“Njia ya Mungu ya Maisha” Mkusanyiko wa 1998-1999 Wakaribia!
KATIKA Marekani peke yake, mikusanyiko 198 imeratibiwa kuanzia Mei hadi Septemba. Yaelekea kwamba, mojawapo ya makusanyiko hayo ya siku tatu litakuwa katika jiji ambalo haliko mbali na nyumbani kwako. Katika sehemu zilizo nyingi, programu itaanza kwa muziki kila siku—kuanzia Ijumaa hadi Jumapili—saa 3:30 asubuhi.
Programu ya Ijumaa asubuhi itakazia ripoti za maendeleo ya kuhubiriwa kwa Ufalme katika sehemu tofauti za ulimwengu. Na kichwa cha mkusanyiko kitakaziwa na hotuba ya msingi, “Fidia ya Kristo—Njia ya Mungu ya kuleta Wokovu.”
Alasiri, mfululizo wa hotuba “Wazazi—Ikazieni Kikiki Njia ya Mungu Katika Watoto Wenu,” utaandaa madokezo juu ya jinsi ya kuwachochea wachanga wampende na kumtumikia Yehova. Programu ya alasiri itamalizika kwa hotuba “Je, Kuna Uhai Baada ya Kifo?”
Programu ya Jumamosi asubuhi yakazia kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kufanya wanafunzi, katika sehemu tatu zenye kufuatana “Kuwasaidia Watu Waingie Katika Njia Iendayo Kwenye Uhai,” “Ugumu wa Kuwafikia Watu,” na “Kuwafundisha Wanafunzi Mambo Yote Ambayo Kristo Aliamuru.” Kwenye umalizio wa programu ya asubuhi, kutakuwa na uandalizi kwa ajili ya wanafunzi wapya kubatizwa.
Hotuba ya kufungua Jumamosi alasiri, “Kutumikia Ukitazamia Uhai wa Milele,” yatutia moyo tufikirie kwa sala sababu zetu za kibinafsi za kumtumikia Mungu. Hotuba “Kuthamini ‘Zawadi Zikiwa Wanadamu’ Ambao Hufundisha Njia ya Mungu” na “Vueni Utu wa Kale na Kujivika Utu Mpya” zatoa uchunguzi wa mstari kwa mstari na wenye kuelimisha juu ya Waefeso sura ya 4. Halafu, onyo la upole la Kimaandiko litaandaliwa katika hotuba “Endeleeni Kuwa Bila Doa Kutoka Katika Ulimwengu” na katika mfululizo wa hotuba wenye sehemu tatu “Vijana—Fuateni Njia ya Mungu.” Programu ya alasiri yamalizika kwa hotuba “Utu wa Muumba na Njia Zake.”
Programu ya Jumapili asubuhi itakazia mfululizo wa hotuba wenye sehemu tatu utakaozungumzia sura za kumalizia za kitabu cha Biblia cha Ezekieli na vilevile kutumika kwazo kiunabii. Drama yenye mavazi kamili ambayo yategemea uaminifu wa wale vijana watatu Waebrania, ndiyo inayomalizia programu ya asubuhi. Jambo kuu la mkusanyiko alasiri, ni hotuba ya watu wote, “Njia ya Pekee Iongozayo Kwenye Uhai Udumuo Milele.”
Bila shaka utatajirishwa kiroho kwa kuwapo siku zote tatu. Unakaribishwa kwa moyo mweupe kwenye kila kipindi, ambavyo vyote, bila shaka, vitafanywa bila wewe kudaiwa malipo. Ili kujua mahali pa mkusanyiko palipo karibu zaidi na nyumbani kwako, pata habari kutoka kwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.