Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 405-uku. 409
  • Watakatifu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Watakatifu
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mtu Akisema—
  • Watakatifu wa Kweli Wanaweza Kukusaidiaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Je, Tunapaswa Kusali kwa Watakatifu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Je, Kuna Upatano Kati ya “Hekalu la Mungu” na Sanamu Zilizoko Ugiriki?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Je, Ni Sawa Kusali kwa Watakatifu?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 405-uku. 409

Watakatifu

Maana: Kulingana na fundisho la Kanisa Katoliki, watakatifu ni wale waliokufa na sasa wako pamoja na Kristo mbinguni na ambao Kanisa limewatambua kwa ajili ya utakatifu wenye kutokeza na usafi wa adili. Imani ya Baraza la Trent inasema kwamba watakatifu wanapaswa kuombwa wakiwa wapatanishi kwa Mungu na kwamba masalio ya watakatifu na pia mifano ya watakatifu inapasa kuheshimiwa. Dini nyingine, pia, huomba msaada wa watakatifu. Dini fulani hufundisha kwamba washiriki wao wote ni watakatifu na hawana dhambi. Biblia inataja watakatifu mara nyingi. Inawaita wale wafuasi 144,000 wa Kristo watiwa-mafuta kwa roho kuwa watakatifu.

Je, Biblia hufundisha kwamba ni lazima mtu afikie utukufu wa mbinguni kwanza kabla ya kutambuliwa kuwa mtakatifu?

Bila shaka Biblia inawataja watakatifu, ambao wako mbinguni. Yehova anaitwa “Mtakatifu [Kigiriki, haʹgi·on].” (1 Pet. 1:15, 16; ona Mambo ya Walawi 11:45.) Yesu Kristo aliitwa “Mtakatifu [haʹgi·os] wa Mungu” wakati alipokuwa duniani. Pia anaitwa “mtakatifu [haʹgi·os]” akiwa mbinguni. (Marko 1:24; Ufu. 3:7, BHN) Malaika pia ni ‘watakatifu.’ (Mdo. 10:22, UV) Neno lilelile la msingi katika Kigiriki cha kwanza linatumiwa kuhusu hesabu fulani ya watu duniani.

Mdo. 9:32, 36-41, UV: “Petro alipokuwa akizunguka-zunguka pande zote akawatelemkia na watakatifu [ha·giʹous] waliokaa Lida. Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake Tabitha [aliyekuwa amekufa] . . . [Petro] akaelekea yule maiti, akanena, Tabitha, ondoka. Naye akafumbua macho yake, na alipomwona Petro akajiinua, akaketi. Akampa mkono, akamwinua; hata akiisha kuwaita wale watakatifu na wajane akamweka mbele yao, hali yu hai.” (Kwa wazi, watakatifu hao hawakuwa mbinguni bado, wala si mtu mashuhuri kama Petro peke yake aliyeonwa kuwa mtakatifu.)

2 Kor. 1:1; 13:12, 13, UV: “Paulo, mtume wa Kristo Yesu kwa mapenzi ya Mungu, na Timotheo ndugu yetu; kwa kanisa la Mungu lililoko Korintho, pamoja na watakatifu [ha·giʹois] wote walioko katika nchi yote ya Akaya.” “Salimianeni kwa busu takatifu. Watakatifu wote wawasalimu.” (Hao Wakristo wote wa kwanza waliotakaswa kwa damu ya Kristo na kutengwa kwa ajili ya utumishi wa Mungu wakiwa na tarajio la kuwa warithi pamoja na Kristo waliitwa watakatifu. Bila shaka haikungojewa mpaka wafe ndipo watambuliwe kuwa watakatifu.)

Je, ni jambo linalopatana na Maandiko mtu kusali kwa “watakatifu” ili wamwombee kwa Mungu?

