Je, Una Maoni ya Kimungu juu ya Vinywaji Vyenye Alkoholi?
MIAKA 20 hivi iliyopita, waakiolojia walifukua jengo zee la matofali ya matope karibu na mji wa Urmia, Iran. Ndani yalo walikuta gudulia la kauri ambalo, kulingana na wanasayansi, ni la maelfu ya miaka, la wakati ambapo makazi ya kibinadamu ya mapema sana yalipoanzishwa. Majuzi, tekinolojia ya karibuni zaidi ilitumiwa katika kulichunguza gudulia hilo. Wanasayansi walishangaa kupata ndani yalo uthibitisho wa kikemikali wa kale zaidi wa utengenezaji wa divai.
Pia Biblia huthibitisha waziwazi kwamba tangu nyakati za kale divai, bia, na vinywaji vingine vyenye alkoholi vimenywewa. (Mwanzo 27:25; Mhubiri 9:7; Nahumu 1:10) Sawa na vyakula vingine, Yehova hutupa sisi tukiwa mtu mmoja-mmoja uchaguzi—kunywa vinywaji vyenye alkoholi au la. Mara nyingi Yesu alikunywa divai pamoja na milo yake. Yohana Mbatizaji aliepukana na alkoholi.—Mathayo 11:18, 19.
Biblia hukataza kujitia kupita kiasi katika unywaji. Ulevi ni dhambi dhidi ya Mungu. (1 Wakorintho 6:9-11) Kwa kupatana na hilo, Mashahidi wa Yehova hawaruhusu wowote wanaokuwa walevi wasiotubu kubaki katika kutaniko la Kikristo. Wale katika kutaniko wanaochagua kunywa vinywaji vyenye alkoholi lazima wafanye hivyo kwa kiasi.—Tito 2:2, 3.
Maoni Yasiyo ya Kimungu
Watu wengi leo hawana maoni ya kimungu juu ya vinywaji vyenye alkoholi. Ni rahisi kuona kwamba Shetani anaendeleza matumizi mabaya ya zao hili la kale. Kwa kielelezo, katika visiwa fulani vya Pasifiki Kusini, ni desturi kwa wanaume kukusanyika ili kunywa kiasi kikubwa cha kinywaji kilichochachishwa cha kutengenezewa nyumbani. Vipindi hivyo huenda vikaendelea kwa muda wa saa kadhaa navyo hufanywa mara nyingi—wanaume wengi hujihusisha katika zoea hilo kila siku. Wengine huliona zoea hilo kuwa tu sehemu ya utamaduni. Nyakati nyingine bia na mvinyo hunywewa badala ya—au pamoja na—kinywaji cha kutengenezewa nyumbani. Mara nyingi ulevi hutokea.
Katika nchi nyingine ya Pasifiki, kiasi katika unywaji wa alkoholi wa wanaume ni jambo ambalo karibu halijulikani. Kwa kawaida, wanapokunywa wanakunywa ili walewe. Kwa kawaida, katika siku ya mshahara kikundi cha wanaume watakutana na kununua katoni kadhaa za bia, kila katoni ikiwa na chupa 24. Wanaacha kunywa pombe iishapo tu. Likiwa tokeo, ulevi wa hadharani ni wa kawaida sana.
Vinywaji vilivyochachishwa, kama vile divai ya mnazi na vinywaji vingine vya kienyeji, hutumiwa kidesturi katika nchi za Afrika. Desturi katika jumuiya fulani hutaka kwamba lazima alkoholi itolewe wageni-waalikwa wanapotumbuizwa. Kidesturi, mkaribishaji mwenye ukaribishaji-wageni huandaa alkoholi nyingi kuliko iwezayo kunywewa na yule anayemzuru. Katika eneo moja, kuweka chupa 12 za bia mbele ya kila mtu anayezuru ndiyo desturi.
Kampuni nyingi za Japani huwapangia waajiriwa wazo safari za kwenda kwa basi. Kiasi kikubwa cha vinywaji vyenye alkoholi huletwa safarini, na ulevi huruhusiwa. Baadhi ya matembezi hayo ya kupangwa na kampuni huendelea kwa siku mbili au tatu. Kulingana na gazeti Asiaweek, katika Japani, “kuanzia kwa wakulima wa mchele mpaka wanasiasa matajiri, kidesturi, kipimo cha kuwa mwanamume kimekuwa kiasi cha pombe awezacho kunywa.” Mielekeo hiyohiyo inaonwa katika nchi nyingine za Asia. Gazeti Asiaweek lataarifu kwamba “Watu wa Korea Kusini sasa hunywa mivinyo mingi wakiwa mtu mmoja-mmoja kuliko wanywaji kwingineko ulimwenguni.”
Kunywa kupita kiasi kumekuwa zoea ambalo limeenea katika makoleji huko Marekani. Kwa mujibu wa The Journal of the American Medical Association, “wanaokunywa kupita kiasi walio wengi hawajioni kuwa wanywaji wenye tatizo.”a Hilo halipaswi kushangaza kwa sababu katika nchi nyingi vyombo vya habari huendeleza unywaji kuwa utendaji wa ujasiri, ulio wa kimtindo, na wa hekima ya kilimwengu. Mara nyingi propaganda hiyo hukusudiwa vijana hasa.
Katika Uingereza, unywaji wa bia umeongezeka maradufu katika kipindi cha miaka 20, na unywaji wa pombe kali umeongezeka mara tatu. Wanywaji wanaanza wakiwa wachanga zaidi, na wanawake wengi zaidi wanakunywa. Mielekeo inayofanana na hiyo inaonwa katika nchi za Ulaya Mashariki na za Amerika ya Latini. Hilo lakaziwa na viwango vinavyoongezeka vya uraibu wa alkoholi na vifo vya barabarani vinavyohusika na alkoholi. Kwa wazi, kuna ongezeko la wazi katika matumizi mabaya ya alkoholi ulimwenguni pote.
Kiasi Kinachopita Kiasi Ni Kipi?
Maoni ya Biblia juu ya vinywaji vyenye alkoholi ni yenye usawaziko. Kwa upande mmoja, Maandiko husema kwamba divai ni zawadi kutoka kwa Yehova Mungu ‘ifurahishayo mtu moyo wake.’ (Zaburi 104:1, 15) Kwa upande ule mwingine, ikilaumu kujitia kupita kiasi Biblia hutumia maneno kama “ulevi,” “mazidio ya kunywa divai, sherehe zenye kelele za ulevi, mashindano ya kunywa,” “kutumia mvinyo sana,” na kuwa “waliofanywa watumwa wa divai nyingi sana.” (Luka 21:34; 1 Petro 4:3; 1 Timotheo 3:8; Tito 2:3; linganisha NW.) Lakini ni kiasi gani kilicho “divai nyingi sana”? Mkristo aweza kuamuaje yaliyo maoni ya kimungu juu ya vinywaji vyenye alkoholi?
Si vigumu kutambua ulevi. Matokeo yao yanafafanuliwa katika Biblia kwa maneno haya: “Ni nani apigaye, Yowe? Ni nani aliaye, Ole? Ni nani mwenye ugomvi? Ni nani mwenye mguno? Ni nani aliye na jeraha zisizo na hesabu? Ni nani aliye na macho mekundu? Ni wale wakaao sana kwenye mvinyo; waendao kutafuta divai iliyochanganyika . . . Macho yako yataona mambo mageni; na moyo wako utatoa yaliyopotoka.”—Mithali 23:29-33.
Alkoholi nyingi sana yaweza kusababisha kuchanganyikiwa mambo, maono ya uwongo, kukosa fahamu, na miparaganyo mingineyo ya akili na mwili. Chini ya uvutano wa alkoholi, mtu aweza kushindwa kudhibiti tabia yake, akisababisha madhara kwake mwenyewe au kwa wengine. Walevi wanajulikana kuwa wahusika katika mwenendo wenye dhihaka, wenye kuudhi, au usio wa adili.
Kunywa kufikia hatua ya kulewa, kukiwa na matokeo yako yaliyotajwa juu, bila shaka ni kunywa kupita kiasi. Hata hivyo, mtu aweza kudhihirisha ukosefu wa kiasi bila kuonyesha ishara zote za kawaida za ulevi. Kwa sababu hiyo, lile swali la kama mtu amekunywa kupita kiasi hubishaniwa mara nyingi. Mpaka uko wapi kati ya kiasi na kujitia kupita kiasi?
Linda Salama Uwezo Wako Mbalimbali wa Kufikiri
Biblia haiweki mipaka kwa kuandaa asilimia ya ukolevu wa alkoholi katika damu au kwa kipimo kinginecho. Alkoholi huwa na athari tofauti-tofauti katika watu mbalimbali. Hata hivyo, kanuni za Biblia hutumika kwa Wakristo wote nazo zaweza kutusaidia kukuza maoni ya kimungu juu ya vinywaji vyenye alkoholi.
Amri ya kwanza, Yesu alisema, ni “[kumpenda] Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote.” (Mathayo 22:37, 38) Alkoholi ina matokeo ya moja kwa moja juu ya akili, na kujitia kupita kiasi kutaingilia utii wako wa amri hii iliyo kuu kuliko zote. Kwaweza kuingilia kwa uzito uamuzi mzuri, uwezo wa kutatua matatizo, kudhihirisha hali ya kujizuia, na utendaji mwingine mbalimbali wa maana wa akilini. Maandiko hutuonya kwa upole hivi: “Shika hekima kamili na busara. Basi yatakuwa uzima kwa nafsi yako, na neema shingoni mwako.”—Mithali 3:21, 22.
Mtume Paulo huwasihi Wakristo hivi: “Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri kuzuri.” (Warumi 12:1, NW) Je, Mkristo angeweza “kukubalika kwa Mungu” ikiwa anakunywa alkoholi kufikia hatua ya kuacha ‘nguvu zake za kufikiri kuzuri’? Kwa kawaida, mnywaji asiye na kiasi hujenga hali ya kutoathiriwa na alkoholi hatua kwa hatua. Huenda akahisi kwamba kunywa kwake sana—kwake yeye—ni chini ya kiwango cha ulevi. Hata hivyo, huenda akawa anakuza hali yenye kudhuru ya kutegemea alkoholi. Je, mtu huyo angeweza kuutoa mwili wake ukiwa “dhabihu iliyo hai, takatifu”?
Kiasi chochote cha alkoholi kinachoharibu “hekima [yako] itumikayo na uwezo [wako] wa kufikiri” ukiwa Mkristo ni alkoholi ya kupita kiasi kwako wewe.
Ni Nini Kinachoathiri Maoni Yako juu ya Alkoholi
Mkristo apaswa kuchunguza ikiwa mtazamo wake kuelekea unywaji waathiriwa na mielekeo au desturi za kisasa. Kuhusu vinywaji vyenye alkoholi, bila shaka usingetaka kufanya machaguo yako kwa kutegemea mielekeo ya kitamaduni au propaganda ya vyombo vya habari. Katika kuuchunguza mtazamo wako mwenyewe, jiulize hivi, ‘Je, mtazamo wangu juu ya unywaji waathiriwa na yale yakubalikayo katika jumuiya? Au unywaji wangu waongozwa na kanuni za Biblia?’
Ingawa Mashahidi wa Yehova hawapingi mazoea ya kidesturi, wanatambua kwamba Yehova huchukia mazoea mengi yanayokubaliwa leo. Jumuiya fulani huruhusu utoaji-mimba, kutiwa damu mishipani, ugoni-jinsia-moja, na ndoa ya wake wengi. Hata hivyo Wakristo hutenda kulingana na maoni ya Mungu juu ya mambo hayo. Ndiyo, maoni ya kimungu yatamtia Mkristo hamasa achukie mazoea hayo licha ya kama yanakubalika kidesturi au sivyo.—Zaburi 97:10.
Biblia husema juu ya “mapenzi ya mataifa,” yanayotia ndani “mazidio ya kunywa divai” na “mashindano ya kunywa.” Maneno “mashindano ya kunywa” hutoa wazo la vikusanyiko vilivyopangwa kukiwa na kusudi hususa la kunywa kiasi kikubwa cha alkoholi. Yaonekana kwamba katika nyakati za Biblia watu fulani waliojivunia ule ulioonwa kuwa uwezo wao wa kunywa pombe nyingi bila kulewa walijaribu kuwashinda wengine, au walijaribu kuona ni nani ambaye angeweza kunywa zaidi. Mtume Petro anarejezea mwenendo wa aina hiyo ‘dimbwi la chini la ufasiki’ ambamo Wakristo waliotubu hawashiriki tena.—1 Petro 4:3, 4, NW.
Je, kungekuwa kupatana na akili kwa Mkristo kutwaa maoni ya kwamba maadamu halewi, kwa kweli haidhuru ni wapi, wakati gani, na kiasi anachokunywa? Twaweza kuuliza hivi, Je, hayo ni maoni ya kimungu? Biblia husema hivi: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31) Kikundi cha wanaume wanaokusanyika ili kunywa kiasi kikubwa cha alkoholi hadharani huenda wasilewe wote, lakini je, mwenendo wao ungemletea Yehova utukufu? Biblia huonya kwa upole hivi: “Msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”—Warumi 12:2.
Epuka Kuwakwaza Wengine
Kwa kupendeza, mara nyingi zile tamaduni zenyewe zinazovumilia kujitia kupita kiasi hupinga jambo hilo wakati mwenye kunywa sana anapodai kuwa mtu wa Mungu. Katika jumuiya moja ndogo katika Pasifiki Kusini, mtazamaji alisema hivi: “Nawastahi sana nyinyi watu. Mwahubiri kweli. Lakini tatizo tuonalo ni kwamba wanaume wenu hunywa alkoholi nyingi mno.” Kulingana na ripoti, watu mmoja-mmoja waliohusika hawakulewa, hata hivyo hilo jambo halikuonekana waziwazi kwa walio wengi katika hiyo jumuiya. Watazamaji waliweza kufikia mkataa kwa urahisi kwamba sawa na wanaume wengine walio wengi wanaohusika katika vipindi vya unywaji, Mashahidi hulewa pia. Je, mhudumu Mkristo anayejihusisha katika vipindi virefu vya unywaji aweza kudumisha sifa nzuri na atimilize huduma yake ya hadharani akiwa na uhuru wa kusema?—Matendo 28:31.
Ripoti kutoka kwa nchi moja ya Ulaya yaonyesha kwamba nyakati fulani ndugu na dada hufika kwenye Jumba la Ufalme wakiwa na harufu kali ya alkoholi. Hilo limesumbua dhamiri za wengine. Biblia huonya hivi kwa upole: “Ni vyema kutokula nyama wala kunywa divai wala kutenda neno lo lote ambalo kwa hilo ndugu yako hukwazwa.” (Warumi 14:21) Maoni ya kimungu juu ya vinywaji vyenye alkoholi yatamsukuma Mkristo mkomavu kujali dhamiri za wengine, hata ikiwa yamaanisha kukaa bila kutumia alkoholi chini ya hali fulani.
Wakristo Wako Tofauti kwa Njia ya Wazi
Kwa kuhuzunisha, ulimwengu huu umemuudhi Yehova sana kwa kutumia vibaya vitu vizuri ambavyo amewapa wanadamu, kutia na vinywaji vyenye alkoholi. Kila Mkristo aliyejiweka wakfu apaswa kujitahidi kuepuka maoni yasiyo ya kimungu ambayo yameenea sana. Hivyo watu wataweza ‘Kupambanua [“kuona tofauti,” NW] kati ya wenye haki na waovu, na kati ya yeye amtumikiaye Mungu na asiyemtumikia.’—Malaki 3:18.
Kuhusu vinywaji vyenye alkoholi, “tofauti” kati ya Mashahidi wa Yehova na ulimwengu yapaswa kuwa wazi sana. Kunywa vinywaji vyenye alkoholi si jambo kuu maishani mwa Wakristo wa kweli. Wao hawajaribu kujua mipaka yao ya kunywa alkoholi bila kuathiriwa, wakikaribia kwa hatari sana ulevi; wala hawaruhusu vinywaji vyenye alkoholi viharibu au kuingilia kwa njia yoyote kumtumikia kwao Mungu kwa nafsi yao yote na wakiwa na akili safi.
Wakiwa kikundi, Mashahidi wa Yehova wana maoni ya kimungu juu ya vinywaji vyenye alkoholi. Namna gani wewe? Kila mmoja wetu aweza kuhesabu baraka za Yehova huku tukifuata agizo la Biblia “tukatae katakata kukosa kumwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na tuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo uliopo wa mambo.”—Tito 2:12, NW.
[Maelezo ya Chini]
a “Kunywa kupita kiasi kulifafanuliwa kuwa kunywa vinywaji vitano au zaidi mfululizo kwa wanaume na vinne au zaidi mfululizo kwa wanawake.”—The Journal of the American Medical Association.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]
Wasikilize Wapendwa Wako
Mnywaji asiye na kiasi mara nyingi ndiye ni wa mwisho kutambua kwamba ana tatizo. Watu wa ukoo, marafiki, na wazee Wakristo hawapaswi kusita kuwatolea msaada wapendwa ambao wanakosa kiasi. Kwa upande mwingine, wapendwa waonyeshapo kutostareheshwa na tabia yako ya kunywa alkoholi, yamkini wana sababu nzuri kwa hilo. Fikiria wanayosema.—Mithali 19:20; 27:6.