Mwisho wa Umaskini Wakaribia
YESU alimaanisha nini aliposema: “Kwa maana sikuzote mna maskini pamoja nanyi”? (Mathayo 26:11) Je, alimaanisha kwamba umaskini ungekuwapo milele, bila utatuzi wowote?
Yesu alijua kwamba maadamu mfumo wa sasa wa utawala wa kibinadamu utaendelea kuwapo, umaskini ungekuwako. Alijua kwamba haungeondolewa daima na aina yoyote ya serikali ya kibinadamu au mfumo wowote wa kiuchumi au wa kijamii. Na rekodi ya historia huthibitisha jambo hili.
Kotekote katika maelfu ya miaka ya historia ya kibinadamu, kila aina ya serikali na kila aina ya mfumo wa kiuchumi na kijamii imejaribiwa, na bado umaskini ungaliko. Kwa kweli, licha ya maendeleo katika maeneo kama vile sayansi, viwanda, na dawa, ukweli usioweza kukanushika ni kwamba tufeni pote idadi ya watu walionaswa na umaskini inazidi kuongezeka.
Yesu alijua vema kabisa sababu nyingi ambazo zingetokeza umaskini, kama vile njaa kali, ukame, uvamizi wa majeshi ya maadui, serikali mbaya, uchumi usiosimamiwa vizuri, matajiri na wenye mamlaka kuwaonea maskini na wanyonge, aksidenti na ugonjwa, na vifo vya waume ambao huwaacha yatima na wajane maskini. Zaidi ya hayo, alijua kwamba watu wangejiletea wenyewe na familia zao umaskini kupitia mazoea mabaya kama vile uvivu, ulevi, kucheza kamari, na uraibu wa dawa za kulevya.
Kwa hiyo Yesu aliposema kwamba “sikuzote mna maskini pamoja nanyi,” alimaanisha kwamba ulipita uwezo wa shirika lolote la ulimwengu la kuondoa umaskini. Alimaanisha kwamba maadamu mfumo wa sasa wa utawala wa kibinadamu ungaliko, kungekuwako na watu maskini.
Ingawa tatizo la umaskini ni la kale, hatupaswi kukata kauli kwamba ama Yesu ama Baba yake wa kimbingu hawawajali maskini. Wala hatupaswi kukata kauli kutokana na maneno ya Yesu kwamba umaskini hautaisha kamwe. Jambo hili ni dhahiri kutokana na inayosema Biblia kuhusiana na habari hii.
Umaskini na Sheria ya Kimusa
Kwa kielelezo, fikiria Sheria ambayo Mungu aliwapa taifa la kale la Israeli kupitia Musa. Uandalizi mmoja wa Sheria ulikuwa kwamba kila familia ya Israeli ilipewa urithi wa shamba katika Kanaani. (Kumbukumbu la Torati 11:8-15; 19:14) Ni Walawi pekee ambao hawakupokea fungu lolote. Badala yake, kwa sababu ya kazi yao ya kipekee kwenye hekalu, walitegemezwa kwa kupokea sehemu ya kumi ya mazao ya nchi.—Hesabu 18:20, 21, 24.
Zaidi ya hayo, sheria za urithi chini ya Sheria ya Kimusa zilihakikisha kwamba shamba lingeendelea kuwa la familia au kabila ambayo ilikuwa imeipokea hapo mwanzoni. (Hesabu 27:8-11) Hata ikiwa mtu aliuza shamba lake, lingekuwa la mmilikaji mpya kwa muda tu. Baada ya muda shamba hilo lingerudishwa kwa familia iliyoliuza.
Kwa wale waliokuwa maskini kwa sababu mbalimbali, kama vile kutotunza vizuri shamba lao au kufuja mali zao, Sheria ilihakikisha kwamba wao wangeweza kuokota masazo ya chakula katika mashamba ya wengine, mashamba ya matunda, na mashamba ya mizabibu. (Mambo ya Walawi 23:22) Zaidi ya hayo, Mwisraeli aliyekuwa na uhitaji angeweza kuazima pesa bila kulazimika kulipa riba. Kwa kweli, maskini walipaswa kuonyeshwa roho ya ukarimu.—Kutoka 22:25.
