Je, Kuna Upatano Kati ya “Hekalu la Mungu” na Sanamu Zilizoko Ugiriki?
SIKU hii ya kiangazi yenye joto jingi, jua lapiga mawe yenye kumetameta. Joto hilo la kupita kiasi halionekani kupunguza roho na azimio lenye bidii la songamano la wasafiri wenye ujitoaji wa dini ya Othodoksi ya Kigiriki wanaoelekea kwenye kikanisa kilicho juu ya kilima.
Wamwona mwanamke mzee mchovu, aliyesafiri toka mwisho ule mwingine wa nchi, akijitahidi kuendelea kutembea ingawa amechoka. Juu zaidi ya kilima mwanamume mwenye bidii anatoka jasho jingi huku akijaribu kwa kutazamia sana kupenya katikati ya umati wenye kusukumana. Na msichana kijana, ambaye bila shaka ana maumivu na akiwa na sura ionyeshayo kutazamia sana, atambaa kwa magoti yake yanayotoka damu nyingi. Kusudi lao ni nini? Wafike kwa wakati, wasali mbele ya sanamu ya “mtakatifu” anayesherehekewa na, ikiwezekana, waiguse na kuibusu.
Mandhari zinazofanana na hiyo zafanywa tena na tena kotekote ulimwenguni mahali mbalimbali palipotengwa kwa utoaji wa adhama kwa “watakatifu.” Yaonekana, wasafiri wote hao wamesadikishwa kwamba kwa njia hiyo wanafuata njia ya Mungu ya kumfikia, hivyo wakionyesha ujitoaji wao na imani yao. Kitabu Our Orthodox Christian Faith chataarifu hivi: “Twawakumbuka [“watakatifu”], na kuwahesabia watakatifu hao utukufu na heshima . . . , nasi twaomba sala zao mbele ya Mungu kwa niaba yetu na dua zao na msaada wao katika mahitaji mengi ya maisha zetu. . . . Twawageukia Watakatifu wafanya-maajabu . . . kwa mahitaji yetu ya kiroho na ya kimwili.” Pia, kulingana na kanuni za kisinodi za Kanisa Katoliki la Kiroma, “watakatifu” wanapaswa kutolewa sala wakiwa waombezi kwa Mungu, na maiti na pia mifano ya “watakatifu” yapasa kupewa adhama.
Hangaiko la msingi la Mkristo wa kweli lapaswa kuwa kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Kwa sababu hiyo acheni tuchunguze mambo fulani ya hakika juu ya njia ambayo utoaji wa adhama kwa “watakatifu” ulianzishwa kuwa sehemu ya mazoea ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo. Uchunguzi huo watazamiwa kuwa wenye kuelimisha sana kwa wote wanaotamani kumfikia Mungu kwa njia inayokubalika Kwake.
Jinsi “Watakatifu” Walivyokubaliwa
Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo huwaita “watakatifu,” Wakristo wote wa mapema waliosafishwa kwa damu ya Kristo na waliowekwa kando kwa ajili ya utumishi wa Mungu wakiwa wanaotazamiwa kuwa warithi-washirika pamoja na Kristo. (Matendo 9:32; 2 Wakorintho 1:1; 13:13)a Wanaume na wanawake, wenye kutokeza na wa hali ya chini kutanikoni, wote walifafanuliwa kuwa “watakatifu” walipokuwa wakiishi hapa duniani. Hata kabla hawajafa walijulikana kuwa watakatifu katika maana ya Kimaandiko.
Lakini, baada ya karne ya pili W.K., huku Ukristo wa uasi-imani ulipokuwa ukisitawi, mwelekeo ulikuwa kujaribu kufanya Ukristo uwe maarufu, dini ambayo ingevutia watu wapagani na ikubaliwe nao kwa utayari. Wapagani hao waliabudu miungu mingi, nayo dini mpya ilikuwa ikikazia ibada ya Mungu mmoja. Kwa hiyo uridhiano ungewezekana kupitia kukubaliwa kwa “watakatifu,” ambao wangechukua mahali pa miungu ya kale, nusu miungu, na mashujaa wa kingano wa kale. Kikitoa maelezo juu ya hilo, kitabu Ekklisiastiki Istoria (Historia ya Kanisa) chataarifu hivi: “Kwa wale waliokuwa wakigeuzwa imani toka upagani hadi Ukristo, ilikuwa rahisi kuwatambua mashujaa wao waliowaacha katika wale wafia-imani na kuanza kuwapa heshima ambayo hapo mbele waliwapa wale wa zamani. . . . Hata hivyo, mara nyingi sana, kuwatolea watakatifu heshima hiyo kukapata kuwa ibada ya sanamu ya moja kwa moja.”
Kitabu kingine cha marejezo hufafanua jinsi “watakatifu” walivyoingizwa katika Jumuiya ya Wakristo: “Katika kutolea heshima watakatifu wa Kanisa Othodoksi la Kigiriki, twapata viishara vya wazi vya uvutano wenye nguvu ambao dini ya kipagani ilikuwa nao. Sifa ilizohesabiwa miungu ya Olimpia kabla [watu] hawajageuzwa kuwa Wakristo sasa zilihesabiwa watakatifu. . . . Tangu miaka ya mapema ya hiyo dini mpya, twaona wafuasi wayo wakimweka Nabii Eliya mahali pa mungu-jua (Phoebus Apollo), wakijenga makanisa juu ya, au karibu na, magofu ya mahekalu au vihekalu vya kale vya mungu huyo, hasa juu ya vilima na milima, kila mahali ambapo Wagiriki wa kale walimheshimu mtoa-nuru Phoebus Apollo. . . . Hata walimtambulisha mungu wa kike Bikira Athena kuwa Bikira Maria mwenyewe. Hivyo, lile pengo lililotokezwa sanamu ya Athena ilipovunjwa liliondolewa nafsini mwa mwabudu sanamu aliyegeuzwa imani.”—Neoteron Enkyklopaidikon Lexikon (Kamusi Mpya ya Kiensaiklopidia), Buku 1, kurasa 270-271.
Mathalani, chunguza hali iliyokuwako Athene mwishoni mwa karne ya nne W.K. Wengi wa wakazi wa jiji hilo walikuwa wangali wapagani. Mojawapo ya desturi zao takatifu zaidi ilikuwa yale mafumbo ya Kieleusini, tukio lenye hatua mbili,b lililofanywa mwezi wa Februari kila mwaka katika mji wa Eleusis, kilometa 23 kaskazini-magharibi ya Athene. Ili kuhudhuria mafumbo hayo, Waathene wapagani walilazimika kupitia ile Njia Takatifu (Hi·e·raʹ Ho·dosʹ). Wakijaribu kuandaa mahali badala pa ibada, viongozi wa hilo jiji walithibitika kuwa werevu kwelikweli. Kwenye barabara hiyohiyo, karibu kilometa kumi kutoka Athene, nyumba ya watawa iitwayo Daphni ilijengwa ili kuwavutia wapagani na ili kuwazuia wasihudhurie hayo mafumbo. Kanisa la hiyo nyumba ya watawa lilijengwa juu ya msingi wa hekalu la kale lililotengwa kwa mungu wa Kigiriki Daphnaios, au Pythios Apollo.
Uthibitisho wa kuunganishwa kwa miungu ya kipagani na ule utoaji wa adhama kwa “watakatifu” waweza kupatikana pia katika kisiwa cha Kithira, Ugiriki. Kwenye mojawapo ya vilele vya kisiwa hicho kuna vikanisa viwili vidogo vya Byzantium—kimojawapo chavyo kimewekwa wakfu kwa “Mtakatifu” George, kile kingine kwa Bikira Maria. Ufukuzi mbalimbali ulifunua kwamba hapo palikuwa mahali pa kile kihekalu cha kilele cha Kiminoa ambacho kilitumika kikiwa mahali pa ibada miaka ipatayo 3,500 iliyopita. Katika karne ya sita au ya saba W.K., “Wakristo” walimjengea “Mtakatifu” George kikanisa chao kwenye mahali penyewe pa hicho kihekalu cha kilele. Hatua hiyo ilikuwa ya ufananisho kwelikweli; kitovu hicho cha hali ya juu cha dini ya Kiminoa kilidhibiti njia za baharini za Bahari ya Aegea. Hayo makanisa mawili yalijengwa huko ili kudumisha kibali cha Bibi Mheshimiwa Wetu na “Mtakatifu” George, wa pili akisherehekewa siku ileile ambayo yule “mlinda mabaharia,” “Mtakatifu” Nicholas anasherehekewa. Gazeti la habari likiripoti juu ya uvumbuzi huo lilisema hivi: “Leo kasisi [wa dini ya Othodoksi ya Kigiriki] atakwea mlima, kama vile tu kasisi wa Kiminoa alivyokuwa akifanya katika nyakati za kale,” ili kutoa utumishi wa kidini!
Akitoa muhtasari wa kadiri uasi-imani wa Ukristo ulivyokuwa umechochewa na dini ya Kigiriki ya kipagani, mtafiti wa kihistoria atokeza jambo hili: “Msingi wa kipagani wa dini ya Kikristo mara nyingi hubaki vilevile katika itikadi maarufu, hivyo ikitoa ushahidi juu ya hali ya kudumu ya desturi.”
‘Kuabudu Kile Tujuacho’
Yesu alimwambia yule mwanamke Msamaria hivi: ‘Sisi twaabudu kile tujuacho. Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta wa namna hiyo wamwabudu yeye.’ (Yohana 4:22, 23) Ona kwamba kuabudu kwa kweli ni kwa lazima! Kwa hiyo haiwezekani kumwabudu Mungu kwa kukubalika bila ujuzi sahihi wa hiyo kweli na kuipenda kwa kina. Dini ya kweli ya Kikristo lazima iwe na msingi katika kweli, wala si katika desturi na mazoea yaliyoazimwa kutoka upagani. Twajua jinsi ambavyo Yehova huhisi watu wanapojaribu kumwabudu kwa njia yenye kosa. Mtume Paulo aliandikia Wakristo katika jiji la kale la Ugiriki, Korintho: “Kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali? . . . Hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu?” (2 Wakorintho 6:15, 16) Jaribio lolote la kupatanisha hekalu la Mungu na sanamu lachukiwa naye.
Zaidi ya hayo, kwa njia iliyo wazi sana, Maandiko hayaruhusu lile wazo la kusali kwa “watakatifu” ili wawe kama waombezi kwa Mungu. Katika sala yake ya kigezo, Yesu alifundisha kwamba sala zapasa kutolewa kwa Baba pekee, kwa kuwa aliwaelekeza wanafunzi wake hivi: “Basi, nyinyi lazima msali kwa njia hii: ‘Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe.’” (Mathayo 6:9) Yesu aliendelea kutaarifu hivi: “Mimi ndiyo njia na kweli na uhai. Hakuna ajaye kwa Baba ila kupitia mimi. Mkiomba jambo lolote katika jina langu, hakika nitalifanya.” Naye mtume Paulo alitaarifu hivi: “Kuna Mungu mmoja, na mpatanishi mmoja kati ya Mungu na wanadamu, mwanadamu, Kristo Yesu.”—Yohana 14:6, 14; 1 Timotheo 2:5.
Ikiwa kwa kweli twataka sala zetu zisikiwe na Mungu, ni jambo la maana kwamba tumfikie yeye kwa njia ambayo neno lake laelekeza. Akikazia njia pekee inayofaa ya kumfikia Yehova, Paulo aliandika hivi pia: “Kristo Yesu ndiye aliyekufa, ndiyo, afadhali zaidi kusema ni yeye aliyefufuliwa kutoka kwa wafu, aliye katika mkono wa kuume wa Mungu, ambaye pia hutuombea.” “Aweza pia kuokoa kikamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu yeye yuko hai sikuzote ili kuwaombea.”—Waroma 8:34; Waebrania 7:25.
‘Kuabudu kwa Roho na Kweli’
Ukristo wa uasi-imani haukuwa na wala nguvu za kiroho wala utegemezo wa roho takatifu ya Mungu kuwachochea wapagani waache ibada yao isiyo ya kweli na kufuata mafundisho yenye kweli ya Yesu Kristo. Ilifyonza itikadi na mazoea ya kipagani katika kutafuta kwayo wageuzwa imani, mamlaka, na umaarufu. Kwa sababu hiyo haikutokeza Wakristo thabiti, wenye kukubalika kwa Mungu na Kristo, bali waamini bandia, “magugu” yasiyofaa kwa Ufalme.—Mathayo 13:24-30.
Hata hivyo, wakati huu wa mwisho, chini ya uelekeo wa Yehova kuna utendaji wa maana katika kurudisha ibada ya kweli. Watu wa Yehova ulimwenguni pote, yajapokuwa malezi yao ya kitamaduni, kijamii, au kidini, wanajaribu kupatanisha maisha na itikadi zao na viwango vya Biblia. Ikiwa wataka kujifunza mengi zaidi juu ya jinsi ya kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli,” tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova mahali unapoishi. Watafurahi sana kukusaidia kumtolea Mungu utumishi mtakatifu unaokubalika, kwa kutegemea nguvu zako za kufikiri kuzuri na ujuzi sahihi wa Neno lake. Paulo aliandika hivi: “Nawasihi sana nyinyi kwa huruma za Mungu, akina ndugu, mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri kuzuri. Na komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Nao Wakolosai aliwaambia hivi: “Sisi, tangu siku tuliposikia juu ya hilo, hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba ili nyinyi mpate kujazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho, kusudi mtembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili mnapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.”—Waroma 12:1, 2; Wakolosai 1:9, 10.
[Maelezo ya Chini]
a Tafsiri fulani za Biblia hutafsiri neno la Kigiriki haʹgi·os kuwa “mtakatifu.”
b Eleusini Kubwa Zaidi ilifanywa Septemba ya kila mwaka katika Athene na Eleusis.
[Sanduku katika ukurasa wa 28]
Matumizi Yasiyo Yamkini ya Parthenoni
Maliki “Mkristo” Theodosius 2, akiwa na amri kuhusu jiji la Athene (438 W.K.), alikomesha kawaida na mafumbo ya kipagani, akafunga mahekalu ya kipagani. Baadaye yangeweza kugeuzwa kuwa makanisa ya Kikristo. Takwa pekee la kugeuzwa kwenye mafanikio kwa hekalu lilikuwa kulitakasa kwa kuweka msalaba ndani yalo!
Mojawapo mahekalu ya kwanza kugeuzwa lilikuwa Parthenoni. Marekebisho makubwa yalifanyika ili kufanya Parthenoni listahili kwa kufaa kutumiwa kuwa hekalu la “Kikristo.” Tangu 869 W.K., lilitumika likiwa kathedro ya Athene. Mwanzoni liliheshimiwa kuwa kanisa la “Hekima Takatifu.” Hilo lingaliweza kuwa kikumbusha cha kukusudiwa cha lile jambo la hakika la kwamba “mwenye” hekalu hilo wa awali, Athena, alikuwa mungu wa kike wa hekima. Baadaye liliwekwa wakfu kwa “Bibi Mheshimiwa Wetu Mwathene.” Baada ya karne nane za kutumiwa na kanisa la Othodoksi, hilo hekalu liligeuzwa kuwa kanisa la Katoliki la Mtakatifu Maria wa Athene. “Urejelezaji” huo wa Kidini wa Parthenoni uliendelea wakati ambapo, katika karne ya 15, Waturuki wa Ottoman waliligeuza kuwa msikiti.
Leo Parthenoni, hekalu la kale la Kidori la Athena Parthenosi (“Bikira”), mungu wa kike wa Kigiriki wa hekima, hutembelewa na maelfu ya watalii likiwa tu kazi nzuri ya ujenzi wa Kigiriki.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Nyumba ya watawa ya Daphni—mahali badala pa ibada pa wapagani wa Athene la kale