Kuishi Kulingana na Wakfu wa Kikristo Katika Uhuru
“Iliko roho ya Yehova, kuna uhuru.”—2 WAKORINTHO 3:17.
1. Mashahidi wa Yehova wamejiweka wakfu kwa nani, na kwa nini wao hutumia wakala za kisheria?
MASHAHIDI WA YEHOVA huamini kwamba dini yao itadumu milele. Kwa hiyo wao hutazamia kumtumikia Mungu “kwa roho na kweli” kwa umilele wote. (Yohana 4:23, 24) Wakiwa viumbe hai walio huru kuchagua, Wakristo hao wamejitoa wakfu kabisa kwa Yehova Mungu nao wameazimia kuishi kulingana na wakfu huo. Kwa sababu hiyo, wao hutegemea Neno la Mungu na roho takatifu yake. Waendeleapo kufuatia kwa moyo wote mwendo wao wa wakfu wa Kikristo katika uhuru wenye kupewa na Mungu, hao Mashahidi hustahi istahilivyo fungu la “mamlaka zilizo kubwa” za kiserikali na kutumia ifaavyo njia na maandalizi ya kisheria. (Waroma 13:1; Yakobo 1:25) Kwa mfano, Mashahidi hutumia Watch Tower Society kuwa chombo cha kisheria—mojawapo ya vyombo vingi katika nchi mbalimbali—ili kuwawezesha kutimiza kazi yao ya kuwasaidia wanadamu wenzao, hasa katika njia za kiroho. Lakini hao Mashahidi wako wakfu kwa Mungu, wala si kwa wakala wowote wa kisheria, nao wakfu wao kwa Yehova utadumu milele.
2. Kwa nini Watch Tower Society na wakala kama hizo za kisheria huthaminiwa sana na Mashahidi wa Yehova?
2 Wakiwa watumishi walio wakfu kwa Mungu, Mashahidi wa Yehova wanawajibika kufuata maagizo ya Yesu ya “[kufanya] wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha.” (Mathayo 28:19, 20) Kazi hii itaendelea hadi mwisho wa mfumo wa mambo, kwa kuwa Yesu alisema hivi pia: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:3, 14) Kila mwaka, vifaa vya uchapaji vya Watch Tower Society na mashirika ya kisheria kama hilo huwaandalia Mashahidi wa Yehova mamilioni ya Biblia, vitabu, broshua, na magazeti ya kutumia katika utendaji wao wa kuhubiri wa ulimwenguni pote. Kwa hiyo vyombo hivyo vya kisheria ni vyenye thamani kubwa katika kuwasaidia watumishi wa Mungu walio wakfu waishi kulingana na wakfu wao kwake.
3. Hapo awali Mashahidi wa Yehova walitumia neno “Sosaiti” katika maana gani?
3 Huenda mtu fulani akabisha kwamba jinsi Mashahidi wazungumzavyo juu ya Watch Tower Society—au mara nyingi zaidi “Sosaiti”—huonyesha kwamba wao huiona kuwa zaidi ya chombo cha kisheria tu. Je, hawaioni kuwa mamlaka ya mwisho juu ya mambo ya ibada? Kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu chaelewesha hoja hiyo kwa kufafanua hivi: “Mnara wa Mlinzi [la Juni 1, 1938 (la Kiingereza)] lirejezeapo “Sosaiti,” hilo halimaanishi, chombo cha kisheria tu, bali kikundi cha Wakristo watiwa-mafuta kilichosimamisha chombo hicho cha kisheria na ambacho hukitumia.”a Hivyo neno hilo lilimaanisha “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Mashahidi walitumia neno “Sosaiti” katika maana hiyo kwa ujumla. Bila shaka shirika la kisheria na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” si maneno yanayotumiwa kwa kubadilishana. Waelekezi wa Watch Tower Society hupigiwa kura, ilhali Mashahidi wanaofanyiza “mtumwa mwaminifu” hutiwa mafuta na roho takatifu ya Yehova.
4. (a) Mashahidi wengi hujielezaje ili kuepuka kutoelewana? (b) Kwa nini tuwe wenye usawaziko kwa habari ya istilahi?
4 Ili kuepuka kutoelewana, Mashahidi wa Yehova hujaribu kuwa waangalifu juu ya jinsi wajielezavyo. Badala ya kusema, “Sosaiti hufundisha,” Mashahidi wengi hupendelea semi kama, “Biblia husema” au, “naelewa Biblia yafundisha.” Katika njia hiyo wao hukazia ule uamuzi wa kibinafsi ambao kila Shahidi amefanya katika kukubali mafundisho ya Biblia na pia kuepuka kutoa mawazo yasiyo ya kweli ya kwamba Mashahidi wamefungwa kwa njia fulani na amri za farakano fulani la kidini. Bila shaka, madokezo juu ya istilahi hayapaswi kamwe kuwa habari ya kubishaniwa. Kwa vyovyote, istilahi ni ya maana kwa kadiri tu izuiavyo kutoelewana. Usawaziko wa Kikristo wahitajiwa. Biblia hutuonya kwa upole “[tu]sipigane kuhusiana na maneno.” (2 Timotheo 2:14, 15) Maandiko pia hutaarifu kanuni hii: “Msipotamka usemi wenye kueleweka kwa urahisi kupitia hiyo lugha, linalosemwa litajulikanaje?”—1 Wakorintho 14:9.
Roho ya Mungu Hupunguza Uhitaji wa Sheria
5. Andiko la 1 Wakorintho 10:23 lapaswa kuelewekaje?
5 “Mambo yote yaruhusika kisheria; lakini si mambo yote yenye faida,” akaandika mtume Paulo. Aliongeza hivi: “Mambo yote yaruhusika kisheria; lakini si mambo yote yajengayo.” (1 Wakorintho 10:23) Kwa wazi Paulo hakumaanisha kwamba yaruhusika kisheria kufanya mambo ambayo Neno la Mungu hulaumu moja kwa moja. Kwa kulinganisha na sheria zipatazo 600 zilizopewa Israeli la kale, kuna amri chache za moja kwa moja zinazoongoza maisha ya Kikristo. Kwa sababu hiyo, mambo mengi huachiwa dhamiri ya mtu. Mtu ambaye amejiweka wakfu kwa Yehova huonea shangwe uhuru ambao hutokana na uongozi wa roho ya Mungu. Baada ya kuifanya kweli iwe yake mwenyewe, Mkristo hufuata dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia na hutegemea mwelekezo wa Mungu kupitia roho takatifu. Hilo humsaidia Mkristo aliye wakfu kuamua jambo ‘litakalojenga’ na litakalokuwa ‘lenye faida’ kwake na kwa wengine. Yeye hung’amua kwamba maamuzi afanyayo yataathiri uhusiano wake wa kibinafsi na Mungu, ambaye amejiweka wakfu kwake.
6. Kwenye mikutano ya Kikristo, twaweza kuonyeshaje kwamba tumeifanya kweli iwe yetu wenyewe?
6 Shahidi huonyesha kwamba ameifanya kweli kuwa yake mwenyewe kwa kutoa maelezo kwenye mikutano ya Kikristo. Mwanzoni, huenda akakariri mambo yataarifiwayo katika kichapo kinachosomwa. Hata hivyo, baada ya muda atafanya maendeleo kufikia hatua ya kueleza mafundisho ya Biblia katika maneno yake mwenyewe. Hivyo atoa uthibitisho wa kwamba anasitawisha uwezo wake wa kufikiri, si kurudia tu yale ambayo wengine wamesema. Kuunda mawazo katika maneno yake mwenyewe na kuyaeleza maneno sahihi ya kweli katika njia yenye kuhisiwa moyoni kutamletea furaha na kutaonyesha kwamba amesadikishwa akilini mwake mwenyewe.—Mhubiri 12:10; linganisha Waroma 14:5b.
7. Watumishi wa Yehova wameamua nini kwa uhuru?
7 Mashahidi wa Yehova huchochewa na upendo kwa Mungu na wanadamu wenzao. (Mathayo 22:36-40) Ni kweli kwamba, wamefungamanishwa pamoja kwa ukaribu na kile kifungo cha upendo kama cha Kristo wakiwa ushirika wa ndugu wa ulimwenguni pote. (Wakolosai 3:14; 1 Petro 5:9) Lakini akiwa kiumbe hai aliye huru kuchagua, kila mmoja ameamua kibinafsi kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu, kuendelea kutokuwemo kisiasa, kujiepusha na damu, kuepuka aina fulani ya vitumbuizo, na kuishi kulingana na viwango vya Biblia. Hayo si maamuzi walazimishwayo kufanya. Ni maamuzi yaliyo sehemu ya njia ya maisha ichaguliwayo na wawezao kuwa Mashahidi kabla hawajapata kuchukua hatua za wakfu wa Kikristo.
Je, Wanapaswa Kutoa Hesabu kwa Baraza Linaloongoza?
8. Ni swali gani ambalo lahitaji kueleweshwa wazi?
8 Biblia huonyesha wazi kwamba Wakristo wa kweli hawamtumikii Mungu kwa kushurutishwa. Yasema hivi: “Yehova ndiye Roho; na iliko roho ya Yehova, kuna uhuru.” (2 Wakorintho 3:17) Lakini jambo hilo la hakika laweza kupatanishwaje na lile wazo la “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” pamoja na Baraza Linaloongoza lake?—Mathayo 24:45-47.
9, 10. (a) Kanuni ya ukichwa hutumikaje katika kutaniko la Kikristo? (b) Kufuata kanuni ya ukichwa kulisababisha nini katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza?
9 Ili kujibu swali hilo, lazima tukumbuke ile kanuni ya Kimaandiko ya ukichwa. (1 Wakorintho 11:3) Kwenye Waefeso 5:21-24, Kristo atambulishwa kuwa “kichwa cha kutaniko,” mmoja ambaye liko “katika ujitiisho” kwake. Mashahidi wa Yehova huelewa kwamba mtumwa mwaminifu na mwenye busara hufanyizwa na ndugu wa kiroho wa Yesu. (Waebrania 2:10-13) Jamii hiyo ya mtumwa iliyo aminifu imewekwa rasmi ili iandalie watu wa Mungu ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao.’ Wakati huu wa mwisho, Kristo amemweka rasmi mtumwa huyo “juu ya mali zake zote.” Kwa hiyo wadhifa wake hustahili kustahiwa na yeyote yule adaiye kuwa Mkristo.
10 Kusudi la ukichwa ni kuhifadhi muungano na kuhakikisha kwamba “mambo yote [yanatukia] kwa adabu na kwa mpango.” (1 Wakorintho 14:40) Ili kutimiza hilo katika karne ya kwanza, Wakristo kadhaa watiwa-mafuta kutoka katika jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara walichaguliwa ili kuwakilisha kikundi chote kizima. Kama vile matukio yaliyofuata yalivyothibitisha, usimamizi wa baraza linaloongoza la karne ya kwanza ulikuwa na kibali na baraka ya Yehova. Wakristo wa karne ya kwanza walikubali mpango huo kwa mteremo. Ndiyo, kwa hakika waliyakaribisha na kushukuru kwa sababu ya matokeo yake mazuri.—Matendo 15:1-32.
11. Baraza Linaloongoza la leo lapasa kuonwaje?
11 Thamani ya mpango wa namna hiyo ingalipo leo. Kwa sasa, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lafanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta kumi, wote wakiwa na miongo kadhaa ya uzoefu wa Kikristo. Wao hutoa mwelekezo wa kiroho kwa Mashahidi wa Yehova, kama vile baraza linaloongoza la karne ya kwanza lilivyofanya. (Matendo 16:4) Kama vile Wakristo wa mapema, Mashahidi huwategemea kwa mteremo ndugu wakomavu wa Baraza Linaloongoza kwa ajili ya mwelekezo na mwongozo wenye kutegemea Biblia katika mambo ya ibada. Ingawa washiriki wa Baraza Linaloongoza ni watumwa wa Yehova na wa Kristo, kama walivyo Wakristo wenzao, Biblia hutuagiza hivi: “Iweni watiifu kwa wale ambao wanaongoza miongoni mwenu na kuwa wenye kunyenyekea, kwa maana wao wanafuliza kulinda juu ya nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wapate kufanya hili kwa shangwe na si kwa kutweta, kwa maana hili lingekuwa lenye hasara kwenu.”—Waebrania 13:17.
12. Kila Mkristo mmoja-mmoja apaswa kutoa hesabu kwa nani?
12 Je, wadhifa wa uangalizi ambao Maandiko hugawia Baraza Linaloongoza humaanisha kwamba kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova lazima atoe hesabu kwalo juu ya kazi zake? Sivyo kulingana na maneno ya Paulo kwa Wakristo katika Roma: “Lakini kwa nini wewe wahukumu ndugu yako? Au kwa nini wewe pia wadharau ndugu yako? Kwa maana sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu . . . Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Waroma 14:10-12.
