Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 6/15 kur. 4-8
  • Mungu Aliipuliziaje Biblia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mungu Aliipuliziaje Biblia?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jitihada Zenye Uangalifu Wenye Bidii Zahitajiwa
  • Shauri Lenye Kutumika —Kutoka kwa Nani?
  • Waandikaji wa Kibinadamu—Kwa Nini?
  • Biblia—Iliandikwa na Wanadamu Lakini Hata Hivyo Ni Ujumbe wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Ni Nani Aliyeitunga Biblia?
    Amkeni!—2007
  • ‘Waliongozwa na Roho Takatifu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Hekima ya “Neno la Mungu”
    Mkaribie Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 6/15 kur. 4-8

Mungu Aliipuliziaje Biblia?

UWASILIANO ni wenye kuvutia zaidi leo kuliko wakati mwingine wowote katika historia. Simu, mashine za faksi, kompyuta,—miaka mingi ambayo imepita ni nani angeweza kufikiria wakati ambapo ujumbe mbalimbali ungepelekwa karibu popote pale ulimwenguni mara moja?

Lakini aina ya uwasiliano iliyo ya kuvutia zaidi ni moja ambayo mwanadamu hawezi kuijua kabisa—upulizio wa kimungu. Yehova alipulizia waandikaji wa kibinadamu wapatao 40 kutokeza Neno lake lililoandikwa, Biblia Takatifu. Kama vile wanadamu walivyo na njia zaidi ya moja ya uwasiliano, hivyo Yehova alitumia njia kadhaa za uwasiliano ili kuyapulizia Maandiko.

Imla. Mungu aliwasilisha ujumbe mbalimbali mahususi ambao baadaye ulitiwa katika rekodi ya Biblia.a Kwa kielelezo, fikiria kanuni mbalimbali zinazofanyiza agano la Sheria. “Andika maneno haya,” Yehova akamwambia Musa, “kwa kuwa mimi nimefanya agano nawe, na pamoja na Israeli, kwa mujibu wa maneno haya.” (Kutoka 34:27) “Maneno” hayo, ambayo ‘yalipitishwa na malaika,’ yaliandikwa na Musa na yanaweza sasa kupatikana katika vitabu vya Biblia vya Kutoka, Mambo ya Walawi, Hesabu, na Kumbukumbu la Torati.—Matendo 7:53.

Manabii wengine wengi, wakitia ndani Isaya, Yeremia, Ezekieli, Amosi, Nahumu, na Mika, walipokea ujumbe mbalimbali mahususi kutoka kwa Mungu kupitia malaika. Nyakati nyingine wanaume hawa walianza matamko yao kwa fungu hili la maneno: “BWANA asema hivi.” (Isaya 37:6; Yeremia 2:2; Ezekieli 11:5; Amosi 1:3; Mika 2:3; Nahumu 1:12) Kisha waliandika yale ambayo Mungu alisema.

Maono, Ndoto, na Njozi. Ono ni mwono, mandhari, au ujumbe uliobandikwa juu ya akili ya mtu huku akiwa yu macho, kwa kawaida kupitia njia zisizo za kawaida. Kwa kielelezo, Petro, Yakobo, na Yohana, “walipopata kuamka kabisa,” waliona ono la Yesu aliyegeuka umbo. (Luka 9:28-36; 2 Petro 1:16-21) Katika visa fulani ujumbe uliwasilishwa katika ndoto, au ono la usiku, ukikazwa katika akili iliyofichika ya mpokeaji alipokuwa amelala. Hivyo Danieli aandika juu ya “njozi za [“maono ya,” NW] kichwa changu kitandani mwangu”—au, kama vile mtafsiri Ronald A. Knox anavyoitafsiri, “nilipokuwa nimelala huku nikitazama katika ndoto yangu.”—Danieli 4:10.

Mtu ambaye Yehova alitia katika njozi alikuwa kwa wazi amefyonzwa kabisa katika hali ya kukazia fikira kwa kina, ingawa alikuwa angalau hajalala kabisa. (Linganisha Matendo 10:9-16.) Katika Biblia neno la Kigiriki linalotafsiriwa “njozi” (ekʹsta·sis) humaanisha ‘kuondolea mbali au uhamisho.’ Ladokeza wazo la kubadilisha hali ya kawaida ya akili. Hivyo, mtu aliye katika njozi angekuwa hatambui mazingira yake ingawa angekuwa akipokea kikamili hilo ono. Mtume Paulo yamkini alikuwa katika njozi kama hiyo wakati “ali[po]nyakuliwa kuingia katika paradiso na kusikia maneno yasiyotamkika ambayo hairuhusiki kisheria mtu kuyasema.”—2 Wakorintho 12:2-4.

Tofauti na wale walionakili ujumbe mbalimbali wa kiimla kutoka kwa Mungu, waandikaji wa Biblia waliopokea maono au ndoto au walioona njozi, mara nyingi walikuwa na uhuru wa kufafanua katika maneno yao wenyewe yale waliyoona. Habakuki aliambiwa hivi: “Iandike njozi [“ono,” NW] ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili aisomaye apate kuisoma kama maji.”—Habakuki 2:2.

Je, hilo lamaanisha kwamba sehemu hizo za Biblia hazikupuliziwa kabisa kama zile zilizoto-lewa kiimla? La hasha. Kupitia roho yake, Yehova alikazia imara ujumbe wake katika akili ya kila mwandikaji, ili mawazo ya Mungu na si ya mwanadamu yawasilishwe. Ingawa Yehova aliruhusu mwandikaji ateue maneno yafaayo, yeye aliongoza akili na moyo wa mwandikaji ili kwamba asiache habari muhimu na mwishowe hayo maneno yalionekana kwa kufaa kuwa ya Mungu.—1 Wathesalonike 2:13.

Ufunuo wa Kimungu. Biblia ina unabii—historia iliyofunuliwa na kuandikwa kimbele—jambo hilo linapita kabisa uwezo wa kibinadamu tu. Kielelezo kimoja ni kupanda na kuanguka kwa “mfalme wa Ugiriki,” Aleksanda Mkubwa, kulikokuwa kumetabiriwa miaka ipatayo 200 kimbele! (Danieli 8:1-8, 20-22, NW) Biblia pia hufunua matukio ambayo hayakuonekana kamwe kwa macho ya kibinadamu. Uumbaji wa mbingu na dunia ni kielelezo kimoja. (Mwanzo 1:1-27; 2:7, 8) Kisha kuna mazungumzo yaliyotukia huko mbinguni, kama yale yaliyoripotiwa katika kitabu cha Ayubu.—Ayubu 1:6-12; 2:1-6.

Ikiwa hayakufunuliwa moja kwa moja na Mungu kwa mwandikaji, Mungu aliyajulisha matukio hayo kwa mtu fulani hivyo, hayo yakawa sehemu ya historia ya mdomo au iliyoandikwa, ambayo ilipitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kilichofuata hadi yakawa sehemu ya rekodi ya Biblia. (Ona sanduku ukurasa wa 7.) Kwa vyovyote, twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ndiye aliyekuwa Chanzo cha habari hiyo yote, na aliwaongoza waandikaji hivi kwamba masimulizi yao hayakutiwa doa na mambo yasiyo sahihi, utiaji chumvi, au ngano. Petro aliandika hivi kuhusu unabii: “Wanadamu walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.”b—2 Petro 1:21.

Jitihada Zenye Uangalifu Wenye Bidii Zahitajiwa

Ingawa waandikaji wa Biblia ‘walichukuliwa na roho takatifu,’ hata hivyo kufikiri kwa uangalifu kulihitajika upande wao. Kwa kielelezo, Solomoni ‘alitafakari, akatafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi. Akatafuta-tafuta ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyoofu, yaani maneno ya kweli.’—Mhubiri 12:9, 10.

Waandikaji fulani wa Biblia walishiriki katika utafiti kwa kadiri kubwa ili kuandika habari zao. Kwa kielelezo, Luka, aliandika hivi kwa habari ya simulizi lake la Gospeli: “Nimefuatisha kwa uangalifu mambo yote tangu awali kwa usahihi, [kuandikia] hayo kwa utaratibu wenye kufuatana vizuri.” Bila shaka, roho ya Mungu ilibariki jitihada za Luka, pasipo shaka ikimsukuma kupata hati za kihistoria zenye kuaminika na kuhoji mashahidi wa kujionea wenye kutegemeka, kama vile wanafunzi waliokuwa hai na yawezekana mama ya Yesu, Maria. Roho ya Mungu basi ingemwongoza Luka kurekodi hiyo habari kwa usahihi.—Luka 1:1-4.

Tofauti na Gospeli ya Luka, ile ya Yohana ilikuwa simulizi la mambo aliyojionea mwenyewe, ambayo iliandikwa miaka ipatayo 65 baada ya kufa kwa Yesu. Roho ya Yehova pasipo shaka ilinoa kumbukumbu la Yohana ili lisidhoofishwe na kupita kwa wakati. Hilo lingekuwa lenye upatano na yale ambayo Yesu alikuwa amewaahidi wafuasi wake: “Msaidiaji, roho takatifu, ambayo Baba atapeleka katika jina langu, hiyo itawafundisha nyinyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.”—Yohana 14:26.

Katika visa fulani waandikaji wa Biblia walitia ndani mitungo kutoka kwenye hati zenye ushahidi wa kujionea za waandikaji wa kihistoria wa mapema zaidi, ambao si wote waliokuwa wamepuliziwa. Yeremia alitumia njia hiyo kwa kadiri kubwa kutunga kitabu cha Kwanza na cha Pili cha Wafalme. (2 Wafalme 1:18) Ezra alirejezea angalau vyanzo 14 visivyopuliziwa ili kukusanya habari kwa ajili ya kitabu cha Kwanza na cha Pili cha Mambo ya Nyakati, kutia ndani “taarifa za mfalme Daudi” na “kitabu cha wafalme wa Yuda na Israeli.” (1 Mambo ya Nyakati 27:24; 2 Mambo ya Nyakati 16:11) Musa hata alinukuu kutoka “chuo [“kitabu,” NW] cha Vita vya BWANA”—yaonekana kilikuwa rekodi yenye kutegemeka ya vita vya watu wa Mungu.—Hesabu 21:14, 15.

Katika visa hivyo roho takatifu ilihusika kiutendaji, ikisukuma waandikaji wa Biblia kuteua habari zenye kutegemeka, ambazo wakati huo zilipata kuwa sehemu ya rekodi ya Biblia iliyopuliziwa.

Shauri Lenye Kutumika —Kutoka kwa Nani?

Biblia ina ushauri mwingi sana wenye kutumika unaotegemea uchunguzi wa kibinafsi wenye umakini. Kwa kielelezo, Solomoni aliandika hivi: “Mwanadamu hapati jema kupita kula na kunywa, na kuiburudisha roho yake kwa mema katika kazi yake. Hayo nayo naliona ya kwamba hutoka mkononi mwa Mungu.” (Mhubiri 2:24) Paulo alisema kwamba shauri lake kwa habari ya ndoa lilikuwa “kulingana na kauli [yake],” ingawa aliongezea kusema: “Hakika nafikiri mimi pia nina roho ya Mungu.” (1 Wakorintho 7:25, 39, 40) Paulo bila shaka alikuwa na roho ya Mungu, kwa maana kama ilivyosemwa na mtume Petro, yale ambayo Paulo aliandika yalikuwa “kulingana na hekima aliyopewa.” (2 Petro 3:15, 16) Hivyo, kwa kuongozwa na roho ya Mungu, yeye alikuwa akitoa kauli yake.

Waandikaji wa Biblia walipoonyesha usadikisho huo mbalimbali wa kibinafsi, walifanya hivyo tayari wakiwa wamejifunza na kutumia maandiko yaliyopatikana kwao. Twaweza kuwa na uhakika kwamba maandishi yao yalipatana na kufikiri kwa Mungu. Waliyorekodi yakawa sehemu ya Neno la Mungu.

Bila shaka, Biblia ina taarifa za watu fulani ambao kufikiri kwao kulikuwa kwenye makosa. (Linganisha Ayubu 15:15 pamoja na 42:7.) Inatia ndani pia taarifa chache zilizowasilisha hisi zenye maumivu makali za watumishi wa Mungu, ingawa taarifa hizo hazikuwasilisha habari kwa undani.c Ingawa mwandikaji alitoa taarifa hizo za kibinafsi, huyo mwandikaji alikuwa bado akiongozwa na roho ya Mungu ili kuandika rekodi iliyo sahihi, ambayo ilitumika kutambulisha na kufichua kusababu kwenye makosa. Zaidi ya hayo, katika kila kisa muktadha unaweka mambo wazi kwa msomaji yeyote mwenye kusababu ikiwa kufikiri kwa mwandikaji ni halali.

Kwa ufupi, twaweza kuwa na uhakika kwamba Biblia nzima ni ujumbe wa Mungu. Kwa kweli, Yehova alihakikisha kwamba habari zote ilizo nazo zilifaa kusudi lake na ziliandaa maagizo muhimu kwa ajili ya wale wanaotamani kumtumikia.—Waroma 15:4.

Waandikaji wa Kibinadamu—Kwa Nini?

Kwa kutumia wanadamu kuiandika Biblia, Yehova huonyesha hekima yake kubwa. Fikiria hili: Ikiwa Mungu angewakabidhi malaika jambo hilo, je, Biblia ingekuwa inavutia kwa namna ileile? Ni kweli, tungesisimuka kusoma juu ya sifa na shughuli za Mungu kutokana na maoni ya malaika. Lakini kama ingekosa kikolezo cha kibinadamu, huenda ikawa tungekuwa na tatizo la kuelewa ujumbe wa Biblia.

Kwa kutoa kielezi: Biblia ingeripoti tu kwamba Mfalme Daudi alifanya uzinzi na kuua kimakusudi na kwamba baada ya hapo alitubu. Hata hivyo ni jambo zuri zaidi kama nini kupata maneno ya Daudi mwenyewe, kama vile alivyoonyesha maumivu makali yenye kuhuzunisha juu ya matendo yake na kumwomba Yehova msamaha! “Dhambi yangu i mbele yangu daima,” akaandika. “Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.” (Zaburi 51:3, 17) Kwa sababu hiyo, Biblia ina uchangamfu, mambo tofauti-tofauti, na uvutio ambao kikolezo cha kibinadamu huipatia.

Ndiyo, Yehova alichagua njia iliyo bora zaidi kutupatia Neno lake. Hata ingawa wanadamu wanyonge na wenye udhaifu mbalimbali walitumiwa, walichukuliwa na roho takatifu ili maandishi yao yasiwe na makosa. Hivyo, Biblia ina thamani iliyo bora zaidi. Shauri layo ni thabiti, na unabii wayo kwa habari ya Paradiso ya wakati ujao duniani ni mambo yenye kutegemeka.—Zaburi 119:105; 2 Petro 3:13.

Kwa nini usilifanye kuwa zoea kusoma sehemu fulani ya Neno la Mungu kila siku? Petro aliandika hivi: “Fanyizeni hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya neno, ili kupitia hilo mpate kukua kufikia wokovu.” (1 Petro 2:2) Kwa kuwa imepuliziwa na Mungu, utapata Andiko lote kuwa “ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

[Maelezo ya Chini]

a Katika angalau kisa kimoja, kile cha zile Amri Kumi, hiyo habari iliandikwa moja kwa moja “kwa chanda cha Mungu.” Kisha Musa akayanakili tu maneno hayo juu ya hatikunjo au juu ya vifaa vingine.—Kutoka 31:18; Kumbukumbu la Torati 10:1-5.

b Neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “wakichukuliwa,” pheʹro, linatumiwa katika njia nyingine kwenye Matendo 27:15, 17 ili kufafanua meli inayochukuliwa na upepo. Hivyo roho takatifu ‘iliongoza mwendo wa’ waandikaji wa Biblia. Iliwasukuma kukataa habari yoyote iliyokuwa ya uwongo na kutia ndani tu ile iliyokuwa ya hakika.

c Kwa vielelezo, linganisha 1 Wafalme 19:4 na mstari wa 14 na wa 18; Ayubu 10:1-3; Zaburi 73:12, 13, 21; Yona 4:1-3, 9; Habakuki 1:1-4, 13.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Musa Alipata Wapi Habari Yake?

MUSA aliandika kitabu cha Biblia cha Mwanzo, lakini yote aliyorekodi yalitukia muda mrefu kabla ya kuzaliwa kwake. Basi, alipata habari hizo kutoka wapi? Yawezekana zilikuwa zimefunuliwa moja kwa moja na Mungu, au huenda ikawa ujuzi juu ya baadhi ya hayo matukio ulikuwa umepitishwa kwa mdomo kutoka kizazi kimoja hadi kile kingine. Kwa kuwa wanadamu waliishi kwa muda mrefu zaidi katika nyakati za mapema, mengi ya yale ambayo Musa alirekodi katika Mwanzo yangeweza kuwa yalipitishwa kutoka Adamu hadi Musa kupitia viunganishi vitano vya kibinadamu—Methusela, Shemu, Isaka, Lawi, na Amramu.

Kwa kuongezea, huenda Musa akawa alitafuta habari katika rekodi zilizoandikwa. Kwa habari hiyo, yastahili kuonwa kwamba mara nyingi Musa hutumia hili fungu la maneno “hivi ndivyo vizazi vya [“historia ya,” NW],” kabla ya kutaja jina la mtu atakayezungumziwa. (Mwanzo 6:9; 10:1; 11:10, 27; 25:12, 19; 36:1, 9; 37:2; italiki ni zetu.) Wasomi fulani husema kwamba neno la Kiebrania lililotafsiriwa hapa “historia,” toh·le·dhohthʹ, larejezea hati ya kihistoria iliyopo ikiwa tayari imeandikwa ambayo Musa alitumia kuwa chanzo cha maandishi yake. Bila shaka, hilo haliwezi kusemwa kwa kuthibitishwa.

Yawezekana kwamba habari zilizomo ndani ya kitabu cha Mwanzo zilipatikana kupitia hizo njia tatu zilizotajwa hapo juu—nyingine kwa ufunuo wa moja kwa moja, nyingine kwa kupitisha kwa mdomo, na nyingine zikatoka kwenye rekodi zilizoandikwa. Jambo la muhimu ni kwamba roho ya Yehova ilimpulizia Musa. Kwa sababu hiyo, yale aliyoyaandika yanaonwa kwa haki kuwa neno la Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Katika njia tofauti-tofauti, Mungu alipulizia wanadamu kuiandika Biblia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki