Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Nguvu Zenye Kusafisha za Neno la Mungu
YARIPOTIWA kwamba waraibu walio wengi wa dawa za kulevya hurudia tabia zao baada ya kuachiliwa kutoka katika vituo vya kurekebisha tabia. Lakini Neno la Mungu laweza kutimiza mambo ambayo kwa kawaida hospitali mbalimbali hushindwa kufanya. (Waebrania 4:12) Watu wengi wamesaidiwa na Neno na roho ya Mungu kushinda uraibu wa dawa za kulevya na kutumia lile shauri: “Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho, tukikamilisha utakatifu katika hofu ya Mungu.”—2 Wakorintho 7:1.
Hilo latolewa kielelezo na jambo lililoonwa kutoka Myanmar. Mtu aliyeshindana na uraibu wa dawa za kulevya kwa miaka mingi asimulia hivi: “Nilikuwa mraibu wa dawa za kulevya nilipokuwa tineja. Nilijaribu mara nyingi kuacha, lakini sikuweza. Ili kutegemeza tabia yangu ya kutumia dawa za kulevya, niligeukia wizi. Tokeo ni kwamba, mwaka wa 1988, nilifungwa gerezani kwa mwaka mmoja.
“Baada ya kuachiliwa kwangu kutoka gerezani, nilianza tena kuwasiliana na marafiki wangu wa zamani. Upesi baada ya hapo nikarudia zoea la kutumia dawa za kulevya. Mwendo huo wa kujidhuru mwenyewe uliwafanya washiriki wa familia waache kushirikiana nami kabisa. Kwa kuongezea, mtazamo wangu wa kuasi uliwafanya wengi katika jumuiya waniogope, nao pia wakaanza kuniepuka.
“Kisha siku moja jambo lisiloepukika lilitokea—nilipatwa na athari za kutumia dawa za kulevya kwa kuzidi kipimo. Nilirudishwa gerezani tena, wakati huu kwa miaka mitatu. Ingawa maisha gerezani yalikuwa magumu sana, kwa njia fulani niliweza kusalimika.
“Baada ya kurudi nyumbani kutoka gerezani, niliomba familia yangu msamaha kwa sababu ya makosa ya wakati uliopita. Walinikubali kwa neema, lakini kwa mara nyingine tena, marafiki walinishawishi kurudia njia zangu za awali.
“Hatimaye, nyanya yangu alimpendekezea pasta mwenyeji kwamba nihudhurie shule fulani ya Biblia. Huyo pasta akakubali. Hata hivyo, kabla sijaanza kuhudhuria, shangazi yangu, ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, akasema kwamba ikiwa kwa kweli nilitaka kujifunza Biblia, napaswa kujifunza na Mashahidi.
“Nilienda kwenye Jumba la Ufalme nami nikajulishwa kwa mtu aliyekubali kujifunza Biblia pamoja nami. Wengi wa wahudhuriaji walinisalimu kwa uchangamfu na kunifanya nihisi kuwa nimekaribishwa.
“Baada ya kuanza funzo la Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, mahali pa tamaa ya dawa za kulevya palichukuliwa na tamaa ya kumkaribia Mungu. Mwaka mmoja baadaye nilikuwa nimefanya maendeleo kufikia kuweka maisha yangu wakfu kwa Yehova Mungu, na kuonyesha wakfu wangu kwa ubatizo wa maji.
“Majuzi, nilipokuwa nikienda kutoka nyumba hadi nyumba, nilikutana na mmoja wa waliokuwa washiriki wangu wa kutumia dawa za kulevya. Hakuweza kufahamu mabadiliko yenye kutokeza niliyokuwa nimefanya. Hilo lilifungua njia ya kutoa ushahidi, nami niliweza kuzungumza naye juu ya tumaini la Ufalme.
“Hatimaye nimepata kusudi la kweli na maana ya uhai. Sasa naweza kuwasaidia wengine waache tabia zenye kuvunja moyo za kutumia dawa za kulevya, kwa sababu ya msaada wa Mungu na shauri kutokana na Neno lake.”