“Yenye Nguvu na Yenye Kusadikisha”
“KUANZIA kesho nitaitumia katika kazi ya kuhubiri, kwa sababu hoja zake kwa kweli ni zenye nguvu na zenye kusadikisha,” akaandika mmoja wa Mashahidi wa Yehova kutoka Ufaransa. Shahidi kutoka Marekani aliandika hivi: “Niliisoma mara moja na natamani sana kuitumia katika huduma ya shambani, kwa vile sisi hukutana na watu wengi wenye ubaridi na wasioitumaini Biblia.” Hao walikuwa wakifafanua nini? Ile broshua ya kurasa 32 yenye kichwa Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyotolewa na Watch Tower Society kwenye “Imani Katika Neno la Mungu” Mikusanyiko ya Wilaya iliyofanywa katika 1997/1998.
Kichapo hiki kilitayarishwa kwa ajili ya wasomaji fulani mahususi—wale ambao huenda wakawa wameelimika lakini wajua machache sana juu ya Biblia. Wengi wa watu hao wana maoni dhahiri juu ya Biblia, ingawa wao hawajaisoma kamwe kibinafsi. Kusudi la hiyo broshua ni kumsadikisha msomaji kwamba, Biblia yastahili angalau kuchunguzwa. Hiyo broshua haimlazimishi msomaji kukubali maoni ya kwamba Biblia imepuliziwa na Mungu. Badala yake, yaruhusu mambo ya hakika yajisemee. Maneno yake si makuu bali ni ya wazi na ya moja kwa moja.
Kama vile maelezo yaliyo juu yaonyeshavyo, wale waliokuwapo kwenye mikusanyiko walikuwa na hamu ya kuitumia broshua hiyo katika huduma yao ya shambani. Kwa kielelezo, katika Ufaransa kampeni ya pekee ilipangwa kufanywa Agosti 23 na 24 wakati ambapo mamia ya maelfu ya wageni vijana kutoka ulimwengu pote walipokusanyika Paris kwa ajili ya Siku ya Ulimwengu ya Vijana. Mashahidi wapatao 2,500 (hasa wa umri wa kati ya miaka 16 hadi 30) waliangusha nakala 18,000 za hiyo broshua katika lugha ya Kifaransa, Kihispania, Kiingereza, Kiitalia, Kijerumani, na Kipoland.
Kwa vyovyote, acheni tuitumie broshua hiyo, Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, katika huduma yetu. Kichapo hicho na kithibitike kuwa chenye thamani katika kuwasadikisha watu wenye akili kwamba, wapaswa kujichunguzia Biblia.