13. Kwa nini Mashahidi wa Yehova huripoti utendaji wao wa kuhubiri?
13 Hata hivyo, je, si kweli kwamba Mashahidi mmoja-mmoja watarajiwa kuripoti utendaji wao wa kuhubiri? Ndiyo, lakini kusudi la kufanya hivyo lafafanuliwa waziwazi katika kitabu cha Mashahidi cha maagizo, kisemacho: “Wafuasi wa kwanza wa Yesu Kristo walipendezwa na ripoti za maendeleo katika kazi ya kuhubiri. (Marko 6:30) Wakati kazi ilipositawi, ripoti zenye takwimu ziliandikwa pamoja na masimulizi ya mambo yaliyoonwa yenye kutokeza juu ya wale walioshiriki kuhubiri habari njema. . . . (Matendo 2:5-11, 41, 47, NW; 6:7; 1:15; 4:4) . . . Lilikuwa jambo lenye kutia moyo kama nini kwa wafanya kazi hao Wakristo waaminifu kusikia ripoti za mambo yaliyokuwa yakitimizwa! . . . Hali moja na hiyo, tengenezo la kisasa la Yehova linajaribu kutunza maandishi halisi ya kazi inayofanywa kwa utimizo wa andiko la Mathayo 24:14, NW.”
14, 15. (a) 2 Wakorintho 1:24 hutumikaje kuhusu Baraza Linaloongoza? (b) Wakristo mmoja-mmoja wapaswa kufanya uamuzi wa kibinafsi kwa msingi gani, wakitambua jambo gani la hakika?
14 Baraza Linaloongoza ni uandalizi wenye upendo na kielelezo cha imani kistahilicho kuigwa. (Wafilipi 3:17; Waebrania 13:7) Kwa kushikamana kwao na kumfuata kwao Kristo akiwa kigezo, wao waweza kurudia maneno haya ya Paulo: “Si kwamba sisi ndio mabwana-wakubwa juu ya imani yenu, bali sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu, kwa maana ni kwa imani yenu kwamba nyinyi mnasimama.” (2 Wakorintho 1:24) Kwa kuchunguza kwa makini mielekeo, Baraza Linaloongoza huvuta uangalifu kwenye manufaa ya kutii shauri la Biblia, hutoa madokezo juu ya kutumia sheria na kanuni za Biblia, huonya dhidi ya hatari zilizofichika, na huwaandalia “wafanyakazi wenzi” kitia-moyo kihitajiwacho. Hivyo hutekeleza usimamizi-nyumba wake wa Kikristo, husaidia kudumisha shangwe yao, na huwajenga katika imani ili waweze kusimama imara.—1 Wakorintho 4:1, 2; Tito 1:7-9.
15 Shahidi akifanya uamuzi kwa kutegemea shauri la Biblia litolewalo na Baraza Linaloongoza, yeye hufanya hivyo kwa hiari yake mwenyewe kwa sababu kujifunza kwake mwenyewe Biblia kumemsadikisha kwamba hiyo ndiyo njia ifaayo. Kila Shahidi huathiriwa na Neno la Mungu mwenyewe ili atumie shauri timamu la Kimaandiko litolewalo na Baraza Linaloongoza, akitambua kabisa kwamba maamuzi afanyayo yataathiri uhusiano wake wa kibinafsi na Mungu, ambaye amejiweka wakfu kwake.—1 Wathesalonike 2:13.
Wanafunzi na Askari-Jeshi
16. Ingawa maamuzi kuhusu mwenendo ni jambo la kibinafsi, kwa nini baadhi ya Mashahidi wa Yehova hutengwa na ushirika?
16 Lakini ikiwa maamuzi juu ya mwenendo ni jambo la kibinafsi, kwa nini baadhi ya Mashahidi wa Yehova hutengwa na ushirika? Hakuna mtu ambaye huamua bila msingi maalumu kwamba kutenda dhambi fulani kwastahili kutengwa na ushirika. Badala ya hivyo, tendo hilo latakikana Kimaandiko wakati mshiriki wa kutaniko ashirikipo katika dhambi nzito bila kutubu, dhambi kama zile zinazoorodheshwa katika sura ya 5 ya Wakorintho wa Kwanza. Hivyo, ingawa huenda Mkristo akatengwa na ushirika kwa sababu ya kufanya uasherati, yeye hutengwa na ushirika iwapo tu mtu huyo akataa kukubali msaada wa Kikristo wa wachungaji wenye upendo. (1 Wakorintho 5:1-5, 9-13) Mashahidi wa Yehova hawako peke yao katika kufuata zoea hilo la Kikristo. Kichapo The Encyclopedia of Religion chataarifu hivi: “Jumuiya yoyote ile hudai haki ya kujilinda dhidi ya washiriki wasiojipatanisha ambao huenda wakatisha hali njema ya shirika. Katika mazingira ya kidini mara nyingi haki hiyo imeimarishwa na ile itikadi kwamba kikwazo [kutenga na ushirika] huathiri msimamo wa mtu mbele ya Mungu.”
17, 18. Kufaa kwa kutenga na ushirika kwaweza kutolewaje kielezi?
17 Mashahidi wa Yehova ni wanafunzi wa Biblia. (Yoshua 1:8; Zaburi 1:2; Matendo 17:11) Programu ya elimu ya Biblia iandaliwayo na Baraza Linaloongoza yaweza kulinganishwa na utaratibu wa masomo ya shule upangwao na baraza la elimu. Ingawa hilo baraza lenyewe silo chanzo cha habari ifundishwayo, hilo hupanga utaratibu wa masomo, huamua njia ya ufundishaji, nayo hutoa mielekezo ihitajiwayo. Yeyote akikataa waziwazi kuishi kulingana na matakwa ya hilo shirika na kuwatokezea wanafunzi wenzake magumu, au kuiletea shule aibu, aweza kufukuzwa. Wenye mamlaka shuleni wana haki ya kutenda kwa manufaa ya wanafunzi wote kwa ujumla.
18 Mbali na kuwa wanafunzi, Mashahidi wa Yehova ni askari-jeshi wa Yesu Kristo, walioagizwa “[wapigane] pigano bora la imani.” (1 Timotheo 6:12; 2 Timotheo 2:3) Kwa kawaida, mwenendo usiomstahili Mkristo wenye kuendelea waweza kutokeza kukataliwa na Mungu. Akiwa ameandaliwa uhuru wa kuchagua, askari-jeshi Mkristo aweza kuamua apendavyo, lakini lazima ahimili matokeo ya uamuzi wake. Paulo asababu hivi: “Hakuna mtu anayetumikia akiwa askari ajihusishaye mwenyewe katika shughuli za kibiashara za maisha, ili aweze kupata kibali cha yule aliyemwandika kuwa askari-jeshi. Zaidi ya hayo, ikiwa yeyote ashindana hata katika michezo, havikwi taji isipokuwa awe ameshindana kulingana na kanuni.” (2 Timotheo 2:4, 5) Wakristo wakomavu, kutia na wale wa Baraza Linaloongoza, hudumu kabisa chini ya Kiongozi wao, Yesu Kristo, wakishika “kanuni” ili waweze kushinda zawadi ya uhai udumuo milele.—Yohana 17:3; Ufunuo 2:10.
19. Baada ya kuchunguza mambo ya hakika juu ya wakfu wa Kikristo, twaweza kuwa na uhakika juu ya nini?
19 Je, mambo ya hakika hayaonyeshi wazi kwamba Mashahidi wa Yehova ni watumishi wa Mungu, wala si watumwa wa wanadamu? Wakiwa Wakristo walio wakfu wanaoonea shangwe uhuru ambao kwa ajili ya huo Kristo aliwaweka huru, wao huacha roho ya Mungu na Neno lake liongoze maisha zao huku wakimtumikia kwa muungano pamoja na ndugu zao katika kutaniko la Mungu. (Zaburi 133:1) Uthibitisho mbalimbali wa hilo wapaswa kufutilia mbali ukosefu wowote wa uhakika juu ya chanzo cha nguvu yao. Pamoja na mtunga-zaburi, wao waweza kuimba hivi: “BWANA ni nguvu zangu na ngao yangu. Moyo wangu umemtumaini, nami nimesaidiwa; basi, moyo wangu unashangilia, na kwa wimbo wangu nitamshukuru.”—Zaburi 28:7.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa mwaka wa 1993 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Ungejibuje?
◻ Watch Tower Society na wakala nyingine mbalimbali za kisheria husaidiaje Mashahidi wa Yehova?
◻ Wakristo hunufaikaje kutokana na fungu la Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova?
◻ Kwa nini watu wa Yehova huripoti utendaji wao wa kuhubiri?
◻ Kumtenga na ushirika Mkristo aliye wakfu kwafaa chini ya hali gani?
[Picha katika ukurasa wa 19]
Baraza linaloongoza la karne ya kwanza lilihakikisha kuwepo kwa muungano wa mafundisho
[Picha katika ukurasa wa 23]
Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wanafurahia uhuru ambao kwa ajili ya huo Kristo aliwaweka huru