Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 11/15 kur. 5-8
  • Haki kwa Wote—Itakujaje?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Haki kwa Wote—Itakujaje?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ufalme wa Mungu na Haki
  • Ufalme wa Mungu na Shetani
  • Ufalme wa Mungu na Kutokamilika kwa Mwanadamu
  • Ufalme wa Mungu na Wewe
  • Ulimwengu Wenye Haki Si Ndoto!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Yehova Ni Mpenda-haki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Watawala Katika Makao ya Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 11/15 kur. 5-8

Haki kwa Wote​—Itakujaje?

KWA sababu gani Yehova akaruhusu dhuluma iwe nyingi sana duniani? Kwa sababu wanadamu walichagua hivyo! Hapo kwanza, mambo yalikuwa tofauti. Walipoumbwa mara ya kwanza, Adamu na Hawa hawakuumizwa na mzigo wa kutokamilika. Walikuwa sehemu ya uumbaji ambao Mungu alitangaza kuwa ni ‘mwema sana.’ (Mwanzo 1:31; Kumbukumbu la Torati 32:4) Zaidi ya hayo, hakukuwako Shetani, na mwanadamu alikuwa akitawalwa moja kwa moja na Mungu. Kwa hiyo, hapo mwanzo hakukuwako dhuluma.

Lakini hali hiyo haikuendelea. Kiumbe wa kiroho mkamilifu aliasi akawa Shetani. Kwa kujificha katika nyoka, alimtamanisha Hawa kwa tumaini lisilotimilika la kuwa huru. Mungu alikuwa amewekea katazo moja tu wanadamu hao wawili wa kwanza. Hawakupaswa kula tunda la mti fulani. Kama wangefanya hivyo, wangekufa. Lakini Shetani alimwambia Hawa hivi: “Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”​—Mwanzo 3:1-5.

Hawa, kisha Adamu, wakavunja sheria ya Mungu. Walitaka kuwa kama Mungu, kujifanyia maamuzi yao wenyewe juu ya yaliyo mema na yaliyo mabaya. Kwa hiyo, wakajiondosha kwa Mungu na kufungua njia ya kusimamisha utawala wa kibinadamu, pamoja na matatizo yao yote.

Adamu na Hawa pia walipatwa na badiliko la kimwili. Mungu aliwahukumia kifo, sawa na alivyokuwa amesema angefanya. Wakawa wasiokamilika, na hilo likaongoza kwenye kupotoka kwa jamii yote ya kibinadamu​—watoto wao. Mtume Paulo alieleza hivi: “Kwa mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12) Kwa njia hiyo visababishi vikuu vya dhuluma vikatokea.

Hata hivyo, tunasoma hivi: “Mfalme huifanya nchi iendelee kusimama kwa haki.” (Mithali 29:4, NW) Jamii ya kibinadamu ‘haitasimama’ kabisa wala kuwa imara kabisa mpaka haki iwepo duniani pote. Je! hilo litatokea wakati wo wote?

Ufalme wa Mungu na Haki

Kwa kuwa Yehova Mungu “hupenda haki,” tunaweza kuwa na uhakika jambo hilo litatokea. (Zaburi 37:28) Lakini jinsi gani? Maneno ya Sala ya Bwana yanatuambia hivyo. Kwa karne nyingi Wakristo wenye moyo mweupe wamesali hivi: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Kwa hiyo, kupitia Ufalme wa Mungu, mambo ambayo Mungu anataka yatatimizwa hatimaye hapa duniani.

Ufalme wa Mungu ni serikali halisi. Ni ya kimbingu, kwa hiyo ni yenye nguvu zaidi ya serikali yo yote ya kibinadamu. Pia ina Mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu, Mfalme huyo ni Yesu Kristo, ambaye anahangaikia sana haki. (Zaburi 72:12-14) Yehova anaahidi kwamba atabariki utawala huo wa Ufalme chini ya Kristo, “kuuthibitisha na kuutegemeza kwa hukumu na kwa haki.”​—Isaya 9:7.

Unabii mwingi mbalimbali unaotimia leo unathibitisha kwamba Ufalme huo tayari upo. (Luka 21:31, 32) Tayari Yesu ni Mfalme! Lakini yeye ataletaje haki kwa wanadamu vijapokuwa vipingamizi vyote vilivyoko? Ebu tuone.

Mungu anakusudia kwamba Ufalme wake chini ya Kristo uwe serikali ya ulimwengu wote. Yehova anasema hivi kwa njia ya unabii: “Naye [Kristo] atatawala vilevile toka bahari hata bahari, na toka Muto hata miisho ya dunia.” (Zaburi 72:8, ZSB) Jambo hilo litakapotimizwa duniani pote, chanzo kikuu kimoja cha dhuluma kitakwisha. Mwanadamu hatajitawala tena. Lakini jambo hilo lingewezaje kutokea wakati ambao kuna serikali nyingi sana leo, kila moja ikiwa yenye wivu mkubwa kwa ajili ya enzi yake yenyewe?

Uhakika ni kwamba Mungu ameweka kipimo cha wakati ambao serikali za kibinadamu zitafanya kazi, na kipimo hicho cha wakati kimekwisha fika. Akizungumza juu ya serikali zote zenye kutukuza taifa za siku zetu, nabii Danieli aliandika: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”​—Danieli 2:44.

Kwa njia hiyo, serikali moja ya ulimwengu wote, Ufalme wa Mungu, karibuni itachukua mahali pa serikali zenye kutukuza taifa za leo itawale wanadamu kwa haki. Hilo litakuwa badiliko lenye kuleta mazuri kama nini! Hata hivyo, bado kutakuwa kumebaki tatizo la Shetani. Ufalme wa Mungu utashughulikaje naye?

Ufalme wa Mungu na Shetani

Shetani alitokea mapema katika historia ya wanadamu, naye ndiye wa kwanza kumdokezea Hawa wazo la kumwasi Mungu. Kwa hiyo, alipokuwa akitoa hukumu juu ya Adamu na Hawa kwa ajili ya dhambi yao, Mungu hakusahau Shetani. Alitabiri kuja kwa “uzao” ambao ungempinga Shetani, na hatimaye kumharibu: “Nami nitaweka uadui... kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Ikawa kwamba uzao huo ulioahidiwa alikuwa ni Yesu Kristo. (Wagalatia 3:16) Mipambano miwili yenye kutokeza imekwisha tokea kati ya Shetani na Yesu ikiwa ni utimizo mdogo wa unabii huo wa kale.

Wa kwanza ulionekana kuwa ni ushindi kwa Shetani. Aliongoza Yesu auawe juu ya mti wa mateso. Kwa njia hiyo “kisigino” cha Yesu ‘kikapondwa.’ Lakini ushindi wa Shetani haukuendelea muda mrefu. Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu na kukwezwa kwenye cheo cha juu mbinguni. (Matendo 2:23, 24, 32-36) Muda si muda, akiwa huko alitawazwa na Yehova Mungu awe Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Kisha mpambano mwingine wa kihistoria ukatokea.

Matokeo yake yamesimuliwa katika Biblia: “Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.” Matokeo yakawa nini? Furaha katika mbingu, sasa zikiwa zimesafishwa kuwapo kwa Shetani kwenye kuchafua. Lakini “ole kwa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:9, 12) Tunaishi katika huo “wakati mchache.” Dhuluma nyingi tunayoona leo inaletwa na “ghadhabu nyingi” ya Shetani.

Hata hivyo, karibuni utakuja mpambano mwingine kati ya Shetani na Yesu Kristo. Biblia inausimulia mpambano huo pia: “Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; akamtupa katika [shimo refu], akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie.”​—Ufunuo 20:2, 3.

Jambo hilo litatokea karibuni, wakati Ufalme wa Mungu utakapochukua mahali pa serikali zenye kutukuza taifa za ulimwengu huu. Hatimaye hilo litaongoza kwenye mpambano wa mwisho wakati, kama ambavyo Biblia inavyoeleza kwa njia ya kiunabii, “yule Ibilisi. .. [atakapotupwa] katika ziwa la moto na kiberiti” aharibiwe, kule ‘kupondwa kichwa’ kwa mwisho.​—Ufunuo 20:10.

Kwa hiyo, kizuizi kingine cha haki kitakuwa kimeondolewa. Lakini bado hilo linatuacha na tatizo la asili ya mwanadamu ya kutokamilika. Dhuluma nyingi katika ulimwengu inaletwa na wanadamu wenyewe. Ufalme wa Mungu unaweza kufanya nini kuhusu hilo?

Ufalme wa Mungu na Kutokamilika kwa Mwanadamu

Kutokamilika kwa mwanadamu kulianza wakati Adamu na Hawa walipofanya dhambi. (Warumi 5:12) Wazao wote wa Adamu, isipokuwa mmoja, wamekuwa watenda dhambi, isipokuwa Yesu. Yeye alizaliwa kwa njia ya kimuujiza bila dhambi, na maishani mwake mwote alibaki akiwa mwaminifu na bila dhambi. (Waebrania 7:26) Kwa njia hiyo, angeweza kutoa uhai mkamilifu wa kibinadamu kuwa ukombozi kwa ajili ya wanadamu wasiokamilika. Yeye aliondoa tatizo la kutokamilika kwa kibinadamu. “Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa.”​—1 Wakorintho 15:22.

Karibuni, wale wanaosisitiza kudhulumu watakuta kwamba hawana mahali kwenye dunia safi chini ya Ufalme wa Mungu. Lakini wale wenye imani katika dhabihu ya Yesu watavuna baraka kubwa. “Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi.” (Mithali 2:21, 22) Kwa njia hiyo kitu kingine kinachozuia haki kitaondolewa.

Ufalme wa Mungu na Wewe

Ndiyo, Yesu, akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, karibuni ataondoa vizuizi vyote vikubwa vinavyozuia kusiwepo haki kwa wote duniani. Kisha wanadamu wataona ahadi hii ikitimizwa: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea . . . na katika hizo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13, NW) Katika dunia hiyo yenye uadilifu hakutakuwako nafasi ya dhuluma.

Bila shaka, baraka hizo zingali ni za wakati ujao. Hata sasa, ijapo hivyo, Ufalme wa Mungu chini ya Kristo Yesu unatenda, na tunaweza kufaidika kutokana nao. Yesu mwenyewe alitabiri kwamba katika siku zetu “habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14, NW) Unabii huo unatimizwa. Wengi wanaitikia kuhubiri huko na kujitiisha chini ya Ufalme huo hata sasa. Kwa njia hiyo maneno haya ya kiunabii yanawafaa:

“Itakuwa katika siku za mwisho, . . . mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la [Yehova] katika Yerusalemu.”​—Isaya 2:2, 3.

Mamilioni duniani pote wanaojipatanisha na unabii huo wanajifunza Biblia na kujifunza kuishi katika njia ambayo Mungu anataka waishi. Kati ya mambo mengine, wanajaribu kuishi kulingana na maneno ya nabii Mika: ‘Kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wao.’ (Mika 6:8) Hivyo wanaonyesha unyofu wa tamaa yao ya kutaka kuishi chini ya serikali ya haki. Hata sasa wanafurahia baraka nyingi kutoka kwa serikali hiyo unabii wa Isaya unapotimizwa: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu.”​—Isaya 32:1.

Je! wewe unatamani kuona ulimwengu wenye kujaa haki? Ikiwa ndivyo, weka tumaini lako katika Ufalme wa Mungu. Shirikiana sasa na watu wenye tamaa iyo hiyo. Halafu tazama mbele ukiwa na uhakika wa kuishi milele chini ya utawala wa Mungu ambaye ‘hupenda haki na hukumu.’​—33:5.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Yesu alihurumia wenye taabu na wenye hali ya chini. Utawala wake kutoka mbinguni utategemezwa na haki

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki