Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 5/1 kur. 4-7
  • Karibuni, Hakuna Atakayekuwa Maskini!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Karibuni, Hakuna Atakayekuwa Maskini!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Msaada kwa Walio Maskini
  • Msaada wa Kukabiliana na Umaskini
  • Hatimaye, Hakuna Umaskini Tena!
  • Umaskini Unaoongezeka—Tisho kwa Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Mwisho wa Umaskini Wakaribia
    Amkeni!—1998
  • Fuata Kielelezo Cha Yesu Kwa Kuwahangaikia Maskini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Ulimwengu Usio na Umaskini Unakaribia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 5/1 kur. 4-7

Karibuni, Hakuna Atakayekuwa Maskini!

“MSIOGOPE; kwa kuwa mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote.” (Luka 2:10) Maneno haya yenye kutia moyo yalisikiwa na wachungaji waliostaajabu karibu na Bethlehemu usiku ambao Yesu alizaliwa. Kwa kupatana na tangazo hilo, wakati wa huduma yake ya kidunia, Yesu alitilia “habari njema” mkazo mwingi. Leo, tutegemeapo pesa sana kutupa mahitaji yetu, twaweza kunufaishwaje na habari njema kuhusu Yesu?

Yesu Kristo aliwahubiri “maskini habari njema.” (Luka 4:18) Kulingana na Mathayo 9:35, “Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme.” Ujumbe wake ulikuwa wenye kutia moyo hasa waliokumbwa na umaskini. “Alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Kweli, Yesu alisema, “Maskini mnao sikuzote pamoja nanyi,” lakini hatupaswi kuamua kutokana na maneno haya kwamba hakuna tumaini kwa wenye uhitaji. (Yohana 12:8) Kadiri mfumo huu udumupo, maskini wataendelea kuwapo, hata umaskini wao utokezwe na nini. Neno la Mungu halipuuzi uhalisi wa umaskini, lakini halikazii upande usiofaa. Badala ya hilo, linatoa msaada kwa walio maskini kukabili masumbufu ya maisha.

Msaada kwa Walio Maskini

Imesemwa kwa msingi: “Hakuna mzigo mkubwa unaoweza kubebwa na mtu kuliko kujua hakuna anayejali wala anayeelewa.” Hata hivyo, ijapokuwa walio wengi hawana huruma, bado kuna habari njema kwa walio maskini—kwa sasa na vilevile kwa wakati ujao.

Kwa kusikitisha, wengi hawajali sana kusaidia walio maskini. Kulingana na The World Book Encyclopedia, wengine huamini kwamba “watu katika jamii hushindania kuishi na . . . watu mmoja-mmoja wenye uwezo hupata nguvu na mali.” Wale ambao huamini nadharia hii, iitwayo Udarwini wa kijamii, huenda wakaona walio maskini kuwa watu wavivu au wenye kutumia pesa vibaya. Hata hivyo, wale wafanyao kazi ngumu katika sehemu za mashambani, wafanyakazi kutoka sehemu nyinginezo, na wengineo, licha ya kulipwa mishahara midogo, mara nyingi hufanya kazi kwa bidii sana kulisha familia zao.

Katika nchi nyingi umaskini ni jambo la kawaida sana. Kwa hiyo, maskini—walio wengi—hawafanywi kuhisi kwamba wameshindwa kufaulu. Hata hivyo, katika nchi hizo kuna watu wanaoishi kwa anasa sana miongoni mwa umaskini. Nyumba zenye starehe, za bei ghali zimejengwa kando ya vibanda vyenye msongamano vyenye kudhuru afya. Watu wenye kulipwa mishahara mikubwa huendesha magari yao ya thamani katika barabara zenye watu wengi fukara wasioajiriwa. Katika nchi hizo walio maskini hutambua taabu yao kwa uchungu. Kwa kweli, “walio maskini hutaabishwa si kwa chakula kisichojenga mwili, nyumba mbaya, na matibabu yasiyofaa tu, bali pia kutokana na masumbufu ya kila siku juu ya hali yao,” chasema The World Book Encyclopedia. “Wakiwa hawawezi kupata kazi nzuri, wao hupoteza hali yao ya kujiheshimu na kuona kuwa hawafai kitu.” Basi, wengine walio maskini sana hukabilije hali yao? Habari njema kuhusu Yesu inahusianaje na kuikabili hali hiyo?

Kwanza, kumbuka kwamba umaskini huenda ukaongezwa na tabia zisizo za hekima. Fikiria vielelezo kadhaa. Valdecir akubali kwamba mkeye na watoto wake wachanga wajapopungukiwa na chakula, yeye aliharibu pesa ili aendeleze mtindo-maisha usio wa adili. Yeye asema: “Ingawa nilikuwa nimeajiriwa, nilikuwa daima sina pesa zozote bali sikuzote nilikuwa na tikiti za bahati nasibu mfukoni mwangu.” Kwa sababu ya kunywa na kuvuta sigareti kupita kiasi, Milton, alipoteza biashara iliyokuwa na waajiriwa 23. Yeye asema: “Nilitumia siku nyingi barabarani, nikiwa siwezi kwenda nyumbani, na familia yangu iliumia sana kwa ajili yangu.”

João vilevile aliharibu mshahara wake kwa mambo mabaya. “Nilikuwa nikilala nje siku nyingi. Mapato yangu yote hayakutosha mambo hayo mabaya na mahusiano na wanawake. Hali hiyo ikawa isiyovumilika, na mke wangu alitaka tutengane.” Kuongezea matatizo yake ya kiuchumi na ya ndoa, alikuwa na matatizo mengine pia. Yeye asema: “Nilifanya fujo na watu wa ukoo na majirani na hasa nilikuwa na matatizo kazini. Kama tokeo, mara nyingi sikuwa na kazi.” Júlio alikuwa mzoevu wa dawa za kulevya. Hata hivyo, aeleza: “Kwa kuwa mshahara wangu daima haukutosha kudumisha tabia yangu ya uzoevu wa dawa za kulevya, nilianza kufanya kazi ya kuuza dawa hizo ili isinibidi kununua dawa za kulevya.”

Akiwa amelelewa katika familia maskini ya watoto wanane, José alitaka awe na mali. Akiona kwamba hatapoteza jambo lolote, akiwa pamoja na vijana wengineo alianza kunyang’anya watu vitu kinguvu. Akiwa hajui la kufanya, kijana mwingine akawa mshiriki wa genge hilo liitwalo Wagongavichwa. Yeye aeleza: “Kwa kuwa wengi wetu tulikuwa maskini sana, tulipata uradhi fulani katika kuvunja vitu na kushambulia watu.”

Hata hivyo, leo wanaume hawa na familia zao hawataabishwi tena na ukosefu mkubwa wa vitu au hisia za uchungu na udhiko. Hawako tena katika hali ya kutoweza kujisaidia au ya kukosa matumaini. Kwa nini? Kwa sababu walijifunza habari njema ambazo Yesu alihubiri. Walitumia shauri la Biblia na kushirikiana na watu mmoja-mmoja wenye nia kama hiyo katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Nao wamejifunza mambo fulani ya maana sana kuhusu mali na umaskini.

Msaada wa Kukabiliana na Umaskini

Kwanza, walijifunza kwamba ikiwa kanuni za Biblia zinatumiwa, matokeo mabaya ya umaskini yaweza kupunguzwa. Biblia hushutumu ukosefu wa adili, ulevi, kucheza kamari, na matumizi mabaya ya dawa za kulevya. (1 Wakorintho 6:9, 10) Vitu hivyo ni ghali sana. Vyaweza kufanya tajiri awe maskini, na maskini awe maskini hata zaidi. Kuacha mambo haya mabaya na mengine kama hayo husaidia sana kuboresha hali ya kiuchumi ya familia.

Pili, walipata kujua kwamba kuna mambo ya maana zaidi katika maisha kuliko mali. Maoni yaliyosawazika yanaelezwa katika maneno haya yaliyopuliziwa: “Hekima ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi; na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.” (Mhubiri 7:12) Ndiyo, pesa ni ya lazima. Lakini hekima na ujuzi wenye msingi wa Biblia wa makusudi ya Mungu ni wa maana hata zaidi. Kwa kweli, kwa mtu asiye na hekima, kuwa na pesa nyingi kwaweza kuwa mzigo sawa na kuwa na chache sana. Mwandikaji wa Biblia alisali kwa hekima: “Usinipe umaskini wala utajiri; unilishe chakula kilicho kadiri yangu. Nisije nikashiba nikakukana, nikasema, BWANA ni nani? Wala nisiwe maskini sana nikaiba, na kulitaja bure jina la Mungu wangu.”—Mithali 30:8, 9.

Tatu, waligundua kwamba mtu akiishi kulingana na habari njema aliyohubiri Yesu, hahitaji kamwe kuhisi ameachwa. Habari njema inahusu Ufalme wa Mungu. Ujumbe huo unaitwa “habari njema ya ufalme,” na katika siku yetu inahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu. (Mathayo 24:14) Yesu alituambia kwamba tungetegemezwa tukiweka tumaini letu katika Ufalme huo. Alisema: “Utafuteni kwanza ufalme [wa Mungu], na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” (Mathayo 6:33) Mungu haahidi magari yenye madoido na nyumba za anasa. Yesu alikuwa akisema juu ya mahitaji ya maisha, vitu kama chakula na mavazi. (Mathayo 6:31) Lakini mamilioni leo waweza kushuhudia kwamba ahadi ya Yesu inategemeka. Mtu, hata mtu aliye maskini sana, haachwi kabisa akiuweka Ufalme kwanza.

Nne, walipata kujua kwamba mtu awekaye Ufalme wa Mungu kwanza haonei uchungu magumu ya kiuchumi. Ndiyo, mtu aliye maskini apaswa kufanya kazi kwa bidii. Lakini akimtumikia Mungu, ana uhusiano wenye upendeleo na Muumba wake, ambaye Biblia husema: “Maana hakulidharau teso la mteswa, wala hakuchukizwa nalo; wala hakumficha uso wake, bali alipomlilia akamsikia.” (Zaburi 22:24) Kuongezea hayo, mtu aliye maskini ana msaada wa kukabili matatizo ya maisha. Yeye hufurahia uhusiano mchangamfu pamoja na Wakristo wenzake na ana ujuzi na uhakika wa mapenzi ya Yehova yaliyofunuliwa. Mambo haya ‘ni ya kutamanika kuliko dhahabu, kuliko wingi wa dhahabu safi.’—Zaburi 19:10.

Hatimaye, Hakuna Umaskini Tena!

Mwishowe, watu mmoja-mmoja watiio habari njema hujifunza kwamba Yehova Mungu amekusudia kutatua matatizo ya umaskini kabisa kupitia Ufalme wake. Biblia huahidi: “Kwa maana mhitaji hatasahauliwa daima; matumaini ya wanyonge hayatapotea milele.” (Zaburi 9:18) Ufalme ni serikali halisi, iliyosimamishwa mbinguni Yesu Kristo akiwa Mtawala. Karibuni, Ufalme huo utachukua nafasi ya serikali za binadamu ili usimamie mambo ya binadamu. (Danieli 2:44) Kisha, akiwa Mfalme aliyewekwa, Yesu “atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.”—Zaburi 72:13, 14.

Likitazamia mbele wakati huo, Mika 4:3, 4 lasema: “Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha BWANA wa majeshi kimesema hivi.” Ni nani anayesemwa hapa? Bila shaka, ni wote wajinyenyekezao chini ya Ufalme wa Mungu. Ufalme huo utatatua matatizo yote yanayotaabisha binadamu—hata tatizo la ugonjwa na kifo. “Amemeza mauti hata milele; na Bwana MUNGU atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isaya 25:8; 33:24) Huo utakuwa ulimwengu tofauti kama nini! Na ukumbuke, twaweza kuamini ahadi hizo kwa sababu zimepuliziwa na Mungu mwenyewe. Yeye asema: “Watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.”—Isaya 32:18.

Uhakika katika Ufalme wa Mungu hushinda ukosefu wa kujistahi ambao mara nyingi huletwa na umaskini. Mkristo aliye maskini anajua kwamba anafaa machoni pa Mungu sawa na Mkristo aliye na mali. Mungu huwapenda wote wawili sawasawa, na wote wawili wana tumaini lilelile. Wote wanatazamia mbele kwa hamu nyingi kwenye wakati ambapo, chini ya Ufalme wa Mungu, umaskini utakuwa jambo lililopita. Huo utakuwa wakati mtukufu kama nini! Hatimaye, hakuna atakayekuwa maskini!

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kwa nini uharibu pesa kwa uchezaji kamari, uvutaji sigareti, kunywa kupita kiasi, utumiaji mbaya wa dawa za kulevya, au mtindo-maisha usio wa adili?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yehova Mungu atatatua matatizo ya umaskini wa binadamu kupitia Ufalme wake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki