Je! Ajali Huongoza Wakati Wako Ujao?
KILA mwaka maelfu mengi ya watu huuawa kwa matukio yasiyotazamiwa nyumbani mwao, kazini au wakati wa kusafiri. Maelfu zaidi huumizwa sana wakati matukio yasiyotazamiwa yanapotukia. Kwa sababu gani? Watu wengi huona mambo haya kama accident, matukio yasiyosababishwa na cho chote. Je! kweli haya ni accident?
Watu fulani husema sivyo. Wanaamini kwamba kila tukio katika maisha ya mtu, kutia na wakati wa kufa kwa mtu, ni ajali iliyoamriwa mbele. Napoleon Bonaparte aliandika hivi wakati mmoja: “Saa yetu imeandikwa, na hakuna mtu awezaye kudai dakika ya kuishi zaidi ya ile ambayo ajali iliamuru mbele.”
Miongoni mwa wale wanaoshikilia kwamba ajali huongoza wakati wao ujao ni wengi wanaomwamini Mungu. Wanaona kwamba bila shaka Mungu anajua matukio yote ya wakati ujao. Na, juu ya wazo hilo, wanafikiri kwamba matukio yote ya wakati ujao yamekwisha kuamriwa mbele na Mungu, kwa maana jambo ambalo Mungu ajua mapema haliwezi kukosa kutukia. Wengine wanaendeleza wazo hili wasadiki kiitwacho predestination, maana yake ati Mungu amewaandikia wengine kati ya jamii ya kibinadamu wokovu na wengine mateso ya milele.
Je! kweli Mungu ametangulia kujua mambo yote ambayo yametukia katika historia yote? Je! sasa anajua hakika kila jambo ambalo viumbe vyake watafanya katika siku zijazo? Je! ajali (fate) hiyo yaongoza wakati wako ujao?
Biblia yaonyesha wazi kwamba mambo mengi yanayowapata watu ni yale yanayotukia kwa kusudi zuri, kwa maana “wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Mhu. 9:1, NW) Halafu, tena, Yehova Mungu huwapa viumbe wake wenye akili pendeleo na daraka la hiari. Israeli wa kale walitiwa moyo ‘wachague uzima’ kwa kumsikiliza Yehova Mungu. Nabii Sefania aliwasihi wapole ‘wamtafute Yehova.’ (Kum. 30:19, 20; Sef. 2:3) Katika Ufunuo 22:17, Neno la Mungu linatoa mwito kwa “yeye atakaye” afaidike na mipango ya Mungu ya wokovu.
Maandiko yaliyoongozwa yaonyesha Yehova kuwa Mungu mwenye rehema, mwenye haki, asiye na upendeleo na mwenye upendo. (Kum. 4:31; 32:4; Matendo 10:34; 1 Yohana 4:8) Je! Mungu wa namna hiyo angetia watu moyo wachague kilicho chema ikiwa amekwisha kujua tayari kwamba ajali ilizuia wengi kufanya hivyo?
KUTANGULIA KUJUA NI TOFAUTI NA AJALI
Ni kweli kwamba Mungu aweza kutangulia kujua mambo kabla hayajatokea. Maandiko yamtaja kama atangazaye “mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado.” (Isa. 46:10) Lakini kujua mapema jambo fulani si sawa na kulisababisha. Kwa mfano, huenda mpima hewa (meteorologist) akatabiri kwa usahihi kwa sababu anajua sana mifano au ishara za hali ya hewa. Lakini hakuna mtu ambaye angedai kwamba alisababisha ile hali ya hewa iliyotabiriwa.
Mungu anapotabiri jambo ambalo watu mmoja mmoja au vikundi watafanya, mara nyingi anafanya hivyo kwa kutazama mifano au dalili ambazo zimekwishaonekana. Basi, wakati wa kutabiri kwamba taifa la Israeli lingevunja agano lake, Yehova alisema: “Nayajua mawazo yao.” (Kum. 31:21) Unabii juu ya mwendo wa uaminifu wa kidunia wa Yesu ulikuwa juu ya vile Yehova alivyotangulia kumjua wakati wa maelfu ya miaka yake ya kuwako kabla ya kuwa binadamu.—Yohana 6:62; 17:5, 25.
Ikiwa Yehova anachagua kufanya hivyo, yeye aweza kujua tabia za uzazi za watoto watakaozaliwa baadaye na kwa njia hiyo ajue watasitawisha tabia gani. Kwa wazi ilikuwa juu ya msingi huu kwamba, kwa habari ya wana-mapacha wa Isaka, Yakobo na Esau, Yehova akatabiri hivi: “Mkubwa atamtumikia mdogo.” (Mwa. 25:23) Kwa habari ya wachache (kama Mwamuzi Samsoni Mwisraeli na Mfalme Koreshi wa Uajemi) Mungu alitabiri mambo fulani ambayo mmoja mmoja angefanya kabla hawajazaliwa. (Amu. 13:3-5; Isa. 44:28–45:3) Lakini ajali haikuongoza hata kidogo kila tendo au tukio katika maisha za watu hawa.
Lakini ikiwa Mungu ana uwezo wa kutangulia kujua yatakayotukia, je! uwezo wake wa kutangulia kujua siyo ajali isiyobadilika inayoongoza matukio yote ya wakati ujao? La, hasha. Kwa sababu gani? Kwa sababu maoni hayo hayasawazishi vizuri yale ambayo Mungu aweza kufanya na yale ambayo hufanya hasa. Ijapo Yehova Mungu ana uwezo wa kutangulia kuyajua mambo yatakavyokuwa, aweza kuchagua asitumie sana uwezo huo. Kwa mfano, fikiria namna Mungu anavyotumia nguvu zake. Ijapo ni Mwenye Nguvu Zote, Mungu hatumii sana nguvu zake katika kila hali, lakini anazitumia kwa kadiri inavyokuwa lazima kutimiza kusudi lake. Vilevile, Mungu ana kiasi cha kutumia maarifa yake ya mbele.
Jambo hili laweza kuonwa kutokana na maandiko ya Biblia yanayosimulia Mungu kuwa akichunguza hali fulani ili apate kuzijua. Twakumbuka kwamba Yehova alimwarifu Ibrahimu juu ya uamuzi wake kuchunguza mambo katika Sodoma na Gomora “nione kama wanayotenda ni kiasi cha kilio kilichonijia; na kama sivyo, nitajua.”—Mwa. 18:20, 21.
NAMNA GANI JUU YA IMANI YA KWAMBA MUNGU AMEWAANDIKIA WENGINE WOKOVU NA WENGINE MATESO YA MILELE (PREDESTINATION)?
Lakini namna gani maandiko yanayosema juu ya wengine kama “wateule . . . kama vile Mungu Baba alivyotangulia kuwajua,” ‘waliochaguliwa kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu,’ ‘waliotangulia kuchaguliwa, wafanywe wana wa Mungu’? (1 Pet. 1:1, 2; Efe. 1:3-5, 11) Juu ya msingi wa mitajo ya Biblia kama hii, viongozi wa kidini kama Augustine, Martin Luther na John Calvin walifundisha kwamba Adamu na Hawa waliandikiwa ajali ya kutokumtii Mungu hata kabla ya kuumbwa kwao; na kwamba wazao wao wote walichaguliwa mapema ama wapate wokovu ama wapate uharibifu wa milele.
Lakini je! mistari hiyo kweli yafundisha kwamba watu fulani waliandikiwa wokovu au mateso ya milele? Ikiwa ndivyo, lingekuwa jambo lisilowezekana kwa ye yote wa wateule (waliochaguliwa) kupoteza kibali ya Mungu. Hata hivyo mitume wale wale walioandika maneno yaliyotangulia (Petro na Paulo) walionyesha kwamba wengine ‘walionunuliwa’ na ‘kutakaswa’ kwa damu ya Kristo wangekosa imani hata wasitubu na kujiletea wenyewe uharibifu.—2 Pet. 2:1, 2, 20-22; Ebr. 6:4-6; 10:26-29.
Kwa hiyo yale maandiko yaliyotangulia kutajwa bila shaka yanamaanisha kutangulia kuchaguliwa kwa kundi la Kikristo kama jamii.
Kundi la Kikristo lilichaguliwaje “kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu”? Katika Luka 11:50, Yesu aliunganisha “msingi” na Habili. Hivyo ilikuwa kabla ya kuzaliwa Habili, lakini si kabla Adamu na Hawa hawajachagua kutokumtii Mungu, kwamba Mungu akatangulia kuichagua jamii ambayo ingekuwa warithi pamoja na Kristo katika ufalme wake.—Ufu. 20:6.
Kama katika habari ya Israeli wa kale, Mungu anawasihi watu leo ‘warudi na kugeuka mbali na makosa na kuishi.’ (Eze. 18:23, 30-32, ZSB) Petro aliandika kwamba Mungu “asiyetaka mutu mumoja kupotea, lakini wote wafike kutubu.” (2 Pet. 3:9, Z8B) Hilo lingekuwaje kweli hivyo kama ajali ingekuwa imekwisha kuandikia wengi, labda mamilioni ya maisha laana ya milele? Na je! fundisho la Biblia lingeweza kuwa la kweli kwamba Kristo Yesu “alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote” ikiwa ajali ingezuia wengi wasifaidike nao?—1 Tim. 2:6, NW.
Hapana, ajali haiongozi wala wakati wako ujao wala ule wa mtu mwingine ye yote mwenye akili. Wewe una uhuru wa kuchagua kumtumikia Mungu au kutokumtumikia. Lakini “kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake” kwa uchaguzi anaofanya. (Rum. 14:12) Uchaguzi wako utakuwa nini?