Maisha Yangu Nikiwa Mkoma—Mwenye Shangwe na Baraka za Kiroho
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ISAIAH ADAGBONA
Nilikulia Akure, Nigeria. Familia yangu ililima viazi vikuu, ndizi, mihogo, na kakao. Baba yangu hakutaka niende shuleni. Aliniambia hivi: “Wewe ni mkulima. Hakuna yeyote atakayekwambia usome viazi vikuu.”
HATA hivyo, nilitaka kujifunza kusoma. Nyakati za jioni, nilisimama na kusikiliza kwenye dirisha la nyumba fulani ambapo watoto walikuwa wakifundishwa na mwalimu wa kibinafsi. Huo ulikuwa mwaka wa 1940 nilipokuwa na umri wa miaka 12. Baba ya hao watoto aliponiona, angenipazia sauti na kunifukuzia mbali. Lakini nilifuliza kurudi. Nyakati nyingine mwalimu hakuja, nami ningenyemelea kuingia ndani na kutazama vitabu vya hao watoto pamoja nao. Nyakati nyingine waliniazima vitabu vyao. Hivyo ndivyo nilivyojifunza kusoma.
Najiunga na Watu wa Mungu
Punde si punde nilipata Biblia, nikaisoma kwa ukawaida kabla ya kwenda kulala. Jioni moja nilisoma Mathayo sura ya 10, ionyeshayo kwamba wanafunzi wa Yesu wangechukiwa na kunyanyaswa na watu.
Nilikumbuka kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wamekuja nyumbani kwangu, wakatendewa vibaya. Nikaelewa kwamba huenda hao wakawa watu ambao Yesu alikuwa amesema juu yao. Pindi iliyofuata Mashahidi walipozuru, nilipata gazeti kutoka kwao. Nilipoanza kushirikiana nao, nikaanza kudhihakiwa. Lakini, kadiri watu walivyojaribu kunivunja moyo, ndivyo nilivyokuwa mwenye shangwe zaidi na kusadikishwa zaidi kwamba nilikuwa nimepata dini ya kweli.
Kilichonivutia kwelikweli juu ya Mashahidi kilikuwa kwamba, tofauti na vikundi vingine vya kidini katika eneo langu, hawakuchanganya ibada yao na desturi na mapokeo ya dini ya kipagani ya kienyeji. Kwa kielelezo, ingawa familia yangu ilienda kwenye kanisa Anglikana, baba yangu alikuwa na kihekalu cha Ogun, mungu wa Wayoruba.
Baada ya baba kufa, nilipaswa kurithi hicho kihekalu. Sikukitaka, kwa kuwa nilijua kwamba Biblia ililaumu ibada ya sanamu. Nilifanya maendeleo ya kiroho kwa msaada wa Yehova, na Desemba 1954, nikabatizwa.
Ukoma Washambulia
Mapema mwaka huo, nilitambua uvimbe na ukosefu wa hisia kwenye miguu yangu. Ikiwa ningekanyaga makaa yenye moto, hakukuwa na uchungu wowote. Baada ya muda, vidonda vyekundu-vyekundu vikatokea kwenye kipaji na midomo yangu. Wala mimi wala familia yangu hatukujua kilichokuwa kibaya; tulifikiri ulikuwa ukurutu. Niliwaendea wataalamu 12 wa mitishamba nikitafuta tiba. Hatimaye mmoja wao akatuambia kwamba ulikuwa ukoma.
Ulikuwa mshtuko kama nini! Nilikasirika na sikulala vema. Nilikuwa na majinamizi. Lakini ujuzi wangu juu ya kweli ya Biblia na kumtegemea Yehova kulinisaidia kutazamia wakati ujao nikiwa na uhakika.
Watu walimwambia mama yangu kwamba ikiwa ningemwendea mwaguzi ili kutoa dhabihu, ningepata nafuu. Nilikataa kwenda, nikijua kwamba tendo hilo lingemchukiza Yehova. Wakitambua kwamba nilikuwa nimeazimia kutomwendea mwaguzi, rafiki za mama yangu walidokeza kwamba achukue kola na kugusa kipaji changu nayo. Kisha angeweza kumpa mwaguzi hiyo kola ili huyo mwaguzi aitumie katika dhabihu kwa niaba yangu. Sikutaka kushiriki hata kidogo katika hilo nami nikamwambia hivyo. Hatimaye alijiuzulu kunihusisha katika dini ya kipagani.
Kufikia wakati nilipoenda hospitali, ukoma ulikuwa umeendelea sana. Nilikuwa na vidonda kotekote mwilini mwangu. Hospitalini, walinipa dawa, na ngozi yangu ikarudia kawaida yake hatua kwa hatua.
Walifikiri Nilikuwa Mfu
Lakini huo haukuwa mwisho wa matatizo yangu. Mguu wangu wa kuume uliambukizwa vibaya, na mwaka wa 1962 ilikuwa lazima ukatwe. Baada ya huo upasuaji, kulikuwa na magonjwa ya ziada. Madaktari hawakutarajia niishi. Mishonari mweupe alikuja kufanya sherehe ya mwisho ya ibada. Nilikuwa mdhaifu sana nisiweze kusema, lakini muuguzi fulani alimwambia kwamba mimi nilikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Huyo kasisi aliniambia hivi: “Je, wataka kubadilika na kuwa Mkatoliki ili uweze kwenda mbinguni?” Hilo lilinifanya nicheke kindani. Nilisali kwa Yehova anipe nguvu ya kujibu. Kwa jitihada nyingi nilifaulu kusema, “La!” Huyo kasisi akageuka na kwenda zake.
Hali yangu ilizidi kuwa mbaya hadi wafanyakazi wa hospitali wakafikiri nilikuwa mfu. Waliufunika uso wangu kwa shiti. Ingawa hivyo, hawakunipeleka katika chumba cha kuhifadhia maiti, kwa kuwa daktari au muuguzi alihitaji kuthibitisha kwamba nilikuwa mfu. Hakukuwa na daktari yeyote kwenye zamu, na wauguzi wote walikuwa wameenda kwenye karamu. Kwa hiyo waliniacha katika wadi usiku kucha. Daktari alipowazuru wagonjwa asubuhi iliyofuata, hakuna aliyekuja katika kitanda changu, kwa sababu bado nilikuwa nimefunikwa nikidhaniwa nimekufa. Hatimaye, mtu fulani aliona ile “maiti” chini ya shiti ikisonga!
Nilipata nafuu, na Desemba 1963 walinihamisha hadi Makao ya Hospitali ya Ukoma ya Abeokuta Nigeria yaliyoko kusini-magharibi. Nimeishi huko tangu wakati huo.
Kupingwa kwa Kuhubiri Kwangu
Kulikuwa na wakoma wapatao 400 katika hayo makao nilipofika, nami nilikuwa Shahidi pekee. Niliandikia Sosaiti, nao waliitikia haraka kwa kuelekeza kwamba Kutaniko la Akomoje liwasiliane nami. Kwa hiyo niliwasiliana na akina ndugu sikuzote.
Mara tu nilipofika katika hayo makao, nilianza kuhubiri. Pasta wa mahali hapo hakufurahia hilo, naye aliniripoti kwa ofisa wa usitawi aliyekuwa akisimamia hiyo kambi. Huyo ofisa wa usitawi alikuwa mwanamume mwenye umri mkubwa zaidi aliyetoka Ujerumani. Aliniambia kwamba sikuwa na haki ya kufundisha Biblia kwa sababu sikuwa na cheti chochote cha masomo ya kufanya hivyo; kwa kuwa sikuwa na sifa za kustahili, ningewafundisha watu isivyo sahihi. Ikiwa ningeendelea, ningeweza kufukuzwa kutoka katika hayo makao na kunyimwa matibabu. Hakuniruhusu nimjibu kwa kusema lolote.
Kisha akatoa mwelekezo kwamba yeyote asijifunze Biblia nami. Tokeo likawa kwamba, wale waliokuwa wameonyesha kupendezwa wakaacha kunijia.
Nilimtwika Yehova jambo hilo katika sala, nikimwomba hekima na mwelekezo. Jumapili iliyofuata, nilienda katika kanisa Baptisti kwenye hayo makao, ingawa sikushiriki katika ibada za kidini. Kulikuwa na kipindi wakati wa ibada ambapo waliokuwapo wangeweza kuuliza maswali. Niliinua mkono wangu na kuuliza hivi: “Ikiwa watu wote wazuri wanaenda mbinguni na watu wote wabaya wanaenda mahali pengine, kwa nini Isaya 45:18 husema kwamba Mungu aliifanya dunia ili ikaliwe?”
Kulikuwa na minong’ono mingi miongoni mwa kutaniko. Hatimaye, pasta mishonari akasema kwamba hatuwezi kuzijua njia za Mungu. Ndipo, nikajibu swali langu mwenyewe kwa kusoma maandiko yaonyeshayo kwamba 144,000 wataenda mbinguni, kwamba waovu wataangamia, na kwamba watu wenye haki wataishi duniani milele.—Zaburi 37:10, 11; Ufunuo 14:1, 4.
Kila mmoja alipiga makofi kwa kuthamini hilo jibu. Kisha huyo pasta akasema hivi: “Pigeni makofi mara ya pili kwa kuwa mtu huyu kwa kweli aijua Biblia.” Baada ya ibada, baadhi ya watu walinijia na kusema hivi: “Wajua mengi kuliko ajuayo pasta!”
Mkazo wa Kunifukuza Waendelea
Hilo lilikomesha sehemu kubwa ya mnyanyaso, na watu wakaanza kujiunga nami tena ili kujifunza Biblia. Hata hivyo, kulibaki wapinzani waliomkaza ofisa wa usitawi aniondolee mbali. Wapata mwezi mmoja baada ya ile ibada ya kanisa, aliniita na kusema hivi: “Mbona waendelea kuhubiri? Katika nchi yangu, watu hawawapendi Mashahidi wa Yehova, na ndivyo ilivyo hapa. Mbona wanisababishia taabu? Hujui kwamba naweza kukufukuza?”
Nilijibu: “Papa, nakustahi kwa sababu tatu. Kwanza, kwa sababu una umri mkubwa zaidi kuliko mimi, na Biblia husema twapaswa kustahi nywele zenye mvi. Sababu ya pili inifanyayo nikustahi ni kwamba uliacha nchi yako ukaja hapa kutusaidia. Sababu ya tatu ni kwamba u mwenye fadhili, mkarimu, na huwasaidia walio katika taabu. Lakini wafikiri una haki gani ya kunifukuza? Rais wa nchi hawafukuzi Mashahidi wa Yehova. Mtawala wa kidesturi wa eneo hili hatufukuzi. Hata ukinifukuza kutoka katika kambi hii, Yehova bado atanitunza.”
Sikuwa nimepata kuzungumza naye kwa njia ya moja kwa moja hivyo hapo awali, nami ningeweza kuona kwamba maneno yangu yalikuwa na uvutano. Alienda zake bila kusema neno. Baadaye, wakati ambapo mtu fulani alilalamika juu yangu, alijibu hivi kwa kutamauka: “Sitajihusisha tena katika tatizo hilo. Ikiwa una tatizo na kuhubiri kwake, zungumza naye!”
Darasa la Kujifunzia Kusoma na Kuandika
Kuhubiri kwangu kuliendelea kupingwa na wale waliohudhuria kanisa Baptisti kwenye hiyo kambi. Kisha nikapata wazo fulani. Nilimwendea ofisa wa usitawi na kumwomba kama ningeweza kuanzisha darasa la kujifunzia kusoma na kuandika. Alipouliza nilitaka kulipwa kiasi gani, nilisema ningefundisha bila malipo.
Waliandaa darasa, ubao, na chokaa, hivyo nikaanza kuwafundisha wakazi wenzangu kusoma. Tulikuwa na darasa kila siku. Dakika 30 za kwanza, nilikuwa nikifundisha kusoma, kisha nilikuwa nikisimulia au kueleza hadithi fulani kutoka katika Biblia. Baadaye, tulikuwa tukisoma simulizi hilo kutoka katika Biblia.
Mwanafunzi mmoja alikuwa mwanamke aliyeitwa Nimota. Alikuwa na upendezi wenye kina wa mambo ya kiroho naye aliuliza maswali ya kidini kanisani na msikitini. Hakujibiwa maswali yake huko, kwa hiyo alikuwa akinijia na kuniuliza. Hatimaye, aliweka maisha yake wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Mwaka wa 1966 tukaoana.
Walio wengi katika kutaniko letu leo walijifunza kusoma na kuandika katika darasa hilo. Sikuwa na hekima ya kudokeza darasa hilo. Bila shaka baraka ya Yehova ilikuwa dhahiri. Hakuna yeyote aliyejaribu kunizuia nisihubiri baada ya hilo.
Jumba la Ufalme Kambini
Kufikia wakati ambapo Nimota nami tulioana, wanne kati yetu tulikuwa tukikutana kwa ukawaida ili kujifunza Mnara wa Mlinzi pamoja. Kwa mwaka mmoja hivi, tulikutana chumbani ambamo vidonda vya ukoma vilikuwa vikioshwa. Kisha ofisa wa usitawi, ambaye kufikia sasa alikuwa amekuwa rafiki yangu, akaniambia hivi: “Si vizuri kumwabudu Mungu wenu katika chumba cha matibabu.”
Alisema kwamba tungeweza kukutana katika kibanda cha seremala ambacho hakikuwa kikitumika. Baada ya muda, kibanda hicho kilibadilishwa kuwa Jumba la Ufalme. Mwaka wa 1992, tukisaidiwa na ndugu wa mji huo, tulilimaliza. Kama uwezavyo kuona katika picha kwenye ukurasa wa 24, jumba letu ni jengo zuri—lililopigwa plasta na kupakwa rangi, lenye sakafu ya saruji na paa nzuri.
Kuwahubiria Wenye Ukoma
Kwa miaka 33 eneo langu limekuwa makao ya wenye ukoma. Kuwahubiria wakoma kulikuwaje? Hapa Afrika watu wengi huamini kwamba mambo yote hutoka kwa Mungu. Kwa hiyo washikwapo na ukoma, wao huamini kwamba Mungu anahusika kwa njia fulani. Baadhi yao hushuka moyo sana kwa sababu ya hali yao. Wengi wana hasira na husema: “Usizungumze nasi juu ya Mungu mwenye upendo na rehema. Ikiwa hilo lingalikuwa kweli, ugonjwa huu ungalitoweka!” Kisha sisi husoma na kusababu juu ya andiko la Yakobo 1:13, lisemalo hivi: ‘Mungu hamjaribu yeyote na mambo maovu.’ Halafu hueleza kwa nini Yehova huruhusu ugonjwa uwapate watu, na huonyesha ahadi yake ya dunia iliyo paradiso ambapo hakuna yeyote atakayekuwa mgonjwa.—Isaya 33:24.
Wengi wameitikia ifaavyo habari njema. Tangu nije katika kambi hii, Yehova amenitumia kusaidia watu zaidi ya 30 wafikie wakfu na ubatizo, wote wakiwa wakoma. Wengi wamerudi nyumbani kwao baada ya kuponywa, na wachache wamekufa. Sasa tuna wahubiri wa Ufalme 18, na watu wapatao 25 huhudhuria mikutano kwa ukawaida. Wawili kati yetu hutumika tukiwa wazee, na tuna mtumishi wa huduma mmoja na painia wa kawaida mmoja. Nina furaha kama nini kuona wengi sana hivyo wakimtumikia Yehova kwa uaminifu katika kambi hii! Nilipokuja hapa, nilihofu kwamba ningekuwa peke yangu, lakini Yehova amenibariki kwa njia ya pekee.
Shangwe ya Kuwatumikia Ndugu Zangu
Nilitumia madawa ya ukoma tangu 1960 hadi miaka mitano iliyopita. Sasa nimepona kabisa, kama walivyo wengine kutanikoni. Ukoma uliacha alama yake—nilipoteza sehemu ya chini ya mguu wangu, nami siwezi kunyoosha mikono yangu—lakini maradhi hayo yametoweka.
Kwa kuwa nimepona, wengine huuliza kwa nini siondoki kambini na kurudi nyumbani. Kuna sababu kadhaa kwa nini nakaa huku, lakini sababu kuu ni kwamba nataka kuendelea kuwasaidia ndugu huku. Shangwe ya kutunza kondoo wa Yehova hupita chochote ambacho familia yangu yaweza kunipa nikirudi nyumbani.
Ninashukuru kwelikweli kwamba nilimjua Yehova kabla ya kupata kujua kwamba nilikuwa na ukoma. La sivyo, huenda ningalijiua. Kumekuwa na magumu na matatizo mengi kwa miaka kadhaa, lakini si madawa yaliyonitegemeza—Yehova ndiye aliyenitegemeza. Nikumbukapo wakati uliopita, nina shangwe; na nifikiriapo wakati ujao chini ya Ufalme wa Mungu, ninakuwa na shangwe hata zaidi.
[Sanduku katika ukurasa wa 25]
Mambo ya Hakika Juu ya Ukoma
Huo Ni Nini?
Ukoma wa siku ya kisasa ni maradhi yasababishwayo na basila iliyotambuliwa mwaka wa 1873 na Armauer Hansen. Kwa kuitambua kazi yake, madaktari huuita ukoma kuwa maradhi ya Hansen pia.
Hiyo basila huharibu neva, mifupa, macho, na viungo fulani. Uwezo wa kuhisi hupotea, mara nyingi mikononi na miguuni. Yasiposhughulikiwa, maradhi hayo yaweza kusababisha kukatika-katika kwa uso na mikono na miguu. Huua mara chache sana.
Je, Kuna Tiba?
Watu wenye aina za ukoma zisizo mbaya sana hupona bila matibabu yoyote yale. Visa vilivyo vibaya zaidi vyaweza kutibiwa kwa madawa.
Dawa ya kwanza ya kuzuia ukoma, iliyotokezwa miaka ya 1950, ilifanya kazi polepole na ikazidi kuwa isiyo na matokeo kwa sababu basila ya ukoma ilisitawisha ukinzani dhidi yake. Dawa mpya zilitokezwa, na tangu mapema miaka ya 1980, Multi-Drug Therapy (MDT) yalipata kuwa matibabu yaliyotumiwa ulimwenguni kote. Matibabu hayo huchanganya matumizi ya dawa tatu—Dapsone, Rifampicin, na Clofazimine. Ingawa MDT huua hiyo basila, hairekebishi madhara yaliyofanywa tayari.
Matibabu ya MDT yana matokeo sana katika kuponya maradhi hayo. Kwa sababu hiyo, idadi ya watu wenye ukoma imepungua haraka sana kutoka milioni 12 katika mwaka wa 1985 hadi wapatao milioni 1.3 kufikia katikati ya mwaka wa 1996.
Huambukizwa Kadiri Gani?
Ukoma hauambukizwi sana; watu wengi wana mfumo wa kingamaradhi wenye nguvu za kutosha kuukabili. Kuambukizwa kutokeapo, kwa kawaida hutokea kwa watu ambao huishi karibu-karibu kwa muda mrefu na wale walio nao.
Madaktari hawana uhakika juu ya jinsi ambavyo hiyo basila huingia mwili wa kibinadamu, lakini wao hukisia kwamba hiyo huingia kupitia ngozi au mapua.
Matazamio ya Wakati Ujao
Kuna mradi wa “kuondosha [ukoma] ukiwa tatizo la afya ya watu wote” kufikia mwaka wa 2000. Hilo lamaanisha kwamba idadi ya ukoma katika nchi yoyote ile haitazidi mtu 1 katika watu 10,000. Chini ya Ufalme wa Mungu utaondolewa kabisa.—Isaya 33:24.
Vyanzo: Shirika la Afya Ulimwenguni; Muungano wa Kimataifa wa Mashirika ya Kupambana na Ukoma; na kichapo Manson’s Tropical Diseases, Chapa ya 1996.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
Je, Ukoma wa Leo Ni Sawa na Ule wa Nyakati za Biblia?
Vitabu vya mafundisho ya kitiba leo hufafanua ukoma katika maneno dhahiri; jina la kisayansi la kiini kihusikacho ni Mycobacterium leprae. Bila shaka, Biblia si kitabu cha kitiba. Neno la Kigiriki na la Kiebrania litafsiriwalo “ukoma” katika tafsiri nyingi za Biblia ni pana zaidi katika maana. Kwa kielelezo, ukoma wa Biblia ulitokeza dalili zilizoonekana katika mwanadamu na pia katika nguo na nyumba, jambo ambalo basila haifanyi.—Walawi 13:2, 47; 14:34.
Zaidi, dalili katika wanadamu ambazo hutambulisha ukoma leo hazifanani kabisa na ufafanuzi wa ukoma katika nyakati za Biblia. Wengine hudokeza kwamba huenda hilo likawa kwa sababu ya uhakika wa kwamba hali ya maradhi hubadilika kadiri wakati upitavyo. Wengine huamini kwamba ukoma urejezewao katika Biblia hufafanua idadi kubwa ya maradhi, ambayo huenda yakahusisha au yasihusishe maradhi yasababishwayo na M. leprae.
Kamusi Theological Dictionary of the New Testament yataarifu kwamba maneno ya Kigiriki na ya Kiebrania yatafsiriwayo kwa kawaida kuwa ukoma “hurejezea ugonjwa uleule, au kikundi kilekile cha magonjwa . . . Ikiwa ugonjwa huo ndio tuitao sasa ukoma ni jambo liwezalo kuzusha maswali. Lakini utambulisho dhahiri wa kitiba wa huo ugonjwa hauathiri kadirio letu juu ya masimulizi ya kuponya [wakoma kulikofanywa na Yesu na wanafunzi wake].”
[Picha katika ukurasa wa 24]
Kutaniko nje ya Jumba la Ufalme katika kambi ya wakoma
[Picha katika ukurasa wa 26]
Isaiah Adagbona na mke wake, Nimota