Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 8/15 kur. 3-4
  • Mbona Kuna Tatizo la Ukosefu wa Tumaini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mbona Kuna Tatizo la Ukosefu wa Tumaini?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ishara ya Nyakati
  • Tumaini Laweza Kupatikana Tena!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Unaweza Kugeukia Wapi Ukiwa na Matumaini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kuliimarisha Tumaini Letu Katika Uadilifu wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Ongeza Uhakika Sasa Juu ya Wakati Ujao
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 8/15 kur. 3-4

Mbona Kuna Tatizo la Ukosefu wa Tumaini?

‘JE, UNAWEZA kwa kweli kutumaini yeyote siku hizi?’ Huenda ukawa umemsikia mtu fulani aliyevunjika moyo akiuliza swali hilo. Au huenda hata ukawa ulijiuliza swali hilo uliposumbuliwa sana kihisia-moyo na jambo fulani lililokupata maishani mwako.

Bila shaka, ulimwenguni pote kuna ukosefu wa tumaini katika mashirika na katika watu wengine. Mara nyingi, ukosefu huo wa tumaini ni halali. Je, kuna yeyote kwa kweli awezaye kutarajia wanasiasa watimize ahadi walizotoa kabla ya kuchaguliwa? Uchunguzi wa mwaka wa 1990 wa wanafunzi 1,000 huko Ujerumani ulionyesha kwamba asilimia 16.5 ya wanafunzi walitumaini kwamba wanasiasa wangeweza kutatua matatizo ya ulimwengu, ilhali wanafunzi asimilia 33 walikuwa na shaka kubwa. Wengi walisema kwamba walikosa tumaini katika uwezo wa wanasiasa wa kutatua matatizo na pia katika utayari wao wa kufanya hivyo.

Gazeti la habari la Stuttgarter Nachrichten lililalamika hivi: “Wanasiasa walio wengi hutanguliza masilahi yao wenyewe, kisha ikiwezekana tu, yale ya waliowapigia kura.” Watu wa nchi nyinginezo hukubaliana na hilo. Gazeti la habari la The European lilisema hivi juu ya nchi moja: “Madharau ya vijana na pia wazee kuelekea wanasiasa, yana msingi mzuri.” Lilisema kwamba ‘kwa kawaida wapiga-kura huviondoa madarakani vyama vya kisiasa.’ Gazeti la habari hilo liliendelea kusema hivi: “Yeyote anayetumia wakati miongoni mwa vijana [huko] hutambua mara moja kukosa kwao tumaini na kuhisi kuwa wametengwa.” Hata hivyo, serikali ya kidemokrasi haiwezi kuwa na mafanikio makubwa ikikosa kutumainiwa na umma. Wakati mmoja, John F. Kennedy, Rais wa zamani wa Marekani alisema hivi: “Kutumainiwa na umma ndio msingi wa serikali yenye matokeo.”

Kuhusiana na tumaini katika nyanja za kifedha, hali ambazo kwa ghafula hubadilika kuwa mbaya na mipango isiyofanikiwa ya kupata utajiri haraka-haraka, imefanya wengi wasitesite. Masoko ya hisa yalipopanda na kushuka bila kuzuilika katika Oktoba 1997, gazeti la habari fulani lilizungumza kuhusu “ukosefu mwingi wa tumaini ambao nyakati nyingine haupatani na akili,” na pia juu ya “uenezaji wa ukosefu huo wa tumaini.” Lilisema pia kwamba ‘tumaini limefifia sana [katika nchi moja ya Asia] hivi kwamba hali hiyo yatishia kule kuwepo kwa serikali.’ Kifupi, gazeti la habari hilo lilitaarifu jambo hili lililo dhahiri: “Uchumi mbalimbali hutegemea tumaini.”

