Je, Biblia Hufundisha Itikadi Katika Ajali?
MASINGIZIO! UCHONGEZI! Mshiriki wa jumuiya mwenye kustahiwa anapoona kwamba jina au sifa yake njema imeharibiwa kwa sababu ya ripoti isiyo ya kweli, anahisi ni lazima asahihishe mambo. Huenda hata akachukua hatua ya kisheria dhidi ya wale waliosababisha hayo masingizio.
Kwa kweli nadharia ajali ni uchongezi dhidi ya Mungu Mweza Yote. Nadharia hiyo hudai kwamba Mungu binafsi ndiye husababisha misiba na matukio mabaya yote yanayowakumba wanadamu. Ikiwa una itikadi katika ajali, huenda ukawazia kwamba Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima amefanya orodha inayosomwa kama ifuatavyo: ‘Leo, John atajeruhiwa katika aksidenti ya gari, Fatou atashikwa na malaria, nyumba ya Mamadou itaharibiwa katika dhoruba’! Je, kweli ungesukumwa kumtumikia Mungu wa aina hiyo?
‘Lakini ikiwa si Mungu anayesababisha taabu zetu, ni nani basi anayefanya hivyo?’ ndivyo waulizavyo wale ambao wana itikadi katika ajali. Ousmane, yule kijana aliyetajwa katika makala iliyotangulia, alijiuliza vivyo hivyo. Lakini haikuwa lazima akisie-kisie wala adhanie-dhanie ili kujua kweli. Alijifunza kwamba Mungu amejiondolea uchongezi huo kupitia mafundisho yanayopatikana katika Neno Lake lililopuliziwa, Biblia. (2 Timotheo 3:16) Acheni basi tufikirie yale ambayo Biblia husema juu ya jambo hili.
Ni Nani wa Kulaumiwa?
Gharika, dhoruba, matetemeko ya dunia—mara nyingi misiba hiyo mikubwa huitwa matendo ya Mungu. Hata hivyo Biblia haionyeshi kwamba Mungu husababisha misiba hiyo. Fikiria msiba uliotokea karne kadhaa zilizopita katika Mashariki ya Kati. Biblia hutuambia kwamba mwokokaji pekee wa msiba huo mkubwa aliripoti hivi: “Moto wa Mungu [usemi wa Kiebrania ambao mara nyingi humaanisha umeme] umeanguka kutoka mbinguni na kuwateketeza kondoo, na wale watumishi, na kuwaangamiza.”—Ayubu 1:16.
Ingawa labda mtu huyo mwenye hofu kuu alifikiri kwamba Mungu ndiye aliyesababisha ule moto, Biblia huonyesha kwamba Mungu hakuwa wa kulaumiwa. Jisomee Ayubu 1:7-12, na utapata kujua kwamba umeme haukusababishwa na Mungu, bali na Mpinzani wake—Shetani Ibilisi! Si kwamba matukio yote mabaya husababishwa na Shetani moja kwa moja. Lakini ni wazi kwamba hakuna sababu ya kumlaumu Mungu.
Kwa uhalisi, mara nyingi watu ndio wa kulaumiwa mambo yanapoharibika. Kushindwa shuleni, kazini, au katika mahusiano ya kijamii huenda kukasababishwa na ukosefu wa jitihada na mazoezi mazuri au labda na ukosefu wa ufikirio kwa wengine. Vivyo hivyo, magonjwa, aksidenti, na vifo huenda yakawa tokeo la kupuuza mambo. Kwani, kule kufunga tu mshipi wa kiti mtu aendeshapo gari hupunguza sana uwezekano wa mtu kuuawa katika aksidenti ya gari. Mshipi wa kiti usingefanya hali iwe tofauti ikiwa “ajali” isiyoweza kugeuzwa ilikuwa ikidhibiti mambo. Utunzaji ufaao wa kitiba na usafi wa kutunza afya pia hupunguza kwa njia ya kutokeza idadi ya vifo vya mapema. Hata misiba fulani inayoitwa “matendo ya Mungu” kwa kweli ni matendo ya mwanadamu—urithi wenye kuhuzunisha wa mwanadamu kuitawala dunia vibaya.—Linganisha Ufunuo 11:18.
