Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 9/1 kur. 389-399
  • Biblia—Iliandikwa na Wanadamu Lakini Hata Hivyo Ni Ujumbe wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Biblia—Iliandikwa na Wanadamu Lakini Hata Hivyo Ni Ujumbe wa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NAMNA WAANDIKAJI WA BIBLIA WALIVYOPOKEA HABARI YAO
  • SEHEMU YA ROHO TAKATIFU YA MUNGU
  • MAONI YA KIBINADAMU​—YENYE AU BILA MSAADA WA KIMUNGU?
  • WAANDIKE HEKIMA YA MUNGU YAFUNULIWA KATIKA KUTUMIA WANADAMU NENO LAKE
  • JE! UJUMBE WA MUNGU UMEPELEKWA KWA NJIA YENYE KUTEGEMEKA?
  • Mungu Aliipuliziaje Biblia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Ni Nani Aliyeitunga Biblia?
    Amkeni!—2007
  • Hekima ya “Neno la Mungu”
    Mkaribie Yehova
  • ‘Waliongozwa na Roho Takatifu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 9/1 kur. 389-399

Biblia​—Iliandikwa na Wanadamu Lakini Hata Hivyo Ni Ujumbe wa Mungu

1. Kutokana na maoni ya kibinadamu, waandikaji wa Biblia walikuwa watu wa namna gani?

BIBLIA iliandikwa na watu wapata 40 wakati wa muda kama karne kumi na sita. Watu hawa walikuwa wasiokamilika, wenye udhaifu na makosa. Kama wanadamu, hawakuwa tofauti na watu wengine. Mmoja wao, Paulo, aliwaambia watu ambao kwa makosa walimtazama yeye na mmisionari mwenzake Barnaba kama miungu: “Sisi pia ni wanadamu wenye udhaifu ule ule kama ninyi.” (Matendo 14:15, NW) Kutokana na maoni ya kibinadamu, wengi wa waandikaji wa Biblia walikuwa si watu wenye elimu na uwezo wa pekee. Kati yao walikuwamo watu wa kawaida sana, watu ambao kazi zao zilikuwa za wachungaji na wavuvi wa samaki.

2. Iliwezekanaje kwa wanadamu wasiokamilika kufanyiza maandishi ambayo kweli ni “neno” la Mungu?

2 Basi, iliwezewanaje wanadamu hawa wasiokamilika waandike maandishi ambayo kweli ni ujumbe wa Mungu? Hawakuandika kwa kutaka kwao wenyewe kwa ghafula, bali waliongozwa na Mungu. “Kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu,” akasema mtume Paulo juu ya sehemu ya Maandiko Matakatifu iliyopatikana katika wakati wake.​—2 Tim. 3:16, Swahili Congo Bible.

3, 4. Sababu gani kuwa na mashaka juu ya kuongozwa kwa Biblia na Mungu ni kwenye hatari sana?

3 Labda wewe unaikubali Biblia kama ikiwa Neno la Mungu lililoongozwa na yeye. Lakini ukubali wako una nguvu gani? Je! unaweza kuvumilia jaribu? Nabii Yeremia alisema hivi: “Neno la [Yehova] limefanywa shutumu kwangu, na dhihaka, mchana kutwa.” (Yer. 20:8) Je! wewe ungekuwa na nia ya kupatwa na matusi, kuteswa na hata kulifia? Wakati wa mkazo wa taabu na upinzani, hata mashaka kidogo juu ya kuongozwa kwa Neno la Mungu yaweza kutokeza mashaka makubwa zaidi, yakiharibu imani na kupunguza nguvu ya mtu ya kushinda jaribu. (Yak. 1:6) Walakini ikiwa unasadikishwa kweli kweli kwamba Biblia ni Neno la Mungu na kwamba kulifuata ndilo jambo peke yake la kufanya, utaweza sana kushinda mkazo na kupinga kufuata mwendo unaoonekana kuwa unafaa.

4 Mtu anayewaza kwamba labda sehemu fulani ya Biblia ilitungwa tu na fikira za kibinadamu atajaribu kuonyesha ana sababu nzuri kwa kutokuangalia yale ambayo inasema kwa kutaka kuepuka taabu. Hata hivyo katika kufanya hivyo anaweza kweli kuwa akiliacha tumaini la uzima wa milele. Yesu Kristo alisema hivi: “Mtu ye yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza ataiponya.” (Luka 17:33) Kwa hiyo, ni zaidi ya kutaka sana kuangalia namna Biblia, kitabu kilichoandikwa na wanadamu, ilivyo Neno la Mungu kweli kweli. Uhai wetu wenyewe watiwa ndani.

NAMNA WAANDIKAJI WA BIBLIA WALIVYOPOKEA HABARI YAO

5. Kuambiwa kwa mdomo kulikuwa na sehemu gani katika kufanyiza maandishi ya Biblia?

5 Kati ya “njia nyingi” zilizotumiwa kupelekea watu duniani ujumbe wa Mungu ilikuwa kuambiwa kwa mdomo. (Ebr. 1:1, 2) Sehemu za Biblia zilizosemwa kwa mdomo zinatia Amri Kumi (pia zilitolewa kwa mwandiko katika mbao mbili za mawe) na sheria nyingine zote zilizo katika agano la Mungu alilofanya na Waisraeli. Yehova Mungu alipeleka agano hili la Torati kupitia kwa malaika. (Matendo 7:53) Baada ya hapo Musa aliagizwa hivi: “Andika maneno haya.” (Kut. 34:27) Zaidi ya Musa manabii pia walipokea ujumbe wa wazi kisha huu ukaandikwa. (Kwa mifano, tazama 2 Samweli 7:5-16; Isaya 7:3-9 na Yeremia 7:1-34.) Ujumbe huu wa wazi kwa kawaida ulisemwa na malaika wa Mungu mwenye kuwakilisha.​—Mwa. 31:11-13.

6. Eleza hali ya ndoto, njozi na hali kama usingizi, na sehemu zao katika kupeleka ujumbe wa Mungu kwa wanadamu.

6 Nyakati nyingine Yehova Mungu alitumia ndoto, njozi na hali kama za usingizi ili kuwapelekea wanadamu ujumbe wake (Hes. 12:6; 1 Sam. 3:4-14; 2 Sam. 7:17; Dan. 9:20-27) Kwa habari ya ndoto, au “njozi za usiku,” mtu aliyelala usingizi alitiliwa picha kama ile ya sinema iliyopeleka ujumbe au kusudi la Mungu katika akili yake. Wengine walioona njozi walikuwa macho kabisa na walikaziwa habari kwa njia ya picha katika akili yenye fahamu. (Mt. 17:2-9; Luka 9:32) Njozi fulani zilipokewa wakati mtu alipokwisha kuingia katika hali kama ya usingizi. Ijapokuwa alikuwa mwenye fahamu, alivutwa sana na njozi hata alisahau kabisa kila jambo lililokuwa karibu naye. (Matendo 10:10-16; 11:5-10) Mwisho, waandikaji wa Biblia waliopokea habari kupitia kwa ndoto, njozi au hali kama za usingizi walipaswa wachague maneno na semi za kusimulia waliyokuwa wameona katika maneno yenye kutoa maana.​—Hab. 2:2; Ufu. 1:1, 11.

7. Waandikaji wa Biblia walipataje habari ya zile sehemu za kihistoria?

7 Sehemu kubwa ya Biblia inasimulia historia​—mambo yaliyopata watu, jamaa, makabila na mataifa. Waandikaji wa Biblia walipataje habari hii? Nyakati nyingine waliyaona matukio yenyewe ambayo waliandika. Lakini mara nyingi iliwapasa wapate habari kutokana na vyanzo vingine, wakiangalia habari za kihistoria zilizokuwa zimekwisha kuwako, habari za vizazi au hata watu waliokuwa na uwezo wa kutoa habari yenye kuaminika, mtu aliyeona hasa au kwa njia nyingine. Hii ilitaka uchunguzi mkubwa na wa uangalifu upande wa mwandikaji. Ezra, kuhani na mnakiliji mwenye ujuzi, alitumia vyanzo vya habari 20 ili aandike vitabu viwili vya Mambo ya Nyakati. Mganga Luka, akiandika juu ya Injili yake, alisema hivi “Nimejitafutia usahihi wa mambo hayo yote tangu mwanzo, kukuandikia kwa taratibu.” (Luka 1:3) Habari ya mambo ya kweli yaliyotukia (kama ilivyo katika Mwanzo na kitabu cha Ayubu) juu ya mwanzo wa wanadamu na matukio ya mapema zaidi, mazungumzo katika mbingu zisizoonekana na mengine kama hayo, yalifuniliwa na Mungu ama kwa waandikaji ama, kwanza, kwa wengine. Ikiwa watu wengine kuliko waandikaji walijulishwa, bila shaka ilipelekwa kwa mdomo au kwa mwandiko mpaka ilipokuja kuwa sehemu ya maandishi ya Biblia.

8. Kilikuwa chanzo gani cha mengi ya maneno yenye hekima na mengi ya mashauri yanayopatikana katika Bibiia?

8 Zaidi ya historia, Biblia ina wingi wa maneno yenye hekima na shauri. Waandikaji walitumia yale ambayo wao wenyewe waliona na yale ya wengine, wakifanya hivyo kwa kujifunza na kwa matumizi ya Maandiko yaliyopatikana kwao. Mara nyingi tunasoma katika Biblia misemo inayoonyesha hili. Juu ya aliyokuwa ameona juu ya kuangalia kwa Mungu watumishi wake, mtunga Zaburi Daudi alitangaza hivi: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.” (Zab. 37:25) Mwandikaji mwenye hekima wa Mhubiri, Sulemani mwana wa Daudi, alikata shauri hivi kutokana na aliyoona: “Mwanadamu hapati jema kupita kula na kunywa, na kuiburudisha [nafsi] yake kwa mema katika kazi yake. Hayo nayo naliona ya kwamba hutoka mkononi mwa Mungu.” (Mhu. 2:24) Mpango wa habari ukiwa juu ya yale ambayo yanampata mwanadamu ulimtaka mwandikaji ajitahidi sana. Hili laonekana wazi kutokana na Mhubiri 12:9, 10, tunaposoma hivi: “Mhubiri alikuwa na hekima, aliendelea kuwafundisha watu maarifa; naam, akatafakari, akatafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi. Huyo Mhubiri akatafuta-tafuta ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.”

SEHEMU YA ROHO TAKATIFU YA MUNGU

9. Je! Maandiko Matakatifu ni ujumbe wa Mungu katika njia ndogo tu kwa vile jitihada nyingi ya kibinadamu ilitumiwa katika kuandika Biblia?

9 Kwa kuwa jitihada nyingi sana ya kibinadamu ilitiwa katika kuandika Biblia, je! hii inamaanisha kwamba Biblia ni Neno la Mungu katika njia ndogo tu? Je! zile sehemu zilizoandikwa kwa kuambiwa na Mungu ndio ujumbe wa Mungu peke yake? Hapana, kwa maana zote, si sehemu fulani za Biblia tu, ziliongozwa na Mungu. Hili liko hivyo kwa sababu Yehova Mungu, kupitia kwa roho au nguvu yake ya utendaji aliwaongoza waandikaji wa Biblia. Akikubali hili, mtunga Zaburi Daudi alitangaza hivi: “Roho ya [Yehova] ilinena ndani yangu, na neno lake likawa ulimini mwangu.”​—2 Sam. 23:2.

10. Eleza kwa mfano maana ya usemi huu ‘neno la Mungu’ kuhusiana na habari ya Biblia.

10 Lile “neno” la Mungu katika ulimi wa Daudi halikuwa “neno” moja, bali ujumbe mwingi. Hili ni wazi kutokana na namna Biblia inavyoutumia usemi huu “neno.” Kwa mfano, mmoja wa watumishi wa nabii Elisha alimwambia mkuu wa jeshi Mwisraeli Yehu hivi: “Nimetumwa na neno kwako, Ee jemadari.” (2 Fal. 9:5) “Neno” hilo lilikuwa ujumbe wa Mungu. Lilimweka Yehu kama mteule wa Mungu atawale juu ya ufalme wa Israeli wa kabila kumi na kumwagiza afikilize hukumu juu ya nyumba ya kifalme ya Ahabu. (2 Fal. 9:6-10) Vile vile, tunasoma katika Yeremia 23:29 kwa habari ya wazi ya ujumbe na si kwa habari ya “neno” moja: “Je! neno langu si kama moto? asema [Yehova]; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande?” “Neno” moja haliwezi kuwa na matokeo yenye kuharibu hivyo, lakini ujumbe wenye nguvu unaweza kufanya hivyo ukitiwa nguvu. Mungu alitumiaje roho yake atie ujumbe huo wenye nguvu katika akili za waandikaji wa Biblia na kuhakikisha kwamba uliendelea kuwa “neno” Lake?

11. Ni katika njia gani unabii wa Biblia ‘hautokani na tafsiri yo yote ya kipekee’?

11 Kwa habari ya sehemu ya roho ya Mungu juu ya unabii, Biblia inatuambia hivi: “Hakuna unabii wa Andiko utokanao na tafsiri yo yote ya kipekee. Kwa maana unabii haukuletwa wakati wo wote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu wakati walipoongozwa kwa roho takatifu.” (2 Pet. 1:20, 21, NW) Hii yamaanisha kwamba unabii wa Biblia haukutokana na uchanganuzi wa mwandikaji mwenyewe na fasiri ya matukio na maelekeo ya kibinadamu ya wakati huo na kwa lile ambalo alidhani haya yangeongoza. Badala yake, akili ya mwandikaji iliamshwa na roho ya Mungu naye aliongozwa auseme ujumbe ulioongozwa na Mungu, kwa kawaida katika maneno yake mwenyewe. Hivyo maneno hayo yalikuwa yale ya mwandikaji, lakini ule ujumbe ulikuwa ule wa Yehova Mungu.

12. Roho ya Mungu ilikuwa na sehemu gani katika kuongoza kuandikwa kwa matukio ya zamani?

12 Lakini je! ile habari iliyokuja kuwa sehemu ya Biblia mara nyingi haikuandikwa miaka mingi yakiwa yamekwisha kutukia yale matukio yaliyosimuliwa? Ndiyo, hii ni kweli, kwa mfano, juu ya habari za huduma ya kidunia ya Yesu. Hata hivyo, roho ya Mungu ilikuwa na daraka la kufanyizwa kwa maandishi sahihi. Hili ni wazi kutokana na maneno ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba atatuma katika jina langu, hiyo itawafundisha ninyi mambo yote niliyowaambia ninyi.” (Yohana 14:26, NW) Hivyo, basi, roho ya Mungu ndiyo iliyokumbusha kwa usahihi ile habari iliyotiwa katika maandishi ya Biblia.

13. Kuna ushuhuda gani kwamba roho ya Mungu iliongoza kuchaguliwa kwa habari iliyotiwa katika Biblia?

13 Kwa njia ya roho yake, Yehova Mungu pia alihakikisha kwamba yaliyoandikwa yalifaa kusudi lake, yakitoa agizo linalohitajiwa na wale wanaotamani kuwa na kuendelea kuwa watumishi wake waliokubaliwa. Yeye aliongoza kuchaguliwa kwa habari iliyotakiwa itiwe ndani. Ndiyo sababu mtume Paulo aliweza kusema hivi: “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Rum. 15:4) Na kwa kutaja waziwazi yaliyowapata Waisraeli katika wakati wa Musa, alieleza hivi: “Mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya [taratibu ya mambo ya Kiyahudi].”​—1 Kor. 10:11.

14. Je! Yehova Mungu ‘aliigiza’ matukio yaliyohusu makosa ya Waisraeli ili mambo haya yaweze kuandikwa kuwaonya Wakristo? Eleza.

14 Haitupasi tukate shauri kutokana na hili kwamba katika kila jambo Mungu alikuwa akitenda kama “Mwigizaji” mkuu wa mambo, akiigiza kwa makusudi matukio ambayo yangekuwa mifano ambayo kutoka hiyo watumishi wake wangepata masomo ya kuonya na kutia moyo katika nyakati za baadaye. Sivyo, lakini kama katika matukio ambayo mtume alitaja, Waisraeli kwa kuchagua na tamaa zao wenyewe waligeuzwa na hali wakati walipoanza kunung’unika, kuabudu sanamu na kufanya uasherati. Mungu hakuwaongoza wafanye hivyo. (1 Kor. 10:1-10) Kwa kuwa Waisraeli walikuwa watu wa Mungu wa agano, uhakika wa kwamba walikubali washawishwe unaongeza mkazo kwenye onyo ambalo mtume anatoa nyumaye: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.”​—1 Kor. 10:12.

