Wenye Shukrani kwa Sababu ya Urithi Wenye Nguvu wa Kikristo
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA GWEN GOOCH
Shuleni niliimba wimbo wa kidini wenye maneno, ‘Yehova Mkuu aliyetawazwa katika utukufu wake.’ Mara nyingi nilijiuliza, ‘Yehova huyu ni nani?’
WAZAKUU wangu walikuwa wenye kumhofu Mungu. Mapema katika karne hii, walishirikiana na Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Baba yangu alifaulu katika biashara lakini hapo kwanza hakuwapitishia watoto wake watatu ule urithi wa Kikristo aliokuwa amepewa.
Baba alipompatia ndugu yangu, Douglas, dada yangu, Anne, na mimi vijitabu vyenye kichwa His Works na Who Is God? ndipo tu nilipopata kujua kwamba Yehova ni jina la Mungu wa kweli. (Zaburi 83:18) Nilisisimuka! Lakini ni nini kilichokuwa kimeamsha tena upendezi wa Baba?
Mwaka wa 1938, alipoona mataifa yakijitayarisha kwa ajili ya vita, Baba aling’amua kwamba ingehitaji mengi zaidi ya jitihada za kibinadamu ili kurekebisha matatizo ya ulimwengu. Nyanya alimpa kitabu Enemies, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Kwa kukisoma, alipata kujua kwamba adui halisi wa wanadamu ni Shetani Ibilisi na kwamba ni Ufalme wa Mungu pekee ndio ungeweza kuleta amani ya ulimwengu.a—Danieli 2:44; 2 Wakorintho 4:4.
Vita ilipokaribia, familia yetu ilianza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova katika Wood Green, London Kaskazini. Juni 1939 tulienda Alexandra Palace mahali palipokuwa karibu ili kusikiliza hotuba ya watu wote, “Serikali na Amani,” iliyotolewa na Joseph F. Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo. Hotuba ya Rutherford katika Madison Square Garden huko New York City ilisambazwa kwa redio hadi London na miji mikubwa mingine. Tuliweza kuisikia hotuba hiyo waziwazi hivi kwamba wakati ambapo kikundi cha wafanya-ghasia chenye makelele katika New York kilisababisha vurugu, niligeuka na kutazama nione ikiwa ilikuwa ikitukia katika ukumbi wetu!
Bidii ya Baba kwa Ajili ya Kweli ya Biblia
Baba alisisitiza kwamba kila Jumamosi jioni familia yetu yote ishiriki pamoja katika funzo la Biblia. Funzo letu lilikazia habari ya Biblia iliyokuwa katika Mnara wa Mlinzi lililoratibiwa kuzungumziwa siku iliyofuata. Nikitolea kielezi athari ambayo mafunzo hayo yalikuwa nayo, hadi leo lile simulizi juu ya Yoshua na mazingiwa ya jiji la Ai lililozungumziwa katika Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1939, la Kiingereza, lingali bayana akilini mwangu. Nilichochewa kwelikweli na simulizi hilo hivi kwamba nilichunguza marejezo yake yote katika Biblia yangu mwenyewe. Nilipata kuona utafiti huo kuwa wenye kuvutia sana—na bado nauona hivyo.
Kushiriki na wengine mambo tuliyokuwa tukijifunza kulikaza kikiki mafundisho ya Biblia moyoni mwangu. Siku moja Baba alinipa kinanda cha gramafoni pamoja na mahubiri ya Biblia yaliyorekodiwa, kijitabu tulichotumia kwa ajili ya funzo la Biblia, na maelezo ya mahali alipokaa mwanamke mmoja mzee-mzee. Kisha akaniomba nimtembelee.
“Nitasema nini, na nifanye nini?” nikauliza.
“Yote yako hapo,” Baba akajibu. “Cheza kinanda tu, usome maswali, mwombe mwenye nyumba asome majibu, kisha usome maandiko.”
Nilifanya alivyoniambia, na katika njia hiyo nikajifunza jinsi ya kuongoza funzo la Biblia. Kwa kutumia Maandiko hivyo katika huduma yangu, nikaja kuyaelewa vizuri zaidi.
Ugumu wa Miaka ya Vita
Vita ya Ulimwengu ya Pili ilizuka mwaka wa 1939, na mwaka uliofuata nilibatizwa katika kuonyesha wakfu wangu ili kumtumikia Yehova. Nilikuwa na umri wa miaka 13 tu. Kisha nikaamua kuwa painia, kama vile wahudumu wa wakati wote waitwavyo. Nilitoka shule mwaka wa 1941 na kwenye ule mkusanyiko wa Leicester nilijiunga na Douglas katika utendaji wa kuhubiri wakati wote.
Mwaka uliofuata, Baba alitiwa gerezani kwa sababu ya kukataa kwake shughuli za vita kwa kudhamiria. Sisi watoto tulikuja pamoja ili kumsaidia mama yetu, tukimsaidia atunze nyumba yetu katika wakati huo mgumu wa vita. Kisha, mara tu Baba alipoachiliwa kutoka gerezani, Douglas aliitwa ajiunge na utumishi wa kijeshi. Kichwa cha habari cha gazeti la mahali hapo kilisema, “Sababu Iliyomfanya Mwana Achague Kwenda Gerezani Kama Baba Yake.” Ushahidi mzuri ulitokea, kwa kuwa fursa ilikuwa imetolewa ya kueleza kwa nini Wakristo wa kweli hawashiriki kuua wanadamu wenzao.—Yohana 13:35; 1 Yohana 3:10-12.
Wakati wa miaka hiyo ya vita, Mashahidi wengi katika huduma ya wakati wote walizuru nyumbani kwetu kwa ukawaida, nayo mazungumzo yenye kujenga yaliyotegemea Biblia yalikuwa na uvutano wenye kudumu. Miongoni mwa ndugu Wakristo hao waaminifu mlikuwemo John Barr na Albert Schroeder, ambao sasa ni washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Wazazi wangu walikuwa wenye ukaribishaji-wageni kwelikweli, nao walitufundisha kuwa vivyo hivyo.—Waebrania 13:2.
Tayari Kutoa Jibu
Mara baada ya kuanza upainia, nilikutana na Hilda katika huduma ya mlango hadi mlango. Alijulisha wazi kwa hasira: “Mume wangu anawapigania watu kama nyinyi! Mbona hamfanyi lolote kuelekea jitihada za vita?”
“Wajua mengi kiasi gani kuhusu ninayofanya?” nikauliza. “Je, wajua ni kwa nini nimekuja kwako?”
“Basi,” akajibu, “afadhali uingie ndani unieleze.”
Niliweza kueleza kwamba tulikuwa tukiandaa tumaini la kweli kwa watu waliokuwa wakiteseka kwa sababu ya matendo yasiyopendeza ambayo yalikuwa yakifanywa—mara nyingi katika jina la Mungu. Hilda alisikiliza kwa uthamini, akawa mwanafunzi wangu wa kwanza wa Biblia aliye wa kawaida. Amekuwa Shahidi mtendaji sasa kwa miaka zaidi ya 55.
Mwishoni mwa vita, nilipokea mgawo mpya wa upainia katika Dorchester, mji ulio kusini-magharibi mwa Uingereza. Hiyo ndiyo iliyokuwa mara ya kwanza niliyopata kuishi nje ya nyumbani. Kutaniko letu dogo lilikutana kwenye mkahawa, jengo la karne ya 16 lililoitwa “The Old Tea House.” Tulihitaji kupanga upya meza na viti kwa ajili ya kila mmojawapo ya mikutano yetu. Palikuwa tofauti kabisa na Jumba la Ufalme nililokuwa nimezoea. Hata hivyo, chakula cha kiroho na ushirika wenye upendo uleule wa ndugu na dada Wakristo ulikuwapo.
Wakati uleule wazazi wangu walihamia Tunbridge Wells, kusini mwa London. Nilirudi nyumbani ili Baba, Anne, na mimi tuweze kupainia pamoja. Upesi kutaniko letu lilikua kutoka Mashahidi 12 hadi 70, kwa hiyo familia yetu ikaombwa kuhamia Brighton katika pwani ya kusini, mahali ambapo uhitaji wa wapiga-mbiu wa Ufalme ulikuwa mkubwa zaidi. Wengi walijiunga kwa bidii katika kuhubiri na familia yetu ya mapainia, nasi tuliona Yehova akibariki sana kazi yetu. Upesi hilo kutaniko moja likawa makutaniko matatu!
Mwaliko Usiotarajiwa
Katika kiangazi cha mwaka wa 1950, familia yetu ilikuwa miongoni mwa wajumbe 850 kutoka Uingereza waliohudhuria Ongezeko la Theokrasi Kusanyiko la Kimataifa katika Yankee Stadium ya New York City. Mapainia wengi ambao wangekuja katika mkusanyiko huo kutoka ng’ambo walipelekewa fomu za maombi ya kuhudhuria Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, iliyokuwa karibu na South Lansing, New York. Douglas, Anne, na mimi tulikuwa miongoni mwao! Baada ya kutumbukiza ombi langu lililojazwa katika sanduku la barua, nakumbuka nikifikiri, ‘Sasa kwa kweli nimefanya jambo fulani! Maisha yangu yataelekea wapi?’ Lakini azimio langu lilikuwa: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isaya 6:8) Nilisisimuka nilipopokea mwaliko wa kubaki baada ya huo mkusanyiko ili kuhudhuria darasa la 16 la Gileadi, pamoja na Douglas na Anne. Sisi sote tulijua kwamba tungeweza kutumwa tukiwa wamishonari sehemu yoyote ulimwenguni.
Baada ya kuonea shangwe huo mkusanyiko pamoja tukiwa familia, wakati ulifika wazazi wetu warudi Uingereza—peke yao. Sisi watoto watatu tuliwapungia mikono tukiwaaga walipokuwa wakisafiri kurudi nyumbani kwa meli iitwayo Mauritania. Huko kulikuwa kuachana kwenye kuchochea hisia kama nini!
Migawo ya Mishonari
Darasa la 16 la Gileadi lilifanyizwa na wanafunzi 120 kutoka sehemu zote za ulimwengu, kutia na wengine waliokuwa wameteseka katika kambi za mateso za Nazi. Kwa kuwa darasa letu lilifundishwa Kihispania, tulitarajia kupewa mgawo wa kwenda baadhi ya nchi zenye watu wanaozungumza Kihispania katika Amerika Kusini. Wazia mshangao wetu siku ya kuhitimu tulipopata kujua kwamba Douglas alipewa mgawo wa kwenda Japani na Anne na mimi kwenda Siria. Kwa hiyo sisi wasichana tulilazimika kujifunza Kiarabu, na ndivyo ilivyokuwa hata wakati ambapo mgawo wetu ulibadilishwa kuwa Lebanoni. Tulipokuwa tukingojea viza zetu, George Shakashiri, mpanga-chapa kamili wa Mnara wa Mlinzi la Kiarabu wa Watch Tower Society, alitufundisha Kiarabu mara mbili kwa juma.
Ilisisimua kama nini kwenda katika nchi ya Biblia tuliyokuwa tumejifunza juu yake darasani! Keith na Joyce Chew, Edna Stackhouse, Olive Turner, Doreen Warburton, na Doris Wood waliandamana nasi kwenda huko. Tulipata kuwa familia ya mishonari yenye furaha kama nini! Shahidi mwenyeji alizuru makao yetu ya mishonari ili kutusaidia zaidi katika lugha. Wakati wa kipindi cha mafundisho yetu ya kila siku, tulijizoeza utoaji mfupi, ambao baada yake tulienda nje na kuutumia katika kazi yetu ya kuhubiri.
Tulitumia miaka yetu kadhaa ya kwanza tukiwa Tripoli, ambapo kulikuwa na kutaniko tayari. Joyce, Edna, Olive, Doreen, Doris, Anne, na mimi tuliwasaidia wake na binti za Mashahidi wenyeji kushiriki katika mikutano na pia katika huduma ya waziwazi. Kufikia wakati huo, ndugu na dada zetu Wakristo, wakifuata desturi za huko, hawakuketi pamoja mikutanoni, nao dada hao Wakristo walishiriki katika huduma ya kutoka nyumba hadi nyumba mara chache sana. Tulihitaji usaidizi wao wa lugha katika kuhubiri kwetu waziwazi, nasi tuliwatia moyo kushiriki kazi hiyo wao wenyewe.
Kisha Anne nami tulipewa mgawo wa kusaidia kikundi kidogo cha Mashahidi katika jiji la kale la Sidoni. Muda mfupi baadaye, tuliombwa kurudi kwenye jiji kuu, Beirut. Mbegu za kweli ya Biblia zilikuwa zimepandwa miongoni mwa jumuiya ya watu wenye kuzungumza Kiarmenia huko, kwa hiyo tulijifunza lugha hiyo ili kuwasaidia.
Mabadiliko ya Migawo
Nilikuwa nimekutana na Wilfred Gooch kabla ya kuondoka Uingereza. Alikuwa ndugu mwenye bidii, mwenye kujali, aliyekuwa ametumikia katika Betheli ya London. Wilf alikuwa mshiriki wa darasa la 15 la Gileadi, lililohitimu wakati wa ule mkusanyiko wa Yankee Stadium wa mwaka wa 1950. Mgawo wake wa mishonari ulikuwa ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Nigeria, nasi tuliandikiana barua kwa wakati fulani. Mwaka wa 1955 sote wawili tulihudhuria ule mkusanyiko “Ufalme Mshindi” katika London, na punde baadaye tukaanza kuchumbiana. Mwaka uliofuata, tulioana huko Ghana, nami nikajiunga na Wilf katika mgawo wake wa mishonari huko Lagos, Nigeria.
Baada ya kumwacha Anne huko Lebanoni, aliolewa na ndugu mzuri Mkristo aliyekuwa amejifunza kweli ya Biblia katika Yerusalemu. Wazazi wangu hawakuweza kuhudhuria arusi zetu, kwa kuwa Douglas, Anne, na mimi tulifunga ndoa katika sehemu tofauti-tofauti za ulimwengu. Hata hivyo, waliridhika kujua kwamba sisi sote tulikuwa tukimtumikia Mungu wetu, Yehova, kwa furaha.
Kazi Katika Nigeria
Kwenye ofisi ya tawi ya Lagos, nilipewa mgawo wa kusafisha vyumba vya washiriki wanane wa familia yetu ya tawi na pia kutayarisha milo yao na kufua mavazi yao. Kwangu ilionekana kana kwamba sikuwa nimepata mume tu bali pia nilipata familia papohapo!
Wilf nami tulijifunza utoaji mfupi mbalimbali wa Biblia katika Kiyoruba, nasi tulithawabishwa kwa sababu ya jitihada zetu. Mwanafunzi mchanga tuliyemfikia sasa ana mwana na binti ambao watumikia katika familia kubwa ya Betheli ya Nigeria ya washiriki wapatao 400.
Mwaka wa 1963, Wilf alipokea mwaliko wa kuhudhuria mtaala wa miezi kumi wa mafundisho ya pekee katika Brooklyn, New York. Baada ya kumaliza, bila kutarajia alipewa mgawo wa kurudi Uingereza. Nilikuwa nimebaki Nigeria, nikapewa taarifa ya siku 14 nikutane na Wilf huko London. Niliondoka nikiwa na shaka, kwa sababu Nigeria kulikuwa kumekuwa mgawo wa kufurahisha. Baada ya kutumikia miaka 14 ng’ambo, ilichukua muda kuzoea maisha katika Uingereza tena. Hata hivyo, tulikuwa wenye shukrani kwa sababu ya kuwa karibu kwa mara nyingine tena na wazazi wetu waliokuwa wakizeeka na kuweza kusaidia kuwatunza.
Twategemezwa na Tumaini Letu
Tangu mwaka wa 1980, nilipendelewa kuandamana na Wilf alipokuwa akisafiri kwenda nchi nyingi akiwa mwangalizi wa kanda ya dunia. Hasa nilitazamia kwa hamu ziara zetu za kurudi Nigeria. Baadaye tulienda pia Skandinevia, West Indies, na Mashariki ya Kati—kutia na Lebanoni. Ulikuwa msisimuko wa pekee kujikumbusha mambo yenye kufurahisha na kuona wale niliokuwa nimewajua wakiwa matineja wachanga ambao walikuwa wakitumikia wakiwa wazee Wakristo.
Kwa kuhuzunisha, mume wangu mpendwa alikufa masika ya mwaka wa 1992. Alikuwa na umri wa miaka 69 tu. Lilikuwa pigo kali hasa kwa kuwa lilitukia ghafula. Baada ya miaka 35 ya ndoa, imechukua muda kuzoea. Lakini nimepokea msaada na upendo mwingi kutoka kwa familia yangu ya Kikristo ya ulimwenguni pote. Nimekuwa na mambo yaliyoonwa mengi yenye kufurahisha ya kufikiria.
Wazazi wangu wote wawili waliweka kielelezo bora cha uaminifu-maadili wa Kikristo. Mama alikufa mwaka wa 1981 na Baba mwaka wa 1986. Douglas na Anne waendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Douglas na mke wake, Kam, wamerudi London, ambako wamebaki baada ya kumtunza Baba. Anne na familia yake wako Marekani. Sisi sote twathamini sana tumaini na urithi wetu wenye kupewa na Mungu. Twaendelea kuonyesha “mtazamo wa kungoja,” tukitazamia kwa hamu wakati ambapo waishio, pamoja na wapendwa wao waliofufuliwa, watatumikia milele pamoja wakiwa washiriki wa familia ya kidunia ya Yehova.—Maombolezo 3:24, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Masimulizi ya maisha ya baba yangu, Ernest Beavor, yalikuwako katika Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1980, (la Kiingereza).
[Picha katika ukurasa wa 23]
Kisaa kuanzia upande wa juu wa kushoto:
Gwen akiwa na umri wa miaka 13 akifanya onyesho la funzo la kigezo kwenye Jumba la Ufalme la Enfield
Familia ya mishonari katika Tripoli, Lebanoni, mwaka wa 1951
Gwen na mumewe aliyekufa, Wilf