“Wakati na Tukio Lisilotazamiwa”
Ni kweli, kuna matukio mengi yenye kuhuzunisha ambayo visababishi vyayo si dhahiri sana. Lakini, ona yale Biblia husema kwenye Mhubiri 9:11: “Nikarudi, na kuona chini ya jua, ya kwamba si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” “NW”] huwapata wote.” (Italiki ni zetu.) Kwa hiyo hakuna sababu ya kuamini kwamba Muumba ndiye anayesababisha aksidenti au kwamba wahasiriwa wa aksidenti wanaadhibiwa kwa njia fulani.
Yesu Kristo mwenyewe alibisha dhidi ya kusababu kwa kinadharia ajali. Akirejezea msiba uliojulikana sana na wasikilizaji wake, Yesu aliuliza hivi: “Wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? Nawaambia, Sivyo.” (Luka 13:4, 5) Ni dhahiri kwamba Yesu aliona “wakati na tukio lisilotazamiwa” (NW) kuwa sababu ya msiba huo, wala si uamuzi wa Mungu.
Madhara ya Kutokamilika
Lakini, namna gani kuhusu visababishi vya vifo na magonjwa visivyo dhahiri? Biblia hutoa ufafanuzi huu wa waziwazi wa hali ya binadamu: “Katika Adamu wote wanakufa.” (1 Wakorintho 15:22) Kifo kimekumba wanadamu tangu baba yetu wa zamani Adamu alipotembea kijia cha kutokutii. Sawa na vile Mungu alivyokuwa ameonya, Adamu aliwaachia wazao wake urithi wa kifo. (Mwanzo 2:17; Warumi 5:12) Basi, mwishowe magonjwa yote yanatokana na mzazi wetu mmoja wa kale Adamu. Udhaifu wetu mbalimbali tuliorithi unachangia pia hali za kutofaulu na za kushindwa tunazokuwa nazo maishani.—Zaburi 51:5.
Fikiria lile tatizo la umaskini. Mara nyingi itikadi katika ajali imewatia moyo wenye kuteseka wajiruhusu tu kuendelea katika maisha magumu. ‘Hii ndiyo ajali yetu,’ wao huamini. Hata hivyo, Biblia huonyesha kwamba jambo la kulaumiwa si ajali bali kutokamilika kwa binadamu. Wengine wanakuwa maskini ‘wanapovuna wapandacho’ kupitia uvivu au kutumia mali vibaya. (Wagalatia 6:7; Mithali 6:10, 11) Mamilioni yasiyohesabika ya watu yanaishi katika umaskini kwa sababu yanadanganywa na watu walio na mamlaka wenye pupa. (Linganisha Yakobo 2:6.) “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake,” Biblia husema. (Mhubiri 8:9, Union Version ya Kiswahili chapa ya 1952) Hakuna uthibitisho wowote wa kumwona Mungu au ajali kuwa kisababishi cha umaskini wote.
Itikadi Katika Ajali—Matokeo Yayo Yenye Kudhuru
Hoja nyingine zaidi yenye ushawishi dhidi ya itikadi katika ajali ni jinsi nadharia ajali iwezavyo kuwaathiri waamini wayo. Yesu Kristo alisema: “Kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya.” (Mathayo 7:17) Acheni tufikirie ‘tunda’ moja la nadharia ajali—njia inayoathiri hisi ya mtu ya kuwa na daraka.
Hisi timamu ya kuwa na daraka la kibinafsi ni jambo la maana. Ndilo jambo moja linalochochea wazazi waandalie familia zao, wafanyakazi kufanya kazi zao kwa bidii, waunda-vitu waandae kifaa bora. Itikadi katika ajali huenda ikazima hisi hiyo ya kuwa na daraka. Kwa kielelezo, ebu wazia kwamba gari la mtu lina usukani wenye kasoro. Ikiwa ni mwenye kuona daraka upesi, anatengeneza kasoro hiyo kwa sababu ya kufikiria uhai wake mwenyewe na uhai wa abiria zake. Kwa upande mwingine, mwenye itikadi katika ajali, huenda akapuuza hiyo hatari, akisababu kwamba uharibifu utatokea ikiwa tu ni ‘mapenzi ya Mungu’!
Ndiyo, itikadi katika ajali huenda ikasababisha kwa urahisi hali ya kutojali, uvivu, kushindwa kwa mtu kukubali daraka la vitendo vyake, na vitabia hasi vinginevyo vingi.
Kizuizi kwa Uhusiano Wetu Pamoja na Mungu?
Jambo lenye kudhuru zaidi ya yote ni kwamba, itikadi katika ajali yaweza kuzuia hisi ya mtu ya kuwa na daraka, au wajibu, kuelekea Mungu. (Mhubiri 12:13) Mtunga-zaburi awasihi sana wanadamu wote ‘waonje waone ya kuwa BWANA yu mwema.’ (Zaburi 34:8) Mungu huwawekea matakwa fulani wale ambao wangefurahia wema wake.—Zaburi 15:1-5.
Mojawapo matakwa hayo ni toba. (Matendo 3:19; 17:30) Hilo latia ndani kukiri makosa yetu na kufanya mabadiliko yanayohitajiwa. Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, sisi sote tuna makosa mengi ya kutubu. Lakini ikiwa mtu aamini kwamba yeye ni mhasiriwa hoi wa ajali, ni vigumu kwake kuhisi uhitaji wa kutubu au wa kuchukua daraka la makosa yake.
Mtunga-zaburi alisema hivi kuhusu Mungu: “Fadhili zako ni njema kuliko uhai.” (Zaburi 63:3) Hata hivyo, itikadi katika ajali imesadikisha mamilioni ya watu kwamba Mungu ndiye chanzo cha huzuni yayo. Kwa asili, hilo limefanya watu wengi wawe na uchungu wa moyo kumwelekea yeye, wakiufunga mlango unaoelekea kwenye hali ya kuwa na uhusiano wa karibu kwelikweli pamoja na Muumba. Kwani, ungehisije upendo kwa mtu uliyemwona kuwa mwenye kusababisha matatizo na majaribu yako yote? Kwa njia hiyo nadharia ajali huweka kizuizi kati ya Mungu na mwanadamu.
Kuwekwa Huru na Udhalimu wa Ajali
Wakati mmoja kijana Ousmane, aliyetajwa mwanzoni, alikuwa mtumwa wa itikadi katika ajali. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova walipomsaidia kuchanganua tena mawazo yake kwa kuitumia Biblia, Ousmane alisukumwa kuacha itikadi yake katika ajali. Matokeo yakawa hisi yenye kina ya kuwa na kitulizo na mtazamo mpya, chanya kuelekea maisha. La maana zaidi, amepata kumjua Yehova kuwa Mungu aliye “mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.”—Kutoka 34:6.
Ousmane amepata pia kung’amua kwamba, ingawa Mungu hapangi kila jambo moja-moja katika maisha zetu, analo kusudi kwa ajili ya wakati ujao.a Andiko la 2 Petro 3:13 (Habari Njema kwa Watu Wote) lasema hivi: “Kufuatana na ahadi zake, twangojea mbingu mpya na dunia mpya ambayo imejaa uadilifu.” Mashahidi wa Yehova wamesaidia mamilioni ya watu yakuze tumaini la kuishi milele yakiwa sehemu ya “dunia [hii] mpya” iliyoahidiwa. Wangependa kukusaidia pia.
Ukuapo katika ujuzi sahihi wa Biblia, utapata kung’amua kwamba wakati ujao wako hautegemei ajali fulani iliyoamuliwa kimbele ambayo huwezi kudhibiti. Maneno ya Musa kwa Waisraeli wa kale yanahusu jambo hili vizuri: “Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako; kumpenda BWANA, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye.” (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Ndiyo, unaweza kufanya chaguo kuhusiana na wakati ujao wako. Si ajali inayodhibiti mambo.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kupata mazungumzo ya kikamili juu ya uwezo wa Mungu wa kujua kimbele, ona Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 1984, kurasa 3-7, la Kiingereza.
[Picha katika ukurasa wa 6, 7]
Misiba hii haikuwa ‘matendo ya Mungu’
[Hisani]
U.S. Coast Guard photo
WHO
UN PHOTO 186208 /M. Grafman