Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 4/1 kur. 9-13
  • Jipeni Moyo Kadiri Ukombozi Ukaribiavyo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jipeni Moyo Kadiri Ukombozi Ukaribiavyo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Nyakati za Hatari Zilizo Ngumu Kushughulika Nazo”
  • Hakuna Wokovu Kupitia Wanadamu
  • Ukombozi Wakaribia —Kwa Ajili ya Nani?
  • Mkombozi Mkuu
  • Ukombozi Mbalimbali Katika Wakati Uliopita
  • Tayarisha kwa Ajili ya Kukombolewa Kuingia Ndani ya Ulimwengu Mpya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Ukombozi Kupitia Ufalme wa Mungu Uko Karibu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Kichwa cha Mazungumzo
    Huduma Yetu ya Ufalme—1991
  • Je, Unathamini Yale Ambayo Yehova Amefanya Ili Kukukomboa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 4/1 kur. 9-13

Jipeni Moyo Kadiri Ukombozi Ukaribiavyo

“Nipo pamoja nawe, asema BWANA, ili nikuokoe [“nikukomboe,” “NW”].”—YEREMIA 1:19.

1, 2. Kwa nini familia ya kibinadamu inahitaji ukombozi?

UKOMBOZI! Ni neno lenye kufariji kama nini! Kukombolewa kwamaanisha kuokolewa, kuwekwa huru kutokana na hali mbaya isiyofurahisha. Huko hutia ndani wazo la kuletwa kwenye hali nzuri zaidi, na zenye furaha zaidi.

2 Sasa jamii ya kibinadamu yahitaji ukombozi huo sana kama nini! Watu kila mahali wanalemewa na kuvunjwa moyo na matatizo magumu—ya kiuchumi, ya kijamii, ya kimwili, ya kiakili, na ya kihisia-moyo. Watu walio wengi hawaridhishwi na wametamaushwa na jinsi ulimwengu unavyoelekea nao wangependa hali ibadilike iwe nzuri.—Isaya 60:2; Mathayo 9:36.

“Nyakati za Hatari Zilizo Ngumu Kushughulika Nazo”

3, 4. Kwa nini kuna uhitaji mkubwa zaidi wa ukombozi sasa?

3 Kwa kuwa karne hii ya 20 imekuwa na kuteseka kwingi zaidi ya karne nyingine yoyote, kuna uhitaji mkubwa zaidi wa ukombozi sasa kuliko wakati mwingine wowote. Leo, zaidi ya watu bilioni moja wanaishi katika ufukara, na watu wapatao milioni 25 wanaongezeka kwenye idadi hiyo kila mwaka. Kila mwaka watoto wapatao milioni 13 hufa kutokana na utapiamlo au sababu nyingine zinazohusiana na umaskini—watoto zaidi ya 35,000 kila siku! Na mamilioni ya watu wazima hufa mapema kutokana na magonjwa mbalimbali.—Luka 21:11; Ufunuo 6:8.

4 Vita na misukosuko ya kiraia yamesababisha kuteseka kwingi sana. Kitabu Death by Government chasema kwamba vita, zogo la kikabila na la kidini, na serikali mbalimbali kuwaua kimakusudi wengi wa raia zazo zenyewe “zimesababisha vifo vya watu zaidi ya milioni 203 katika karne hii.” Chaendelea kusema hivi: “Idadi kamili ya waliokufa ingeweza kuwa karibu watu milioni 360. Ni kana kwamba spishi yetu imeangamizwa kabisa na Tauni Nyeusi. Kwa kweli imeangamizwa kabisa, sio kwa viini bali kwa tauni ya Mamlaka.” Mwandishi Richard Harwood alisema hivi: “Vita vya ujahili vya karne zilizopita kwa ulinganifu vilikuwa vidogo na visivyotokeza kamwe.”—Mathayo 24:6, 7; Ufunuo 6:4.

5, 6. Ni nini kinachofanya wakati wetu uwe wenye kusononesha sana?

5 Kwa kuongezea zile hali za kusononesha za miaka ya majuzi ni lile ongezeko kubwa katika uhalifu wenye jeuri, ukosefu wa adili, na kuvunjika kwa familia. William Bennett, aliyekuwa Katibu wa Elimu wa Marekani hapo zamani alisema kwamba katika miaka 30 idadi ya watu wa Marekani iliongezeka kwa asilimia 41, lakini uhalifu wenye jeuri uliongezeka kwa asilimia 560, kuzaliwa kwa watoto haramu kwa asilimia 400, talaka kwa asilimia 300, na kiwango cha kujiua kwa matineja kwa asilimia 200. John DiIulio, Jr., Profesa wa Chuo Kikuu cha Princeton alionya juu ya idadi yenye kuongezeka ya “wanyama-wawindaji walio hodari,” ambao “huua kimakusudi, hushambulia, hubaka, hunyang’anya, huvunja nyumba na kusababisha matatizo mazito ya kijumuiya. Hawahofu fedheha ya kukamatwa, maumivu ya kufungwa, au utungu wa dhamiri.” Katika nchi hiyo, kuua watu wengine sasa ndiko kisababishi kikuu cha pili cha vifo miongoni mwa wenye umri wa kati ya miaka 15 na miaka 19. Na watoto wengi zaidi walio chini ya umri wa miaka minne wanakufa kutokana na kutumiwa vibaya kuliko kutokana na maradhi.

6 Uhalifu na ujeuri wa aina hiyo haupatikani katika taifa moja tu. Nchi nyingi huripoti maelekeo hayohayo. Lenye kuchangia hayo ni lile ongezeko la matumizi ya dawa za kulevya yanayofisidi mamilioni ya watu. Gazeti la habari la Australia Sydney Morning Herald lilisema hivi: “Ulanguzi wa dawa za kulevya wa kimataifa umekuwa biashara ya pili kwa ukubwa ulimwenguni ikifuata biashara ya silaha.” Jambo lingine ni ujeuri na ukosefu wa adili ambao kwa sasa umejaa katika televisheni. Katika nchi nyingi, kufikia wakati ambapo mtoto hufikia umri wa miaka 18, huwa ameona makumi ya maelfu ya matendo ya ujeuri katika televisheni na matendo yasiyo ya adili yasiyohesabika. Huo ni uvutano mkubwa wenye kufisidi, kwa kuwa utu wetu hufanyizwa kwa yale tunayolisha akili zetu kwa ukawaida.—Waroma 12:2; Waefeso 5:3, 4.

7. Unabii wa Biblia ulitabirije hali mbaya zilizopo leo?

7 Unabii wa Biblia ulitabiri kwa usahihi mwelekeo huu mbovu wa matukio katika karne yetu. Ulisema kwamba kungekuwako vita vya tufeni pote, mweneo wa maradhi, upungufu wa chakula, na uasi-sheria wenye kuongezeka. (Mathayo 24:7-12; Luka 21:10, 11) Na tunapofikiria unabii uliorekodiwa kwenye 2 Timotheo 3:1-5, ni sawa na kusikiliza taarifa ya habari ya kila siku. Huo hutambulisha muhula wetu kuwa “siku za mwisho” nao hufafanua watu kuwa ‘wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wasiotii wazazi, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu.’ Hivyo ndivyo ulimwengu ulivyo kabisa leo. Kama alivyokiri William Bennett: “Kuna ishara nyingi mno za . . . ustaarabu uliooza.” Hata imesemwa kwamba ustaarabu uliisha wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.

8. Kwa nini Mungu alileta lile Furiko katika siku ya Noa, na hilo lahusianaje na siku yetu?

8 Hali sasa ni mbaya zaidi kuliko ile ya kabla ya Furiko la siku ya Noa, ‘dunia ilipojaa dhuluma.’ Wakati huo, watu kwa ujumla walikataa kutubu njia zao mbaya. Hivyo, Mungu akasema: “Wameijaza dunia dhuluma, basi nitawaharibu pamoja na dunia.” Gharika ilikomesha ulimwengu huo wenye jeuri.—Mwanzo 6:11, 13; 7:17-24.

Hakuna Wokovu Kupitia Wanadamu

9, 10. Kwa nini tusiwategemee wanadamu waandae ukombozi?

9 Je, jitihada za kibinadamu zaweza kutukomboa kutokana na hali hizi mbaya? Neno la Mungu lajibu hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Zaburi 146:3; Yeremia 10:23) Maelfu ya miaka ya historia yamethibitisha kweli hizo. Wanadamu wamejaribu kila mfumo uwezao kuwaziwa wa kisiasa, wa kiuchumi, na wa kijamii, lakini hali zimekuwa mbaya zaidi. Kungalikuwa na suluhisho la kibinadamu, ingalikuwa wazi kufikia sasa. Badala ya hivyo, uhalisi ni kwamba “mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9, Union Version chapa ya 1989; Mithali 29:2; Yeremia 17:5, 6.

10 Miaka michache iliyopita, Zbigniew Brzezinski, aliyekuwa mshauri wa usalama wa kitaifa hapo zamani, alisema hivi: “Mkataa usioepukika wa uchanganuzi wowote usiopendelea upande wowote wa mielekeo ya tufeni pote ni kwamba msukosuko wa kijamii, ghasia za kisiasa, matatizo ya kiuchumi, na ugomvi kati ya mataifa huenda yakasambaa zaidi.” Aliongeza hivi: “Tisho wanaloelekeana nalo wanadamu [ni] mchafuko wa utawala duniani pote.” Makadirio hayo juu ya hali za ulimwengu ni yenye nguvu hata zaidi leo. Ukieleza juu ya muhula huu wa ujeuri ulioongezeka, uhariri katika gazeti Register la New Haven, Connecticut, ulitangaza hivi: “Yaonekana tumeenda sana tusiweze kusimama.” La, kuharibika kwa ulimwengu huu hakutasimama, kwa kuwa unabii juu ya “siku [hizi] za mwisho” ulisema hivi pia: “Watu waovu na walaghai wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi, wakiongoza vibaya na kuwa wenye kuongozwa vibaya.”—2 Timotheo 3:13.

11. Kwa nini hali zinazozidi kuharibika hazitarekebishwa na jitihada za kibinadamu?

11 Wanadamu hawawezi kubadili mielekeo hiyo kwa kuwa Shetani ndiye “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4) Ndiyo, “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19; ona pia Yohana 14:30.) Kwa hakika Biblia husema hivi juu ya siku yetu: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameteremka kwenu, akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Shetani ajua kwamba utawala wake na ulimwengu wake wakaribia kwisha, kwa hiyo yeye ni kama “simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.”—1 Petro 5:8.

Ukombozi Wakaribia —Kwa Ajili ya Nani?

12. Ukombozi wakaribia kwa ajili ya nani?

12 Hali za dunia zinazozidi kuwa ngumu ni uthibitisho wenye kutokeza kwamba badiliko kubwa—kwelikweli, ukombozi mtukufu—wakaribia! Kwa ajili ya nani? Ukombozi wakaribia kwa ajili ya wale wanaokazia uangalifu zile ishara za kuonya na wanaotenda kupatana nazo. Yohana wa Kwanza 2:17 huonyesha jambo ambalo lazima lifanywe: “Ulimwengu [mfumo wa mambo wa Shetani] unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—Ona pia 2 Petro 3:10-13.

13, 14. Yesu alikaziaje uhitaji wa kukaa macho?

13 Yesu alitabiri kwamba jamii yenye ufisadi ya leo itafagiliwa mbali karibuni katika wakati wa taabu “namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu hadi sasa, la, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Hiyo ndiyo sababu alionya hivi: “Kazieni uangalifu kwa nyinyi wenyewe kwamba mioyo yenu isiwe kamwe yenye kulemewa na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara hiyo kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wote wale wanaokaa juu ya uso wa dunia yote. Basi, fulizeni kuwa macho wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia.”—Luka 21:34-36.

14 Wale ‘wanaokazia uangalifu’ na ‘kufuliza kuwa macho’ watatafuta mapenzi ya Mungu na kuyafanya. (Mithali 2:1-5; Waroma 12:2) Hao ndio ‘watakaofanikiwa kuponyoka’ uharibifu wa mfumo wa Shetani utakaoletwa hivi karibuni. Nao wanaweza kuwa na uhakika kamili kwamba watakombolewa.—Zaburi 34:15; Mithali 10:28-30.

Mkombozi Mkuu

15, 16. Mkombozi mkuu ni nani, na kwa nini tuna hakika kwamba hukumu zake zitakuwa adilifu?

15 Ili watumishi wa Mungu wakombolewe, Shetani na mfumo wake wote wa mambo ahitaji kuondolewa. Hilo lataka chanzo cha ukombozi chenye nguvu zaidi ya wanadamu. Chanzo hicho ni Yehova Mungu, Mwenye Enzi Kuu Mkuu Kuliko Wote, Muumba mweza yote wa ulimwengu wote mzima wenye kutisha. Yeye ndiye Mkombozi mkuu: “Mimi, naam, mimi, ni BWANA, zaidi yangu mimi hapana mwokozi.”—Isaya 43:11; Mithali 18:10.

16 Katika Yehova hukaa kiasi kikubwa zaidi cha nguvu, hekima, haki, na upendo. (Zaburi 147:5; Mithali 2:6; Isaya 61:8; 1 Yohana 4:8) Kwa hiyo atekelezapo hukumu zake, twaweza kuwa na hakika kwamba matendo yake yatakuwa maadilifu. Abrahamu aliuliza hivi: “Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?” (Mwanzo 18:24-33) Paulo alitangaza hivi: “Je, kwa Mungu kuna ukosefu wa haki? Hilo lisipate kuwa hivyo kamwe!” (Waroma 9:14) Yohana aliandika hivi: “Ndiyo, Yehova Mungu, Mweza-Yote, ni ya kweli na ya uadilifu maamuzi yako ya kihukumu.”—Ufunuo 16:7.

17. Watumishi wa Yehova wa wakati uliopita wameonyeshaje uhakika katika ahadi zake?

17 Yehova anapoahidi ukombozi, bila shaka atautimiza. Yoshua alisema hivi: “Halikuanguka neno lolote katika jambo lolote lililokuwa ni jema ambalo BWANA alikuwa amelinena.” (Yoshua 21:45) Solomoni alitaarifu hivi: “Halikukosa kupatikana neno lolote katika ahadi yake njema.” (1 Wafalme 8:56) Mtume Paulo alisema kwamba Abrahamu “hakusitasita kwa ukosefu wa imani, . . . akisadikishwa kikamili kwamba alilokuwa ameahidi [Mungu] alikuwa na uwezo pia wa kufanya.” Sara hali kadhalika “alimkadiria [Mungu] kuwa mwaminifu yeye aliyekuwa ameahidi.”—Waroma 4:20, 21; Waebrania 11:11.

18. Kwa nini watumishi wa Yehova leo wanaweza kuwa na uhakika kwamba watakombolewa?

18 Tofauti na wanadamu, Yehova ni mwenye kutumainika kabisa, wa kweli katika neno lake. ‘BWANA wa majeshi ameapa, akisema, Hakika yangu kama vile nilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa; na kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotokea.’ (Isaya 14:24) Kwa hiyo Biblia isemapo kwamba “Yehova ajua jinsi ya kukomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, bali kuweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya siku ya hukumu ili kukatiliwa mbali,” twaweza kuwa na uhakika kwamba hilo litatukia. (2 Petro 2:9) Hata watishwapo kuharibiwa na adui wenye nguvu, watumishi wa Yehova hujipa moyo kwa sababu ya nia yake, inayoonyeshwa katika ahadi yake kwa mmojawapo wa manabii wake: “Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana nipo pamoja nawe, asema BWANA, ili nikuokoe.”—Yeremia 1:19; Zaburi 33:18, 19; Tito 1:2.

Ukombozi Mbalimbali Katika Wakati Uliopita

19. Yehova alimkomboaje Loti, kukiwa na ufanani gani kwa wakati wetu?

19 Twaweza kutiwa moyo sana kwa kukumbuka baadhi ya matendo ya Yehova ya kuokoa ya wakati uliopita. Mathalani, Loti ‘alitaabishwa sana’ na uovu wa Sodoma na Gomora. Lakini Yehova aliona “kilio” dhidi ya majiji hayo. Kwa wakati ufaao, alituma wajumbe wasihi Loti na familia yake waondoke eneo hilo mara moja. Tokeo likawa nini? Yehova “alimkomboa Loti mwadilifu,” na “kugeuza majiji ya Sodoma na Gomora kuwa majivu.” (2 Petro 2:6-8; Mwanzo 18:20, 21) Leo pia, Yehova huona kilio kwa habari ya uovu mzito wa ulimwengu huu. Wajumbe wake wa siku ya kisasa watakapokuwa wamemaliza kazi yao muhimu ya kuhubiri kufikia kiwango anachotaka, atatenda dhidi ya ulimwengu huu na kuwakomboa watumishi wake kama alivyomkomboa Loti.—Mathayo 24:14.

20. Fafanua ukombozi wa Yehova wa Israeli la kale kutoka Misri.

20 Katika Misri ya kale mamilioni ya watu wa Mungu walifanywa watumwa. Yehova alisema hivi juu yao: “Nimesikia kilio chao . . . nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe.” (Kutoka 3:7, 8) Hata hivyo, baada ya kuwaacha watu wa Mungu waende, Farao alibadili akili yake, akawafuatia akiwa na jeshi lake lenye uweza. Waisraeli walionekana wamenaswa kwenye Bahari Nyekundu. Hata hivyo Musa alisema hivi: “Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA atakaowafanyia leo.” (Kutoka 14:8-14) Yehova alitenganisha Bahari Nyekundu, na Waisraeli wakaponyoka. Majeshi ya Farao yakawafuatia mbio, lakini Yehova alitumia nguvu zake hivi kwamba “bahari ikawafunikiza; wakazama kama risasi ndani ya maji makuu.” Baadaye Musa alichachawa katika kumwimbia Yehova hivi: “Ni nani aliye kama wewe, mtukufu katika utakatifu, mwenye kuogopwa katika sifa zako, mfanya maajabu?”—Kutoka 15:4-12, 19.

21. Watu wa Yehova waliokolewaje kutoka Amoni, Moabu, na Seiri?

21 Kwenye pindi nyingine, mataifa adui ya Amoni, Moabu, na Seiri (Edomu) yalitisha kuwaharibu watu wa Yehova. Yehova alisema hivi: “Msiogope, wala msifadhaike kwa ajili ya jeshi kubwa hili; kwani vita si yenu bali ni ya Mungu. . . . Hamtahitaji kupigana vita . . . simameni mkauone wokovu wa BWANA ulio pamoja nanyi.” Yehova aliwakomboa watu wake kwa kuwavuruga wale adui wengi hivi kwamba walichinjana.—2 Mambo ya Nyakati 20:15-23.

22. Ni ukombozi gani wa kimuujiza kutoka Ashuru alioandaa Yehova kwa ajili ya Israeli?

22 Serikali ya Ulimwengu ya Ashuru ilipokuja dhidi ya Yerusalemu, Mfalme Senakeribu alimdhihaki vikali Yehova kwa kuwaambia watu waliokuwa ukutani hivi: “Katika miungu yote ya nchi hizi [nilioshinda] waliookoa nchi yao na mkono wangu hata BWANA auokoe Yerusalemu na mkono wangu?” Kwa watumishi wa Mungu alisema hivi: “Wala msimwache Hezekia kuwatia moyo wa kumtumaini BWANA; akisema, BWANA bila shaka atatuokoa.” Kisha Hezekia akasali kwa bidii kwa ajili ya ukombozi, “falme zote za dunia zipate kujua kwamba wewe ndiwe BWANA, wewe peke yako.” Yehova aliwaangamiza askari-jeshi 185,000 wa Ashuru, na watumishi wa Mungu wakakombolewa. Baadaye, Senakeribu alipokuwa akiabudu mungu asiye wa kweli, wana wake walimuua.—Isaya, sura ya 36 na ya 37.

23. Ni maswali yapi juu ya ukombozi leo yanayohitaji kujibiwa?

23 Kwa kweli twaweza kujipa moyo tuonapo jinsi Yehova alivyowakomboa kiajabu watu wake katika nyakati zilizopita. Namna gani leo? Hivi karibuni watumishi wake waaminifu wataingia katika hali gani hatari ambayo itataka ukombozi wake wa kimuujiza? Kwa nini amengoja hadi sasa kabla ya kuleta ukombozi wao? Kutakuwa na utimizo gani wa maneno haya ya Yesu: “Mambo haya yaanzapo kutukia, jisimamisheni wenyewe wima na kuinua vichwa vyenu juu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia”? (Luka 21:28) Na ukombozi wa watumishi wa Mungu ambao tayari wamekufa utakujaje? Makala ifuatayo itachunguza maswali hayo.

Maswali ya Kupitia

◻ Kwa nini kuna uhitaji mkubwa wa ukombozi?

◻ Kwa nini tusiwategemee wanadamu waandae ukombozi?

◻ Ukombozi wakaribia kwa ajili ya nani?

◻ Kwa nini twaweza kuwa na uhakika katika ukombozi wa Yehova?

◻ Ni vielelezo gani vya ukombozi wa wakati uliopita vinavyotia moyo?

[Picha katika ukurasa wa a10]

Abrahamu alikuwa miongoni mwa wale waliokuwa na uhakika kamili katika Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki