Ufuatiaji wa Haki—Kwa Kutukia au kwa Kuchagua?
“INGAWA kwa desturi mimi si mwenye kufuatia haki, nyakati nyingine mimi hufuatia haki kwa kutukia.” Ndivyo asemavyo mlaghai Autolycus katika kitabu The Winter’s Tale kilichoandikwa na William Shakespeare. Hilo latolea kielezi udhaifu wa msingi wa kibinadamu—mwelekeo wetu wa kufanya kosa, utokanao na ‘moyo mdanganyifu.’ (Yeremia 17:9; Zaburi 51:5; Waroma 5:12) Lakini je, hilo lamaanisha kwamba hatuna uchaguzi wowote katika hilo jambo? Je, tabia yenye wema wa adili ni jambo la kutukia tu? La hasha!
Kabla ya wana wa Israeli kuingia Bara Lililoahidiwa, Musa alisema nao walipokuwa wamepiga kambi kwenye nyanda za Moabu. Aliweka mbele yao machaguo mawili yaliyo dhahiri. Wangeweza kutii amri za Mungu na kupokea baraka yake au kuzikataa na kuvuna matunda machungu ya dhambi. (Kumbukumbu la Torati 30:15-20) Uchaguzi ulikuwa wao.
Kwa kuwa sisi ni viumbe hai walio huru kuchagua, sisi pia tuna uchaguzi. Hakuna yeyote—kutia na Mungu—atulazimishaye kufanya lililo zuri au kufanya lililo baya. Hata hivyo, huenda watu fulani wakauliza hivi kwa kufaa, ‘Ikiwa mioyo yetu ina mwelekeo wa kufanya lililo baya, twawezaje kufanya lililo zuri?’ Daktari wa meno hukagua kwa uangalifu meno ili aone mmomonyoko au wozo kabla haujaendelea kupita kiasi. Vivyo hivyo, twahitaji kuchungua mioyo yetu ya kitamathali tukitafuta udhaifu mbalimbali au wozo wa maadili. Kwa nini? Kwa sababu “kutoka moyoni huja mawazowazo maovu, mauaji-kimakusudi, uzinzi, uasherati, wizi, shuhuda zisizo za kweli, makufuru,” akasema Yesu.—Mathayo 15:18-20.
Ili kuhifadhi jino, daktari wa meno lazima aondoe kikamili wozo wowote unaopatikana. Hali kadhalika, hatua ya kukata maneno yahitajiwa ili kuondolea moyo “mawazowazo maovu” na tamaa zenye kosa. Kwa kusoma na kufikiria Neno la Mungu, Biblia, twapata kujua njia za Muumba wetu na pia twajifunza kufanya lililo sawa.—Isaya 48:17.
Mfalme Daudi wa Israeli alitumia kwa faida yake usaidizi zaidi uliohitajiwa katika vile vita vya kufanya lililo sawa. Alisali hivi: “Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.” (Zaburi 51:10) Ndiyo, kwa kumtegemea Yehova Mungu kwa sala, sisi pia twaweza kushinda mwelekeo wetu wa kufanya lililo baya na kukuza ‘roho iliyofanywa upya’ ili kufanya lililo zuri. Kwa njia hiyo, hatutaacha ufuatiaji wa haki utukie tu. Huo utakuwa uchaguzi.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Kama ilivyo katika kisa cha Daudi, sala kwa Yehova inaweza kutusaidia kufanya lililo zuri