Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 11/1 kur. 23-25
  • Jihadhari na “Waepikurea”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jihadhari na “Waepikurea”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Waepikurea Walikuwa Akina Nani?
  • Je, Wafanana na Ukristo?
  • Ule Upande Mbaya wa Uepikurea
  • Hatari Yenye Hila
  • Uepikurea Leo?
  • Ninawezaje Kuepuka Kupendezwa na Watu Wasiofaa?
    Amkeni!—2005
  • Kirihi Kabisa Mwendo Wenye Aibu wa Ulimwengu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • “Wamtafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wampate”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Kuishi kwa Ajili ya Sasa Au kwa Ajili ya Wakati Ujao wa Milele?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 11/1 kur. 23-25

Jihadhari na “Waepikurea”

“Yeye ni mtu mwema sana! Yeye huishi kupatana na viwango vya juu vya adili. Havuti sigareti, hatumii vibaya dawa za kulevya, au kutumia lugha chafu. Kwa hakika, ni mwema zaidi kuliko watu fulani ambao hudai kuwa Wakristo!”

JE, UMEWASIKIA watu fulani wakitumia kusababu huko ili kutetea urafiki usiofaa ambao wao hukuza? Je, hilo lathibitika kuwa kweli chini ya uchunguzi wa Kimaandiko? Kielelezo kutoka kutaniko la Kikristo la mapema hufafanua jambo hilo.

Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alionya kutaniko la Korintho hivi: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” Labda, Wakristo fulani walikuwa wakishirikiana na watu mmoja-mmoja walioathiriwa na falsafa ya Kigiriki, kutia na ile ya Waepikurea. Waepikurea walikuwa akina nani? Kwa nini wangetokeza tisho la kiroho kwa Wakristo wa Korintho? Je, kuna watu kama wao leo, ambao twapaswa kujihadhari nao?—1 Wakorintho 15:33.

Waepikurea Walikuwa Akina Nani?

Waepikurea walikuwa wafuasi wa mwanafalsafa Mgiriki, Epikurasi, aliyeishi kutoka 341 hadi 270 K.W.K. Alifundisha kwamba raha ndiyo iliyokuwa jambo la pekee au kuu maishani. Je, hilo lamaanisha kwamba Waepikurea waliishi maisha yenye kuchukiza, bila kanuni, wakiishia kufanya mazoea yenye kushusha katika utafutaji wenye kuendelea wa furaha? Kwa kushangaza, Epikurasi hakuwafundisha wafuasi wake waishi kwa njia hiyo! Badala ya hivyo, alifundisha kwamba raha hupatikana vizuri zaidi kwa kuishi kupatana na busara, moyo mkuu, kujidhibiti, na haki. Alitetea ufuatiaji, si wa raha ya papo hapo na ya kupita upesi sana, bali raha idumuyo muda wote wa maisha. Hivyo huenda ikawa Waepikurea walionekana wenye wema wa adili walipolinganishwa na watu wenye kuzoea dhambi nzito.—Linganisha Tito 1:12.

Je, Wafanana na Ukristo?

Ikiwa ungekuwa mshiriki wa kutaniko la Korintho la mapema, je, ungevutiwa na Waepikurea? Huenda ikawa watu fulani walisababu kwamba yale yaliyoonekana kuwa maadili ya juu zaidi ya Waepikurea yaliwafanya wawe washiriki salama wa Wakristo. Wakitoa sababu zaidi, huenda ikawa Wakorintho waliona mambo yenye kuonekana kuwa yalingana kati ya viwango vya Waepikurea na vile vya Neno la Mungu.

Kwa kielelezo, Waepikurea walitumia kiasi katika ufuatiaji wao wa furaha. Walithamini sana raha za akili kuliko raha za kimwili. Alichokula mtu hakikuwa cha maana kuliko uhusiano wake na mtu aliyekula naye. Waepikurea hata waliepuka kujihusisha kisiasa na utendaji kosa kisiri. Ingeweza kuwa rahisi kama nini kudhania hivi: “Wako kama sisi!”

Hata hivyo, je, Waepikurea kwa kweli walikuwa kama Wakristo wa mapema? La, hasha. Waliokuwa na uwezo wa ufahamu uliozoezwa ifaavyo wangeweza kugundua tofauti zenye maana. (Waebrania 5:14) Je, waweza kufanya hivyo? Acheni tuchunguze kwa ukaribu mafundisho ya Epikurasi.

Ule Upande Mbaya wa Uepikurea

Ili kusaidia watu washinde hali ya kuhofu miungu na kifo, Epikurasi alifundisha kwamba miungu haipendezwi na wanadamu na haiingilii mambo ya kibinadamu. Kulingana na Epikurasi, miungu haikuumba ulimwengu wote mzima, na uhai ulikuja kuweko kwa aksidenti. Je, hilo halikupingana kwa wazi na fundisho la Biblia kwamba kuna “Mungu mmoja,” aliye Muumba, na kwamba hujali viumbe vyake vya kibinadamu?—1 Wakorintho 8:6; Waefeso 4:6; 1 Petro 5:6, 7.

Epikurasi pia alifundisha kwamba hakuwezi kuwa na uhai baada ya kifo. Bila shaka, hilo lilikuwa kinyume cha fundisho la Biblia la ufufuo. Kwa kweli, mtume Paulo alipozungumza kwenye Areopago, yaelekea Waepikurea walikuwa miongoni mwa waliotofautiana na Paulo juu ya fundisho la ufufuo.—Matendo 17:18, 31, 32; 1 Wakorintho 15:12-14.

Huenda ikawa kwamba sehemu iliyokuwa hatari zaidi katika falsafa ya Epikurasi ilikuwa pia ndiyo yenye hila zaidi. Kule kukana kwake kuwako kwa uhai baada ya kifo kulimwongoza kwenye mkataa wa kwamba mwanadamu apaswa aishi maisha yenye furaha kadiri iwezekanavyo katika wakati wake mfupi duniani. Kama vile tumeona, wazo lake halikuwa lazima kuishi maisha yenye dhambi bali, badala yake, kuonea shangwe wakati wa sasa, kwa kuwa hakuna uhai baada ya kifo.

Hivyo, Epikurasi alipinga utendaji kosa kisiri ili kuepukana na hofu ya kugunduliwa, tisho hakika kwa furaha ya sasa. Alitia moyo kuwa na kiasi ili kuepukana na matokeo ya kujitia kupita kiasi, kizuizi kingine cha furaha ya sasa. Pia alitia moyo kuwa na mahusiano mazuri na wengine kwa sababu kufanya kwao hivyohivyo kungeleta manufaa. Bila shaka, kuepuka utendaji kosa kisiri, kuzoea kiasi, na kukuza urafiki ni vitendo vyenye kustahili pongezi. Hivyo ni kwa nini falsafa ya Epikurasi ilikuwa hatari kwa Mkristo? Kwa sababu shauri lake lilitegemea mtazamo wake huu usio na imani: “Acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa.”—1 Wakorintho 15:32.

Ni kweli, Biblia huonyesha watu jinsi ya kuishi kwa furaha sasa. Hata hivyo, yashauri hivi: “Jitunzeni wenyewe katika upendo wa Mungu, huku mkingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa tazamio la uhai udumuo milele.” (Yuda 21) Ndiyo, Biblia hukazia zaidi ule wakati ujao wa milele, si wa sasa ambao unapita upesi sana. Upendezi mkubwa wa Mkristo ni kumtumikia Mungu, naye hupata kwamba amwekapo Mungu kwanza, yeye ni mwenye furaha na kutosheka. Kwa njia hiyohiyo, badala ya kujishughulisha sana na mapendezi yake kibinafsi, Yesu alitumia nishati zake bila ubinafsi akitumikia Yehova na kusaidia watu. Aliwafundisha wanafunzi wake kutendea wengine mema, bila kutumaini kutendewa hivyohivyo, lakini watende hivyo kwa sababu ya kuwapenda kikweli. Kwa wazi, vichocheo vya msingi vya Uepikurea na Ukristo ni tofauti kabisa.—Marko 12:28-31; Luka 6:32-36; Wagalatia 5:14; Wafilipi 2:2-4.

Hatari Yenye Hila

Ingawa Waepikurea walikazia sana kuwa wenye furaha, kinyume na hilo, furaha yao ilikuwa kidogo hata chini ya hali zenye kufaa zaidi. Akikosa “furaha ya BWANA,” Epikurasi aliyaita maisha “zawadi yenye huzuni.” (Nehemia 8:10) Wakristo wa mapema walikuwa wenye furaha kama nini kwa kulinganishwa! Yesu hakuwa akipendekeza maisha yasiyo na furaha ya kujinyima. Kwa kweli, kufuata mwendo wake ndio njia ya kupata furaha kubwa zaidi.—Mathayo 5:3-12.

Ikiwa washiriki fulani wa kutaniko katika Korintho walifikiri wangeweza kushirikiana na wale walioathiriwa na kufikiri kwa Epikurasi bila kuhatarisha imani yao, walikosea. Wakati Paulo alipokuwa akiwaandikia Wakorintho barua yake ya kwanza, baadhi yao walikuwa tayari wamepoteza imani katika ufufuo.—1 Wakorintho 15:12-19.

Uepikurea Leo?

Ijapokuwa Uepikurea ulitoweka karne ya nne W.K., leo kuna wale ambao hukubali maoni hayohayo ya ishi kwa ajili ya sasa. Watu hao hawana imani au wana imani kidogo katika ahadi ya Mungu ya uhai wa milele. Lakini, baadhi yao wana viwango vya juu vya mwenendo kwa kulinganishwa.

Huenda Mkristo akashawishiwa kufanyiza uhusiano wa karibu na watu wa namna hiyo, labda akisababu kwamba sifa zao nzuri hustahilisha urafiki. Hata hivyo, ingawa hatujifikirii kuwa bora zaidi, lazima tukumbuke kwamba “mashirika mabaya” yote—kutia na wale ambao uvutano wao ni wenye hila zaidi—“huharibu mazoea yenye mafaa.”

Falsafa ya ishi kwa ajili ya sasa pia hutokea katika semina fulani za kibiashara, vitabu vya kuboresha hali yako mwenyewe, riwaya, sinema, programu za televisheni, na muziki. Ingawa hayaendelezi mwenendo wenye dhambi moja kwa moja, je, maoni hayo yasiyo na imani yangeweza kutuathiri katika njia zenye hila? Kwa kielelezo, je tungeweza kuwa tukijishughulisha sana na hali ya kujiridhisha wenyewe hivi kwamba twasahau suala la enzi kuu ya Yehova? Je, tungeweza kukengeushwa ‘tufanye machache katika utumishi,’ badala ya “[ku]wa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana”? Au tungeweza kuongozwa vibaya kutilia shaka uhaki na manufaa za viwango vya Yehova? Twahitaji kujihadhari dhidi ya kuathiriwa na ukosefu wa adili wa moja kwa moja, jeuri, na uwasiliani-roho na vilevile dhidi ya wale ambao wameathiriwa na maoni ya kilimwengu!—1 Wakorintho 15:58; Wakolosai 2:8.

Kwa hiyo, acheni tukuze ushirika, kimsingi na wale wanaofuata mwongozo wa Yehova kwa moyo wote. (Isaya 48:17) Tokeo ni kwamba, mazoea yetu yenye mafaa yataimarishwa. Imani yetu itatiwa nguvu. Tutaishi kwa furaha si sasa tu bali katika wakati ujao, tukiwa na tazamio la uhai udumuo milele.—Zaburi 26:4, 5; Mithali 13:20.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Epikurasi alifundisha kwamba miungu haipendezwi na wanadamu

[Hisani]

Kwa hisani ya The British Museum

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki