Ukristo Ukitenda Katikati ya Msukosuko
MAMBO yote yalianza ghafula siku moja Aprili 1994. Ndege ilianguka na kuua rais wa Burundi na wa Rwanda. Mnamo saa chache ujeuri wa viwango vyenye kushtua uliikumba Rwanda. Kwa kipindi kilichozidi kidogo miezi mitatu, Warwanda zaidi ya 500,000—wanaume, wanawake, na watoto—walikuwa wamekufa. Watu fulani hurejezea kipindi hicho kuwa “maangamizi ya jamii nzima-nzima.”
Nusu ya wakazi wa Rwanda milioni 7.5 walilazimika kukimbia. Hiyo ilitia ndani watu milioni 2.4 waliotafuta kimbilio katika nchi jirani. Huko kulikuwa kutoka kukubwa zaidi na kwa haraka zaidi kwa wakimbizi katika historia ya kisasa. Kambi za wakimbizi zilianzishwa haraka-haraka katika Zaire (sasa iitwayo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo), Tanzania, na Burundi. Baadhi ya kambi hizo—zikiwa kambi kubwa zaidi ulimwenguni—zilikuwa kimbilio la watu 200,000.
Miongoni mwa wakimbizi mlikuwemo Mashahidi wa Yehova, watu wapendao amani na ambao hutumia kanuni za Biblia maishani mwao. Katika nchi yoyote ile ambamo waishi, wao hudumisha kutokuwamo kabisa na hutumia ile kanuni iliyo ndani ya maneno haya ya Isaya 2:4: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Mashahidi wa Yehova watambuliwa sana kuwa kikundi cha kidini ambacho hakikushiriki katika hayo maangamizi ya jamii nzima-nzima katika Rwanda.
Yesu Kristo alisema kwamba wafuasi wake “si sehemu ya ulimwengu.” Hata hivyo, kwa sababu wao “wamo ulimwenguni,” hawawezi kuponyoka sikuzote msukosuko wa mataifa. (Yohana 17:11, 14) Wakati wa yale maangamizi ya jamii nzima-nzima katika Rwanda, Mashahidi wapatao 400 walipoteza uhai wao. Mashahidi na watu wenye kupendezwa na ujumbe wa Ufalme wapatao 2,000 walipata kuwa wakimbizi.
Je, kutokuwa sehemu ya ulimwengu kwamaanisha kwamba Mashahidi wa Yehova hawafanyi lolote maafa yazukapo? La. Neno la Mungu husema hivi: “Ikiwa ndugu au dada yumo katika hali ya uchi na anakosa chakula cha kutosha kwa siku, lakini mtu fulani kati yenu awaambia wao: ‘Nendeni kwa amani, fulizeni kujipasha moto na kulishwa vizuri,’ lakini nyinyi hamwapi mahitaji ya lazima ya mwili wao, ina manufaa gani? Hivyo, pia, imani ikiwa haina kazi, imekufa ndani yayo yenyewe.” (Yakobo 2:15-17) Kupenda jirani pia huwasukuma Mashahidi wawasaidie wale wasioshiriki maoni yaleyale ya kidini.—Mathayo 22:37-40.
Ingawa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walitamani sana kuwasaidia waamini wenzao waliokabili hali ya maafa katika Rwanda, Ulaya Magharibi ilipewa mgawo wa kusimamia jitihada ya kutoa msaada. Katika kiangazi cha 1994, kikoa cha Mashahidi waliojitolea kutoka Ulaya kiliharakisha ili kusaidia ndugu na dada Wakristo katika Afrika. Kambi zilizopangwa vizuri na hospitali za muda zilijengwa kwa ajili ya wakimbizi wa Rwanda. Kiasi kikubwa cha mavazi, mablanketi, chakula, na fasihi za Biblia kililetwa kwa ndege au kusafirishwa kwa njia nyinginezo. Watu zaidi ya 7,000 walioathiriwa—idadi ipatayo mara tatu ya Mashahidi wa Yehova katika Rwanda ya wakati huo—walinufaika na jitihada hiyo ya kutoa msaada. Kufikia mwezi wa Desemba mwaka huo, maelfu ya wakimbizi, kutia na waliokuwa Mashahidi wa Yehova, walirudi Rwanda ili kuanza upya maisha zao.
Vita Katika Kongo
Mwaka wa 1996, shughuli za vita zilizuka katika eneo la mashariki la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Eneo hilo lapakana na Rwanda na Burundi. Tena kulikuwa na ubakaji na mauaji. Katikati ya risasi zenye kupita kasi na vijiji vilivyokuwa vikichomeka, watu walikimbia ili kusalimisha uhai wao. Mashahidi wa Yehova walinaswa katika huo msukosuko, na wapatao 50 wakafa. Baadhi yao waliuawa na risasi zilizokosa shabaha. Wengine walichinjwa kwa sababu walikuwa wa kikundi fulani cha kikabila au walionwa kuwa adui kimakosa. Kijiji kimoja ambako Mashahidi 150 waliishi kiliharibiwa kwa moto. Katika vijiji vingine dazani za nyumba na Majumba ya Ufalme fulani yalichomwa. Wakiwa bila nyumba wala mali, Mashahidi walikimbilia maeneo mengine na wakasaidiwa na waabudu wenzao huko.
Njaa hufuata vita, kwa kuwa mazao huharibiwa, akiba ya chakula huporwa, na ugavi huzuiliwa. Chakula kipatikanacho ni ghali. Katika Kisangani, mwanzoni mwa Mei 1997, kilogramu moja ya viazi iligharimu dola tatu, gharama ipitayo uwezo wa kifedha wa watu wengi. Watu walio wengi wangeweza kugharimikia mlo mmoja tu kwa siku. Bila shaka, maradhi hufuata upungufu wa chakula. Utapiamlo hudhoofisha uwezo wa mwili wa kupigana na malaria, maradhi ya kuhara, na matatizo ya tumbo. Hasa watoto huteseka na kufa.
Kukagua Uhitaji
Mashahidi wa Yehova katika Ulaya waliitikia tena huo uhitaji kwa uharaka. Kufikia Aprili 1997 kikoa cha kutoa msaada cha Mashahidi kilichotia ndani madaktari wawili wa kitiba kilikuwa kimekuja kwa ndege kikiwa na dawa na fedha. Katika Goma Mashahidi wenyeji tayari walikuwa wamepata halmashauri za kutoa msaada zikague hiyo hali ili msaada wa papo hapo uweze kutolewa. Hicho kikoa kililichunguza hilo jiji na maeneo yaliyolizunguka. Wajumbe walitumwa ili kupata ripoti kutoka sehemu za mbali zaidi. Habari ilipatikana pia kutoka Kisangani, umbali wa zaidi ya kilometa 1,000 magharibi mwa Goma. Ndugu wenyeji walisaidiwa kusimamia jitihada za kutoa msaada katika Goma, ambako Mashahidi 700 huishi.
Mmoja wa wazee Wakristo katika Goma alisema hivi: “Tulichochewa sana kuona ndugu zetu waliokuwa wamekuja kutoka mbali sana ili kutusaidia. Kabla hawajaja, tulisaidiana. Ndugu walilazimika kukimbia kutoka mashambani kwenda Goma. Baadhi yao walikuwa wamepoteza nyumba zao, na waliacha mashamba yao. Tuliwachukua nyumbani mwetu na kushiriki nao mavazi yetu na chakula kidogo tulichokuwa nacho. Yale ambayo tungeweza kufanya mahali hapa hayakuwa mengi. Baadhi yetu tulikuwa tukiugua kutokana na utapiamlo.
“Hata hivyo, ndugu kutoka Ulaya walileta fedha zilizotuwezesha kununua chakula, kilichokuwa adimu na ghali sana. Hicho chakula kilikuja wakati wa maana sana, kwa kuwa wengi hawakuwa na chakula chochote nyumbani mwao. Tuligawanya hicho chakula kwa Mashahidi na wasio Mashahidi. Ikiwa huo msaada haukuja wakati ambapo ulikuja, wengi zaidi wangalikufa, hasa watoto. Yehova aliwaokoa watu wake. Wasio Mashahidi walivutiwa sana. Wengi wao walieleza juu ya muungano na upendo wetu. Baadhi yao walikiri kwamba dini yetu ndiyo ya kweli.”
Ingawa chakula kilinunuliwa mahali hapo na dawa zilitumiwa, mengi zaidi yalihitajiwa. Kulikuwa na uhitaji wa mavazi na mablanketi, na vilevile ugavi mkubwa zaidi wa chakula na dawa. Usaidizi ulihitajiwa pia ili kujenga upya nyumba zilizokuwa zimeharibiwa.
Watu Watoa kwa Ukarimu
Ndugu katika Ulaya walikuwa na hamu tena ya kusaidia. Ofisi ya Mashahidi wa Yehova katika Louviers, Ufaransa, ilitoa mwito huo katika makutaniko huko Rhône Valley, na pia katika Normandy, na sehemu za eneo la Paris. Hapo kanuni nyingine ya Kimaandiko ilitumika: “Yeye apandaye kwa uhaba atavuna pia kwa uhaba; na yeye apandaye kwa wingi atavuna pia kwa wingi. Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.”—2 Wakorintho 9:6, 7.
Maelfu ya watu walichukua kwa shangwe hiyo fursa ya kutoa. Masanduku na mifuko ya nguo, viatu, na vitu vingine vilimiminika kwenye Majumba ya Ufalme kisha vikasafirishwa hadi ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa. Huko wajitoleaji 400 walikuwa tayari kushiriki katika hatua iliyofuata ya kampeni ya “Help Zaire” (“Isaidie Zaire”). Bidhaa zilizochangwa zilipomiminika, wajitoleaji hao walitenganisha, kukunja, na kupakia hayo mavazi katika masanduku yaliyorundikwa thelathini-thelathini katika bao la kubebea mizigo. Watoto walikuwa wamefikiria ndugu na dada zao wachanga katika Afrika na walikuwa wamepeleka vichezeo—vigari vyenye kumetameta, pia, wanasesere, na wanasesere wa dubu. Hivyo vilipakiwa pamoja na mahitaji ya lazima ya maisha. Kwa ujumla, masanduku tisa ya meta 12 yalijazwa na kupelekwa Kongo.
Ni msaada kiasi gani ambao umepelekwa Afrika ya Kati kwa msaada wa maelfu ya Mashahidi katika Ubelgiji, Ufaransa, na Uswisi? Kufikia Juni 1997 jumla ya kiasi ilikuwa kilogramu 500 za dawa, tani 10 za biskuti zenye kiwango cha juu cha protini, tani 20 za vyakula vingine, tani 90 za mavazi, jozi 18,500 za viatu, na mablanketi 1,000. Fasihi za Biblia pia zilipelekwa huko kwa ndege. Yote hayo yalithaminiwa sana, yakiwafariji wakimbizi na kuwasaidia ili wavumilie majaribu yao. Gharama ya ugavi ilijumlika kuwa karibu dola 1,000,000 za Marekani. Michango hiyo ilikuwa uthibitisho wenye nguvu wa udugu na upendo miongoni mwa wamtumikiao Yehova.
Ugawanyaji Katika Kongo
Bidhaa zilipoanza kufika Kongo, ndugu wawili na dada mmoja walikuja kutoka Ufaransa ili kufanya kazi na halmashauri za kutoa msaada za huko. Kuhusu shukrani zilizoonyeshwa na Mashahidi wa Kongo, Joseline alisema hivi: “Tulipokea barua nyingi za kuonyesha uthamini. Dada mmoja maskini alinipa kipambo cha malakiti. Wengine walitupatia picha zao wenyewe. Tulipokuwa tukiondoka, dada walinibusu, kunikumbatia, na kutoa machozi. Nilitoa machozi pia. Wengi walitoa maelezo kama vile, ‘Yehova ni mwema. Yehova hutufikiria.’ Kwa hiyo wao watambua kwamba Mungu astahili kusifiwa kwa ajili ya utoaji huo. Tulipokuwa tukigawanya chakula, ndugu na dada walimsifu Yehova kwa nyimbo za Ufalme. Lilikuwa jambo lenye kutia huruma sana.”
Daktari wa kitiba aitwaye Loic alikuwa mshiriki wa kikoa hicho. Wengi walimiminika ndani ya Jumba la Ufalme na kungojea kwa subira zamu yao ya kupata msaada wake. Akitaka kufanya jambo fulani pia, dada mmoja Mkongo alitayarisha na kuchanga maandazi 40 kwa ajili ya wale waliokuwa wakingojea kumwona daktari. Kwa kuwa watu wapatao 80 walikuwa wakingojea, kila mmoja wao alipokea andazi nusu.
Msaada kwa Wasio Mashahidi
Msaada huo wa huruma haukupewa Mashahidi wa Yehova pekee. Wengine pia walinufaika, kama vile wengi walivyonufaika mwaka wa 1994. Hilo lapatana na andiko la Wagalatia 6:10, ambalo lataarifu hivi: “Basi, kwa kweli maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo, acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”
Mashahidi waligawa dawa na mavazi kwenye shule kadhaa za msingi na makao ya watoto yatima karibu na Goma. Hayo makao ya watoto yatima ni nyumba ya watoto 85. Katika safari ya mapema zaidi ya kuchunguza hali, kikoa cha kutoa msaada kilizuru hayo makao ya watoto yatima na kuahidi kuwaletea ugavi wa masanduku 50 ya biskuti zenye kiwango cha juu cha protini, masanduku ya mavazi, mablanketi 100, dawa, na vichezeo. Hao watoto walipanga laini katika ua na kuwaimbia hao wageni. Kisha wakatoa ombi la pekee—je, wangeweza kuwa na mpira hivi kwamba wangeweza kucheza soka?
Majuma kadhaa baadaye hicho kikoa cha kutoa msaada kilitimiza ahadi zao za kuleta ugavi. Akiwa amevutiwa na ukarimu na yale aliyokuwa amesoma katika fasihi za Biblia alizokuwa amepewa, mkurugenzi wa hayo makao ya watoto yatima alisema kwamba alikuwa akielekea kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Na je, hao watoto walipewa mpira? “La,” akajibu Claude, msimamizi wa kikoa cha kutoa msaada kutoka Ufaransa. “Tuliwapa mipira miwili.”
Kambi za Wakimbizi
Msaada haukutolewa Kongo tu. Maelfu ya wakimbizi walikuwa wamekimbia kutoka katika kanda ya vita kwenda nchi jirani ambako kambi tatu za wakimbizi zilikuwa zimejengwa haraka-haraka. Mashahidi walisafiri kwenda huko, pia, ili kuona mambo ambayo yangeweza kufanywa. Ripoti hii ilipotayarishwa, hizo kambi zilikuwa kimbilio la wakimbizi 211,000, wengi wao kutoka Kongo. Wakimbizi wapatao 800 walikuwa Mashahidi na watoto wao na watu mmoja-mmoja wenye kupendezwa na habari njema ya Ufalme. Tatizo la papo hapo katika hizo kambi lilikuwa ukosefu wa chakula. Kwenye kambi moja, kulikuwa na chakula cha kutosha siku tatu tu, nacho kilitia ndani maharagwe yaliyokuwa yamekaa kwa miaka mitatu.
Hata hivyo, hao Mashahidi walikuwa na furaha. Ingawa walikuwa na fasihi chache za Biblia, waliongoza mikutano iliyofanyika nje kwa ukawaida ili kujijenga kiroho. Pia walikuwa wenye shughuli wakihubiria wengine kambini habari njema ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14; Waebrania 10:24, 25.
Kikoa cha uchunguzi cha Mashahidi kilitia ndani daktari mmoja wa kitiba. Ingawa wenye mamlaka walikiruhusu kikoa hicho kitumie siku chache tu kwenye kila kambi, waliwasiliana kitiba. Waliwaachia wazee Wakristo dawa na fedha. Hivyo, ndugu waliweza kubaki hai. Pia walitumaini kwamba Mashahidi katika kambi mbalimbali wangeweza kurudi upesi katika nchi yao ya nyumbani.
Vipi juu ya wakati ujao? Yesu Kristo alitabiri kwamba siku yetu ingekuwa siku ya msukosuko, wakati uliotiwa alama na vita na upungufu wa chakula. (Mathayo 24:7) Mashahidi wa Yehova wajua kwamba Ufalme wa Mungu pekee ndio utakomesha kuteseka kulioko duniani. Chini ya utawala wake, makao yetu ya kidunia yatakuwa paradiso ya amani, wingi wa chakula, na furaha idumuyo milele kwa ajili ya wanadamu watiifu. (Zaburi 72:1, 3, 16) Kwa wakati uliopo, Mashahidi watatangaza habari njema ya Ufalme huo wa kimbingu na pia wataendelea kuwasaidia waabudu wenzao na watu wengine katika nyakati za uhitaji.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Tangu 1994, Mashahidi wa Yehova katika Ulaya pekee wamepeleka zaidi ya tani 190 za chakula, mavazi, dawa, na ugavi mwingine wa kitulizo kwenye eneo la Maziwa Makubwa ya Afrika
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Upendo wa Kikristo Wadhihirishwa
Miongoni mwa walioshiriki kwa hamu katika mradi wa “Help Zaire” katika Ufaransa alikuwa Ruth Danner. Akiwa mtoto, alitiwa gerezani katika kambi ya mateso ya Nazi kwa sababu ya imani yake ya Kikristo. Alieleza hivi: “Tulikuwa wenye furaha sana kufanya jambo fulani kwa ajili ya ndugu na dada zetu katika Afrika! Lakini kuna kitu kilichonifanya niwe na furaha maradufu. Mwaka wa 1945, tuliporudi nyumbani kutoka Ujerumani, hatukuwa na chochote. Hata mavazi tuliyovaa yalikuwa ya kuazimwa. Ingawa hivyo, upesi tulipokea msaada wa kimwili kutoka kwa ndugu zetu katika Amerika. Kwa hiyo jitihada ya kutoa msaada iliniwezesha kuonyesha fadhili tulizoonyeshwa muda mrefu uliopita. Ni pendeleo lililoje kuwa sehemu ya familia kubwa ya ndugu wanaodhihirisha upendo wa Kikristo!”—Yohana 13:34, 35.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Karibuni—paradiso ya kidunia yenye wingi wa chakula kwa ajili ya wote