Umaskini Unaoongezeka—Tisho kwa Wote
WAKATI habari ya umaskini unaoongezeka inapotokea, mtu ataelekea kutaja maneno ya Yesu Kristo: “Maskini mnao sikuzote pamoja nanyi.”—Yohana 12:8.
Yesu alikuwa na maana gani? Je! alikuwa akisema kwamba Mungu haangalii maskini? Na je! hawana tumaini, dawa?
Tatizo la umaskini wa ulimwengu limeongezeka likawa tisho kubwa zaidi hata watu walipokuwa wakijaribu kulitatua. Kwa upande mwingine, mapato ya mataifa mengi yaliongezeka miaka ya karibuni. Wakati wa miaka ya 1960 taifa moja la Amerika ya Kusini liliongeza mapato yake yakawa zaidi kwa wastani ya persenti ya 3.1 kwa mwaka kwa kila mtu. Matajiri waliendelea vizuri. Lakini wakati uo huo persenti 40 ya watu walio maskini zaidi walipungukiwa na mapato. Jambo ilo hilo lilionekana katika nchi nyingine.
Hivyo, kujapokuwa na mipango ya kiserikali, maneno ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Kurt Waldheim yanaonyesha tisho la umaskini halijapungua. Anasema hivi: “Jambo lenye kuharibu zaidi la utamaduni wetu wa karibuni wa ulimwengu ni umaskini mwingi kabisa wenye kuenea sana kati ya theluthi mbili za idadi ya ulimwengu.”
TATIZO LA UMASKINI
Tisho halisi la umaskini hata hivyo linaonekana katika maisha za watu wanaoukabili kila siku. Si jambo jepesi kueleza, kwa maana huenda mtu akawa “maskini” katika nchi moja na bado aonekane afadhali akiwa na mali zile zile mahali penginepo.
Wafanya kazi wenye kuhama katika mataifa ya Uzunguni wana maisha magumu. Kwa mfano, katika United States, jamaa ya Waamerika wa Mexico wanaweza kufanya kazi ya mavuno mashambani kila zao linapoiva. Ingawa wanafanya kazi saa nyingi, jamaa nzima pamoja, huenda wasiweze kuchuma pesa nyingi kama mwanafunzi aliyesomea utengenezaji wa mabomba ya maji. Wengine wanakaribia sana kufa njaa hata kukosa kazi ya siku kungemaanisha kutokula siku hiyo—tisho la umaskini ni halisi kwao.
Mambo yenye kulingana na hayo katika sehemu zenye maendeleo zaidi za Ulaya yako Asia na Afrika na vile vile katika mataifa mengine ya Kizungu. Watu wengi, wanaohama wakafanye kazi ambako kuna “ufanisi,” wanalazimika kufanya kazi za kufagia barabara na kusugua vyoo. “Makao” yanakuwa nyumba zenye kusongamana sana zilizojengwa kwa karatasi ngumu na sehemu kuukuu za magari. Hawana umeme wala maji ya mfereji.
Na hali bado ni yenye maendeleo ikilinganishwa na sehemu fulani za Afrika na Asia. Maskini wa mjini mara nyingi wanaishi katika vijumba vinavyolingana na ukubwa karibu wa deski ya afisini; nayo mainzi yanamiminika kila mahali. Na chakula je? Ni takataka wanayopekua-pekua katika marundo ya vitu vilivyotupwa-tupwa! Hata hivyo, ripoti moja yasema, hata maskini hao wa mjini ni afadhali zaidi kuliko wanavijiji wa mashambani: “Wafanya kazi wasio na shamba la kukaa [wanaweza] kula vizuri zaidi kwa kupekua-pekua katika takataka za mjini badala ya kungoja wapate nafasi za kazi zilizo haba katika vijiji. Takataka za mji [zinaleta] faida nyingi zaidi mwilini kuliko . . . vyakula vya vivi hivi vinavyoliwa na maskini.”
Uamini usiamini, hata maskini hao ni afadhali wakilinganishwa na wengine. Mamilioni mengi ya watu hawa hawawezi kupata mtaa mchafu-mchafu wa kuishi. Watu wanaoishi kando kando ya barabara wanatumia barabara kama vyoo na kando za barabara kama vitanda na meko yao.
KWA SABABU GANI KUNA UMASKINI?
Ni nani au ni nini kinachosababisha tisho lenye kuongezeka la umaskini? Majibu mengine yanaonyesha maoni ya kwamba lawama i juu ya maskini wenyewe na mengine yanaonyesha kwamba wao hawana uwezo wa kubadili hali hiyo. Pengine kweli inapatikana kati ya maoni hayo.
Wakati mmoja, watu wengi sana walikuwa wenye haraka ya kulaumu maskini wakisema ni wavivu. Lakini sasa ni watu wachache zaidi wanaosema hivyo. Kwa sababu gani? Kwa sababu kupungua kwa thamani ya pesa kunamaliza pesa za watu wengi zaidi na zaidi zilizochumwa kwa jasho. Sasa wao wenyewe wanafahamu kwamba kweli yako mambo asiyoweza kuzuia mtu yanayoelekea kumfanya “tajiri” au “maskini.”
Haiwezi kukanwa kwamba watu wengine wangekuwa afadhali zaidi kama wangefanya kazi kwa bidii zaidi. Habari zinazotoka katika nchi moja zinasema kwamba wafanya kazi “wanafuata mwendo wao wenyewe: kufanya kazi saa chache, kisha kuweka vyombo vyao chini na kujilaza kidogo.” “Ewe mvivu, utalala hata lini?” ndivyo Biblia inauliza katika Mithali 6:9, kisha inahakikisha hivi katika mstari wa 11: “Hivyo umaskini wako huja.” Bila shaka, katika sehemu nyingine za dunia watu wamedhoofishwa na njaa, au na magonjwa kama hepatitis (uvimbe wa ini), malaria na yellow fever (mojawapo ya homa kuu). Hawawezi kufanya kazi sawa na mtu mwenye nguvu zaidi. Nayo Biblia inaonyesha kwamba uko pia wakati wa “konzi moja pamoja na utulivu [“pumziko,” NW].”—Mhu. 4:6.
Walakini, ushuhuda unaoongezeka unaonyesha kwamba watu wengi zaidi si maskini kwa sababu ni wavivu wala kwa sababu ya kukataa kufanya kazi. Kwa mfano, katika United States karibu milioni 21 za watu wanaofanya kazi wajipatie riziki wanapangwa katika jamii ya “maskini”; karibuni kumetokea usemi unaosema “maskini wanaofanya kazi.” Huenda wafanya kazi wenye kuhamia nchi nyingine wakawa maskini, lakini je! hawakujaribu hata kidogo kwenda kuliko na kazi? Uchunguzi ulionyesha kwamba persenti 75 ya watu wanaoishi kando kando ya barabara wa Calcutta wanafanya kazi wajitafutie riziki; lakini mishahara yao ni midogo sana kutoweza kuwaruzuku wao na jamaa zao vizuri.
Wala mishahara midogo sikuzote haisababishwi na kukosa elimu, ujuzi wala ufundi. Mara nyingi, mahali ambapo mtu anafanya kazi ni mojawapo la mambo yenye kuamua mapato yake. Barry Bluestone, mchunguzi wa mambo ya uchumi wa Chuo Kikuu cha Boston, anasema hivi: “Bawabu (msimama mlangoni) katika kampuni ya kutengeneza motokaa analipwa mshahara wa kumwezesha yeye na jamaa yake wajiruzuku vya kutosha. Kazi iyo hiyo katika viwanda vya kutengenezea nguo ina mshahara mdogo tu.” Na bado kazi nyingi sana za ubawabu zinapatikana katika viwanda vya kutengenezea motokaa. Mara kwa mara kupata mshahara nafuu kunategemea kuwa mahali panapofaa katika wakati unaofaa.—Mhu. 9:11.
Umaskini unajizaa wenyewe, na kuwa tisho lenye kuongezeka kwa njia nyingine. Unakuza utamaduni wake wenyewe—mara nyingi ukitumia chakula, usemi, mavazi na tabia zake wenyewe. Mara nyingi mtu aliyelelewa katika mazingira yenye umaskini “anafikiri” hivyo. Hivyo, gazeti la kila siku la weusi la United States, Columbus (Georgia) Times, linamtaja Walter Washington akisema kwamba ikiwa “makao ya maskini yataondolewa lazima tusaidie maskini waondoe umaskini wa akili . . . Ukijengea mtu nyumba katika makao ya maskini bila kubadili njia yake ya kufikiria mambo, nyumba hiyo itakuwa makao ya maskini.” Maskini waliozoea kuishi katika mitaa michafu-michafu kwa kawaida watachafua nyumba mpya wasipoelimishwa kufanya mambo vingine.
Kule kunakoitwa “kufikiri kimaskini” kunaharibu hali zao zaidi na hata kuongezea tisho la umaskini, kunapoambatana na kiburi kingi cha muda. Tunapashwa habari hizi juu ya watu walio katika jimbo moja la Ulaya ya magharibi lenye umaskini mwingi: “Wao wanakula mkate na vitunguu tu kila siku, wanakuwa na deni nyingi sana ndio waweze kujivunia kuwa na gari.” Huenda matajiri wakaona ni vigumu kuelewa njia hiyo ya kufikiri. Lakini, kwa kweli mara nyingi wao ndio wamelemeza zaidi maskini. Kwa njia gani?
KUKOSA HURUMA JUU YA MASKINI
Mara nyingi watu wanaokula vizuri, wanaovalia vizuri hawajali juu ya hatari zinazowakabili wenye umaskini. Nyakati nyingine watu hawataki kuwa bila huruma kwa makusudi; lakini maisha ya kila siku yanataka wafanye mambo mengi katika wakati walio nao hata inakuwa vyepesi kusahau maskini.
Mafundisho ya kijamii na ya kidini hayakusaidia sana maskini wapate kufikiriwa. Fundisho la mageuzi, pamoja na mawazo yake yenye kuonyesha “wenye kujiweza kabisa ndio wataokoka,” linafanya watu wafikiri wengine wamepaswa kupuzwa kama “wasiojiweza.”
Fundisho lenye makosa la kidini lenye kuonyesha mambo yote yanayotokea yalikuwa yameandikwa zamani na Mungu (yawe mabaya au mazuri) limefanya wengi wategemee bahati. Viongozi wa dini wamesema kwamba wenye ufanisi wa mali za kimwili—si wale wenye sifa za kweli za kiroho—ndio wenye baraka ya Mungu. Ikiwa mtu amekosa mali za ulimwengu huu, makanisa yamefikiri na kusema hayo yalikuwa “mapenzi ya Mungu.”
Looo! maoni hayo yanatofautianaje na maoni yenye huruma lakini yaliyo hakika ya Yesu Kristo! Kwa wazi kulikuwa na umaskini wa kadiri fulani kati ya Wayahudi wakati Yesu alipokuwa duniani. Yeye na mitume wake walipendezwa na kusaidia maskini. Alifundisha kwamba katika wakati unaofaa wapole wangeirithi dunia; tisho la umaskini lingetoweka milele.—Mt. 5:5; 6:10; 11:5; 24:20, 21; Yohana 13:29.
“SIKUZOTE MNAO MASKINI PAMOJA NANYI”
Basi kwa sababu gani Yesu alisema: “Sikuzote mnao maskini pamoja nanyi”? Si kwa sababu hakuwahurumia. Maneno ya Yesu yakifikiriwa katika hali ya mambo yaliyokuwa yanaendelea alipoyasema, yanaonyesha nia inayofaa ambayo imewapasa watu wote wenye kumcha Mungu wawe nayo juu ya maskini.
Yesu alikula katika nyumba ya Simoni, aliyeishi katika mji wa Bethania. Alipokuwa huko, yafuatayo yalitokea: “Basi Mariamu akatwaa ratli ya marhamu ya nardo safi yenye thamani nyingi, akampaka Yesu miguu, akamfuta miguu kwa nywele zake. Nayo nyumba pia ikajaa harufu ya marhamu. Basi Yuda Iskariote, mmojawapo wa wanafunzi wake, ambaye ndiye atakaye kumsaliti, akasema, Mbona marhamu hii haikuuzwa kwa dinari mia tatu, wakapewa maskini? Naye aliyasema hayo, si kwa kuwahurumia maskini; bali kwa kuwa ni mwivi, naye ndiye aliyeshika mfuko, akavichukua vilivyotiwa humo. Basi Yesu alisema, Mwache aiweke kwa siku ya maziko yangu. Kwa maana maskini mnao sikuzote pamoja nanyi; bali mimi hamnami sikuzote.”—Mt. 26:6-13; Marko 14:3-9; Yohana 12:2-8.
Kwa vile alivyofanya, Mariamu alikuwa akijaribu kuonyesha anamthamini Yesu. Kuna mambo mengi ya lazima ambayo kwayo mtu angeweza kutumia mali zake. Mambo mengine, kama vile kumthamini Masihi, Yesu, ambaye alikuwa karibu ya kufa, yangeweza kufanywa vizuri zaidi wakati huo.
Imepaswa ikumbukwe pia kwamba maneno ya Yesu yanahusu sheria ya Mungu waliyopewa Israeli kupitia kwa Musa. (Kum. 15:11) Sheria hiyo ilipotumiwa vizuri, hakuna Myahudi aliyelemewa asiweze kutoka katika umaskini mwingi. Kwa mfano, jamaa isingeweza kunyang’anywa mali kwa wakati usiojulikana. (Tazama Mambo ya Walawi sura ya 25.) Utii wa uaminifu kwa sheria ya Mungu ulizuia watu wengi wasiwe maskini. (Kum. 15:4, 5) Halafu, tena, walioingia katika umaskini walipaswa kutendewa na wengine kwa ukarimu: “Kama akiwapo mtu maskini pamoja nawe, nduguzo mmojawapo . . . usifanye moyo wako kuwa mgumu, wala usimfumbie mkono wako nduguyo maskini.”—Kum. 15:7, 8.
Yesu alijua kwamba umaskini usingeondolewa kabisa mara hiyo kati ya wafuasi wake. Wanafunzi wake wangepatikana katika hali zote za kijamii na za kiuchumi. (1 Kor. 7:17-24) Umaskini ulikuwa ugumu halisi nao walipaswa kupambana nao. Maandishi ya wafuasi wa kwanza wa Yesu yanaonyesha kwamba waliweza kupambana nao.—1 Kor. 16:1, 2; 1 Yohana 3:17, 18.
Kutumia kwa Yesu neno “sikuzote,” alipokuwa akisema, “Maskini mnao sikuzote pamoja nanyi,” kusichukuliwe kama kunamaanisha ‘mpaka wakati usio na kikomo.’ “Sikuzote” (neno la Kigiriki panʹto·te) linawekewa mipaka katika matumizi yake na hali ambamo linaonekana. Hivyo katika Luka 15:31 (NW) baba ya mwana mpotevu anamwambia mvulana wake mkubwa hivi: “Mtoto, wewe umekuwa nami sikuzote.” Kwa wazi “mtoto” huyo hakuwa na baba yake kabla baba yake hajawa na watoto wo wote. Kwa hiyo, pia, maadamu taratibu potovu za kiuchumi zilizopo zinatawala dunia hii, ‘sikuzote kutakuwa na umaskini.’
Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba hali za kupita kiasi za watu wengi kuwa maskini na wachache kuwa matajiri zitakoma karibuni, katika taratibu mpya ya Mungu. Walakini, leo wao wenyewe wanapatikana wakiwa katika hali zote za kiuchumi. Na bado wanaonana kama ndugu na dada, na kufikiriana kwa upendo.
Zaidi ya hayo, walio maskini zaidi wanajua kwamba kutumia kanuni za Biblia katika maisha zao kutawasaidia kuepuka mazoea mabaya kwa mfano,—kucheza kamari, kutumia tumbako na dawa za kutia usingizi—mambo ambayo yanaleta umaskini. Wanakuza sifa ya kuwa wenye bidii, ikifanya iwe vyepesi zaidi kupata na kushikilia kazi. Wakiwa na tumaini la wakati ujao, hawamwonei Mungu wala mwanadamu mwenzao uchungu.
Huenda Wakristo wengine wasione wanatishwa moja kwa moja na umaskini katika wakati huu. Lakini wanajua unaweza kuwatisha kwa njia isiyo ya wazi. Kwa njia gani? Huenda mtu akajifanya mgumu sana asijali hali ya wenye kupatwa na umaskini, akipuza shauri la Neno la Mungu kuwatendea kwa huruma. Kwa njia hiyo umaskini ungeweza kutisha maisha ya kiroho ya mtu.
Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba, ingawa lazima maskini wafanye mabadiliko fulani katika maisha yao, kuna badiliko jingine lililo la maana pia. Hilo ni badiliko ambalo lazima maskini hao wenyewe wafanye katika nia yao juu ya wenye umaskini. Maneno ya zaburi ya Daudi yanafaa: “Heri amkumbukaye mnyonge; [Yehova] atamwokoa siku ya taabu.”—Zab. 41:1.
Je! wewe ungependa kuishi wakati matisho yote ya umaskini yatakuwa yametoweka? Je! ungependa kupata mashauri yanayofaa juu ya namna ya kupambana na umaskini sasa? Ikiwa ndivyo, ulisome gazeti hili kwa kawaida.
[Picha katika ukurasa wa 99]
Yesu alimaanisha nini aliposema: “Maskini mnao sikuzote pamoja nanyi”?—Yohana 12:8.