Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Kukimbilia Tengenezo la Yehova la Kitheokrasi
ZAMANI sana nabii Isaya alisukumwa kutangaza hivi: ‘Mtukuzeni BWANA katika visiwa vya bahari.’ (Isaya 24:15) Mashahidi wa Yehova huviona visiwa vya bahari kuwa sehemu ya “dunia inayokaliwa” ambayo Yesu alisema “lazima habari njema ihubiriwe.”—Mathayo 24:14; Marko 13:10.
Visiwa vya Marquesas viko kilometa zipatazo 1,400 kaskazini-mashariki mwa Tahiti. Visiwa hivyo ni sehemu ya kikundi cha visiwa katika Pasifiki ya Kusini iitwayo French Polynesia. Vikiwa na udongo wa volkeno wenye rutuba, na tabia ya nchi yenye umajimaji na joto la kadiri, mimea husitawi katika visiwa hivi. Hata hivyo, visiwa vya Marquesas pia vinazaa matunda ya aina nyingine. Fikiria kisa cha familia moja iliyoitikia ujumbe wa Ufalme katika kisiwa cha Hiva Oa.
Jean na mke wake, Nadine, hawakufurahia ile iitwayo kwa kawaida jamii yenye kustaarabika ya Ulaya Magharibi ambamo waliishi. Hivyo waliamua kuacha nyuma mtindo-maisha huo wenye shughuli nyingi na kuhama pamoja na mtoto wao kwenda Visiwani Marquesas. Nyumba yao mpya, iliyojengwa kwa mianzi, ilikuwa imefichwa katika bonde lililokuwa mbali. Ili kufikia majirani wao wa karibu zaidi, walilazimika kusafiri kwa miguu kupitia kijia cha mlima wenye mawe kwa muda wa saa mbili. Kijiji kilichokuwa karibu zaidi na chenye daktari, shule na duka kilikuwa umbali wa mwendo wa muda wa saa tatu ukisafiri kwa gari aina ya jeep.
Jean na Nadine hawakupendezwa na dini. Hata hivyo, walishiriki katika mazungumzo juu ya asili ya uhai. Mara nyingi, wangetoa maelezo mengi juu ya nadharia tata za mageuzi. Lakini hakuna yoyote ya nadharia hizo ambayo iliwaletea uradhi.
Baada ya kuishi katika hali ya kujitenga kwa miaka sita, walishangaa kutembelewa na Mashahidi wa Yehova wawili. Hao Mashahidi walikuwa wamejua walipokuwa Jean na Nadine kutoka kwa wanavijiji waliokuwa karibu. Kwa urahisi, maongezi yaliongoza kwenye mazungumzo juu ya nadharia ya mageuzi. Kwa upendezi wa hao wenzi, hao Mashahidi wawili walikuwa wamebeba nakala ya kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Jean na Nadine walifurahi kupata kitabu kilichotoa uchunguzi wa kina juu ya jinsi uhai ulivyopata kuwa hapa.
Muda mfupi baadaye, funzo la Biblia lilianzishwa. Baada ya kipindi cha miaka mitatu, Jean na Nadine walifanya maendeleo bila kuacha. Walisadikishwa kwamba karibuni dunia nzima ingefanywa paradiso. Baada ya familia yao kuongezeka na kuwa yenye watoto watatu, kusafiri kwa muda wa saa nne ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme kukawa jambo gumu kwa kweli. Hata hivyo, jambo hilo halikuwazuia kuhudhuria mikutano. Hatimaye Jean na Nadine walionyesha wakfu wao kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Walifanya hivyo kwenye mkusanyiko uliofanywa katika kijiji kikuu, ambako hudhurio-kilele lilikuwa watu 38!
Ili kusaidia hicho kikundi kidogo cha watangazaji wa Ufalme, hiyo familia iliamua kuacha makao yao yaliyojitenga. Walihamia kijiji kilichokuwa na wakazi wapatao elfu moja, ambako Jean sasa hutumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova la mahali hapo. Familia hiyo, iliyokimbilia visiwani ili kuponyoka ustaarabu, huliona kuwa pendeleo kupata kimbilio la kweli, tengenezo la Yehova la kitheokrasi.