15. Barua ya Yuda inaonyeshaje kwamba roho ya Mungu iliongoza kuchaguliwa kwa habari?

15 Hivyo, badala ya kutokeza mengi ya matukio haya, Yehova Mungu aliacha hali nyingi zitukie tu kulingana na kawaida yazo kisha akawafanya waandikaji waandike yale ambayo Mungu alijua yangekuwa yenye faida wakati ujao. Kwamba uchaguzi wa habari ya maandishi ya Biblia uliongozwa kweli kweli kwa roho ya Mungu inatolewa mfano vizuri katika barua ya mwanafunzi Yuda. Mwanzoni Yuda alikusudia kuandika juu ya wokovu ambao Wakristo wote waliotiwa mafuta walikuwa wakitumainia. Walakini, kwa uongozi wa roho ya Mungu, alifahamu kwamba waamini wenzake walihitaji jambo jinginelo ili washindane kwa kufaa na hali waliyokuwa wakiielekea wakati huo. Akieleza sababu ya kuacha kusudi lake la kwanza, aliandika hivi: “Wapenzi, nilipokuwa nikifanya bidii sana kuwaandikia habari ya wokovu ambao ni wetu sisi sote, naliona imenilazimu kuwaandikia, ili niwaonye kwamba mwishindanie imani waliyokabidhiwa watakatifu mara moja tu. Kwa maana kuna watu waliojiingiza kwa siri, watu walioandikiwa tangu zamani hukumu hii, makafiri, wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi, nao humkana yeye aliye peke yake Mola, na Bwana wetu Yesu Kristo.” (Yuda 3, 4) Yale ambayo Yuda aliandika mwishowe kwa uongozi wa roho ya Mungu yalikuwa ndiyo hasa waamini wenzake walihitaji ili wapinge mavutano yenye kuharibu.

16. Je! waandikaji wa Biblia walitumia nia yao nyakati nyingine katika kuandika habari? Eleza.

16 Je! uhakika wa kwamba roho ya Mungu iliongoza uchaguzi wa habari ya kuandika katika Biblia unamaanisha kwamba wale waliokuwa wakiandika hawakutumia nia yao wenyewe juu ya jambo walilokuwa wakiandika? Sivyo, mara nyingi walikumbuka miradi na wakaandika kwa kulingana. Walijibu maulizo fulani au wakajaribu kueleza mambo yaliyokuwa yametokeza kutokufahamu vizuri. Mfano wa hili ni barua ya pili ya mtume Paulo aliyoandikia kundi katika Thesalonike. Wengine katika kundi hilo walikuwa wamekata shauri kwa makosa kwamba kuwapo kwa Yesu Kristo katika mamlaka ya kifalme kulikaribia. Halafu, pia, walikuwako wale ambao hawakuwa wameona ubora wa shauri lake lililotangulia juu ya ‘kufanya kazi kwa bidii na kuenenda kwa adabu mbele yao walio nje ya kundi.’ Barua ya pili ya Paulo ilifahamisha hili na ikafunua maoni yanayofaa ya Kikristo juu ya mambo haya. (1 The. 4:10-12; 2 The. 2:1-3; 3:10-15) Kwa kuwa waandikaji wa Biblia kama Paulo walikuwa wenye kuitikia uongozi wa roho ya Mungu, mambo ambayo waliandika yalikuwa yenye kupatana sana na kusudi la Mungu na kwa hiyo yenye kutegemeka.

MAONI YA KIBINADAMU​—YENYE AU BILA MSAADA WA KIMUNGU?

17, 18. Tufahamuje maneno ya mtume Paulo juu ya ‘kutoa shauri lake mwenyewe’?

17 Lakini namna gani nyakati zile waandikaji wa Biblia walipotoa kwa wazi maoni yao wenyewe? Kwa mfano, maneno yafuatayo ya mtume Paulo: “Watu wengine nawaambia mimi, wala si Bwana . . .” “Kwa habari za wanawali sina amri ya Bwana, lakini natoa shauri langu.” “Heri [mjane] zaidi akikaa kama alivyo [yaani, bila kuolewa]; ndivyo nionavyo mimi; nami nadhani ya kuwa mimi nami nina [roho ya] Mungu.” (1 Kor. 7:12, 25, 40) Paulo alikuwa na maana gani hasa kwa maneno haya?

18 Mtume hakuweza kuonyesha kwamba hivyo ndivyo Bwana Yesu Kristo alivyofundisha mambo hayo aliyokuwa akizungumza na kwa hiyo akatoa “shauri” lake, Walakini, aliandika kwa uongozi wa roho ya Mungu na hivyo shauri lake lilikuwa na uongozi wa kimungu na likaonyesha maoni ya Mungu mwenyewe. Hili linathibitishwa na uhakika wa kwamba mtume Petro aliunganisha barua za Paulo pamoja na sehemu nyingine ya Maandiko katika kusema hivi: “Uhesabuni uvumilivu wa Bwana wetu kuwa ni wokovu, kama vile na ndugu yetu mpenzi Paulo alivyowaandikia kwa hekima aliyopewa; vile vile kama katika nyaraka zake zote pia, akitoa humo habari za mambo hayo; katika nyaraka hizo yamo mambo ambayo ni vigumu kuelewa nayo; na mambo hayo watu wasio na elimu, wasio imara, huyapotoa, kama vile wayapotoavyo na maandiko mengine, kwa uvunjifu wao wenyewe.”​—2 Pet. 3:15, 16.

19. Biblia ni ujumbe wa Mungu katika njia gani?

19 Hivyo yaweza kuonwa kwamba Biblia nzima ni “neno” au ujumbe wa Mungu kwa vile kila jambo liliandikwa kwa uongozi wa roho yake, ili kutumikia kusudi lake na kutoa mambo kwa uhakika. Wakati wo wote ambapo Biblia inatumia maneno ya wanadamu au inasimulia mambo ambayo walifanya wakiwa katika hali fulani, maneno yanayozunguka fungu la Biblia yanaonyesha wazi kama mwendo wao umepaswa ufuatwe au uepukwe, kuwaza kwao kukubaliwe au kukataliwe.

20. Eleza namna mtu huenda akaitumia Biblia katika njia ya kumhesabia Mungu maoni ya wanadamu wasiokamilika.

20 Chukua kitabu cha Ayubu kama mfano. Sehemu kubwa za kitabu hicho zinazungumza maoni yenye makosa yaliyoonyeshwa na rafiki watatu wa Ayubu na hata na Ayubu mwenyewe nyakati nyingine. Kwa wazi maoni hayo yenye makosa na matumizi mabaya ya mambo ya hakika hayakuongozwa na Mungu. Kwa mfano, Elifazi rafiki ya Ayubu alimshtaki Mungu kwa makosa hivi: “Yeye hawategemei watakatifu wake; naam, mbingu nazo si safi machoni pake.” (Ayubu 15:15) Baadaye Yehova Mungu alimkaripia Elifazi na wenzake kwa sababu ya masingizio yao. Elifazi aliambiwa hivi: “Hasira zangu zinawaka juu yako, na juu ya hao rafiki zako wawili; kwa kuwa ninyi hamkunena yaliyo sawa katika habari zangu, kama alivyonena mtumishi wangu Ayubu.” (Ayubu 42:7) Ijapokuwa Elifazi na rafiki zake kwa wazi hawakuongozwa na Mungu, mwandikaji wa kitabu cha Ayubu aliongozwa na roho ya Mungu katika kuandika maneno yao kwa usahihi. Habari hii inatambulisha na kufunua kuwaza kwa makosa juu ya Mungu kuruhusu uovu. Kwa hiyo, yote ni neno au ujumbe wa Mungu ulioongozwa na yeye. Hata hivyo, hii inaonyesha kwamba yatupasa tutumie uangalifu tunapotumia maneno ya vifungu fulani kutoka Biblia. Yakitumiwa kinyume cha hali yao ifaayo inayozungumza, kinyume cha maneno yanayozunguka fungu, Mungu anaweza akahesabiwa kwa makosa jambo fulani ambalo kwa kweli ni maoni ya wanadamu wasiokamilika.

WAANDIKE HEKIMA YA MUNGU YAFUNULIWA KATIKA KUTUMIA WANADAMU NENO LAKE

21. Kama Yehova Mungu angalitumia malaika waiandike Biblia nzima, je! kweli ingalikuwa yenye maana zaidi kwetu kama wanadamu wasiokamilika?

21 Kutumia kwa Mungu wanadamu waandike “neno” lake ni ushuhuda wa hekima yake kuu katika kutoa lile ambalo wanadamu wasiokamilika wanahitaji hasa. Yeye angaliweza kutumia malaika. Lakini je! “neno” lake lingalikuwa lenye kupendeza kule kule? Kweli, malaika wangaliweza kusimulia sifa za ajabu za Mungu na matendo yake makuu katika kuandika. Wangaliweza kuonyesha wingi wa upendo wao wenyewe kwake na kushukuru kwao zawadi zisizo na mwisho zinazotoka kwake. Lakini je! isingalikuwa vigumu kwetu sisi kama wanadamu wasiokamilika kujishirikisha wenyewe na habari iliyoonyesha semi za viumbe wakamilifu wa kiroho walio na ujuzi na maarifa bora kutupita sisi? Maisha katika makao yao yasingaliweza kusimuliwa waziwazi kama tunavyojua maisha​—furaha yake pamoja na hofu (woga) zake, kukata tamaa na huzuni. Hivyo, kwa kutumia kwake wanadamu, Yehova Mungu alihakikisha kwamba “neno” lake lilikuwa na uchangamshi, namna namna na kupendeza ambako tendo la kibinadamu peke yake lingeweza kulipa.

22. Ikiwa sehemu ya kibinadamu ilikosekana kabisa katika Biblia, inaelekea tunaweza kuwa na matatizo gani katika kuifahamu?

22 Ikiwa sehemu ya kibinadamu ilikosekana kabisa katika Biblia, inaelekea pia tunaweza kuwa na shida kubwa katika kufahamu ujumbe wake. Inaweza kuwa vigumu kuona namna sisi, kama wanadamu wasiokamilika, tungeweza kupata hali yenye kukubalika na Muumba. Kwa mfano, ikiwa maandishi hayo yangetuambia sisi kwamba ‘Mungu ni mwenye rehema’ tu, hii isingetosha ili tufahamu hasa maana ya hili. Sisi wanadamu twahitaji mambo hayo yaelezwe kwetu katika njia ambazo twaweza kufahamu. Kwa kuwa iliandikwa na wanadamu, Biblia inatoa mifano ya kweli kutokana na maisha ya kweli, ikiionyesha kutokana na uwezo wa kibinadamu wa kuona mambo katika hali zake. Inatuambia juu ya wanadamu ambao, ijapokuwa walijua sheria ya Mungu, walishindwa na udhaifu wakawa wenye hatia ya makosa makubwa, mara nyingine habari zikitupa maneno ya watu wenyewe juu ya namna walivyoona na wakatenda. Wakati uo huo tunajifunza kadiri walivyoonyeshwa rehema.

23, 24. Simulia yaliyotukia kwa Daudi pamoja na Bathsheba, tena onyesha tunayojifunza kutokana na haya juu ya Yehova Mungu.

23 Ifikirie habari ya Mfalme Daudi. Alikuwa amejionyesha mwenyewe kuwa mtu mwenye imani kuu. Lakini, ndipo, hali zilipoelekeza kwenye kuvutwa kwake na tamaa mbaya. Daudi akaja kuvutwa sana na uzuri wa mke wa Uria Mhiti, mtu aliyeunga mkono ufalme wa Daudi kwa uaminifu. Aliacha tamaa yake ikue na kwa kweli akamleta Bathsheba, mke wa Uria katika jumba lake la kifalme. Ijapokuwa labda hakufikiria kufanya ngono naye, nyege zake ziliamshwa sana hata akafanya uzinzi. Alipojua kwamba Bath-sheba alikuwa amechukua mimba kwa sababu ya kulala naye, alitafuta kwa haraka njia ya kuficha jambo hili kwa kujaribu kuagiza Uria aende nyumbani kwake akafanye ngono pamoja na mke wake. Njia hii ilipokosa kuwa na matokeo, Daudi alikata tamaa. Kulipatikana njia moja tu ya kuzuia Bath-sheba asifunuliwe kama mwanamke mzinzi pamoja naye na njia hiyo ilikuwa kumwua mume wa Bath-sheba ndipo amchukue awe mke wake mwenyewe. Basi Daudi akafanya mpango ili Uria awekwe mahali ambapo kwa hakika angekufa vitani. Uria akauawa, kisha Daudi akamtwaa Bath-sheba mjane kama mke wake.​—2 Sam. 11:2-27.

24 Wakati nabii Nathani alipomfunulia kosa lake kubwa, Daudi alichomwa moyoni akasikitikia mno dhambi yake. Alipaza sauti hivi: “Nimemfanyia [Yehova] dhambi.” (2 Sam. 12:13) Alipoona kutubu kwa Daudi kwa moyo wote, Yehova alikukubali na, ijapokuwa alimwadhibu, hakumtupilia mbali asiwe mtumishi wake. Kwa hiyo, kulikuwa si kutia chumvi wakati Daudi aliposema katika mojawapo ya zaburi zake hivi: “Wewe, [Yehova], u Mungu wa rehema na neema, mvumilivu, mwingi wa fadhili na kweli.”​—Zab. 86:15.

25. Tunajifunza nini juu ya rehema ya Yehova kwa matendo yake na Waisraeli katika wakati wa Yeremia?

25 Kwa upande mwingine, Biblia inasimulia juu ya wakaaji wasioaminika wa Yerusalemu katika siku za Yeremia. Watu wote walikataa kusikia kusihi kulikotolewa mara nyingi ili watubu. Kwa ukaidi waliendelea kuzoea uasi. Hivyo Yehova Mungu aliondoa rehema yake, ulinzi wake kutoka kwao akawaacha wapate msiba mkuu mikononi mwa Wababeli. Alikataa kusikiliza hata ijapokuwa waliomba sana msaada. Kwa sababu gani? Kwa sababu waliendelea kuwa wasiotubu. Kwa habari ya hili, nabii Yeremia aliandika hivi: “Umetufunika kwa hasira na kutufuatia; umeua, wala hukuona huruma. Umejifunika nafsi yako kwa wingu, maombi yetu yasipite.”​—Omb. 3:43, 44.

26. Mifano kutokana na maisha halisi inatusaidiaje tumjue Yehova?

26 Tunaweza kuona mfano uliosawa wa namna Mungu Yehova alivyo na namna atakavyotutendea sisi kutokana na mifano ya maisha ya kweli. Bila kuangalia ukubwa wa kosa ambalo wanadamu wasiokamilika wanafanya, wanaweza kupata msamaha wa Mungu ikiwa ni wenye kutubu kweli kweli. Lakini ikiwa wanaendelea kuvunja amri zake zenye haki bila kutubu, hawataokoka hukumu yake kali. Kwa kuwa Biblia inafunua ukubwa wa utu wa Mungu kwa namna ambayo sisi wanadamu wasiokamilika twaweza kuvutwa, twaweza kupata kumjua kweli kweli kama mtu.

27. Njia ambayo katika hiyo Biblia iliandikwa inatumikiaje kujaribu mioyo?

27 Njia ambayo katika hiyo Biblia iliandikwa imetumikia kufunua yaliyo katika mioyo ya watu. (Ebr. 4:12) Wale wanaotaka kutafuta yanayoonekana kuwa makosa na mambo yenye kupingana katika Biblia wanaweza kuyaona. Sababu moja ya hili ni kwamba Biblia haielezi mambo yote. Mara nyingi inasimulia mawazo ya watu, maneno na matendo bila ya kuonyesha kukubali au kutokubali kwa moja kwa moja. Ndiyo sababu wakati wa kusoma habari fulani watu wengine wanamtilia Mungu mashaka kama kweli alifanya haki au sivyo katika yale aliyofanya. Ndipo wanapotumia hili kama sababu ya kutofanya mabadiliko katika namna yao ya maisha ambayo Biblia inashauri. Hili linapatana na kusudi la Mungu la kutaka wanaoweza kuwa watumishi wake waliokubaliwa wawe wale wanaompenda kweli kweli na kumfahamu kama alivyo peke yao.​—Kum. 30:11-20; 1 Yohana 4:8-10; 5:2, 3.

28. Watu wanaoona ubora wa Biblia watakuwa na maoni gani juu ya yale yanayoonekana kuwa mambo yenye kupingana? Onyesha.

28 Walakini, mtu ambaye ameifikiria Biblia sana na akaona kwa hakika namna ilivyo uongozi wa ajabu wa maisha haoni yale yanayoonekana kuwa mambo yenye kupingana iwe sababu ya kutokuiamini kama ujumbe ambao Mungu amewapa wanadamu. Yeye hakosi kujua yale yanayoonekana kuwa matatizo. Sivyo hata kidogo. Yeye anafahamu kwamba Biblia ni yenye kupatana, na hivyo anatumia uangalifu asije akakosa kuangalia maneno yanayozunguka vifungu ambayo katika hayo Biblia nzima inasimulia tukio au hali fulani. Kwa mfano, ikiwa ungekuwa na rafiki mzuri sana ambaye ulijua kuwa baba mzuri, mtu aliyeangalia kweli kweli hali njema ya watoto wake. Ikiwa ungesikia kwamba alimchapa mwana wake vikali, je! ungekata shauri papo hapo kwamba hakuwa na sababu nzuri na hakuwa mwenye akili kabisa kufanya hivi? Sivyo; kwa sababu ya kumjua yeye ungefikiri kwamba bila shaka alikuwa na sababu za halali kufanya hivyo. Vivyo hivyo, Biblia inatoa habari ya kutosha juu ya utu, njia na matendo ya Yehova ili kutuwezesha tujue yeye ni Mungu wa namna gani. Kwa hiyo, hata mambo yasipoelezwa zaidi katika hali yo yote, sababu gani ye yote aone vibaya, akifikiri kwamba Mungu si mwenye upendo, si mwenye rehema au si mwenye haki? Kufanya hivyo kungekuwa kukana ushuhuda mwingi ulio katika Biblia nzima kwamba yeye ni Mungu mwenye upendo, rehema na haki.​—Kut. 34:6, 7; Isa. 63:7-9.

29. Sababu gani tusishangae ikiwa tunaona mambo fulani yanayoonekana kuwa yenye kupingana katika Biblia?

29 Bado kuna sababu nyingine imetupasa tuitazamie Biblia kuwa na tofauti ndogondogo ndani yake, mambo yanayoonekana kuwa yenye kupingana, wakati wa kuzungumza habari inayofanana. Zifikirie habari juu ya huduma ya kidunia ya Yesu. Ziliandikwa na wanaume wanne. Kati ya watatu ambao twajua kazi zao, mmoja alikuwa tabibu mwenye elimu, mwingine alikuwa mtoza kodi na wa tatu alikuwa mvuvi wa samaki. Kwa kuwa Yehova Mungu hakusema hasa mambo ambayo iliwapasa watu hawa waandike ila aliwaongoza kwa roho yake tu ili kuhakikisha kwamba habari ambayo waliandika ilikuwa sahihi, bila shaka kungekuwako na tofauti. Kila mwandikaji angaliweza kutia habari nyingi zaidi kuliko mwingine. Mmoja wao, mtume Yohana, hata alisema hivi: “Basi kuna ishara nyingine nyingi alizozifanya Yesu mbele ya wanafunzi wake, zisizoandikwa katika kitabu hiki.” (Yohana 20:30) Hivyo zile habari za Injili ni zenye kusimuliwa kwa ufupi sana, habari fulani zinazopatikana katika Injili moja unakuta zimeachwa katika nyingine. Badala ya kupingana zenyewe kwa zenyewe, habari hizo zinatimiza yale yanayokosekana katika nyingine, kutusaidia tufahamu kisa chote zaidi. Wakati uo huo zile tofauti zinatoa ushuhuda zaidi wa kwamba Biblia ni yenye kutegemeka. Namna gani hivyo? Kwa vile zinaonyesha kwamba waandikaji hawakupatana kwa siri ili wadanganye, hawakufanya shauri pamoja ili watunge hadithi ya uongo.

30. Kwa habari ya Biblia, sababu gani hakuna sababu ya kubisha tofauti ndogo ndogo?

30 Hivyo hakika hakuna sababu watu kubishania mambo madogomadogo. Bila kuangalia elimu yao, hawana haki kweli kuhukumu mambo ambayo wao wenyewe hawakuyaona. Na hata ikiwa wangekuwako mahali ambako mambo hayo yalitukia, wao, pia, wangesimulia habari zenye kukazia hali zilizo tofauti kidogo za yale waliyoona na kusikia. Kwa kweli, kukadiri kuzuri kwa habari za Injili kunaonyesha wazi kwamba haya ni mashuhuda manne yaliyo mbalimbali yanayopatana katika kuithibitisha kweli moja yenye maana: Yesu Kristo ndiye Mwana wa Mungu.​—Yohana 20:31.

JE! UJUMBE WA MUNGU UMEPELEKWA KWA NJIA YENYE KUTEGEMEKA?

31. Ni ulizo gani linalojiitokeza kwa sababu hati za awali za Biblia haziko?

31 Ujumbe wa Mungu kama ulivyo katika Injili nne na katika sehemu inayobaki ya Biblia haukuhifadhiwa katika hati za awali. Zile hati za awali zilipotea zamani, kupitia kwa matumizi au kwa kuharibiwa na hali ya hewa. Basi, twawezaje kuwa na hakika kwamba ujumbe wa Mungu hauna makosa kwa vile umekwisha kunakiliwa mara nyingi kwa muda wa karne nyingi?

32. Biblia yenyewe inasema nini juu ya ubora wenye kudumu wa ujumbe wa Mungu, na hii ilitaka nini juu ya kuhifadhiwa kwake?

32 Biblia yenyewe inavuta fikira kwenye ubora wenye kudumu wa “neno” la Mungu. Katika Isaya 40:8 tunasoma hivi: “Majani yakauka, ua lanyauka; bali neno la Mungu wetu litasimama milele.” Ili maneno haya yatimizwe katika vizazi vya wakati ujao, ingekuwa lazima “neno” la Mungu liwe bila makosa. Kama lisingetegemeka kwa sababu ya wingi wa makosa ya kibinadamu katika kunakili, lingekoma kuwa ujumbe wa Mungu. Lakini je! kuna ushuhuda wo wote kwamba “neno” la Mungu limeendelea katika hali yenye kutegemeka? Bila shaka!

33. Wanakiliji (wenye kunakili au kuandika) walifanya kazi yao namna gani kwa kawaida?

33 Wale waliokuwa wakinakili Maandiko Matakatifu walitumia uangalifu mkuu. Katika kazi yao, waandishi wengi wa Maandiko ya Kiebrania hawakuhesabu maneno tu bali pia herufi zilizonakiliwa. Wakati wo wote kosa dogo zaidi sana lilipopatikana​—kosa la kuandika herufi moja​—sehemu nzima ilikatwa ikawekwa mpya badala yake, ikawekwa ile isiyo na makosa. Yakawa mazoea ya waandishi kusoma kila neno kwa sauti kuu kabla ya kuliandika. Kuandika hata neno moja kutokana na kumbukumbu kulionwa na wengi kuwa dhambi mbaya sana. Wanakiliji wa Maandiko ya Kikristo, ijapokuwa hiyo haikuwa ndiyo kazi yao, walifanya vile vile kazi ya uangalifu. Kwa sababu hiyo makosa machache sana yalifanywa, na hata yale yaliyofanywa hayaharibu sana ule ujumbe.

34. Uchunguzi wa kulinganisha wa hati za kale unaonyesha nini juu ya kutegemeka kwa maandishi ya Biblia kama tuliyo nayo leo?

34 Uchunguzi wa kulinganisha wa maelfu ya hati za kale za Biblia, kutia na nyingine ambazo ni zenye muda kama miaka 2,000, unafunua kwamba bila shaka yale maandishi ya kwanza yalipelekwa kwa njia yenye usahihi. Kwa habari ya maandishi ya kwanza ya Maandiko ya Kiebrania, mwanachuo W. H. Green alisema hivi: “Labda isemwe kwa uaminifu kwamba hakuna maandishi mengine ya kale ambayo yamepelekwa kwa njia yenye usahihi sana kama haya.” Mwanachuo mwenye kujulikana sana Sir Frederic Kenyon juu ya “Chester Beatty Biblical Papyri,” alisema hivi:

“Mkataa wa kwanza na wenye maana kuliko wote kutokana na kuzichunguza (Hati za mafunjo) kwamba zinathibitisha kufaa sana kwa maandishi yaliyoko ni wenye kusadikisha. Hakuna tofauti kuu inayoonyeshwa ama katika Agano la Kale au Jipya. Hakuna mambo ya maana yaliyoachwa au nyongeza za mafungu, na hakuna tofauti zinazogeuza mambo ya maana ya hakika au mafundisho. Tofauti za maandishi zinageuza mambo madogo tu, kama vile taratibu ya maneno au maneno sahihi yanayotumiwa . . . Lakini maana yazo kubwa ni kule kuthibitisha ukamilifu wa maandishi yetu yaliyoko kwa ushuhuda wa tarehe ya zamani kuliko iliyopatikana mpaka wakati huu.”

Vile vile, katika kitabu chake The Bible and Archaeology, alisema hivi:

“Basi ule muda kati ya tarehe za kuandikwa kwa kwanza na ushuhuda wa zamani ulioko unakuwa mdogo sana hata hauwezi kuangaliwa kweli, na msingi wa mwisho wa shaka lo lote kwamba Maandiko yametufikia kweli kama yalivyoandikwa sasa umeondolewa. Uhakika na pia ukamilifu wote wa vitabu vya Agano Jipya waweza kuonwa kama umethibitishwa kabisa.”

35. Biblia yaweza kuleta matokeo gani kwetu leo?

35 Kweli kweli, ujumbe wa Mungu, kama ulivyoandikwa na wanadamu kwa uongozi wa roho yake, umeendelea kuwa wenye kutegemeka mpaka wakati huu. Kuhifadhiwa kwenye kutegemeka kumekuwa si bila kusudi. Ule ujumbe wenyewe waweza kuwa na matokeo mengi yenye kufanyiza mema kwa wale wanaoukubali kama ukitoka kwa Mungu. Hata leo maneno ambayo Wakristo katika Thesalonike waliandikiwa yanaweza kutumiwa kwa mamia ya maelfu ya watu katika dunia yote: “Mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli; litendalo kazi pia ndani yenu ninyi mnaoamini.” (1 The. 2:13) Kama Wathesalonike, wengi leo wamekuwa na nia ya kuteswa kwa ajili ya kufuata sana kwa uaminifu Maandiko Matakatifu, wakisadikishwa kwamba kweli haya ni “neno” la Mungu lililoongozwa na yeye. (1 The. 2:14-16) Je! wewe vile vile unasadikishwa? Je! “neno” au ujumbe huo unatenda kazi ndani yako? Je! unafaidika nalo katika maisha yako ya kila siku?

[Picha katika kurasa za 390-391]

Mungu alitoa Amri Kumi zikiwa zimeandikwa

Malaika walisema neno la Mungu kwa wanadamu

Roho ya Mungu iliongoza uchaguzi wa mambo ya hakika kutokana na maandishi yaliyotangulia

Manabii walipokea njozi kutoka kwa Mungu wakiwa macho

Ujumbe wa kimungu ulitolewa kwa njia ya ndoto

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki