Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 3/1 kur. 25-28
  • Je, Waogopa Kuwa na Itibari Katika Wengine?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Waogopa Kuwa na Itibari Katika Wengine?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuelewa Hofu Hiyo
  • Kwa Nini Ni Lazima Kizuizi Hicho Kiondolewe?
  • Kuwa na Itibari Katika Familia Yako
  • Kuwa na Itibari Katika Kutaniko
  • Jinsi ya Kujenga Mahusiano Yenye Itibari
  • Unaweza Kuwatumaini Ndugu Zako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Wazee Ilindeni Amana Yenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Unaweza Kugeukia Wapi Ukiwa na Matumaini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kuwatumaini Wengine Ni Muhimu kwa Maisha Yenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 3/1 kur. 25-28

Je, Waogopa Kuwa na Itibari Katika Wengine?

‘HAKUNA mtu niwezaye kusema naye. Watu hawataelewa. Wanashughulikia mno matatizo yao wenyewe. Hawana wakati kwa matatizo yangu.’ Wengi huhisi hivyo, kwa hiyo hawafunui mambo kwa wengine. Wengine wanapowauliza hali yao, mara nyingi wao hutaka kuwaambia, lakini hawafanyi hivyo. Hawawezi hata kidogo kufunua mambo kwa uhuru.

Ni kweli, kuna wale ambao hawataki msaada kutoka kwa wengine. Hata hivyo, wengi wanataka msaada sana lakini wanaogopa kufunua mawazo yao, hisia zao, na mambo waliyoona ya kibinafsi sana. Je, wewe ni mmojawapo? Je, kwa kweli hakuna yeyote ambaye waweza kuwa na itibari katika yeye?

Kuelewa Hofu Hiyo

Katika ulimwengu wa leo kuna hali ya kutokuwa na itibari katika wengine. Vijana hawazungumzi na wazazi wao. Wazazi hawawezi kuzungumziana. Ni wachache walio tayari kuzungumza na wale wenye mamlaka. Kwa sababu ya kutoweza kufunulia wengine mambo ya siri, watu fulani wanageukia alkoholi, dawa za kulevya, au mtindo-maisha wa kufanya vyovyote ili kujaribu kuepuka matatizo yao.—Mithali 23:29-35; Isaya 56:12.

Kuwa na uhakika katika wale wenye mamlaka, kama vile makasisi, madaktari, matabibu, na walimu, kumetikiswa na ufunuo mbalimbali usio na mwisho wa ukosefu wa ufuatiaji haki na ukosefu wa adili. Kwa kielelezo, kadirio moja lasema kwamba asilimia zaidi ya 10 ya makasisi wanahusika katika mwenendo mbaya wa kingono. Watu hao “wavunja-itibari,” asema mwandishi mmoja, “wanachimba magenge marefu na nyufa katika mahusiano ya kibinadamu.” Hilo laathirije makutaniko yao? Linaharibu itibari.

Kuenea sana kwa mvunjiko wa adili kumeongoza pia kwenye hali ya hatari katika familia, kufikia hatua ya kwamba familia zenye kasoro karibu ziwe jambo la kawaida, wala si jambo lisilo la kawaida. Wakati mmoja nyumbani mlikuwa mazingira yenye kujenga. Leo mara nyingi ni kama mahali pa kujazia petroli wakati wa chakula. Mtoto akuapo katika familia ambamo hamna “shauku ya kiasili,” tokeo la kawaida ni kutoweza kuwa na itibari katika wengine wakati wa utu mzima.—2 Timotheo 3:3.

Zaidi ya hayo, hali za ulimwengu zizidipo kuwa mbaya, twazidi kuwekwa katika mambo yawezayo kuwa yenye kufadhaisha. Katika hali sawa na hiyo, nabii Mika aliandika hivi: “Usiamini rafiki.” (Mika 7:5) Huenda ukahisi vivyo hivyo baada ya tukio dogo lenye kutamausha, kusalitiwa na rafiki, au tukio kubwa lenye kutisha uhai. Waona vigumu kuwa na itibari katika wengine tena na watiwa ganzi kihisia-moyo, ukiishi kila siku ukiwa nyuma ya kizuizi cha kihisia-moyo. (Linganisha Zaburi 102:1-7.) Ni kweli, mtazamo wa aina hiyo huenda ukakusaidia ukabiliane na hali, lakini “huzuni ya moyo” wako yakunyang’anya shangwe yoyote ya kweli maishani. (Mithali 15:13) Ukweli ni kwamba, ili uwe na afya ya kiroho, ya kihisia-moyo, ya kiakili, na ya kimwili, lazima kizuizi hicho kiondolewe na lazima ujifunze kuwa na itibari katika watu. Je, hilo lawezekana? Ndiyo.

Kwa Nini Ni Lazima Kizuizi Hicho Kiondolewe?

