Wakati wa Kuwapo kwa Mlinzi kama Ezekieli
1. (a) Mungu aliweka jamii ya “mlinzi” wake, tangu wakati gani ili isikizishe onyo, na kwa kusudi gani? (b) Mahali pa kusikizisha onyo hilo, Jumuiya ya Wakristo imefanya nini?
ZAIDI ya miaka 35 kabla ya makombora ya atomiki kulipuliwa katika Mashariki ya Mbali kwa rehema Yehova aliweka mlinzi wake asikizishe onyo la jambo lile ambalo bila shaka sasa limekaribia, katika kizazi hiki. Hata kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kutokea katika mwaka 1914 alikuwa ameweka jamii yake ya “mlinzi” ipate kusikizisha onyo. Hilo lilifanywa lionye si wale tu wanaotaka kujua namna ya kuokoka bali pia kuonya maadui wa Yehova wa kukusudia. Hivyo maadui hao watajua chanzo cha uharibifu huo. Hakuna watu wo wote wenye kutafuta makosa watakaokuwa na msingi wa kulalamika kwamba Yeye hakuwapa onyo la kimbele. Jumuiya ya Wakristo, ambayo ina Biblia Takatifu katika zaidi ya lugha elfu moja, ndiyo ingalipaswa kuwa chombo cha kusikizisha onyo hilo, kwa sababu ya kile inachojidai kuwa. Walakini haijafanya hivyo. Badala yake, imejiunga katika vita viwili vya ulimwengu na vita vinginevyo katika karne hii, ambavyo vimeiharibu dunia kwa kadiri isiyopimika. Basi, ni nani “mlinzi” huyo aliye jamii?
2, 3. (a) Mungu alichagua nani asikizishe onyo la gharika ya duniani pote iliyokuwa Inakuja, naye ametumia nani kusikizisha onyo kama hilo leo. (b) Sababu gani Yehova hawezi kulaumiwa kwa ajili ya kupotezwa kwa uhai wo wote?
2 Katika siku za Noa yeye hakuhubiri peke yake bali pia alitengeneza safina kubwa katika kuthibitisha ujumbe wake aliosema. Jamaa yake ya washiriki saba ilijiunga na Noa katika kazi zake za mlinzi. Waebrania 11:1-7 hutuambia ilishuhudiwa juu ya Noa kwamba Mungu alipendezwa sana naye. Alikuwa shahidi wa Yehova Mungu aliyekubaliwa. Alikuwa “mhubiri wa haki.” (2 Pet. 2:5, NW ) Leo tunaelekeana na “tendo la Mungu” la duniani pote kama gharika ya siku za Noa. Maandishi yanaonyesha anatumia nani ili kusikizisha onyo la jambo hilo juu ya ulimwengu wote? Wakristo waliojitoa kila mahali wanaojulikana kama “Mashahidi wa Yehova.” Basi mpaka sasa Yehova hana lawama. Hakukosa kusikizisha onyo la kimungu kupitia kwa mamilioni ya mashahidi wake!
3 Kwa hiyo daraka la uhai wa kibinadamu utakaopotezwa ulimwenguni pote wakati wa mwisho wa taratibu ya mambo unaokuja halitakuwa la Yehova. Litakuwa juu kabisa ya wale waliokataa kutenda kulingana na onyo la kimungu. Jumuiya ya Wakristo yenyewe imeshindwa kutii onyo hilo linalosikizishwa na mashahidi wa Yehova. Namna gani kama ingejiunga na Mashahidi wa Yehova katika kusikizisha onyo hilo lililotolewa na Mungu? Hiyo ingeleta tofauti kama nini katika mambo ya kibinadamu!
MLINZI KWA ISRAELI WA KALE
4. (a) Yehova alitokeza nani awe nabii kwa watu wake Israeli, naye nabii huyo alifananisha nani? (b) Ezekieli alipewa mgawo gani?
4 Kupitia kwa uwezo wake wa kimungu Yehova alitangulia kujua kwamba hata Jumuiya ya Wakristo ingehitaji kupewa onyo lake la mwisho. Yeye alijua yale ambayo historia ya watu wake waliochaguliwa wa nyakati zilizotangulia Ukristo ilikuwa inaonyesha, au inafananisha. Katika mwaka 613 K.W.K. alitokeza Myahudi ambaye jina lake aliitwa Ezekieli awe nabii kwa watu wake. Kwa hiyo ingawa wakati huo alikuwa mhamishwa katika nchi ya Babeli, Ezekieli alikuwa mlinzi wa Yehova kwa Israeli. Matabiri yake yalipelekwa kusini mpaka Yerusalemu katika nchi ya Yuda. Yale ambayo Yehova alimwambia Ezekieli huko nyuma yanatupendeza sisi leo, kwa maana alifananisha mashahidi wa Yehova waliotiwa mafuta wa leo. Jamii hii iliyotiwa mafuta imetenda kulingana na yale ambayo Yehova alimwambia Ezekieli kwa maneno haya: “Mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi wa nyumba ya Israeli; basi, sikia neno hili litokalo katika kinywa changu, ukawape maonyo haya yatokayo kwangu. Nimwambiapo mtu mbaya, Hakika utakufa; wewe usimpe maonyo, wala husemi na uyo mtu mbaya ili kumwonya, kusudi aache njia yake mbaya na kujiokoa [uhai wake]; mtu yule mbaya atakufa katika uovu wake; lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako.”—Eze. 3:17, 18.
5, 6. (a) Ezekieli alikuwa akiishi katika kipindi gani cha wakati? (b) Sababu gani Mungu asingeweza kulaumiwa kuwa alimlazimisha Ezekieli achukue mgawo mgumu?
5 Kwa nini Yehova alizungumza kwa uzito na Myahudi huyu Ezekieli? Kwa sababu katika mwaka huo wa 613 K.W.K. Ezekieli alikuwa akiishi katika siku za mwisho za ufalme uliohukumiwa maangamizi wa Yuda pamoja na mji wake mkuu katika Yerusalemu. Watu wake katika ufalme huo walikuwa wameingizwa katika agano pamoja na Yehova kupitia kwa mpatanishi Wake, nabii Musa, na kwa hiyo akiwa mshiriki wa watu hao Ezekieli alikuwa na daraka kwa Yehova muda wote wa maisha yake. Pia yeye alikuwa kuhani, ambaye alipaswa kutumikia katika hekalu la Yehova kule Yerusalemu. Kwa hiyo ni jambo la kawaida kwamba alikuwa na deni la Mungu. Kwa hiyo Mungu hangeweza kushtakiwa isivyofaa kuwa alimlazimisha Ezekieli achukue mgawo mgumu, yeye alikuwa amezaliwa chini ya agano la taifa zima naye alipaswa kufanya kazi za makuhani wazao wa Haruni, ambao wakati huo walikuwa wakiongozwa na kuhani mkuu Seraya.—2 Fal. 25:18.
6 Ni watu wa Ezekieli ambao Yehova alikuwa ametangulia kusema hivi juu yao kupitia kwa nabii Isaya: “Ninyi ni mashahidi wangu, asema [Yehova], na mtumishi wangu niliyemchagua.” (Isa. 43:10-12) Kwa hiyo Ezekieli alifananisha jamii iliyo tengenezo ya mashahidi wa Yehova waliotiwa mafuta wakati huu, Waisraeli wa kiroho. Mashahidi hawa waliotiwa mafuta wanaishi katika wakati wa maana zaidi na wenye msiba zaidi kuliko siku za Ezekieli zamani sana.
7. (a) Ni serikali gani iliyokuwa hatarini katika siku za Ezekieli, walakini namna gani leo? (b) Ezekieli alisikizisha onyo kwa muda mrefu kadiri gani kabla ya uharibifu uliotabiriwa kuja?
7 Huko nyuma ilikuwa serikali iliyokuwa ikitawala Ezekieli tu, ufalme mdogo wa Yuda, ndio uliokuwa hatarini. Leo ni kile ambacho kilifananishwa na ufalme huo wa kale, yaani, Jumuiya ya Wakristo, ambayo imo hatarini, pamoja na washiriki wake wote wa kilimwengu. Kwa kweli, taratibu nzima ya mambo ulimwenguni pote imo hukumuni, kama ilivyokuwa kwa ulimwengu uliohukumiwa maangamizi katika siku za Noa. Onyo la Mungu kupitia kwa Ezekieli lilihitajiwa kwa haraka sana, maana Ezekieli alianza kusikizisha onyo hilo miaka minne tu kabla ya jeshi la Wababeli kushambulia nchi ya kwake, au miaka sita kabla hawajaharibu mji uliozingirwa wa Yerusalemu na hekalu lake pia. Wakaaji wengi wa Yerusalemu uliozingiriwa waliuawa na njaa, maradhi yenye kuenea na upanga wa vita. Waokokaji wengi waliburutwa na kupelekwa uhamishoni wakafe katika Babeli iliyokuwa mbali. Kwa hiyo kizazi cha Ezekieli kilikuwa katika hatari ya msiba huo.
8. (a) NI msiba gani wa karne ya kwanza uliokuwa unakaribia unaotusaidia kujua wakati wa uharibifu wa ulimwengu utakaoletwa na Mungu? (b) Wakati huo ni nani waliosikizisha onyo la Mungu, nayo kazi yao ya kuonya ilikuwa ya maana kadiri gani?
8 Kutokana na yale ambayo yamekuwa yakitokea duniani kulingana na unabii wa Biblia, twaweza kukata kauli jinsi tulivyo na wakati mfupi leo. Katika unabii wa Yesu, kama ulivyoandikwa katika Mathayo, sura za 24 na 25, aliwaonya wale wanafunzi wake ambao wangekuwa sehemu ya kwanza ya jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” juu ya uharibifu ambao ungeupata Yerusalemu wakati wa kizazi chao. Hivyo aliwajulisha wanafunzi wake juu ya daraka lao juu ya wakaaji Wayahudi wa jimbo la Yudea. Walikuwa katika hatari kubwa kwa ajili ya msiba wa taifa zima uliokuwa unakaribia. Iwapo, katika wakati huo wenye hatari, jamii ya Kikristo ya “mtumwa” huko nyuma haingeonya na kusihi Wayahudi waliohusika watoke katika eneo la hatari haraka iwezekanavyo, basi wangeshiriki daraka la maisha yaliyopotezwa na uhuru wa Wayahudi ambao hawakuonywa.
9. Ni kwa njia gani Ezekieli alikuwa mfano bora wa “mtumwa” aliyetiwa mafuta wa Mungu leo?
9 Vipi kama Ezekieli wa zamani angekosa kufanya mgawo wake aliopewa wa kuonya watu wa nchi yake waliokuwa hatarini akiwa mbali? Hangeokoka kuharibiwa kwa Yerusalemu katika mwaka 607 K.W.K., maana Yehova angemhesabia kuwa na daraka la damu yao. Ni wazi kwamba Ezekieli alitimiza kwa uaminifu mgawo wake aliopewa na Mungu kwa muda ambao iliwezekana kupashana habari pamoja na Yerusalemu uliohukumiwa maangamizi, maana Yehova alipendezwa kumruhusu aendelee kuishi. Yehova alipendezwa kumtumia aseme unabii katika mwaka wa 27 wa uhamisho katika Babeli. Hiyo ilikuwa miaka 16 baada ya kumwagwa damu nyingi sana katika Yerusalemu mwaka 607 K.W.K. (Eze. 29:17; 40:1) Kwa habari hiyo yeye alikuwa mfano bora sana kwa jamii ya “mtumwa” iliyotiwa mafuta katika nyakati zetu za hatari. Ni kweli kwamba mtu ye yote katika jamii ya “mtumwa” akiacha kusikizisha onyo hilo na kuonya waovu, mtu huyo atalazimika kumtolea Yehova hesabu. Walakini, kwa sehemu kubwa, jamii ya “mtumwa” itajithibitisha kuwa kama Ezekieli. Damu yo yote haitatakiwa kwao.
10. (a) Cheo cha mlinzi ni cha maana kadiri gani? (b) Mungu anaonyeshaje kuhangaikia wale wanaohitaji onyo na mlinzi wake pia?
10 Ni wazi sana kwamba cheo cha mlinzi ni chenye daraka kubwa sana. Wakati wa vita askari akilala anapolinda, anauawa, kwa sababu maisha ya wengine yalitiwa hatarini pamoja na hatari ya kushindwa. (Amu. 7:19) Kwa hiyo Mungu anahangaikia, si maisha ya wale wanaohitaji kuonywa peke yake, bali pia juu ya maisha ya mlinzi wake. Hiyo inaonyeshwa na maneno yake yanayofuata aliyomwambia Ezekieli: “Lakini ukimwonya mtu mbaya, wala yeye hauachi ubaya wake, wala njia yake mbaya, atakufa katika uovu wake; bali wewe umejiokoa [nafsi] yako. Tena mtu mwenye haki aiachapo haki yake, na kutenda uovu, nami nikiweka kikwazo mbele yake, atakufa; kwa sababu hukumwonya, atakufa katika uovu wake, wala matendo yake ya haki aliyoyatenda hayatakumbukwa; lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Bali ukimwonya mwenye haki, kwamba yule mwenye haki asitende dhambi, tena ikiwa yeye hatendi dhambi, hakika ataishi, kwa sababu alikubali kuonywa; nawe umejiokoa [nafsi] yako.”—Eze. 3:19-21; 33:2-9.
11. Kazi ya ‘’mtumwa mwaminifu mwenye akili” inafananaje na ile ya mlinzi?
11 Zaburi 127:1 inasema hivi: “[Yehova] asipoulinda mji yeye aulindaye akesha bure.” Hata hivyo, mlinzi ukutani mwa mji amekabidhiwa ulinzi wa maisha ya watu wanaoishi ndani yake. Yeye anadaraka la kuonya raia juu ya kuhatirishwa kwa maisha na uhuru wao kwa njia yo yote. Kwa haki, asingetaka damu yao itakiwe kwake. Kwa kukesha kwake na kulinda pia anapaswa kusifiwa kwa ajili ya kulinda maisha ya nafsi nyinginezo za kibinadamu. Ndivyo ilivyo kwa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” katika wakati huu ambapo taratibu ya kale ya mambo inakaribia kumalizika. Yehova ameiweka jamii ya “mtumwa” kuwa “mlinzi” wake ili kulinda faida za milele za wote wale wanaodai kuwa watu Wake, kama vile kwa habari ya Ezekieli.
VIONYO VINAVYOTOLEWA NA MLINZI WA KISASA
12, 13. (a) Kwa kuhakikisha kwamba onyo linasikizishwa, Mungu anataka kuona itikio gani? (b) Kusikizisha onyo hilo kunafanya jambo gani liwezekane, walakini namna gani wale wasiotii?
12 Hata hivyo, ni wale tu wanaodai kuwa Wakristo wanaokabiliana na tisho la kuharibiwa mwishoni mwa taratibu hii ya mambo? Hapana, walakini pia wanadini wengineo wote, vilevile wale wanaokataa kujiunga na sehemu yo yote ya matengenezo ya kidini. Muumba wa dunia, Yehova Mungu, anajua jambo hilo. Asingependelea kuharibu ulimwengu wa wanadamu. Tamaa yake kubwa ni kwamba wengi iwezekanavyo waokolewe kutokana na uharibifu wa milele na wajithibitishe kuwa wanastahili uzima katika taratibu yake mpya ya mambo yenye haki. Kwa sababu hiyo amesikizisha onyo lake mbali na karibu.
13 Kwa rehema kwanza alijulisha jamii ya “mtumwa” iliyofananishwa na Ezekieli. Hivyo akafanya jamii hiyo kuwa “mlinzi” wake. Jamii hiyo ya “mlinzi” imepewa hasa mgawo wa kusikizisha onyo la kimungu. Kwa sababu ya onyo lao la wakati unaofaa watu zaidi na zaidi wanawezeshwa kusikia na kutenda kulingana nalo wakiwa na tumaini la kuokolewa waupite mwisho wa ulimwengu wa kale. Kwa habari ya wale wanaokataa kutii onyo linalotolewa na Mungu, damu yao itakuwa juu ya vichwa vyao.
14, 15. (a) Ni nani ambao wamejaribu wakashindwa kunyamazisha wale wanaotoa onyo, lakini ni nani ambao wamesikiliza na kuitikia? (b) Kipindi cha “nia njema upande wa Yehova” kimalizikapo, hiyo itamaanisha nini?
14 Jamii ya “mlinzi” wa Yehova imepata kujulikana ulimwenguni pote. Adui zao wanaliona onyo hilo kuwa la kufitini taratibu yao ya mambo. Lakini yote ni kazi bure! Masikio yao yamesikizishwa onyo hilo kwa sauti kubwa hasa tangu mwaka 1919, mwaka ambao ulimwengu ulianza kupona kutokana na uharibifu ulioletwa na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Kipindi hicho cha wakati kuanzia wakati huo kimekuwa sehemu ya yale Isaya 61:2 (NW ) huita “mwaka wa nia njema upande wa Yehova.” Hiyo inamaanisha hasira yake ingali haijamiminwa juu ya taratibu ya mambo yenye kumkaidi Mungu. Hiyo imetimiza kusudi gani? Imewezesha unabii wa Yesu utimizwe mpaka wakati huu: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mt. 24:4, NW ) Kama matokeo ya jambo hilo, wengi leo ambao ni sehemu ya mabaki warithi wa ufalme huo wameitikia ujumbe wa Ufalme. Hivyo wametumia vizuri “nia njema upande wa Yehova.” Wamefanywa kuwa sehemu ya jamii ya “mlinzi.” Wamejiunga katika kusikizisha onyo la kimungu.
15 “Mwaka” wa mfano uliotolewa kwa ajili ya “nia njema upande wa Yehova” ni kipindi kilichopimwa. Vionyesho vyote vya kisasa vinaonyesha kwamba kimekaribia kumalizika. Kumalizika kwacho kutamaanisha, si “Shangwe ya Mwaka Mpya! ” bali wakati wa badiliko kutoka “nia njema” ya Yehova mpaka ghadhabu yake. Hiyo inamaanisha kuja kwa “siku ya kisasi upande wa Mungu wetu.” (Isa. 61:1, 2, NW ) Itakuwa siku isiyo na matumaini kabisa ambayo haijapata kuonwa na ulimwengu wa wanadamu.
16. Ni jambo gani linalotimizwa na jamii ya “mlinzi” kwa kusikizisha onyo?
16 Hiyo inafanya liwe jambo la haraka jamii ya “mlinzi” isikizishe onyo kwamba “mwaka” wa nia njema ya Yehova u karibu kwisha na “siku ya kisasi” yake i karibu kuanza. Kusikizisha kwao onyo la kimungu kwa utii hakutaokoa taratibu ya mambo ya kale iliyowekwa viraka pamoja na wenye kuiunga mkono sana wasiharibiwe katika “dhiki kubwa” inayokuja. Walakini uhakika huo hauvunji moyo jamii ya “mlinzi.” Wamehakikishiwa kwamba wakigeuza watu waovu waachane na njia yao mbovu na kushika haki wataokolewa wasiharibiwe pamoja na ulimwengu huu wa kale. Kwa hiyo jamii ya “mlinzi” haitakuwa na hatia ya damu kwa habari ya wale ambao wameonywa waachane na uovu wao wenye kuua. Jamii ya “mlinzi” pia imepewa uhakikisho kwamba kwa kuendeleza onyo lao wataepusha watu wengi wenye haki wasiwe wabaya na kujiunga na ulimwengu mwovu na hivyo kujiletea maangamizi waangamie nao katika “dhiki kubwa.” Hilo ni jambo linaloridhisha sana jamii ya “mlinzi.” Utumishi wao hautakuwa wa bure!
17. (a) Jamii ya “mlinzi” imepata thawabu gani? (b) Ni nani ambao wamejiunga nao sasa kusikizisha onyo hilo?
17 Jamii ya “mlinzi” haijamaliza sauti yake katika kutangaza onyo hilo juu ya “siku ya kisasi upande wa Mungu wetu.” Wala haijashusha sauti yake. nayo imeazimia kutofanya hivyo. Kama thawabu macho yao yenye kuangalia sana yanaona tamasha yenye kumtukuza Yehova kama nini! “Mkutano mkubwa” usio na hesabu wa wasikilizaji wenye kuitikia onyo unamiminika mbele ya jamii ya “mlinzi.” (Ufu. 7:9) Macho ya huo “mkutano mkubwa” yanafumbuliwa yaone “upanga” wa mkuu wa kufisha wa Yehova ambao u karibu kukata wapinzani waovu wa ufalme wake wa Kimasihi. Miaka minne kabla Vita ya Ulimwengu ya Pili haijaanza, huu “mkutano mkubwa” ulianza kufanyizwa na kujiweka pamoja na jamii ya “mlinzi.” Kwa rehema Vita ya Ulimwengu ya Pili haikumalizika katika “siku ya kisasi upande wa Mungu wetu.” Wala Vita ya Ulimwengu ya Pili na matokeo yake hayakusimamisha wala kupunguza kumiminika kwa wale wa “mkutano mkubwa” upande wa jamii ya “mlinzi” katikati ya mateso ya ulimwenguni pote. Kwa hiyo wamekuwa na daraka la kujiunga na jamii ya “mlinzi” katika kutangaza onyo la kimungu bila woga. Hawajaepa daraka hilo. Kwa njia hiyo wanataka si kuonyesha utii wao wa upendo kwa Yehova tu bali pia kuonyesha upendo wao kwa jirani zao, wanadamu wenzao.
18, 19. (a) Sasa kuna uhitaji mkubwa sana kwa ajili ya utendaji gani, kupatana na maneno ya Isaya 52:8? (b) Ni jambo gani linalopaswa kutuchochea tushiriki katika kulisikizisha onyo hilo la kimungu?
18 Katika wakati huu ulioendelea sana, katika siku za kumalizia za Jumuiya ya Wakristo na sehemu nyingine yote ya taratibu hii ya mambo maangamizi, kuna uhitaji mkubwa wa tendo la umoja. Zamani sana nabii Ezekieli na nabii wa wakati mmoja naye Yeremia, ingawa walikuwa mamia ya maili mbali—mbali waliunganisha sauti zao katika kuonya taifa lao lililopotoka juu ya “siku ya kisasi” ambayo ilikuwa inakaribia kuwapata. Sasa, katika karne yetu tangu kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, maneno ya Isaya 52: 8 yamehusu watu wa Yehova walio wakf: “Sauti ya walinzi wako! Wanapaza sauti zao, wanaimba pamoja; maana wataona jicho kwa jicho, jinsi [Yehova] arejeavyo Sayuni.” Wote waliokusanywa tena chini ya “Sayuni wa kimbinguni” waliona njozi ile ile kwa msaada wa unabii wa Biblia uliokuwa ukitimia wakati huo; pamoja waliona mkono wa Yehova ukitenda kwa kuwapendelea. Walitokeza ujumbe wa umoja kwa ulimwengu mzima. Leo, zaidi ya miaka 60 baadaye, lazima waendelee kutoa ushuhuda kwa umoja, ila sasa waongeze onyo la haraka juu ya “siku ya kisasi” ya Yehova. “Mkutano mkubwa” unaotoka wa mataifa mengi na lugha nyingi unapaswa kuunganisha sauti zao pamoja na zile za “mlinzi.”
19 Songeni mbele, basi, kwa umoja pamoja na onyo juu ya “siku ya kisasi upande wa Mungu! ” Tujiepushe na hatia ya damu. Hiyo ni kwa sababu tunataka kuokolewa wakati wa “siku ya kisasi.” Jirani zetu wengi wangependa kufurahia wokovu uo huo. Upendo wetu mwingi kwa Yehova na Kristo na upendo wetu wa kibinadamu kwa jirani zetu, wanadamu wenzetu, utusukume mbele bila kuzuiwa tusikizishe onyo hilo lenye kuokoa maisha. Itatutokezea furaha nyingi sana! Na zaidi ya yote, Yehova atatetewa kuwa alijali kwa upendo!
[Picha katika ukurasa wa 19]
Kama vile Ezekieli alivyokuwa ameonya, jeshi la Babeli liliharibu Yerusalemu na kuwahamisha waokokaji wengi
[Picha katika ukurasa wa 21]
Kama Ezekieli, jamii ya “mlinzi” ya kiasasa inasikizisha onyo—ikisaidiwa na “mkutano mkubwa” wa wafanya kazi wenzi