Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 8/15 kur. 12-17
  • Kuishi kwa Ajili ya Sasa Au kwa Ajili ya Wakati Ujao wa Milele?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuishi kwa Ajili ya Sasa Au kwa Ajili ya Wakati Ujao wa Milele?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Fulizeni Kulinda”
  • Misingi ya Itikadi Katika Uhai Udumuo Milele
  • Katika Wakati Ujao Ulio Mbali?
  • Mlinzi Mwaminifu
  • Kuishi kwa Ajili ya Wakati Ujao wa Milele
  • Kutumikia Pamoja na Mlinzi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Wakati wa Kuwapo kwa Mlinzi kama Ezekieli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • “Wafu Watafufuliwa”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • “Ee Mlinzi Habari Gani za Usiku?”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 8/15 kur. 12-17

Kuishi kwa Ajili ya Sasa Au kwa Ajili ya Wakati Ujao wa Milele?

“Tuliokolewa katika tumaini hili.”—WAROMA 8:24.

1. Wafuasi wa Epicurus walifundisha nini, na aina hiyo ya falsafa iliathirije Wakristo fulani?

MTUME Paulo aliwaandikia Wakristo walioishi Korintho hivi: “Ni jinsi gani wengine miongoni mwenu husema hakuna ufufuo wa wafu?” (1 Wakorintho 15:12) Kwa wazi, falsafa yenye kutia sumu ya Mgiriki mwenye hekima Epicurus ilikuwa imepenya miongoni mwa Wakristo wa karne ya kwanza. Hivyo Paulo alivuta uangalifu kwenye fundisho la Epicurus: “Acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa.” (1 Wakorintho 15:32) Wakidharau tumaini lolote la uhai baada ya kifo, wafuasi wa huyo mwanafalsafa waliamini kwamba raha ya kimwili ilikuwa jambo la pekee au lililo kuu maishani mwa mtu. (Matendo 17:18, 32) Falsafa ya Epicurus ilikuwa ya kujifikiria mwenyewe, ya kudharau, na mwishowe ya kushusha.

2. (a) Kwa nini ilikuwa hatari sana kukana ufufuo? (b) Paulo alitiaje nguvu imani ya Wakristo Wakorintho?

2 Kukana huku ufufuo kulikuwa na vidokezi vyenye kina sana. Paulo alisababu hivi: “Ikiwa, kwa kweli, hakuna ufufuo wa wafu, wala Kristo hajafufuliwa. Lakini ikiwa Kristo hajafufuliwa, kuhubiri kwetu ni bure hakika, na imani yetu ni bure. . . . Ikiwa ni katika maisha haya tu tumetumaini Kristo, sisi ndio wa kusikitikiwa zaidi sana kati ya watu wote.” (1 Wakorintho 15:13-19) Ndiyo, bila tumaini la wakati ujao wa milele, Ukristo ungekuwa “ni bure.” Haungekuwa na kusudi. Basi, si ajabu kwamba, chini ya uvutano wa kufikiri huku kwa kipagani, kutaniko la Korintho lilikuwa lenye mazingira ya matatizo. (1 Wakorintho 1:11; 5:1; 6:1; 11:20-22) Kwa hiyo, lengo la Paulo lilikuwa kutia nguvu imani yao katika ufufuo. Akitumia mantiki yenye nguvu, manukuu ya Andiko, na vielezi, alithibitisha bila shaka yoyote kwamba tumaini la ufufuo halikuwa hadithi yenye kubuniwa bali uhalisi wenye uhakika wa kutimizwa. Kwa msingi huu, yeye angeweza kuwasihi waamini wenzake hivi: “Iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.”—1 Wakorintho 15:20-58.

“Fulizeni Kulinda”

3, 4. (a) Kulingana na Petro, ni mtazamo gani wenye hatari ambao ungewashika kabisa watu fulani wakati wa siku za mwisho? (b) Twahitaji kuendelea kujikumbusha nini?

3 Leo, wengi wana mtazamo mbaya, wa kuishi kwa ajili ya leo tu. (Waefeso 2:2) Ni kama vile alivyotabiri mtume Petro. Aliongea juu ya “wadhihaki pamoja na dhihaka zao . . . na kusema: ‘Kuko wapi kuwapo kwake huku kulikoahidiwa? Kwani, kutoka siku baba zetu wa zamani walipolala katika kifo, mambo yote yanaendelea sawasawa kabisa kama kutoka mwanzo wa kuumba.’” (2 Petro 3:3, 4) Waabudu wa kweli wakishindwa na maoni kama hayo, huenda wakawa “wasiotenda ama wasiozaa matunda.” (2 Petro 1:8) Kwa furaha, sivyo ilivyo kwa wengi wa watu wa Mungu leo.

4 Si vibaya kupendezwa na mwisho unaokuja wa mfumo mwovu uliopo. Kumbuka kupendezwa ambako mitume wa Yesu mwenyewe walionyesha: “Bwana, je, wakati huu unarudishia Israeli ufalme?” Yesu alijibu: “Si juu yenu kupata ujuzi wa nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.” (Matendo 1:6, 7) Maneno hayo yana ujumbe wa msingi ambao alikuwa amewasilisha kwenye Mlima wa Mizeituni: “Hamjui ni siku gani Bwana yenu anakuja. . . . Kwenye saa msiyoifikiri kuwa hiyo, Mwana wa binadamu anakuja.” (Mathayo 24:42, 44) Twahitaji kuendelea kujikumbusha shauri hilo! Watu fulani huenda wakashawishwa kuwa na ule mtazamo, ‘Labda yanipasa kutulia kidogo tu na kuchukua mambo kikawaida zaidi.’ Hilo lingekuwa kosa lililoje! Wafikirie Yakobo na Yohana, “Wana wa Ngurumo.”—Marko 3:17.

5, 6. Ni masomo gani tuwezayo kujifunza kutokana na vielelezo vya Yakobo na Yohana?

5 Twajua kwamba Yakobo alikuwa mtume mwenye bidii sana. (Luka 9:51-55) Wakati kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, lazima awe alishiriki daraka lenye utendaji. Lakini wakati Yakobo alikuwa mchanga kwa kadiri, Herode Agripa wa Kwanza aliamuru auawe. (Matendo 12:1-3) Je, tufikiri kwamba Yakobo, kwa kuona uhai wake ukiisha bila kutazamiwa, alihisi huzuni kwa kuwa alikuwa mwenye bidii sana, alikuwa amejikakamua katika huduma? Hata kidogo! Kwa hakika alikuwa mwenye furaha kwamba alikuwa ametumia vizuri zaidi miaka ya uhai wake uliokuwa mfupi kwa kulinganishwa katika utumishi wa Yehova. Sasa, hakuna mmoja wetu awezaye kujua kama uhai wetu waweza kukoma bila kutazamiwa. (Mhubiri 9:11; linganisha Luka 12:20, 21.) Kwa hiyo ni jambo lenye hekima kudumisha kiwango chetu cha bidii na utendaji katika kumtumikia Yehova. Kwa njia hiyo tutadumisha jina letu zuri pamoja naye na tuendelee kuishi tukiwa na wakati ujao wa milele mbele yetu.—Mhubiri 7:1.

6 Kuna kielelezo chenye kutumika kinachohusisha mtume Yohana, aliyekuwepo wakati ambapo Yesu alisihi sana hivi, “Fulizeni kulinda.” (Mathayo 25:13; Marko 13:37; Luka 21:34-36) Yohana alikumbuka maneno hayo, akitumikia kwa idili kwa miongo mingi. Kwa kweli, yaonekana ndiye aliyebaki akiwa hai kati ya mitume wote wengine. Wakati miaka ya Yohana ilipokuwa imeongezeka sana, akiweza kuangalia nyuma kwenye miongo mingi ya utendaji wenye uaminifu, je, aliuona kuwa kosa, maisha yasiyokuwa na mwelekezo au yasiyokuwa na usawaziko? Sivyo, kwa kweli! Bado alikuwa akitazamia kwa hamu wakati ujao. Wakati Yesu aliyefufuliwa aliposema, “Ndiyo; mimi ninakuja upesi,” Yohana alijibu mara moja, “Ameni! Njoo, Bwana Yesu.” (Ufunuo 22:20) Kwa hakika Yohana hakuwa akiishi kwa ajili ya wakati uliopo tu, akiwa na hamu ya ‘maisha ya kawaida’ ya polepole na yenye utulivu. Alikuwa ameazimia kufuliza kutumikia kwa maisha yake yote na nguvu zake zote, hadi wakati wowote ambao Bwana angekuja. Vipi sisi?

Misingi ya Itikadi Katika Uhai Udumuo Milele

7. (a) Tumaini la uhai udumuo milele ‘liliahidiwaje kabla ya nyakati zinazodumu muda mrefu’? (b) Yesu alitoaje nuru kuhusu tumaini la uhai wa milele?

7 Hakikishiwa kwamba tumaini la uhai udumuo milele si ndoto iliyofanyizwa na binadamu au fantasia. Kama lisemavyo andiko la Tito 1:2, ujitoaji-kimungu wetu wategemea “tumaini la uhai udumuo milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi kabla ya nyakati zinazodumu muda mrefu.” Lilikuwa kusudi la Mungu la awali wanadamu wote watiifu waishi milele. (Mwanzo 1:28) Hakuna jambo lolote, hata uasi wa Adamu na Hawa, linaloweza kuzuia kusudi hili. Kama ilivyorekodiwa kwenye Mwanzo 3:15, Mungu aliahidi mara moja “uzao” ambao ungemaliza madhara yote yanayowapata wanadamu. “Uzao” au Mesiya, Yesu, alipofika, alifanya tumaini la uhai wa milele kuwa mojawapo ya mafundisho yake ya msingi. (Yohana 3:16; 6:47, 51; 10:28; 17:3) Kwa kutoa uhai wake mkamilifu uwe fidia, Kristo alijipatia haki halali ya kuwapa wanadamu zawadi ya uhai udumuo milele. (Mathayo 20:28) Baadhi ya wanafunzi wake, 144,000 wakiwa wote, wataishi milele mbinguni. (Ufunuo 14:1-4) Hivyo baadhi ya waliokuwa wakati mmoja wanadamu wawezao kufa ‘watavaa hali ya kutokufa’!—1 Wakorintho 15:53.

8. (a) “Hali ya kutokufa” ni nini, na kwa nini Yehova anawapa wale 144,000? (b) Yesu alitolea “kondoo wengine” tumaini gani?

8 “Hali ya kutokufa” humaanisha zaidi ya kuishi tu bila kufa. Hutia ndani “nguvu ya uhai usioharibika.” (Waebrania 7:16; linganisha Ufunuo 20:6.) Ingawa hivyo, ni nini ambacho Mungu anatimiza kwa kutoa zawadi yenye kutokeza kama hiyo? Kumbuka pingamizi la Shetani kwamba hakuna mmoja wa viumbe wa Mungu ambaye angeweza kutumainiwa. (Ayubu 1:9-11; 2:4, 5) Kwa kuwapa hali ya kutokufa wale 144,000, Mungu huonyesha uhakika kamili katika kikundi hiki kidogo ambacho kwa kutokeza zaidi kimejibu pingamizi la Shetani. Lakini vipi kuhusu wanadamu wanaobaki? Yesu aliwaambia wale washiriki wa kwanza wa “kundi dogo” la warithi wa Ufalme kwamba ‘wangeketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.’ (Luka 12:32; 22:30) Hilo laonyesha kwamba wengine watapokea uhai wa milele duniani wakiwa raia wa Ufalme wake. Ingawa hawa “kondoo wengine” hawapewi hali ya kutokufa, wanapokea “uhai udumuo milele.” (Yohana 10:16; Mathayo 25:46) Hivyo, uhai udumuo milele ni tumaini la Wakristo wote. Si fantasia tu bali jambo ambalo limeahidiwa rasmi na “Mungu, asiyeweza kusema uwongo,” na kulipiwa kwa damu yenye thamani ya Yesu.—Tito 1:2.

Katika Wakati Ujao Ulio Mbali?

9, 10. Kuna dalili gani zilizo wazi kwamba tunakaribia mwisho?

9 Mtume Paulo alitabiri kwamba “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo” zingeonyesha bila shaka kwamba tutakuwa tumefikia “siku za mwisho.” Kadiri jamii ya kibinadamu inayotuzunguka iharibikapo katika hali ya ukosefu wa upendo, pupa, kujipendeza, na kukosa ucha-Mungu, je, hatung’amui kwamba siku ya Yehova ya kutekeleza hukumu zake katika mfumo huu mwovu inakaribia sana? Kadiri jeuri na chuki ziongezekapo, je, hatuoni katika mazingira yetu utimizo wa maneno zaidi ya Paulo: “Watu waovu na walaghai wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi”? (2 Timotheo 3:1-5, 13) Huenda watu fulani kwa kutumainia mema wakatamka “Amani na usalama,” lakini matazamio yote ya amani yatatoweka, kwa kuwa “ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa hapohapo juu yao kama vile maumivu makali ya ghafula ya taabu juu ya mwanamke mwenye mimba; nao hawataponyoka kwa vyovyote.” Hatujaachwa gizani kuhusu maana ya nyakati zetu. Kwa hiyo, “acheni tukae macho na kutunza hisi zetu.”—1 Wathesalonike 5:1-6.

10 Zaidi, Biblia huonyesha kwamba siku za mwisho ni “kipindi kifupi.” (Ufunuo 12:12; linganisha 17:10.) Sehemu iliyo kubwa ya “kipindi kifupi cha wakati” ni dhahiri imepita. Kwa mfano, unabii wa Danieli wafafanua kwa usahihi mapambano kati ya “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” ambayo yameendelea hadi kufikia karne hii. (Danieli 11:5, 6) Lile tu linalobaki kutimizwa ni shambulio la mwisho la “mfalme wa kaskazini,” linalofafanuliwa kwenye Danieli 11:44, 45.—Ona Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1987, na Novemba 1, 1993, kwa ajili ya mazungumzo ya unabii huu.

11. (a) Unabii wa Mathayo 24:14 umetimizwa kwa kadiri gani? (b) Maneno ya Yesu yaliyorekodiwa kwenye Mathayo 10:23 yanaonyesha nini?

11 Pia kuna utabiri wa Yesu kwamba “habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Leo, Mashahidi wa Yehova wanaendeleza kazi yao katika nchi, vikundi vya visiwa, na maeneo 233. Ni kweli, kuna maeneo ambayo hayajahubiriwa bado, na labda katika wakati wa Yehova unaofaa, kutakuwa na fursa ya utendaji zaidi. (1 Wakorintho 16:9) Hata hivyo, maneno ya Yesu kwenye Mathayo 10:23 ni yenye kufanya mtu afikiri: “Hamtakamilisha kwa vyovyote mzunguko wa majiji ya Israeli mpaka Mwana wa binadamu awasili.” Ingawa habari njema bila shaka itatangazwa kotekote duniani, sisi binafsi hatutafikia sehemu zote za dunia mojamoja kwa ujumbe wa Ufalme kabla ya Yesu ‘kuwasili’ akiwa Mfishaji.

12. (a) Ni ‘kutiwa muhuri’ kupi kunakorejezewa kwenye Ufunuo 7:3? (b) Kupungua kwa idadi ya watiwa-mafuta duniani kuna maana gani?

12 Fikiria kwa uangalifu andiko kwenye Ufunuo 7:1, 3, ambalo husema kwamba “pepo nne” za uharibifu zimeshikiliwa “mpaka baada ya sisi tuwe tumetia muhuri watumwa wa Mungu wetu katika vipaji vya nyuso zao.” Hili halirejezei kutiwa muhuri kwa mara ya kwanza, ambako kwatokea wakati wale 144,000 wanapopokea mwito wa kimbingu. (Waefeso 1:13) Hurejezea kutiwa muhuri kwa mara ya mwisho, wanapotambuliwa pasipo kubadilika kuwa “watumwa wa Mungu wetu” waliojaribiwa na walio waaminifu. Idadi ya wana wa Mungu wa kweli watiwa-mafuta walio hai duniani inapunguka sana. Zaidi ya hilo, Biblia husema waziwazi kwamba “kwa sababu ya wale wachaguliwa” sehemu ya kwanza ya dhiki kubwa ‘itakatwa iwe fupi.’ (Mathayo 24:21, 22) Wengi wa wale wanaodai kuwa watiwa-mafuta ni wazee-wazee sana. Tena, je, hilo halionyeshi kwamba mwisho umekaribia sana?

Mlinzi Mwaminifu

13, 14. Daraka la jamii ya mlinzi ni jipi?

13 Katika wakati huohuo, twafanya vizuri kutii mwelekezo wa ‘mtumwa mwaminifu.’ (Mathayo 24:45) Kwa miaka zaidi ya mia moja, “mtumwa” wa siku ya kisasa ametumikia akiwa “mlinzi.” (Ezekieli 3:17-21) Gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1984, lilieleza hivi: “Mlinzi huyo anatazama namna matukio yanavyoendelea kutendeka duniani kwa kutimiza unabii wa Biblia, anatolea watu onyo juu ya ‘dhiki kubwa inayokaribia sana ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu’ kisha anatangaza ‘habari njema za jambo zuri zaidi.’”—Mathayo 24:21; Isaya 52:7.

14 Kumbuka: Ni kazi ya mlinzi kutangaza “aonayo.” (Isaya 21:6-8) Katika nyakati za Biblia, mlinzi angetangaza onyo hata wakati ambapo lile lililotazamiwa kuwa tisho lilikuwa mbali sana kuweza kutambuliwa waziwazi. (2 Wafalme 9:17, 18) Maonyo ya hatari yasiyo ya kweli bila shaka yalitokea huko nyuma. Lakini mlinzi mwema hangejiepusha kusema kwa kuhofu aibu. Kama nyumba yako ingeshika moto, ungehisije ikiwa wazima-moto wangekosa kutokea kwa sababu walifikiri kwamba lilikuwa onyo la hatari lisilo la kweli? Hapana, twatazamia watu hao waitikie haraka kuelekea ishara yoyote ya hatari! Kwa njia hiyohiyo, jamii ya mlinzi imesema wakati inapoelekea kwamba hali zahitaji wafanye hivyo.

15, 16. (a) Kwa nini marekebisho ya uelewevu wetu kuhusu unabii yanafanywa? (b) Twaweza kujifunza nini kutokana na watumishi waaminifu wa Mungu ambao walielewa kimakosa unabii fulani-fulani?

15 Ingawa hivyo, matukio yasitawipo, uelewevu wetu kuhusu unabii umekuwa wazi zaidi. Historia yaonyesha kwamba ni mara chache tu, ikiwa imetukia wakati wowote, ambapo unabii wa kimungu ulieleweka kikamili kabla ya utimizo. Mungu alimwambia Abrahamu hasa ni kwa muda gani uzao ungekuwa ‘mgeni katika nchi isiyo yao,’ yaani, miaka 400. (Mwanzo 15:13) Hata hivyo, Musa, alijitoa mwenyewe kabla ya wakati kuwa mkomboaji.—Matendo 7:23-30.

16 Pia fikiria unabii wa Kimesiya. Kwa kutazama yaliyopita yaonekana wazi kabisa kwamba kifo na ufufuo wa Mesiya ulitabiriwa. (Isaya 53:8-10) Na bado, wanafunzi wa Yesu mwenyewe walishindwa kufahamu ukweli huu. (Mathayo 16:21-23) Hawakuona kwamba unabii wa Danieli 7:13, 14 ungetimizwa wakati ujao wa pa·rou·siʹa, au “kuwapo” kwa Kristo. (Mathayo 24:3) Kwa hiyo walikuwa karibu miaka 2,000 mbali katika kuhesabu kwao wakati walipomwuliza Yesu hivi: “Bwana, je, wakati huu unarudishia Israeli ufalme?” (Matendo 1:6) Hata baada ya kutaniko la Kikristo kuanzishwa vizuri, mawazo yenye makosa na matazamio yasiyo ya kweli yaliendelea kutokea. (2 Wathesalonike 2:1, 2) Ijapokuwa pindi kwa pindi wengine walikuwa na maoni yenye makosa, Yehova bila shaka alibariki kazi ya wale waamini wa karne ya kwanza!

17. Maoni yetu ya marekebisho katika uelewevu wetu kuhusu Andiko yapaswa kuwa nini?

17 Hali kadhalika jamii ya mlinzi ya leo ilibidiwa kuelewesha wazi maoni yake mara kwa mara. Ingawa hivyo, je, yeyote aweza kutia shaka kwamba Yehova amebariki ‘mtumwa mwaminifu’? Mbali na hilo, yakionwa kwa muktadha, je, marekebisho yaliyo mengi ambayo yametokea, si machache kwa kulinganishwa? Uelewevu wetu wa msingi kuhusu Biblia haujabadilika. Usadikisho wetu kwamba tunaishi katika siku za mwisho ni wenye nguvu kuliko wakati mwingine wowote!

Kuishi kwa Ajili ya Wakati Ujao wa Milele

18. Kwa nini lazima tuepuke kuishi kwa ajili ya leo tu?

18 Huenda ulimwengu ukasema, ‘Acheni tule na tunywe, kwa kuwa kesho twafa,’ lakini huu haupasi kuwa mtazamo wetu. Kwa nini ujitahidi bure kupata raha ambazo unaweza kupata katika maisha ya sasa hali unaweza kujitahidi kwa ajili ya wakati ujao wa milele? Tumaini hilo, liwe ni la uhai usioweza kufa mbinguni au uhai udumuo milele duniani, si ndoto, si fantasia. Ni jambo halisi lililoahidiwa na Mungu “asiyeweza kusema uwongo.” (Tito 1:2) Uthibitisho ni mwingi kwamba utimizo wa tumaini letu u karibu! “Wakati ubakio umepunguzwa.”—1 Wakorintho 7:29.

19, 20. (a) Yehova anaonaje dhabihu ambazo tumefanya kwa ajili ya Ufalme? (b) Kwa nini ni lazima tuishi tukiwa na umilele mbele yetu?

19 Ni kweli, mfumo huu tayari umedumu kwa muda mrefu kuliko vile wengi walivyofikiri. Huenda watu wachache sasa wakahisi kwamba kama wangalijua mwanzoni, hawangalitoa dhabihu fulani-fulani. Lakini mtu hapaswi kujuta kuwa alifanya hivyo. Kwa vyovyote, kutoa dhabihu ni sehemu ya msingi ya kuwa Mkristo. Wakristo ‘hujikana wenyewe.’ (Mathayo 16:24) Hatupaswi kufikiri kamwe kwamba jitihada zetu za kumpendeza Mungu ni za bure. Yesu aliahidi hivi: “Hakuna ambaye ameacha nyumba au akina ndugu au akina dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara mia sasa . . . na katika mfumo wa mambo unaokuja uhai udumuo milele.” (Marko 10:29, 30) Miaka elfu moja kutoka sasa, kazi yako, nyumba, na hesabu yako ya benki itakuwa na umaana kadiri gani? Bado, dhabihu ambazo umetoa kwa Yehova zitakuwa na maana miaka milioni moja kutoka sasa—miaka bilioni moja kutoka sasa! “Kwa maana Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu.”—Waebrania 6:10.

20 Kwa hiyo, acheni tuishi tukiwa na umilele mbele yetu, tukiweka macho yetu, “si juu ya vitu vionekanavyo, bali juu ya vitu visivyoonekana. Kwa maana vitu vionekanavyo ni vya muda, lakini vitu visivyoonekana ni vya kudumu milele.” (2 Wakorintho 4:18) Nabii Habakuki aliandika hivi: “Njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia.” (Habakuki 2:3) ‘Kuungojea’ mwisho kwaweza kuathirije njia tunayochukua madaraka yetu ya kibinafsi na ya kifamilia? Makala yetu ifuatayo itashughulikia masuala haya.

Mambo ya Kupitia

◻ Watu wachache leo wameathiriwaje na kule kunakoonekana kuwa kukawia kwa mwisho wa mfumo huu wa mambo?

◻ Ni nini ulio msingi wa tumaini letu la uhai udumuo milele?

◻ Tuoneje dhabihu ambazo tumetoa kwa ajili ya masilahi ya Ufalme?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kazi ya kuhubiri ya tufeni pote lazima ikamilishwe kabla mwisho haujaja

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki