Ulimwengu Wenye Haki Si Ndoto!
“HAKI ndilo hangaiko kubwa la mwanadamu duniani,” akasema kiongozi wa siasa Mmarekani Daniel Webster. Nayo Biblia hutaarifu hivi: “BWANA hupenda haki.” (Zaburi 37:28) Wakiwa wamefanywa kwa mfano wa Mungu, wenzi wa kwanza wa kibinadamu walikuwa na sifa za kimungu,kutia na kuitambua haki.—Mwanzo 1:26, 27.
Maandiko pia husema juu ya ‘watu wa mataifa wasio na sheria wakifanya kwa asili mambo ya sheria.’ Hivyo wao “[huonyesha] kiini cha sheria kuwa imeandikwa katika mioyo yao, huku dhamiri yao ikitoa ushahidi pamoja nao na, kati ya fikira zao wenyewe, wanashtakiwa au hata wanatetewa.” (Waroma 2:14, 15) Ndiyo, wanadamu wana uwezo wa dhamiri—hisi ya ndani zaidi ya kupambanua mema na mabaya. Kwa wazi, uhitaji wa haki ni asili ya mwanadamu.
Wenye kufungamanishwa kwa ukaribu na ule uhitaji wa haki ni ufuatiaji-furaha wa mwanadamu, kwa maana andiko la Zaburi 106:3 lajulisha wazi hivi: “Heri washikao hukumu [“haki,” NW], na kutenda haki [“uadilifu,” NW] sikuzote.” Ingawa hivyo, kwa nini mwanadamu ameshindwa kuleta ulimwengu wenye haki?
Kwa Nini Mwanadamu Ameshindwa?
Sababu ya msingi ya kushindwa kupata ulimwengu wenye haki ni lile waa ambalo tumerithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. Biblia hueleza hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Hilo waa ni dhambi. Ingawa waliumbwa wakiwa wakamilifu, Adamu na Hawa waliamua kuasi dhidi ya Mungu na hivyo wakajifanya watenda-dhambi. (Mwanzo 2:16, 17; 3:1-6) Kwa sababu hiyo, waliwaachia watoto wao mielekeo yenye dhambi na yenye kosa.
Je, vitabia vya utu kama vile pupa na ubaguzi si matokeo ya mielekeo yenye dhambi? Na je, vitabia hivyo havichangii ukosefu wa haki ulimwenguni? Naam, pupa ndio mzizi wa kutumia mazingira vibaya kimakusudi na wa kuonea kiuchumi! Bila shaka ubaguzi ndio usababishao zogo la kikabila na ukosefu wa haki wa kijamii. Vitabia kama hivyo pia hushawishi watu wapokonye, wadanganye, na kutenda katika njia ambayo huwadhuru wengine.
Mara nyingi hata jitihada zenye nia nzuri za kutumia haki na kufanya mema hushindwa kwa sababu ya mielekeo yetu yenye dhambi. Mtume Paulo mwenyewe aliungama hivi: “Lile jema nitakalo silifanyi, bali lile baya nisilotaka ndilo nazoea kulifanya.” Aendelea kueleza hilo shindano, kwa kusema hivi: “Napendezwa na sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona katika viungo vyangu sheria nyingine ikifanya vita dhidi ya sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.” (Waroma 7:19-23) Yaelekea, sisi leo tuna pambano hilohilo. Hiyo ndiyo sababu ukosefu wa haki hutokea mara nyingi sana.
Njia ya kibinadamu ya kutawala pia imechangia ukosefu wa haki ulimwenguni. Katika kila nchi, kuna sheria na vilevile wale ambao huzitekeleza. Na bila shaka, kuna mahakimu na mahakama mbalimbali. Hakika, watu fulani wenye kanuni wamejaribu kutegemeza haki za kibinadamu na kuhakikisha kwamba kuna haki iliyo sawa kwa wote. Na bado, jitihada zao zilizo nyingi zimeshindwa. Kwa nini? Akitoa muhtasari wa mambo mbalimbali yenye kuhusika katika kushindwa kwao, Yeremia 10:23 hutaja hivi: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Akiwa amefarakana na Mungu, mwanadamu hawezi kuanzisha ulimwengu wenye uadilifu na wenye haki waziwazi.—Mithali 14:12; Mhubiri 8:9.
Kizuizi kikubwa kwa jitihada za mwanadamu za kujenga ulimwengu wenye haki ni Shetani Ibilisi. Biblia hutaarifu waziwazi kwamba yule malaika mwasi Shetani ndiye “muua-binadamu” na “mwongo” wa awali na kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (Yohana 8:44; 1 Yohana 5:19) Mtume Paulo humtambulisha kuwa “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (2 Wakorintho 4:3, 4) Akiwa mchukiaji wa uadilifu, Shetani hufanya lolote awezalo ili kuendeleza uovu. Maadamu yeye huongoza ulimwengu, ukosefu wa haki wa namna zote na ole zitokanazo na huo zitawafanya wanadamu kuwa watumwa.
Je, hayo yote humaanisha kwamba ukosefu wa haki ni jambo lisiloepukika katika jamii ya kibinadamu? Je, ulimwengu wenye haki ni ndoto isiyoweza kuwa kweli?
Ulimwengu Wenye Haki Ni Uhalisi—Jinsi Gani?
Ili tumaini la ulimwengu wenye haki liwe uhalisi, yawabidi wanadamu wategemee chanzo kiwezacho kung’oa visababishi vya ukosefu wa haki. Lakini ni nani awezaye kuing’oa dhambi na kumwondosha Shetani na utawala wake? Kwa wazi, hakuna binadamu wala shirika lolote la kibinadamu liwezalo kutimiza kazi hiyo iliyo ngumu sana. Yehova Mungu pekee ndiye awezaye kufanya hivyo! Biblia hutaarifu hivi kumhusu: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu [“ukosefu wa haki,” NW], yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Na akiwa “[m]penda haki,” Yehova hutaka wanadamu wayaonee shangwe maisha katika ulimwengu wenye haki.—Zaburi 37:28.
Akisema juu ya mpango wa Mungu wa kuleta ulimwengu wenye haki, mtume Petro aliandika hivi: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) “Mbingu [hizi] mpya” si mbingu mpya halisi. Mungu alifanya mbingu zetu halisi zikiwa kamilifu, na hizo humletea utukufu. (Zaburi 8:3; 19:1, 2) Hizo “mbingu mpya” ni utawala mpya juu ya dunia. Asili ya “mbingu” za wakati wa sasa ni serikali zilizotengenezwa na watu. Karibuni sana, kwenye vita ya Mungu ya Har–Magedoni, hizo serikali zitapisha “mbingu mpya”—Ufalme wake au serikali yake ya kimbingu. (Ufunuo 16:14-16) Mfalme wa Ufalme huo ni Yesu Kristo. Serikali hiyo itatawala kwa wakati usio dhahiri, ikileta mwisho wenye kudumu kwa utawala wa kibinadamu.—Danieli 2:44.
Basi, ni nini iliyo “dunia mpya”? Hiyo si sayari mpya, kwa maana Mungu aliifanya dunia ikiwa yenye kufaa kabisa kukaliwa na binadamu, na ni mapenzi yake kwamba idumu milele. (Zaburi 104:5) Hiyo “dunia mpya” hurejezea jamii mpya ya watu. (Mwanzo 11:1: Zaburi 96:1) Asili ya hiyo “dunia” ambayo itaharibiwa ni watu ambao hujifanya kuwa sehemu ya mfumo huu mwovu wa mambo. (2 Petro 3:7) Ile “dunia mpya” ambayo itachukua mahali pake itafanyizwa na watumishi wa kweli wa Mungu, wachukiao uovu na kupenda uadilifu na haki. (Zaburi 37:10, 11) Hivyo, ulimwengu wa Shetani utakuwa umetoweka.
Lakini ni nini kilicho akibani kwa ajili ya Shetani? Mtume Yohana alitabiri hivi: “Naye [Kristo Yesu] akalikamata joka kubwa, nyoka wa awali, aliye Ibilisi na Shetani, na kumfunga kwa miaka elfu. Naye akamvurumisha ndani ya abiso na kuifunga na kuitia muhuri juu yake, ili asipate kuongoza mataifa vibaya tena kamwe.” (Ufunuo 20:1-3) Shetani mwenye kufungwa minyororo hatakuwa na uvutano juu ya wanadamu kama vile mfungwa ndani ya gereza lenye kina. Hicho kitakuwa kitulizo kama nini kwa wanadamu, kikija kama mtangulizi wa ulimwengu wenye haki! Na mwishoni mwa miaka elfu, Shetani atapondwa asiweko.—Ufunuo 20:7-10.
Ingawa hivyo, namna gani juu ya dhambi iliyorithiwa? Yehova tayari ameandaa msingi wa kung’oa dhambi. ‘Mwana wa binadamu Yesu Kristo alikuja, kutoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Neno “fidia” huonyesha bei ihitajiwayo kwa ajili ya kukomboa watekwa. Yesu alilipa bei ya uhai wake wa kibinadamu ulio mkamilifu kuwa fidia ili akomboe wanadamu.—2 Wakorintho 5:14; 1 Petro 1:18, 19.
Dhabihu ya fidia ya Yesu yaweza kutunufaisha hata sasa. Kwa kuzoea imani katika hiyo, twaweza kuonea shangwe msimamo safi mbele za Mungu. (Matendo 10:43; 1 Wakorintho 6:11) Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, hiyo fidia itawezesha wanadamu wapone kikamili kutokana na dhambi. Kitabu cha mwisho cha Biblia hufafanua “mto wa maji ya uhai” wa kitamathali ukitiririka kutoka katika kiti cha ufalme cha Mungu, na kandokando ya kingo zake kuna miti ya kitamathali ya matunda ikiwa na majani “ya kuponya mataifa.” (Ufunuo 22:1, 2) Lile ambalo Biblia yaonyesha hapa huwakilisha maandalizi ya kustaajabisha ya Muumba ya kuwapata tena wanadamu kutoka katika dhambi kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. Utumizi kamili wa uandalizi huo utaweka huru wanadamu watiifu kutoka katika dhambi na kifo.
Maisha Katika Ulimwengu Wenye Haki
Fikiria jinsi maisha yatakavyokuwa chini ya utawala wa Ufalme. Uhalifu na jeuri yatakuwa mambo ya wakati uliopita. (Mithali 2:21, 22) Ukosefu wa haki kiuchumi utakuwa umetoweka. (Zaburi 37:6; 72:12, 13; Isaya 65:21-23) Alama zote za ubaguzi wa kijamii, kimbari, kikabila, na vikundi vya kikabila utafutwa. (Matendo 10:34, 35) Vita na silaha za shughuli za vita hazitakuwapo tena. (Zaburi 46:9) Mamilioni ya wafu watarudishwa kwenye uhai katika ulimwengu usio na ukosefu wa haki. (Matendo 24:15) Kila mtu ataonea shangwe afya kamilifu na nzuri. (Ayubu 33:25; Ufunuo 21:3, 4) “Kwa kweli,” Biblia yatuhakikishia kwamba, “[Yesu Kristo] atatokeza hukumu [“haki,” NW].”—Isaya 42:3.
Kwa sasa, ukosefu wa haki waweza kutupata, lakini tusiwe wenye kukosa haki kamwe kwa kulipiza kisasi. (Mika 6:8) Na tudumishe mtazamo chanya, hata wakati ambapo ukosefu wa haki lazima uvumiliwe. Ulimwengu wenye haki ulioahidiwa utakuwa uhalisi karibuni. (2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:11-13) Mungu Mweza-Yote ametoa ahadi yake, nayo ‘ndivyo itakavyokuwa.’ (Isaya 55:10, 11) Sasa ndio wakati wa kujitayarisha kuishi katika ulimwengu huo wenye haki kwa kujifunza mambo ambayo Mungu hutaka tufanye.—Yohana 17:3; 2 Timotheo 3:16, 17.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Alama zote za ukosefu wa haki zitafutwa katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa