Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Kweli za Biblia Zaendelea Kuhubiriwa Katika Ireland
KATIKA miaka ya juzijuzi ile nchi yenye mandhari zenye kuvutia ya Ireland imekuwa mahali pa msukosuko mwingi. Wakati uleule, watu wa Ireland wameitikia vizuri ujumbe wa Biblia wenye tumaini walioletewa na Mashahidi wa Yehova. Mambo yafuatayo yaliyoonwa kutoka Ireland huthibitisha hilo.
■ Katika Dublin mmoja wa Mashahidi wa Yehova na binti yake mchanga walikuwa wakishiriki katika kazi ya kuhubiri mlango hadi mlango. Walikutana na mwanamke aitwaye Cathy aliyekuwa akiwashughulikia sana watoto wake wengi. Huyo Shahidi aliuliza ikiwa binti yake, aliyekuwa akijifunza jinsi ya kuhubiri, angeweza kushiriki ujumbe mfupi tu pamoja na mwanamke huyo. Cathy alikubali, na msichana huyo mdogo akatoa utoaji wa wazi, uliofikiriwa vizuri. Cathy alivutiwa na moyo mweupe na staha ya wazi ya kijana huyo, naye akakubali toleo la trakti ya Biblia.
Baadaye Cathy alifikiria utayarishaji na tabia nzuri ya mgeni wake mchanga. “Nilivutiwa kuona kwamba msichana mdogo aliweza kushiriki ujumbe huo wenye kupendeza bila kujivutia uangalifu,” akasema. “Nikaamua kwamba Mashahidi wa Yehova wazurupo mara nyingine, ningewasikiliza.”
Wakati uleule Cathy alihamia mji mdogo kusini-magharibi mwa Ireland karibu na mpaka wa majimbo ya Cork na Kerry. Wakati fulani baadaye Mashahidi wa Yehova walimtembelea, naye akawaalika ndani. Alikubali funzo la Biblia la kawaida na sasa huhudhuria mikutano ya kutaniko pamoja na watoto wake kadhaa. Cathy anashukuru kwa ajili ya tamaa ya moyoni ya huyo msichana mdogo ya kushiriki habari njema naye.
■ Katika eneo la Tullamore, Mashahidi walikuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja na mwanamke aitwaye Jean kwa kipindi cha zaidi ya miaka saba. Nyakati nyingine alionyesha kupendezwa, akakubali fasihi, lakini nyakati nyinginezo kupendezwa kwake kulififia. Siku moja, Shahidi aitwaye Frances na mwandamani fulani walimtembelea Jean, walimpata akiwa katika hali ya kuudhika sana. “Haidhuru tulilosema,” Shahidi huyo aripoti, “alizidi kuudhika. Hatimaye, akatuambia twende zetu akaufunga mlango kwa mshindo.”
Frances alijiuliza ikiwa kumtembelea zaidi kungetokeza tu hali iyo hiyo. ‘Labda haifai kumtembelea tena ikiwa kwa kweli hapendezwi na ujumbe,’ Frances akafikiri. Hata hivyo, alizungumzia jambo hilo na mume wake, Thomas, na mume huyo alikuwa mwenye tumaini zaidi. Walipokuwa katika eneo hilo mara nyingine, Jean alitembelewa tena. Alikuwa mwenye urafiki, akakubali nakala za magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ziara nyinginezo zilipendeza vilevile, na Thomas na Frances wakaanzisha funzo la Biblia nyumbani la kawaida pamoja naye.
Kwa nini kulikuwa na badiliko hilo? Jean aeleza kwamba wakati alipowaonyesha Mashahidi hali ya kukosa adabu kabisa, alikuwa ametoka kuzaa majuzi na alikuwa ametoka tu hospitalini. Kwa sababu ya kukinyonyesha kitoto chake kilichozaliwa karibuni na kulisha kwa kijiko mtoto wake mwenye umri mkubwa zaidi, alikuwa akilala usingizi wa muda wa saa moja na nusu tu kila usiku. “Jambo ambalo sikutaka kufanya hata kidogo,” asema Jean, “lilikuwa ni kuongea juu ya dini.”
Kabla ya miezi miwili kupita Jean alikuwa akihudhuria mikutano yote ya kutaniko, na kabla ya miezi minne kupita alikuwa akishiriki katika huduma ya shambani. Miezi kumi tangu alipoanza funzo lake la Biblia, alibatizwa. Sasa yale aliyojionea Jean humsaidia katika huduma. Asimulia hivi: “Nikikutana na mtu mwenye kukosa adabu sana, najaribu kuwa mwenye uelewevu zaidi. Sikuzote naandika jambo hilo. Labda hali itabadilika kufikia wakati ninaporudi; na huenda mtu huyo akawa ahisi afadhali na huenda akawa mwenye kuitikia zaidi.”