Yesu Kristo alisema: “Ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, . . . ” Kwa hiyo, sala zinapaswa kuelekezwa kwa Baba. Pia Yesu alisema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba ila kwa njia ya mimi. Mkiniomba neno lolote kwa jina langu, nitalifanya.” (Mt. 6:9; Yoh. 14:6, 14, UV) Kwa hiyo, Yesu aliondoa lile wazo kwamba mtu mwingine yeyote anaweza kuwa mwombezi. Mtume Paulo aliongeza hivi kumhusu Kristo: “Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” “Aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.” (Rom. 8:34; Ebr. 7:25, UV) Ikiwa kwa kweli tunataka sala zetu zisikiwe na Mungu, je, halingekuwa jambo la hekima kumkaribia Mungu katika njia ambayo Neno lake linaelekeza? (Ona pia ukurasa wa 185, 186, chini ya kichwa “Maria.”)

Efe. 6:18, 19, UV: “Mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote; pia na kwa ajili yangu mimi, nipewe usemi kwa kufumbua kinywa changu, ili niihubiri kwa ujasiri ile siri ya Injili.” (Italiki zimeongezwa.) (Hapa Wakristo wanatiwa moyo wawaombee watakatifu bali si kwamba waombe kwao au kupitia wao. New Catholic Encyclopedia, 1967, Buku la 11, uku. 670, hukiri hivi: “Kwa kawaida katika A[gano] J[ipya], sala zote, za watu binafsi na pia sala za maombi ya watu wote, zinaelekezwa kwa Mungu Baba kupitia Kristo.”)

Rom. 15:30, UV: “Ndugu zangu, nawasihi kwa Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa upendo wa Roho, jitahidini pamoja nami katika maombi yenu kwa ajili yangu mbele za Mungu.” (Mtume Paulo, ambaye yeye mwenyewe alikuwa mtakatifu, aliwaomba Wakristo wenzake ambao pia walikuwa watakatifu waombe kwa ajili yake. Lakini ona kwamba Paulo hakuelekeza sala zake kwa hao watakatifu wenzake, wala sala zao kwa ajili yake hazikuchukua mahali pa uhusiano wa kibinafsi ambao Paulo mwenyewe alikuwa nao pamoja na Baba kupitia sala. Linganisha na Waefeso 3:11, 12, 14.)

Zoea la kuheshimu masalio na sanamu za “watakatifu” linapasa kuonwaje?

New Catholic Encyclopedia hukubali hivi: “Kwa hiyo ni ubatili kujaribu kutetea desturi ya kuheshimu masalio ya watakatifu katika Agano la Kale; wala Agano Jipya halikazii mifano ya watakatifu. . . . Inaonekana kwamba [“baba” wa Kanisa] Origen aliliona zoea hilo kuwa ishara ya kipagani ya kuheshimu kitu kinachoonekana.”—(1967), Buku la 12, uku. 234, 235.

Ni jambo linalostahili kuangaliwa kwamba Mungu alimzika Musa, na hakuna mwanadamu aliyegundua mahali ambapo kaburi lake lilikuwa. (Kum. 34:5, 6) Lakini andiko la Yuda 9 linatuambia kwamba malaika mkuu Mikaeli alibishana na Ibilisi juu ya mwili wa Musa. Kwa nini? Kusudi la Mungu la kuuzika mwili huo kwa jinsi hiyo hivi kwamba wanadamu hawangejua mahali pa kuupata lilielezwa waziwazi. Je, yule Mpinzani alitaka kuwapeleka wanadamu kwenye mwili huo ili uwekwe kwenye maonyesho na labda uwe kitu cha kuheshimiwa?

Kuhusu kuheshimiwa kwa mifano ya “watakatifu,” ona kichwa “Sanamu.”

Kwa nini “watakatifu” wa Kikatoliki wanaonyeshwa wakiwa na duara ya mwangaza kuzunguka kichwa?

New Catholic Encyclopedia hukiri hivi: “Sifa ambayo ni ya kawaida sana, inayotumiwa kwa watakatifu wote, ni wingu, umbo la mwangaza linalozunguka kichwa cha mtakatifu. Chanzo cha umbo hilo ni kabla ya Ukristo, na mifano inapatikana katika sanaa za Kigiriki za upagani; duara ya mwangaza ilitumiwa, kama inavyothibitishwa na picha na sarafu, kwa ajili ya nusu miungu na miungu kama vile Neptuni, Jupita, Bakusi, na hasa Apolo (mungu wa jua).”—(1967), Buku la 12, uku. 963.

The New Encyclopædia Britannica husema: “Katika sanaa za Wagiriki na Waroma mungu-jua Helios na maliki Waroma mara nyingi huonekana wakiwa na taji la miale. Kwa sababu ya chanzo chake cha kipagani, umbo hilo liliepukwa katika sanaa za Wakristo wa Kwanza, lakini wingu dogo la mviringo lilitumiwa na maliki Wakristo kwa ajili ya picha zao rasmi. Kuanzia katikati ya karne ya 4, Kristo pia alionyeshwa akiwa na umbo hilo la kimaliki . . . lakini desturi ya kutumia duara ya mwangaza kwa ajili ya Bikira Maria na watakatifu wengine ilianza katika karne ya 6.”—(1976), Micropædia, Buku la 4, uku. 864.

Je, inafaa kuchanganya Ukristo na mifano ya kipagani?

“Pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari [Beliali; Shetani]? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai. . . . Kwa hiyo, Tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema Bwana, msiguse kitu kilicho kichafu, nami nitawakaribisha. Nitakuwa Baba kwenu, nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike, asema Bwana Mwenyezi.”—2 Kor. 6:14-18, UV.

Je, inawezekana washiriki wote wa kikundi cha kidini wawe watakatifu na hivyo wasiwe na dhambi?

Ni kweli kwamba wote waliokuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza walikuwa watakatifu. (1 Kor. 14:33, 34; 2 Kor. 1:1; 13:13, UV, ZSB) Wanasimuliwa kama watu waliopokea “msamaha wa dhambi” na “waliotakaswa” na Mungu. (Mdo. 26:18; 1 Kor. 1:2, UV, ZSB) Hata hivyo, wao hawakudai kuwa hawana dhambi yoyote. Walizaliwa wakiwa wazao wa Adamu mtenda-dhambi. Urithi huo mara nyingi uliwafanya wang’ang’ane ili kufanya yaliyokuwa sawa, kama mtume Paulo alivyokiri kwa unyenyekevu. (Rom. 7:21-25) Na mtume Yohana alisema hivi waziwazi: “Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu.” (1 Yoh. 1:8, UV) Kwa hiyo, kuwa mtakatifu katika maana ambayo neno hilo linatumiwa kuwahusu wafuasi wa kweli wa Kristo hakumaanishi kwamba wao hawana dhambi yoyote katika mwili.

Kwa habari ya kama Wakristo wote wa kweli leo ni watakatifu walio na tumaini la kuishi mbinguni, ona ukurasa wa 200-204.

Mtu Akisema—

‘Je, unaamini watakatifu?’

Unaweza kujibu hivi: ‘Unamaanisha watakatifu gani?’ Mtu huyo akimtaja Maria na/au mitume, labda unaweza kuongeza hivi: (1) ‘Ndiyo, wanatajwa katika Maandiko Matakatifu, nami naamini yaliyoandikwa humo. Lakini hasa napendezwa na yale wanayofanya leo na jinsi yanavyotuhusu sisi, na je, wewe? . . . Nimeona jambo fulani lenye kupendeza sana juu yao humu katika Maandiko Matakatifu, nami ningependa nilisome pamoja na wewe. (Ufu. 5:9, 10)’ [Angalia, kwa ajili ya matumizi ikiwa swali linatokezwa kuhusu maneno yanayotumiwa katika andiko hilo: UV husema “wanamiliki juu ya nchi.” ZSB husema “wanatawala juu ya dunia.” VB husema “wataitawala dunia.” Lakini BHN husema “watatawala duniani.” NAJ husema “watatawala ulimwenguni.”] (2) ‘Uzima chini ya serikali hiyo utakuwaje? (Ufu. 21:2-4)’

Au unaweza kusema (ikiwa wakati fulani wewe ulikuwa Mkatoliki): ‘Kwa miaka mingi nilishiriki katika sikukuu za watakatifu nami nilisali kwao kwa ukawaida. Kisha nikasoma jambo fulani katika Maandiko Matakatifu lililonifanya kufikiria yale niliyokuwa nikifanya. Tafadhali, acha nikuonyeshe jambo hilo. (Ona ukurasa wa 406.)’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki