Ongeza Uhakika Sasa Juu ya Wakati Ujao
1, 2. (a) Kwa ujumla, wanadamu wamo katika hali gani? na kwa sababu gani? (b) Lakini, wengi wanaonyesha uhakika gani?
SASA tumesonga sana katika karne ya 20, na mambo yote yaonyesha kwamba taratibu ya mambo iliyopo itapita pamoja na kizazi hiki kinachokufa. Makumi yote ya miaka iliyopita katika karne hii, wanadamu waliotengana na Mungu wamezidi kuogopa. Ni sawa na alivyotabiri nabii mkuu Yesu Kristo. Alipoulizwa: “Mambo hayo yatakuwa lini? nayo ni nini ishara ya kuwa mambo hayo ya karibu kutukia?” baadhi ya mambo aliyojibu ni kwamba, “Kutakuwa . . . katika nchi dhiki ya mataifa wakishangaa . . . watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatakayoupata ulimwengu.”—Luka 21:7, 25, 26.
2 Kwa hiyo si ajabu kwamba wanadamu wengi, wasiomwamini Yehova wala kumtumaini kwa uhakika, wala Neno lake Biblia, wananyong’onyea wakifikiria mambo ya wakati ujao kwa hofu. Lakini, kama ilivyoonyeshwa katika makala iliyotangulia, wako watu zaidi ya 2,000,000 ulimwenguni pote leo wanaoukabili wakati ujao wakiwa na matumaini mazuri sana. Wana hakika kabisa kwamba taratibu mbovu hii ya mambo itaondolewa karibuni na nafasi yake ichukuliwe na taratibu mpya yenye haki—ufalme wa Mungu ambao Yesu alifundisha Wakristo waombe.—Mt. 6:9, 10.
3. Mtume Paulo atoa onyo gani linalofaa?
3 Kwa sasa huenda wewe ukawa mmoja wa watu hawa, na huenda ukaona una hakika sana kwamba umesimama imara na unayaweza mambo unayokabili huu wakati wa mwisho. Lakini mtume aonya hivi: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (1 Kor. 10:12) Tukitii shauri hilo, yako mambo tunayoweza kufanya sasa tutie uhakika wetu nguvu.
4, 5. Twawezaje kuwa na uhakika thabiti juu ya wakati ujao?
4 Kwanza, yatupasa tukumbuke yasemwayo na Mithali, kwamba msingi wa kumtumaini Yehova kwa uhakika wapaswa kuwa kumjua yeye na matendo aliyotendea wanadamu zamani, na vilevile kujua anayokusudia kufanya sasa na wakati ujao.—Mit. 14:26; 22:19.
5 Hilo laonyesha kujifunza kipekee na katika kundi pia ni mambo ya maana sana. Jifunze uwezavyo juu ya Muumba Mkuu huyu, si kutokana na Neno lake Biblia tu, bali pia kwa kutazama vitu vilivyoumbwa karibu nawe. Mtume Paulo aliwaambia watu wa Listra hivi: “Lakini [Yehova] hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.” (Matendo 14:17) Na Wakristo wa Rumi Paulo aliwaandikia hivi: “Kwa sababu mambo yake [Mungu] yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake.”—Rum. 1:20.
6. Kuchunguza vitu vilivyomo ulimwenguni mwote kwawezaje kufanya mtu azidi kumwamini Muumba na kumtumaini?
6 Zaidi ya kutazama vitu vilivyoumbwa hapa duniani, imetupasa tugeuze fikira zetu kuelekea mbingu zinazoonekana. Kwa kujibu ulizo: “Ni nani aliyeziumba hizi?” Isaya 40:26 yasema: “Aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina; kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake hapana moja isiyokuwapo mahali pake.” Lo! mamilioni mamilioni yote yasiyohesabika ya nyota, yanatoa ushuhuda mkubwa ajabu juu ya ukuu wa milele wa Yehova! Daudi alieleza vizuri aliposema hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.”—Zab. 19:1.
7-9. (a) Ni jambo gani lililotukia siku za Hezekia likaonyesha jinsi malaika walivyo na uwezo? (b) Hilo latiaje nguvu uhakika wetu juu ya wakati ujao?
7 Halafu kuna maelfu maelfu ya malaika wasioonekana. (Ebr. 12:22; Yuda 14, 15) Kumbuka jinsi Mfalme Hezekia, mwabudu wa kale wa Yehova, alivyodhihakiwa na Waashuru: “Ni tumaini gani hili unalolitumainia? . . . unamtumaini nani hata ukaniasi mimi [Senakeribu]?” Karibuni wenye dhihaka hao wapagani wangejifunza kwa nini Mfalme Hezekia alikuwa amemtumaini Yehova na majeshi yake ya malaika, kwa maana, kama habari isemavyo, “Ikawa usiku uo huo malaika wa [Yehova] alitoka, akakiingia kituo cha Waashuru, akawapiga watu mia na themanini na tano elfu.”—2 Fal. 18:19, 20; 19:35; linganisha Isaya 36:1 mpaka 37:38.
8 Naam, bila shaka habari ya hakika kama hii yafaa impe uhakika mkubwa mtu anayemwogopa Yehova leo. Imeandikwa hivi: “Malaika ya [Yehova] anapiga kambi kuzunguka wale wanaomwogopa, na anawaokoa.”—Zab. 34:7, ZSB; linganisha Zaburi 91:11, 12.
9 Ikiwa malaika mmoja tu wa Yehova ni mwenye nguvu hivyo hata aweza kufagilia mbali wanaume 185,000, yatupasa tumtumaini kabisa Yehova uyu huyu na majeshi yake ya malaika yanayoamriwa na Bwana Yesu Kristo leo. Na tukumbuke kwamba Bwana Yesu Kristo huyu si ‘kitoto tena katika hori ya kulia ng’ombe ya Bethlehemu.’ Sasa huyu ndiye “MFALME WA WAFALME, NA BWANA WA MABWANA,” mwenye nguvu na uwezo wa kusema, “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani,” naye amepanda farasi kuwaongoza askari wa mbinguni, jeshi lenye malaika wasio punde ya 100,000,000! Mt. 28:18; Ufu. 5:11; 19:14-16.
USHUHUDA WA KISASA WAONGEZA UHAKIKA
10. Mabaki watiwa mafuta ambao ni wafuasi wa Kristo walijitayarisha kufanya nini mwaka 1919, na walisaidiwa na nani?
10 Kwa sababu ya kutiwa moyo na kusaidiwa hivyo na malaika, “mabaki” wadogo wa wafuasi waliotiwa mafuta wa Kristo Yesu walianza mwaka wa 1919 kuihubiri hii “habari njema ya ufalme . . . katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Kwa muda wa miaka ya katikati tangu ilipoanza kazi hiyo, “mkutano mkubwa” wa watu “wa kila taifa, kabila, na jamaa, na lugha” wameitikia. Wanasimuliwa kama “wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu.”—Ufu. 7:9, 10, 14.
11. Ni mambo gani yametukia miaka 60 iliyopita yakafanya mabaki na “mkutano mkubwa” wamtumaini Yehova?
11 Sasa leo wakati “mabaki” hawa waaminifu wanapoikumbuka miaka ya nyuma wanaweza kusema kama Zaburi 71:5, NW inavyosema: “Kwa maana wewe ndiwe tumaini langu, Ee Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu, uhakika wangu tangu ujana wangu.” Mtu akisoma historia ya Mashahidi wa Yehova ya miaka 60 iliyopita, ataona kwa nini “mabaki” hawa wamekuwa wenye hakika na Yehova hivyo. Yaonekana kama Shetani Ibilisi na mashetani wake walitumia hila na vizuizi vyote ili wazuie kazi yao. Mabaki walishambuliwa sana na matengenezo mbalimbali ya kisiasa na ya kidini katika mataifa mengi ulimwenguni pote. Watawala wenye kutumia nguvu walizuia kazi yao wakawapiga marufuku wasihubiri. Hata katika yale yaitwayo “mataifa huru,” wanadini washupavu na wazalendo wenye siasa ‘walitunga madhara kwa njia ya sheria,’ wakafanya ghasia na kujitahidi kukomesha watu wa Mungu kwa kutaka kususia uhusiano na wenye kuwapendelea.a (Zab. 94:20) Hata wenye imani ya mageuzi, wenye kulaumulaumu Biblia, vilevile yule “mtu wa kiasi,” yaani, mapadre wa Jumuiya ya Wakristo wenye kuasi imani, walijaribu kuchafua kazi ya kufanya wanafunzi ya mashahidi waaminifu wa Mungu.
12. Twapewa uhakikisho gani na Isaya 54:17?
12 Kwa sababu ya hayo yaliyowapata zamani, Mashahidi wa Yehova wa Kikristo huvutwa na ukweli wa Isaya 54:17, linalosema hivi: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa, na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa [Yehova], na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema [Yehova].”
13. Ni mambo gani zaidi yanayotutia imani nguvu?
13 Ebu utazame, pia, ukuzi ulimwenguni pote na ufanisi unaofurahiwa na watu wa Mungu ujapokuwapo upinzani wote wa kishetani! Bila shaka kazi hii ya kuhubiri isingaliweza kupanuka bila ulinzi, baraka na roho ya Yehova iliyo juu ya watu wake. Hili pia huutia nguvu uhakika wa watu wa Mungu juu ya wakati ujao.
SABABU YAWEZEKANA TUSIOGOPE
14, 15. Haitupasi kusahau tofauti ya mambo gani tunapofikiria kama tutaweza kuokoka “dhiki kubwa”?
14 Lakini, kwa kweli, ikiwa “dhiki kubwa” itakuwa yenye maangamizi makubwa kama Maandiko yanavyoonyesha, je! yawezekana wanaomtumikia Mungu waitazamie bila kuogopa na kushikwa na kiherehere? Yatupasa tukumbuke kwamba kuna tofauti kubwa sana kati ya “dhiki kubwa” ambayo Yehova mwenyewe ataletea tengenezo la kinyama la Shetani na wale wote wanaoshikamana nalo, na dhiki ambayo Shetani aletea mashahidi waaminifu wa Yehova sasa, kwa namna ya mateso, marufuku, ghasia na matendo kama hayo ya jeuri yaliyo wazi.
15 Taabu ya namna hii ya pili yatokana na Shetani na haiwezi kuepukwa ikiwa mtu amtumikia Yehova, kwa maana imeandikwa hivi: “Na wote wanaotaka kuishi maisha ya utawa katika Kristo Yesu watapata mateso.” “Lakini saa inakuja, wakati kila mutu anayewaua ninyi atazania ya kama anatumikia Mungu.”—2 Tim. 3:12; Yohana 16:2, ZSB.
16. Ni kwa njia gani mateso yaliyoletwa na Shetani siku zilizopita yametia watu wa Mungu moyo?
16 Lakini, hatutamani wala hatufurahii kuteswa na watu wenye kuarifiwa vibaya na kudanganywa. Watu wa Yehova hawatamani kuwa watu wa kuteswa. Hata Yesu alimwomba Baba yake mara tatu kwamba ingekuwa vizuri kama ingewezekana aepuke kukinywa “kikombe” cha kuonyeshwa kuwa mkufuru Mungu na mvunja Torati yake kwa kutundikwa juu ya mti wa mateso. Lakini, ‘si mapenzi yangu bali mapenzi ya Mungu yatimizwe,’ akasema. (Mt. 26:39-44) Lakini, mtu akiisha kuvumilia mateso, anaweza, kufurahi kwa vile amekuwa mwaminifu kama Ayubu na wanaume na wanawake wengine wa zamani wenye kumwabudu Mungu. Unakumbuka kwamba, mwishowe Ayubu alithawabishwa sana kwa sababu ya kuteswa. (Ayubu 42:10-17) Haya ndiyo yaliyowapata mitume pia wakati walipopigwa vikali kwa amri ya mahakma ya kidini. Baadaye “wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo.”—Matendo 5:40, 41.
17. Tunapokabiliwa na majaribu hayo ya Shetani, tusisahau nini?
17 Hivyo, hata Ibilisi akituletea majaribu na dhiki, imetupasa tuwe na hakika kwamba Yehova ana nia na uwezo wa kutufanya tushinde kabisa. (Rum. 8:37) Yakumbuke maneno yenye kutia moyo katika 1 Wakorintho 10:13: “Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.” Ama ikisemwa kwa njia nyingine, “twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi; sikuzote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu.”—2 Kor. 4:8-10.
18, 19. (a) “Dhiki kubwa” inatofautianaje na mateso wanayopata watumishi wa Mungu? (b) Kwa hiyo watumishi wa Mungu wanaomba nini, na wanahakikishiwa nini?
18 Kwa upande mwingine, ile “dhiki kubwa” iliyotabiriwa katika Mathayo 24:21, 22 inatofautiana kabisa na taabu na mateso yaliyoletwa zamani, hata sasa, na Ibilisi, juu ya watumishi wa Mungu. Ile “dhiki kubwa” ni dhiki ambayo Mungu ataleta juu ya kundi zima la Ibilisi ili ajitetee pamoja na wote wale walio upande wake. Kama ilivyoandikwa katika 2 Wathesalonike 1:6: “Ni haki mbele za Mungu kuwalipa mateso wale wawatesao ninyi.”
19 Kwa sababu hizi watu wa Yehova wanampenda sana na kumshukuru, kisha wanapata uhakika wasidhoofishwe na woga. Watu hawa wanaompenda Yehova wanatazamia kwa shauku sana kuwa mashahidi watakaoona hukumu ya kimungu ikitekelezwa sana katika “dhiki kubwa” inayokuja, hata ikiwa itaogofya namna gani. (Zab. 89:7; Hab. 3:16, 18) Hivyo wanaendelea kusali ‘kwa uhakika kamili kupitia kwa imani’ kwamba ufalme wa Mungu uje na mapenzi na kusudi lake yatimizwe. “Huu ndio uhakika tulio nao kwake yeye,” asema mtume Yohana, “kwamba, haidhuru tunaomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”—1 Yohana 5:14, NW; Efe. 3:12; Mt. 6:9, 10.
USIWEKE KAMWE UHAKIKA WAKO PASIPOFAA
20. Tunapoongeza uhakika wetu, lazima tuepuke mtego gani, na kwa njia gani?
20 Kwa vile “dhiki kubwa” inakuja mbio, sasa sio wakati wa kutojali au kujitegemea. Haitupasi kamwe tutegemee ufahamu wetu wenyewe, hata kuitumaini hekima ya wanadamu wengine, wawe ni wanasiasa, washauri wa mambo ya uchumi, washauri wa mambo ya kijamii au wanadini wenye kutabiri mambo. (Mit. 3:5, 6; Zab. 146:3) Mtu anayemtumaini ‘mwanadamu na kumfanya kinga yake’ “amelaaniwa,” kulingana na kitabu cha Yeremia. Tofauti na hilo, imeandikwa hivi katika Yeremia 17:5-8; “Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea [Yehova], ambaye [Yehova] ni tumaini lake.”
21. Biblia yatuonyaje tusitumaini mali?
21 Mtu anayemtumaini Yehova kwa uhakika hutanguliza ufalme wa Mungu katika maisha yake, na kwa njia hiyo huepuka masumbufu mengi yanayoletwa na matatizo ya kiuchumi. (Mt. 6:25-34) Hasahau yaliyosemwa na Yesu pia, kwamba “uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.” (Luka 12:15) Basi, ni upumbavu kama nini kukusanya mali kwa wingi na kuzitumaini zije zikuokoe na ukali wa “dhiki kubwa!” Mithali 11:4, 28, yasema hivi: “Mali hazifaidii kitu siku ya ghadhabu; . . . azitegemeaye mali zake ataanguka.” Ayubu mwaminifu alikuwa mwangalifu asikosee kwa kutumaini mali za kimwili, akasema: “Ikiwa nimeifanya dhahabu kuwa tumaini langu, na kuiambia dhahabu safi, Wewe u tegemeo langu; . . . [ningemkana] Mungu aliye juu.”—Ayubu 31:24, 28.