Dini pia inashindwa kuchochea watu kuwa na tumaini. Kwa kusikitisha, jarida la kidini la Ujerumani liitwalo Christ in der Gegenwart, laeleza hivi: “Kiwango cha tumaini ambacho watu wa kawaida wanalo katika Kanisa chaendelea kushuka.” Kati ya mwaka wa 1986 na 1992, idadi ya Wajerumani wenye kiwango kikubwa, au angalau kiwango fulani cha tumaini katika kanisa, ilishuka kutoka asilimia 40 hadi asilimia 33. Kwa kweli, katika Ujerumani Mashariki ya zamani, idadi hiyo ilishuka hadi chini ya asilimia 20. Kwa upande mwingine, watu waliokuwa na tumaini ndogo au bila tumaini lolote katika kanisa, waliongezeka kutoka asilimia 56 hadi asilimia 66 katika Ujerumani Magharibi ya zamani, na kuongezeka hadi asimilia 71 katika Ujerumani Mashariki ya zamani.

Kushuka kwa tumaini kumekuwa dhahiri katika nyanja nyinginezo mbali na za siasa, uchumi, na dini—nguzo tatu za jamii ya kibinadamu. Utekelezaji wa sheria ni kielelezo kingine. Njia za kuepa mifumo ya sheria ya uhalifu, matatizo katika kutekeleza sheria kwa haki, na maamuzi ya mahakama yenye kutilika shaka, yamedhoofisha vibaya tumaini la watu. Kulingana gazeti la Time, “kukatishwa tamaa kwa raia na kwa polisi kumefikia kiwango cha kutokuwa na tumaini lolote na mfumo ambao huwaachilia wahalifu hatari kutoka gerezani baada ya muda mfupi tu.” Hata kuwatumaini polisi kumeshuka kwa sababu wameshutumiwa kuwa wafisadi na wakatili.

Kuhusiana na siasa za kimataifa, mazungumzo ya amani yasiyofanikiwa na kuvunjika kwa usimamishaji mapigano, hudhihirisha ukosefu wa tumaini. Bill Richardson, balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, alionyesha wazi kikwazo kikuu cha kupatikana kwa amani katika Mashariki ya Kati, akisema tu hivi: “Kuna ukosefu wa tumaini.”

Wakati uleule, watu binafsi walio wengi hukosa tumaini hata katika watu wa jamaa na marafiki wa karibu, watu hasa ambao wanadamu huwaendea ili kupata msaada na faraja wanapokuwa na matatizo. Hali hiyo ni sawa na ile iliyofafanuliwa na nabii Mwebrania Mika: “Msimwamini rafiki, msimwekee kiongozi tumaini; ilinde milango ya midomo ya kinywa chako ili mkeo alalaye kifuani mwako asijue habari.”—Mika 7:5.

Ishara ya Nyakati

Hivi majuzi mwanasaikolojia Mjerumani aitwaye Arthur Fischer, alinukuliwa akisema hivi: “Tumaini katika maendeleo ya jamii na katika wakati ujao wa mtu binafsi, kwa kweli limeshuka kwa kutazamisha katika nyanja zote. Vijana hushuku kama mashirika ya jamii yanaweza kuwasaidia. Hawana tumaini kamwe, liwe la kisiasa, kidini, au katika shirika jingine lolote.” Si ajabu kwamba mwanasoshiolojia aitwaye Ulrich Beck huzungumzia “utamaduni wa shaka” kuelekea mamlaka za muda mrefu, mashirika, na wataalamu.

Katika utamaduni kama huo, watu huwa na maelekeo ya kujitenga, kukataa mamlaka yote, na kuishi kulingana na viwango vyao binafsi, wakifanya maamuzi yasiyotegemea shauri au mwongozo kutoka kwa wengine. Wengine huwa wenye shaka kupita kiasi, labda hata kukosa ufikirio, wanaposhughulika na wale wasioweza kuwatumaini tena. Mtazamo huo hukuza hali hatari, kama ile iliyofafanuliwa katika Biblia: “Katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu, wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo.” (2 Timotheo 3:1-5; Mithali 18:1) Kwa kweli, tatizo la siku hizi la ukosefu wa tumaini ni ishara ya nyakati, ishara ya “siku za mwisho.”

Kwa hakika, maisha hayawezi kufurahiwa kikamili katika ulimwengu unaosumbuliwa na tatizo la ukosefu wa tumaini na uliojaa watu kama wale waliofafanuliwa hapo juu. Lakini inawezekana kufikiri kwamba mambo yatabadilika? Je, tatizo la siku hizi la ukosefu wa tumaini linaweza kushindwa? Ikiwa ndivyo, ni lini na jinsi gani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki