Wakati Ujao Wako Utakuwaje?
IKIWA Mungu Mweza Yote ni mwenye kujua yote, akijua yote yaliyopita, yaliyopo, na yajayo, je, mambo yote hayakusudiwi kutukia sawasawa kabisa na vile ambavyo Mungu ameyaona kimbele? Ikiwa Mungu ameona kimbele na kuagiza kimbele mwendo na mwisho wa kila binadamu, je, yaweza kusemwa kikweli kwamba tuna hiari ya kuchagua mwendo wa maisha yetu, wakati ujao wetu?
Maswali hayo yamejadiliwa kwa karne nyingi. Huo ubishi bado wagawanya dini zilizo kubwa. Je, uwezo wa Mungu wa kujua kimbele wakati ujao waweza kupatanishwa na hiari ya kibinadamu? Twapaswa kutafuta majibu wapi?
Mamilioni ya watu tufeni pote wangekubali kwamba Mungu amewasiliana na wanadamu kupitia Neno lake lililoandikwa kama lilivyotolewa kupitia wasemaji wake, manabii. Kwa mfano, Qurani hurejezea mafunuo haya kuwa yalitoka kwa Mungu: Taurāh (Torati, Sheria, au vitabu vitano vya Musa), Zabūr (Zaburi), na Injīl (Gospeli, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au “Agano Jipya”), na vilevile yale yaliyofunuliwa kwa manabii wa Israeli.
Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, twasoma hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.” (2 Timotheo 3:16) Kwa wazi, mwongozo au mnurusho wowote ambao sisi hupokea wapaswa kimsingi utoke kwa Mungu mwenyewe. Basi je, halingekuwa jambo la hekima kuchunguza maandishi ya manabii wa zamani wa Mungu? Hayo hufunua nini juu ya wakati ujao wetu?
Wakati Ujao Ulioandikwa Kimbele
Yeyote ambaye ameyasoma Maandiko Matakatifu ajua kwamba, kihalisi yana mamia ya unabii mbalimbali. Matukio ya kihistoria kama vile kuanguka kwa Babiloni, kujengwa upya kwa Yerusalemu (karne ya sita hadi ya tano K.W.K.), kuinuka na kuanguka kwa wafalme wa kale wa Umedi na Uajemi na wa Ugiriki, kulitabiriwa kinaganaga. (Isaya 13:17-19; 44:24–45:1; Danieli 8:1-7, 20-22) Kutimizwa kwa unabii huo mbalimbali ni mojawapo ya ithibati yenye nguvu zaidi kwamba, Maandiko Matakatifu kwa kweli ni Neno la Mungu, kwa maana Mungu peke yake ndiye aliye na uwezo wa kuona kimbele na kuamua yatakayotukia wakati ujao. Katika maana hiyo Maandiko Matakatifu kwa kweli yamerekodi wakati ujao ulioandikwa kimbele.
Mungu mwenyewe ajulisha wazi hivi: “Mimi ni Mungu, wala hapana mwingine; mimi ni Mungu, wala hapana aliye kama mimi; nitangazaye mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado; nikisema, Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote . . . naam, nimenena, nami nitatekeleza; nimekusudia, nami nitafanya.” (Isaya 46:9-11; 55:10, 11) Jina lenyewe ambalo kwalo Mungu alijitambulisha kwa manabii wa kale ni Yehova, ambalo kihalisi lamaanisha “Yeye Husababisha Iwe.”a (Mwanzo 12:7, 8; Kutoka 3:13-15; Zaburi 83:18) Mungu hujifunua mwenyewe kuwa Ndiye ambaye huwa Mtimizaji wa neno lake, Yule ambaye hutimiza makusudi yake.
Kwa hiyo, Mungu hutumia nguvu yake ya ujuzi wa kimbele katika kutimiza makusudi yake. Mara nyingi ameitumia ili kuwaonya waovu juu ya hukumu yake inayokuja na vilevile kutolea watumishi wake tumaini la wokovu. Lakini je, Mungu hutumia nguvu hiyo katika njia isiyo na mipaka? Je, kuna uthibitisho wowote katika Maandiko Matakatifu wa mambo ambayo Mungu amechagua kutoyajua kimbele?
Je, Mungu Hujua Kimbele Kila Kitu?
Majibizano yote ya kuunga mkono fundisho la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu, hutegemea ile dhana kwamba, kwa kuwa kwa wazi Mungu ana nguvu ya kujua kimbele na kuamua matukio ya wakati ujao, ni lazima ajue kila kitu, kutia na matendo ya wakati ujao ya kila mtu. Hata hivyo, je, dhana hiyo ni sahihi? Yale afunuayo Mungu katika Maandiko Matakatifu huonyesha jambo tofauti.
Kwa mfano, Maandiko husema kwamba ‘Mungu alimjaribu Abrahamu’ kwa kumwamuru amdhabihu mwana wake Isaka akiwa toleo la kuteketezwa. Abrahamu alipokuwa karibu kumdhabihu Isaka, Mungu alimzuia na kusema hivi: ‘Sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee.’ (Mwanzo 22:1-12) Je, Mungu angekuwa ametoa taarifa hiyo ikiwa alijua kimbele kwamba Abrahamu angeitii amri hiyo? Je, hilo lingekuwa jaribu la haki?
Zaidi ya hayo, manabii wa kale huripoti kwamba Mungu alijisema kwa kurudia-rudia kuwa ‘anajutia’ jambo fulani alilokuwa amelifanya au alilokuwa akifikiri kulifanya. Kwa mfano, Mungu alisema kwamba ‘alijuta [neno litokanalo na lile la Kiebrania, na·chamʹ] kwa sababu alimtawaza Sauli awe mfalme juu ya Israeli.’ (1 Samweli 15:11, 35; linganisha Yeremia 18:7-10; Yona 3:10.) Kwa sababu Mungu ni mkamilifu, mistari hiyo haiwezi kumaanisha kwamba Mungu alifanya kosa katika kumchagua Sauli awe mfalme wa kwanza wa Israeli. Badala ya hivyo, ni lazima ionyeshe kwamba Mungu alisikitika kwamba Sauli alikuja kukosa imani na utii. Kutumia kwa Mungu usemi kama huo kujirejezea kungekuwa jambo la upuuzi ikiwa alikuwa amejua kimbele matendo ya Sauli.
Usemi huohuo waonekana katika Maandiko ya kale zaidi ambako, katika kuzirejezea siku za Noa, yasema hivi: ‘BWANA akajuta kwa kuwa amemfanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo. BWANA akasema hivi, Nitamfutilia mbali mwanadamu niliyemwumba usoni pa nchi; kwa maana najuta ya kwamba nimemwumba.’ (Mwanzo 6:6, 7) Hilo laonyesha kwa mara nyingine tena kwamba, matendo ya mwanadamu hayaamuliwi kimbele na Mungu. Mungu alijuta, akahuzunika, na hata akaumia kwa sababu uovu wa mwanadamu ulipata kuwa mwingi. Muumba alijuta ya kwamba ilikuwa imekuwa lazima awaharibu wanadamu wote ila Noa na familia yake. Mungu hutuhakikishia hivi: ‘Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu.’—Ezekieli 33:11; linganisha Kumbukumbu la Torati 32:4, 5.
Kwa hiyo, je, Mungu alijua kimbele na hata kuagiza kimbele kutumbukia kwa Adamu katika dhambi, na vilevile matokeo yenye maafa ambayo jambo hilo lingeiletea familia ya kibinadamu? Yale ambayo tumechunguza yaonyesha kwamba hilo haliwezi kuwa kweli. Na zaidi, ikiwa Mungu alijua kimbele hayo yote, angalipata kuwa chanzo cha dhambi alipomwumba mwanadamu, na ndiye huwaletea wanadamu uovu kimakusudi na pia kuteseka kwote. Kwa wazi, jambo hilo haliwezi kupatanishwa na yale Mungu hufunua juu yake mwenyewe katika Maandiko. Yeye ni Mungu mwenye upendo na haki, achukiaye uovu.—Zaburi 33:5; Mithali 15:9; 1 Yohana 4:8.
Miisho Miwili ya Mwanadamu
Maandiko Matakatifu hayafunui kwamba, wakati ujao wa kila mmoja wetu kwa njia fulani umeamuliwa kimbele na Mungu. Badala yake, yale ambayo Maandiko hufunua ni kwamba, Mungu ametabiri miisho miwili tu ambayo yawezekana kwa mwanadamu. Mungu humpa kila mwanadamu hiari ya kuchagua utakaokuwa mwisho wake. Nabii Musa aliwajulisha Waisraeli wazi hivi: ‘Nimekuwekea mbele yako uhai na kifo basi chagua uhai ili uwe hai, wewe na uzao wako; kumpenda BWANA, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uhai wako, na wingi wa siku zako.’ (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Nabii wa Mungu, Yesu, alionya kimbele hivi: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Barabara mbili, miisho miwili. Wakati ujao wetu hutegemea matendo yetu. Kumtii Mungu humaanisha uhai, ilhali kutomtii humaanisha kifo.—Waroma 6:23.
Mungu “anaambia wanadamu kwamba wapaswa wote kila mahali kutubu. Kwa sababu ameweka siku ambayo katika hiyo akusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa.” (Matendo 17:30, 31) Kama vile walio wengi wa wanadamu katika siku ya Noa walivyochagua kutomtii Mungu, wakaharibiwa, ndivyo walio wengi leo huchagua kutotii amri za Mungu. Hata hivyo, Mungu hajaamua tayari ni nani watakaoharibiwa na ni nani watakaopata wokovu. Kwa kweli, Neno la Mungu husema kwamba “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Hata walio waovu sana waweza kutubu, kuwa watiifu, na kufanya mabadiliko yaliyo ya lazima ili kupata upendeleo wa Mungu.—Isaya 1:18-20; 55:6, 7; Ezekieli 33:14-16; Waroma 2:4-8.
Kwa wale watiifu, Mungu aahidi uhai udumuo milele katika paradiso yenye amani, dunia ambayo imesafishwa uovu wote, jeuri, na vita, ulimwengu ambako hakutakuwa na njaa, kuteseka, ugonjwa, na kifo. (Zaburi 37:9-11; 46:9; Isaya 2:4; 11:6-9; 25:6-8; 35:5, 6; Ufunuo 21:4) Hata wafu watafufuliwa na kupewa fursa ya kumtumikia Mungu.—Danieli 12:2; Yohana 5:28, 29.
“Umwangalie sana mtu mkamilifu, umtazame mtu mnyofu,” asema mtunga-zaburi, “maana mwisho wake mtu huyo ni amani. Wakosaji wataangamizwa pamoja, wasio haki mwisho wao wataharibiwa.” (Zaburi 37:37, 38) Je, wakati ujao wako utakuwaje? Ni juu yako kuamua. Wachapishaji wa gazeti hili watafurahia kukutolea habari zaidi ili ikusaidie kujihakikishia wakati ujao wenye furaha na amani.
[Maelezo ya Chini]
a Jina Yehova huonekana mara zaidi ya 7,000 katika Maandiko Matakatifu; ona makala yenye kichwa “Kufumbua Fumbo la Lile Jina Lililo Kuu Zaidi,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1993, ukurasa wa 3-5.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Mungu hutumia nguvu yake ya ujuzi wa kimbele katika kutimiza makusudi yake
[Blabu katika ukurasa wa 8]
Mungu “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” 2 Petro 3:9
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ikiwa Mungu alijua kimbele kwamba Abrahamu angekuwa tayari kumdhabihu mwana wake, je, lingekuwa jaribu la haki?