22. Je! taratibu hii ya mambo itapatwa na “dhiki kubwa” kwa sababu ina udhaifu?
22 Huenda masoko ya mali na bei zikaharibika na wakuu wa serikali wakaanguka, lakini haya siyo mambo ya kuamulia wala kupimia kukaribia kwa uharibifu wa “dhiki kubwa.” Ukumbuke kwamba wakati mamlaka za ulimwengu za zamani zilipoharibiwa na Yehova, hazikuanguka kwa sababu zilikuwa na udhaifu au ubovu ndani yazo zenyewe. Zilikuwa zikiendelea kusitawi kama kawaida wakati Mungu alipoziharibu kwa kutumia majeshi ya nje.
23. Tukikabiliwa na misiba mbalimbali, hata kifo, twawezaje mmoja mmoja kuutazamia wakati ujao tukiwa na hakika?
23 Ijapokuwa huenda watu mmoja mmoja miongoni mwa watu wa Bwana wakafa kati ya sasa na wakati huo, na Maandiko yaonyesha kwamba wengine watakufa [Mt. 10:21; 24:9], watu wa Yehova kama jamii wataokoka “dhiki kubwa.” Hata ikiwa wewe mwenyewe ndiwe utakayepatwa na shida na misiba mikubwa—kama vile kuharibika kwa afya yako, kufiwa na mtu wa jamaa yako, kufiwa na watoto au kupoteza mali za kimwili, au kupatwa na misiba ya kiuchumi na mambo yawayo yote, usiache kamwe kumwamini na kumtumaini Yehova kwa uhakika. Usizitilie shaka kamwe ahadi za Mungu wako. Usiogope kamwe, wala usijifiche kwa sababu ya woga; usimkane kamwe Mungu wako wala usivunje ukamilifu wako. Usisahau kamwe kwamba wako malaika wanaosaidia wale wanaoshikamana na wakf wao kwa Yehova.—2 Fal. 6:14-17; Hab. 3:17, 18.
24. Kwa kuwa “dhiki kubwa” inakaribia mbio, yawapasa watu wa Yehova wawe na nia gani inayoonyeshwa na Maandiko?
24 Hakuna shaka: “Mwenye furaha ni yeye ambaye msaada wake ni Mungu wa Yakobo, ambaye tumaini lake li katika Yehova Mungu wake.” (Zab. 146:5, NW) Basi umfurahie Yehova pamoja na msaada, uongozi, ulinzi na ufanisi wa kiroho ambao amewapa mashahidi wake waaminifu hata sasa, katika wakati huu wa mwisho’—Luka 21:28; 2 Tim. 1:7.
25. Ahadi zilizomo katika Mithali 3:25, 26 zinawapa nani faraja na moyo wa pekee?
25 Sisi watangazaji wa Yehova, na tuwe mashujaa tuendelee kuonya watu habari za siku ya kisasi cha Mungu. (Eze. 3:17) Na tuendelee kuomba ufalme wa Mungu uje na ukali wake wote juu ya taratibu mbovu ya Shetani, uiponde-ponde na kuisaga tikitiki. (Mt. 6:9, 10; Dan. 2:44; Mal. 4:3) Mashahidi wa Yehova waukabilipo ule uharibifu wa tengenezo zima la Ibilisi, wanatiwa sana moyo na ahadi ya Mungu iliyo katika Mithali 3:25, 26, NW: “Wewe hutakuwa na haja ya kuogopa jambo lo lote la ghafula lenye kutisha, wala dhoruba juu ya waovu, kwa sababu inakuja. Kwa maana, ni kweli Yehova mwenyewe atakuwa UHAKIKA WAKO”!
—Kutoka The Watchtower, Jan. 15, 1977,
[Maelezo ya Chini]
a Tazama kitabu Jehovah’s Witnesses in the Divine Purpose.