Yesu Aliwajali Maskini
Karne kadhaa baadaye wakati Yesu alipokuja duniani, aliendelea kuonyesha roho ya ukarimu ambayo alijifunza kutoka kwa Baba yake, Yehova. Yesu alionyesha upendezi wa kibinafsi kwa wale waliokuwa maskini kimwili. Yeye pamoja na wanafunzi wake walikuwa na hazina ya pamoja ambayo walitumia kutoa msaada kwa Waisraeli wenye uhitaji.—Yohana 12:5-8.
Baada ya Yesu kuuawa, Wakristo waliwaonyesha maskini hangaiko hilohilo walipoandaa msaada wa kimwili hasa kwa ndugu na dada zao wa kiroho waliokuwa maskini zaidi. (Waroma 15:26) Wakristo wa kweli leo huonyesha hangaiko lilelile la upendo kwa mmoja na mwenzake.
Bila shaka, Biblia, huku ikionyesha huruma kwa ajili ya wahasiriwa wa hali zenye uonevu, hukaripia wale ambao, kwa kweli, ‘wanakula nyama yao wenyewe’ kwa sababu ya kuwa wavivu. (Muhubiri 4:1, 5, Zaire Swahili Bible) Mtume Paulo aliandika: “Ikiwa yeyote hataki kufanya kazi, wala msimwache ale.” (2 Wathesalonike 3:10) Vivyo hivyo, wale wanaofuja pesa kwa mazoea kama vile dawa za kulevya, tumbaku, au uraibu wa alkoholi waweza kujipata katika umaskini. Hili ni tokeo la matendo yao mabaya; kwa kweli ‘wanavuna walilopanda.’—Wagalatia 6:7.
Usalama Sasa
Biblia huonyesha kwamba Mungu huwaonyesha upendezi wa pekee wale wanaojitahidi kufanya mapenzi yake. Mathalani, kwenye Zaburi 37:25, Daudi ataarifu: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa wala mzao wake akiomba chakula.” Wale walio na mwelekeo mwadilifu hawaahidiwi utajiri, bali linaloonyeshwa hapa ni kwamba Mungu angehakikisha kwamba wana maandalizi ya kimwili ya kutosha ili kuwaendeleza. Na mstari wa 28 wa Zaburi hiyohiyo wataarifu: “BWANA hupenda haki, wala hawaachi watauwa wake.”
Yesu alifanya zaidi ya kuonyesha hangaiko kwa walio maskini kwa kuwasaidia kimwili wakati wa huduma yake duniani. Aliwahakikishia kwamba maadamu walijaribu kufanya mapenzi ya Mungu, Mungu angehakikisha kwamba angalau wangepata mahitaji yao ya msingi, wakati wa sasa na wakati ujao. Yesu alisema yafuatayo:
“Waangalieni kwa mkazo ndege wa mbinguni, kwa sababu hawapandi mbegu au kuvuna au kukusanya ghalani; na bado Baba yenu wa kimbingu huwalisha wao. Je, nyinyi si bora kuliko wao? . . . Pia, katika lile jambo la mavazi, kwa nini mwahangaika? Twaeni somo kutokana na mayungiyungi ya shamba, jinsi yanavyokua; hayamenyeki kwa kazi, wala hayasokoti; lakini nawaambia nyinyi kwamba hata Solomoni katika utukufu wake wote hakupambwa kama moja la haya. Basi, ikiwa Mungu huvisha hivyo mimea ya shambani, ambayo ipo hapa leo na kesho hutupwa ndani ya joko, je, si afadhali zaidi sana yeye atawavisha nyinyi, nyinyi wenye imani kidogo? Kwa hiyo msihangaike kamwe na kusema, ‘Tule nini?’ au, ‘Tunywe nini?’ au, ‘Tuvae nini?’ . . . Kwa maana Baba yenu wa kimbingu ajua mwahitaji vitu hivi vyote.”—Mathayo 6:26-32.
Yesu alimalizia kwa kuwahimiza wafuasi wake: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme [wa Mungu] na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.” (Mathayo 6:33) Ni kitia-moyo kilichoje kwa wale walio maskini lakini ambao hutafuta kufanya mapenzi ya Mungu! Angalia, pia, kwamba Yesu alionyesha kwamba Ufalme wa Mungu ulipaswa kuwa jambo la maana zaidi maishani mwa wafuasi wake. Yesu alijua kwamba wakati Ufalme wa kimbingu wa Mungu ungechukua mamlaka kamili juu ya dunia nzima, ndipo—na ni wakati huo tu—umaskini ungeondolewa.
Hauko Pamoja Nasi Milele
Hivyo, Yesu alitoa tumaini zuri ajabu kwa wakati ujao. Kwa hiyo aliposema “sikuzote mna maskini pamoja nanyi,” alikuwa akirejezea kwenye maisha chini ya mfumo wa sasa wa utawala wa kibinadamu. Hakuwa akirejezea kwenye uhai katika wakati ujao chini ya utawala wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu. Biblia hutabiri: “Maana mhitaji hatasahauliwa daima; matumaini ya wanyonge hayatapotea milele.” (Zaburi 9:18) Na akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Kristo Yesu hatamvumilia yeyote atakayejaribu kuwatumia wengine vibaya na kuwaonea.
Yesu alifanya utawala wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu kuwa kichwa kikuu cha mafundisho yake. (Mathayo 4:17) Chini ya utawala wa Ufalme, hali duniani zitakuwa kama, au zitafanana, na hali mbinguni. Ndiyo sababu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi kwa Mungu: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:10.
Hilo litatukia jinsi gani? Ni kusudi la Mungu kuondoa mfumo mzima wa sasa wa utawala wa kibinadamu kutoka duniani na mahali pake pachukuliwe na Ufalme wake wa kimbingu. Unabii katika Danieli 2:44 hutaarifu: “Katika siku za wafalme hao [walioko sasa] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake [hakuna utawala wa kibinadamu tena]; bali utavunja falme hizi zote [za wakati huu] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”
Kisha, katika ulimwengu mpya chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, dunia nzima itageuzwa kuwa paradiso yenye wingi, bila alama zozote za umaskini. Angalia baadhi ya unabii wa Biblia kuhusu hali zitakazokuwako wakati huo:
“BWANA wa majeshi atawafanyia mataifa yote . . . karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta.” (Isaya 25:6) “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.” (Zaburi 72:16) “Yatakuwako manyunyu ya baraka. Na mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake, nao watakuwa salama katika nchi yao.” (Ezekieli 34:26, 27) “Nchi imetoa mazao yake MUNGU, Mungu wetu, ametubariki.” (Zaburi 67:6) “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi.”—Isaya 35:1.
Zaidi ya hayo, Mika 4:4 huahidi: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.” Wote watakuwa na nyumba zao: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake . . . Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake.” (Isaya 65:21, 22) Si ajabu kwamba Yesu angewaahidi wale walioamini mafundisho yake: ‘Mtakuwa pamoja na mimi katika Paradiso’!—Luka 23:43.
Ndiyo, neno lililopuliziwa la Mungu mwenyewe hufundisha waziwazi kwamba kutakuwa na mwisho kamili wa umaskini. Na wakati huo wakaribia, kwani unabii wa Biblia huonyesha kwamba sasa ulimwengu uko katika “siku [zake] za mwisho,” ukipatwa na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5, 13) Karibuni mfumo wa mambo wa sasa utaondolewa milele na umaskini utaondolewa daima—si kwa jitihada za kibinadamu bali kupitia uingiliaji wa kimungu. Yule Mfalme Yesu Kristo “atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.”—Zaburi 72:12, 13.
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Katika ulimwengu mpya wa Mungu, kutakuwa na makao mazuri na chakula tele kwa wote
[Picha katika ukurasa wa 10]
Katika ulimwengu mpya, hakutakuwako watoto wenye njaa kamwe