hao walipunguza mateso ya wafungwa wenzao kwa kadiri fulani, na hatimaye Unazi ukaangamizwa. Hata hivyo, mfumo wa ulimwengu unaosababisha uonevu huo ungali upo, nao watu wasiojali wangali wengi. Kwa kweli, “kuna kizazi cha watu ambao meno yao ni panga; na vigego vyao ni kama visu. Ili kuwala maskini waondolewe katika nchi, na wahitaji katika wanadamu.” (Mithali 30:14) Yaelekea unajiuliza ni kwa nini hali iko hivyo.
Kwa Nini Kuna Umaskini na Uonevu?
Yesu Kristo alisema hivi wakati mmoja: “Sikuzote mna maskini pamoja nanyi, na wakati wowote ule mtakapo mwaweza sikuzote kuwafanyia mema.” (Marko 14:7) Je, Yesu alimaanisha kwamba umaskini na uonevu haungekoma kamwe? Kama watu wengine wanavyoamini, je, yeye aliamini kwamba kuteseka huko ni sehemu ya mpango wa Mungu wa kuwapa wenye huruma fursa ya kuonyesha kadiri wanavyojali? La! Yesu hakuamini hivyo. Yeye alikuwa tu akitoa hoja kwamba umaskini ungekuwa sehemu ya maisha maadamu mfumo huu wa mambo upo. Lakini Yesu pia alijua jambo hili: Halikuwa kusudi la awali la Baba yake wa kimbingu kuwepo na hali kama hizo duniani.
Yehova Mungu aliiumba dunia iwe paradiso, si mahali palipojaa umaskini, ukosefu wa haki, na uonevu. Alionyesha jinsi alivyojali familia ya kibinadamu kwa kuwafanyia maandalizi ya ajabu ambayo yangefanya maisha yawe yenye furaha zaidi. Fikiria jina lenyewe la bustani hiyo ambamo wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walijikuta! Iliitwa Edeni, yaani, “Raha.” (Mwanzo 2:8, 9) Yehova hakuwaandalia wanadamu mahitaji muhimu tu ili waendelee kuishi katika mazingira yasiyo na furaha, yenye uonevu. Alipomaliza kazi yake ya uumbaji, Yehova alichunguza alichoumba na kutangaza kwamba kilikuwa “chema sana.”—Mwanzo 1:31.
Hivyo basi, kwa nini umaskini, uonevu, na visababishi vingine vya kuteseka vimeenea ulimwenguni pote leo? Mfumo mwovu wa mambo upo kwa sababu wazazi wetu wa kwanza waliamua kumwasi Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Jambo hilo lilizusha suala la kama Mungu ana haki ya kudai utii kutoka kwa viumbe wake. Hivyo, Yehova amewapa wazao wa Adamu uhuru wa muda mfupi. Mungu bado alijali kilichoipata familia ya kibinadamu. Alifanya maandalizi ili kubatilisha madhara yote ambayo yangetokezwa na uasi dhidi yake. Na karibuni sana, Yehova atakomesha umaskini na uonevu—kwa kweli, kuteseka kwote.—Waefeso 1:8-10.
Tatizo Lisiloweza Kutatuliwa na Wanadamu
Kwa karne nyingi tangu kuumbwa kwa mwanadamu, wanadamu wameendelea kuvikataa viwango vya Yehova. (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Kwa kuendelea kuzikataa sheria na kanuni za Mungu, wanadamu wamepigana, naye ‘mwanadamu amekuwa na mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9, Chapa ya 1989) Jitihada zote za kutokeza jamii yenye haki kikweli, ambayo haipatwi na mambo yanayoukumba umma unaoteseka, zimezuiwa na ubinafsi wa wale wanaotaka kufanya mambo kwa njia yao badala ya kujinyenyekeza chini ya enzi kuu ya Mungu.
Kuna tatizo jingine—moja ambalo huenda wengi wakalikatalia mbali kuwa upuuzi wa kishirikina. Mchochezi wa uasi dhidi ya Mungu angali anachochea watu wafanye maovu na kuwa na ubinafsi. Yeye ni Shetani Ibilisi, naye Yesu Kristo alimwita “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 14:30; 2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19) Katika ufunuo aliopewa mtume Yohana, Shetani atambulishwa kuwa chanzo kikuu cha ole—yule “anayeiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.”—Ufunuo 12:9-12.
Hata iwe watu wengine wanawajali wanadamu wenzao kadiri gani, hawataweza kumwondoa Shetani Ibilisi au kubadili mfumo huu unaofanya idadi ya wahasiriwa iongezeke daima. Hivyo basi, ni nini kinachohitajiwa ili kutatua matatizo ya wanadamu? Utatuzi si kuwa tu na mtu anayejali. Kuna uhitaji wa kuwa na mtu fulani mwenye nia na uwezo wa kumwondosha Shetani na mfumo wake wote usio wa haki.
“Mapenzi Yako na Yatendeke . . . juu ya Dunia”
Mungu aahidi kuharibu mfumo huu mwovu wa mambo. Yeye ana nia na uwezo unaohitajiwa kufanya hivyo. (Zaburi 147:5, 6; Isaya 40:25-31) Inatabiriwa hivi katika kitabu cha Biblia cha unabii cha Danieli: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele”—naam, milele. (Danieli 2:44) Yesu Kristo alikuwa akifikiria ufalme huo wa kimbingu, wenye manufaa na wenye kudumu, alipowafundisha wanafunzi wake kuomba Mungu hivi katika sala: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:9, 10.
Yehova atajibu sala hizo kwa kuwa yeye huijali kikweli familia ya kibinadamu. Kulingana na maneno ya kiunabii ya Zaburi 72, Mungu atamwidhinisha Mwana wake, Yesu Kristo, kuwaletea kitulizo chenye kudumu walio maskini, wanaoteseka, na wanaoonewa ambao huunga mkono utawala wa Yesu. Hivyo, mtunga-zaburi mwenye kupuliziwa aliimba hivi: “[Mfalme wa Kimesiya wa Mungu] atawahukumu walioonewa wa watu, atawaokoa wahitaji, atamseta mwenye kuonea. . . . atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.”—Zaburi 72:4, 12-14.
Katika ono linalohusu wakati wetu mtume Yohana aliona “mbingu mpya na dunia mpya,” mfumo wa mambo mpya kabisa ulioanzishwa na Mungu. Ni baraka iliyoje kwa wanadamu wenye kuteseka! Akitabiri yale ambayo Yehova angefanya, Yohana aliandika: “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’ Na Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’ Pia, husema: ‘Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’”—Ufunuo 21:1-5.
Ndiyo, twaweza kuamini maneno hayo, kwa kuwa ni ya uaminifu na ya kweli. Karibuni Yehova atachukua hatua ya kuondoa umaskini, njaa, uonevu, magonjwa, na ukosefu wote wa haki katika dunia. Kama ambavyo gazeti hili limeonyesha mara nyingi kutoka katika Maandiko, uthibitisho mwingi waonyesha kwamba tunaishi wakati ambapo ahadi hizi zitatimizwa. Ulimwengu mpya ulioahidiwa wa Mungu u karibu! (2 Petro 3:13) Karibuni, Yehova ‘atameza mauti hata milele’ na “atafuta machozi katika nyuso zote.”—Isaya 25:8.
Hadi mambo hayo yatukie, twaweza kufurahi kwamba hata sasa kuna watu wanaojali kikweli. Sababu kubwa zaidi ya kufurahi ni kwamba Yehova Mungu mwenyewe anajali kikweli. Karibuni ataondosha uonevu na kuteseka.
Unaweza kutumaini kabisa ahadi za Yehova. Mtumishi wake Yoshua alifanya hivyo. Kwa uhakika kabisa, aliwaambia hivi watu wa kale wa Mungu: “Nanyi nyote mnajua mioyoni mwenu, na rohoni mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena BWANA, Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu hapana neno lo lote mlilopungukiwa.” (Yoshua 23:14) Kwa hiyo, mfumo wa mambo wa sasa udumupo, usiache majaribu ambayo huenda ukakabili yakushinde. Mtwike Yehova hangaiko lako lote, kwa kuwa yeye anajali kikweli.—1 Petro 5:7.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Katika ulimwengu mpya ulioahidiwa wa Mungu, dunia haitakuwa na umaskini, uonevu, magonjwa, wala ukosefu wa haki