Kufunulia wengine mambo ya siri huleta kitulizo kwa moyo wenye usumbufu. Hana alipatwa na jambo hilo. Alikuwa na ndoa nzuri, makao yenye usalama, lakini alisononeka sana. Ingawa “alikuwa na uchungu rohoni,” kwa hekima ‘alimwomba BWANA’ kwa nguvu iliyofanya midomo yake kimya itetemeke. Ndiyo, alimfunulia Yehova mambo ya siri. Kisha akafunua moyo wake kwa Eli, mwakilishi wa Mungu. Tokeo likawa nini? “[Hana] akaenda zake, naye akala chakula, wala uso wake haukukunjamana tena.”—1 Samweli 1:1-18.

Tamaduni zilizo nyingi zimejua manufaa za mazungumzo ya kufunua mambo ya siri. Kwa kielelezo, kushiriki mawazo na mambo yaliyoonwa pamoja na wale ambao wamepatwa na hali hizohizo kwaweza kuthibitika kuwa jambo lenye kunufaisha. Watafiti wanafikia mkataa huu: “Kujitenga kihisia-moyo hutokeza ugonjwa—twahitaji kufunua mambo ili kuendelea kuwa timamu akilini.” Utafiti mwingi wenye kuongezeka wa kisayansi wathibitisha ukweli wa mithali iliyopuliziwa isemayo: “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.”—Mithali 18:1.

Usipofunulia wengine mambo, wao waweza kukusaidiaje? Ingawa Yehova Mungu ni mchunguza mioyo, familia na marafiki hawajui mawazo yako na hisia zako za ndani kabisa—isipokuwa ufunue mambo. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Tatizo likihusisha ukiukaji wa sheria ya Mungu, kuahirisha ungamo la jambo hilo hufanya liwe baya zaidi.—Mithali 28:13.

Kwa hakika, kuna manufaa nyingi zaidi katika kufunulia wengine msononeko wa siri kuliko hatari za kuumizwa. Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba twapaswa kufunua mambo madogomadogo ya kibinafsi bila busara. (Linganisha Waamuzi 16:18; Yeremia 9:4; Luka 21:16.) “Ajifanyiaye rafiki wengi ni kwa uangamivu wake mwenyewe,” Mithali 18:24 yaonya lakini kisha yaongeza hivi: “Yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.” Waweza kupata wapi rafiki wa aina hiyo?

Kuwa na Itibari Katika Familia Yako

Ikiwa una tatizo, je, umejaribu kuzungumza juu yalo pamoja na mwenzi wako wa ndoa au pamoja na wazazi wako? “Kwa habari ya matatizo mengi, jambo linalohitajiwa tu ni kuzungumza juu yayo kirefu,” akiri mshauri mmoja mwenye uzoefu. (Mithali 27:9) Waume Wakristo ‘wawapendao wake zao kama wao wenyewe,’ wake walio “katika ujitiisho kwa waume zao,” na wazazi wachukuao kwa uzito daraka lao walilogawiwa na Mungu la “kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova” watajitahidi kuwa wasikilizaji wenye hisia-mwenzi na washauri wenye kusaidia. (Waefeso 5:22, 33; 6:4) Ingawa hakuwa na mke wala watoto wa kimwili, Yesu aliweka kielelezo cha ajabu kama nini katika habari hii!—Marko 10:13-16; Waefeso 5:25-27.

Namna gani ikiwa tatizo haliwezi kusuluhishwa katika familia? Katika kutaniko la Kikristo, hatuhitaji kuwa peke yetu kamwe. “Ni nani aliye dhaifu, nami si dhaifu?” akasema mtume Paulo. (2 Wakorintho 11:29) Alionya kwa upole hivi: “Endeleeni kuchukuliana mizigo yenye kulemea.” (Wagalatia 6:2; Waroma 15:1) Miongoni mwa ndugu na dada zetu wa kiroho, bila shaka twaweza kupata “ndugu [zaidi ya mmoja ambaye] amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17.

Kuwa na Itibari Katika Kutaniko

Katika yale makutaniko zaidi ya 80,000 ya Mashahidi wa Yehova duniani pote, kuna wanaume wanyenyekevu wanaotumikia wakiwa “wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu.” (2 Wakorintho 1:24) Hao ni wazee. “[“Kila mmoja,” NW],” asema Isaya “atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” Hivyo ndivyo wazee hujitahidi kuwa.—Isaya 32:2; 50:4; 1 Wathesalonike 5:14.

Wazee hutimiza matakwa ya Kimaandiko kabla ya ‘roho takatifu kuwaweka rasmi.’ Kujua hilo kutaimarisha uhakika wako katika wao. (Matendo 20:28; 1 Timotheo 3:2-7; Tito 1:5-9) Yale unayozungumza pamoja na mzee yatabaki siri kabisa. Sifa moja ya ustahili wake ni kuwa mwenye kutumainika.—Linganisha Kutoka 18:21; Nehemia 7:2.

Wazee kutanikoni “wanafuliza kulinda juu ya nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu.” (Waebrania 13:17) Je, hilo halikusukumi uweke itibari yako katika wanaume hao? Kwa asili, si wazee wote walio bora katika sifa zilezile. Huenda wazee fulani wakaonekana kuwa wenye kufikika zaidi, wenye fadhili, au wenye uelewevu kuliko wengine. (2 Wakorintho 12:15; 1 Wathesalonike 2:7, 8, 11) Kwa nini usifunue mambo ya siri kwa mzee ambaye wahisi kuwa starehe naye?

Wanaume hao si wafanyakazi wa kitaaluma wanaolipwa mshahara. Badala ya hivyo, wao ni “zawadi zikiwa wanadamu,” walioandaliwa na Yehova ili kukusaidia. (Waefeso 4:8, 11-13; Wagalatia 6:1) Jinsi gani? Kwa kuitumia Biblia kwa ustadi, watatumia nguvu zayo za kuponya katika hali yako binafsi. (Zaburi 107:20; Mithali 12:18; Waebrania 4:12, 13) Watasali pamoja nawe na kwa ajili yako. (Wafilipi 1:9; Yakobo 5:13-18) Msaada kutoka kwa washauri hao wenye upendo waweza kuchangia sana katika kuponya roho yenye usumbufu na kurudisha amani ya akilini.

Jinsi ya Kujenga Mahusiano Yenye Itibari

Kuomba msaada, shauri, au sikio lenye kusikiliza tu si ishara ya udhaifu au ya kushindwa. Ni kukiri kihalisi tu kwamba sisi si wakamilifu na kwamba hakuna yeyote yule aliye na majibu yote. Kwa hakika, mshauri na msiri mkuu zaidi tuliye naye ni Baba yetu wa kimbingu, Yehova Mungu. Twakubaliana na mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “BWANA ni nguvu zangu na ngao yangu. Moyo wangu umemtumaini nami nimesaidiwa.” (Zaburi 28:7) Twaweza ‘kumfunulia kabisa mioyo yetu’ katika sala wakati wowote ule, tukiwa na uhakika kwamba asikia na atujali.—Zaburi 62:7, 8; 1 Petro 5:7.

Waweza kujifunzaje kuwa na itibari katika wazee na wengine kutanikoni? Kwanza, jichunguze mwenyewe. Je, hofu zako zina msingi thabiti? Je, wewe watilia shaka nia za wengine? (1 Wakorintho 13:4, 7) Je, kuna njia ya kupunguza hatari za kuumizwa? Ndiyo. Jinsi gani? Katika kikao cha kiroho, jaribu kufahamiana na wale unaotaka kuwafunulia mambo ya siri. Zungumza nao kwenye mikutano ya kutaniko. Shiriki pamoja nao katika mahubiri ya nyumba hadi nyumba. Sawa na staha, lazima itibari ichumwe. Kwa hiyo uwe na subira. Kwa kielelezo, upatapo kumjua kuwa mchungaji wa kiroho, uhakika wako kwake, utaongezeka. Funua mahangaiko yako hatua kwa hatua. Akiitikia kwa njia ifaayo, yenye huruma, na ya busara, waweza basi kujaribu kufunua mambo mengine.

Waabudu wenzako wa Yehova, hasa wazee Wakristo, hujitahidi kuiga sifa za Mungu zenye kupendekeza katika mahusiano ya wao kwa wao. (Mathayo 5:48) Hilo latokeza mazingira ya itibari kutanikoni. Mmoja ambaye amekuwa mzee kwa muda mrefu asema hivi: “Lazima ndugu wajue jambo moja: Liwe ni jambo gani mtu afanya, mzee hapotezi upendo wake wa Kikristo kumwelekea mtu huyo. Huenda asipende jambo lililofanywa, lakini bado ampenda ndugu yake na ataka kumsaidia.”

Basi hakuna haja ya kuhisi upweke ukiwa na tatizo. Zungumza na mtu aliye na “sifa za ustahili wa kiroho” awezaye kukusaidia uchukue mzigo wako wenye kulemea. (Wagalatia 6:1) Kumbuka kwamba “uzito katika moyo wa mtu huuinamisha,” lakini “maneno yapendezayo ni kama sega la asali; ni tamu nafsini, na afya mifupani.”—Mithali 12:25; 16:24.

[Sanduku katika ukurasa wa 26]

Huenda Mkristo yeyote akahitajiwa kumtolea msaada mtu wa ukoo, rafiki, au ndugu wa kiroho mwenye tatizo la kibinafsi. Je, wajua jinsi ya kusaidia?

Mshauri Mwenye Matokeo

ni mwenye kufikika: Mathayo 11:28, 29; 1 Petro 1:22; 5:2, 3

huchagua kikao kifaacho: Marko 9:33-37

hujaribu kuelewa tatizo: Luka 8:18; Yakobo 1:19

haitikii kupita kiasi: Wakolosai 3:12-14

husaidia mtu akabiliane na hisia-moyo zenye kuumiza: 1 Wathesalonike 5:14; 1 Petro 3:8

ajua mipaka yake: Wagalatia 6:3; 1 Petro 5:5

hutoa shauri hususa: Zaburi 19:7-9; Mithali 24:26

huweka siri: Mithali 10:19; 25:9

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki