Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je, ingeweza kusemwa kwamba uelewevu uliofanywa uwe wa kisasa juu ya neno “kizazi” kwenye Mathayo 24:34 unaruhusu wazo la kwamba mwisho wa mfumo wa mambo ungeweza kuahirishwa hadi mbali sana wakati ujao?
Bila shaka sivyo ilivyo. Kinyume cha hilo, huo uelewevu ulioboreshwa wa majuzi juu ya jambo hilo wapaswa kutusaidia kufuliza kuutarajia mwisho daima. Kwa nini yaweza kusemwa hivyo?
Kama vile Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1995, lilivyoeleza, Yesu alitumia fungu la maneno “kizazi hiki” kuhusu watu waovu wa wakati huo. (Mathayo 11:7, 16-19; 12:39, 45; 17:14-17; Matendo 2:5, 6, 14, 40) Kwa hakika huo haukuwa ufafanuzi wa urefu hususa wa wakati wenye kuanzia na tarehe mahususi.
Kwa hakika, “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo hilohilo la Mnara wa Mlinzi lilikazia mambo mawili ya msingi: “Kizazi cha watu hakiwezi kuonwa kuwa kipindi chenye miaka fulani hususa” na “Watu wa kizazi kimoja huishi kwa muda mfupi kwa kulinganishwa.”
Mara nyingi sisi hutumia “kizazi” kwa njia hiyo. Kwa kielelezo, huenda tukasema, ‘Askari-jeshi wa kizazi cha Napoléon hawakujua lolote juu ya ndege na bomu za atomu.’ Je, tungekuwa tukirejezea tu askari-jeshi waliozaliwa katika mwaka uleule aliozaliwa Napoléon? Je, tungekuwa tukirejezea tu wale askari-jeshi Wafaransa waliokufa kabla ya Napoléon kufa? Bila shaka sivyo; wala kwa utumizi huo wa “kizazi” kujaribu kuweka idadi fulani ya miaka. Ingawa hivyo, tungekuwa tukirejezea kipindi kifupi kwa kulinganishwa, si mamia ya miaka tangu wakati wa Napoléon hadi wakati ujao.
Ndivyo ilivyo na uelewevu wetu juu ya alichosema Yesu katika unabii wake uliotolewa kwenye Mlima wa Mizeituni. Utimizo wa sehemu tofauti-tofauti wa unabii huo wathibitisha kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo uko karibu. (Mathayo 24:32, 33) Kumbuka kwamba kulingana na Ufunuo 12:9, 10, Ufalme wa Mungu wa kimbingu uliposimamishwa katika 1914, Shetani alitupwa chini kwenye ujirani wa dunia. Kitabu cha Ufunuo chaongeza kwamba Shetani sasa ana hasira kubwa. Kwa nini? Kwa sababu ajua “ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:12.
Hivyo ilifaa kwamba Mnara wa Mlinzi la Novemba 1 lilikuwa na kichwa kidogo “Fulizeni Kulinda!” Fungu lifuatalo lilisema hivi kwa kufaa: “Hatuhitaji kujua wakati hasa wa matukio hayo. Badala ya hivyo, ni lazima tukazie fikira kuwa wenye kulinda, kusitawisha imani thabiti, na kuendelea kujishughulisha katika utumishi wa Yehova—si kuhesabu tarehe fulani.” Kisha likanukuu maneno haya ya Yesu: “Fulizeni kutazama, fulizeni kuwa macho, kwa maana hamjui ni lini ulio wakati uliowekwa rasmi. Lakini lile niwaambialo nyinyi nawaambia wote, Fulizeni kulinda.”—Marko 13:33, 37.