Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 6/15 kur. 267-271
  • Kuikabili “Dhiki Kubwa” kwa Uhakika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuikabili “Dhiki Kubwa” kwa Uhakika
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • HALI INAYOLINGANA NA HIYO LEO
  • DHIKI KUBWA KULIKO ZOTE
  • MAONYESHO YA ZAMANI YA UHAKIKA
  • WENGINE WALIOKOKA “DHIKI” ILIYOUPATA YERUSALEMU
  • Ongeza Uhakika Sasa Juu ya Wakati Ujao
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Sababu Hatukuambiwa “Siku Ile na Saa Ile”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Kuutazamia Wakati Ujao kwa Matumaini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • “Tuambie, Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 6/15 kur. 267-271

Kuikabili “Dhiki Kubwa” kwa Uhakika

“Ni kweli Yehova mwenyewe atakuwa uhakika wako.”​—Mit. 3:26, NW.

1, 2. Watu wote wanapendezwa na nini, na wengine wanaonyeshaje hivyo?

WANADAMU wote wanapendezwa sana na wakati ujao. Kupendezwa na yasiyotukia bado ni kawaida ya wanadamu. Kwa kawaida watu hutia bidii katika utendaji wao wa kila siku wakitumainia wakati ujao. Hufanya daima mipango ya wakati ujao. Tamaa zao, mataraja na matumaini yao yanategemea zaidi mambo wanayosadiki yatatokana na wakati ujao. Ili wawe wenye furaha, ni lazima wawe na uhakika juu ya yatakayotukia wakati ujao.

2 Tamaa hii ya wanadamu ya kutaka kujua mapema matukio yajayo hufanya watu wengi wawaendee wale wanaojidai kuujua wakati ujao​—wachawi, waaguzi na wanajimu. Watu zaidi na zaidi wanapiga falaki na bao kwa kutaka kujifunza mambo ambayo waaguzi wenye kuongozwa na mashetani husema yatatukia.

3. Maoni ya Mashahidi wa Yehova yanatofautianaje na ya wengine juu ya wakati ujao? (Kum, 18:10-12)

3 Walakini, katika habari hii kuna tofauti moja kubwa sana kati ya wale wanaomtumikia Yehova na wale wasiomtumikia. Watu wa Mungu hawawaendei kamwe waaguzi wala wapiga falaki ili wajifunze juu ya matukio yanayokuja. Wala hawaviendei vyanzo vingine vya kishetani kwa kutaka kuujua wakati ujao. Wana sababu nzuri sana ya kutofanya hivyo

4. Watu wa Yehova wana msingi gani unaowafanya wautazamie wakati ujao wakiwa na hakika nyingi?

4 Kweli inayofuata iliandikwa katika Biblia na nabii Amosi, katika sura ya tatu, mstari wa saba,karne ya tisa kabla ya huu Wakati wa Kawaida. “Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu hatafanya jambo isipokuwa amewafunulia watumishi wake manabii siri yake.” (NW) Nao manabii hawa wanawasimulia watu wote wa Mungu jambo la kutazamia katika wakati ujao, na huu ndio msingi wa uhakika wao.

5, 6. (a) Eleza hali iliyokuwa Yerusalemu karne ya kwanza W.K.? (b) Lakini kwa sababu gani Wakristo wa wakati huo hawakuwa na maoni ambayo watu wengi walikuwa nayo?

5 Ebu ifikirie hali iliyokuwa mji wa Yerusalemu karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Watu wote na viongozi wao walikubali kwamba hali zilikuwa mbaya. Hata hivyo, washauri na viongozi wa watu walikuwa wakitabiri nini juu ya wakati ujao? Wengine waliridhika sana na hali iliyokuwako wakataka iendelee kuwa hivyo, isibadilike sana. Wengine waliunga mkono maoni ya kwamba uhuru zaidi, amani zaidi na ufanisi zaidi ungepatikana watu wakiasi na kupindua utawala wa Rumi na kukataa kulipa kodi zake. Walakini, hakuna washauri wa mji huo waliokuwa wakitabiri kwamba Yerusalemu ungeharibiwa kabisa katika dhiki kubwa​—katika kizazi hicho.​—Matendo 5:36, 37.

6 Je! Wakristo wa karne ya kwanza waliwatumaini watu hao wenye hekima ya ulimwengu na ubashiri wao? La, hata kidogo. Yehova alikuwa ametangulia kumfunulia nabii wake mkubwa, Bwana Yesu Kristo, jambo tofauti kabisa, ambalo Yeye alikuwa ameazimu lingetukia upesi katika kizazi hicho. Nabii huyo wa kweli wa Mungu alionya hivi: “Siku zitakuja [juu yako Yerusalemu], adui zako watakapokujengea boma, likuzunguke; watakuzingira na kukuhusuru pande zote; . . . wasikuachie jiwe juu ya jiwe.” Naam, “kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.”​—Luka 19:41-44; Mt. 23:36-38; 24:2, 21.

7. Wakristo walioishi karibu na Yerusalemu waliwezaje kuukabili wakati uliokuwa mbele yao wakiwa na hakika?

7 Je! Wakristo waliokuwa wakiishi ndani na kando ya Yerusalemu walikuwa na sababu yo yote kuukabili msiba huu uliotabiriwa kwa uhakika? Bila shaka. Kwa maana nabii huyu wa kweli wa Mungu aliwaambia pia jinsi wangejua ukikaribia na hatua ambayo wangechukua wajisalimishe. Alisema hivi: “Hapo mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi, ndipo . . . walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani.”​—Luka 21:20, 21.

HALI INAYOLINGANA NA HIYO LEO

8. Ni hali gani kama hizo zilizomo katika Jumuiya ya Wakristo leo?

8 Leo kuna hali inayolingana na hiyo katika Jumuiya ya Wakristo​—⁠tengenezo lile la unafiki linalolingana na mji wa Yerusalemu usio mwaminifu. Walimwengu wa kisasa wanawaendea waaguzi wao wa kisiasa, washauri wa mambo ya uchumi, wanadini wenye kutabiri mambo, na pia wanasayansi wao wenye hekima, na kubashiriwa mambo mengi yatakayotukia wakati ujao. Ijapokuwa kwa kawaida washauri hawa wanakubali upesi kwamba hali ya sasa ya mambo ni yenye kusikitisha, bado wanatabiri kwamba siku fulani, katika njia fulani, “nyakati bora zinakuja.”

9. Je! wewe unatumaini matabiri ya viongozi wa ulimwengu?

9 Sasa, wewe unaamini na kutumaini makisio ya wanadamu hawa? Sivyo ikiwa unaamini sana Biblia na unabii wake. Kwa sababu gani usiyatumaini? Kwa sababu kauli hizi za wanadamu sizo Yehova amefunua kwa kinywa cha manabii wake juu ya mambo yatakayotukia karibuni.

10. Mashahidi wa Yehova wameonyeshaje wana hakika kwamba mambo yanayotabiriwa na Biblia juu ya wakati ujao yatatukia?

10 Miaka mingi Mashahidi Wakristo wa Yehova wamejibidiisha sana kuwaambia wengine habari za Biblia juu ya matukio hayo yasiyoepukika. Wakiwa “juu ya nyumba,” kama tuwezavyo kusema, watu wa Mungu wameutangazia ulimwengu wote mambo ambayo Yehova amefunua juu ya “dhiki kubwa” inayokuja, itakayofikia upeo wake katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,” “mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har–​Magedoni.”​—Mt. 10:26 27; Ufu. 7:14; 16:14, 16.

11. Watu wengi wana maoni gani yenye makosa juu ya uharibifu wa wakati ujao?

11 Usiwe na maoni mabaya juu ya vita hii ya mahali paitwapo Har–​Magedoni. Hii siyo ile vita ambamo mataifa watajaribu kueneza makombora yao yote ya atomiki waliyolundika mno​—yanayosemekana kuwa makubwa kutosha kumaliza idadi ya watu wa ulimwengu ya karibu 4,000,000,-000 (mamilioni milioni nne), hata zaidi ya hapo! Vita hiyo ya makombora ya atomiki siyo “dhiki kubwa” inayokuja ambayo Yehova anatuonya.

12, 13. Maoni ya ujumla ya watu wengi yanatofautianaje na ya Mashahidi wa Yehova, na kwa sababu gani?

12 Basi, je! hilo laonyesha si hatari kubwa inayokaribia wanadamu wote? Kama katika vita yo yote, hili lategemea kabisa upande tulio, upande wa ushindi au wa ushinde. Kwa hakika, wanadamu waliotengwa na Yehova, wapaswa kuogopa sana vita katika Har–​Magedoni. Hii ni kwa sababu wamejipanga na “wafalme wa ulimwengu wote” kwa kupenda au kutopenda, na kwa hiyo wanakusanywa pamoja na wafalme hao kwenye “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.”

13 Lakini sivyo walivyo watu waaminifu wa Yehova! Wamejipanga imara upande wa ushindi, upande wa Mungu, bila kugeuka. Kwa hiyo wanaweza kuikabili “dhiki kubwa” iliyotabiriwa wakiwa na uhakika na kumtumaini kabisa Yehova.

DHIKI KUBWA KULIKO ZOTE

14. Kulingana na Mathayo 24:21, “dhiki” itakayoujia ulimwengu karibuni ni kubwa namna gani?

14 Dhiki isiyo na kifani inayokuja itakuwa kubwa kadiri gani? Akitumia dhiki iliyoupata Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. kama mfano wa unabii, Yesu alisema ingekuwa “ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa,” halafu, ili tusiione kuwa ndogo, akaongeza mkazo kwamba, “wala haitakuwapo kamwe.” Basi, hiyo yamaanisha dhiki kubwa zaidi kuliko Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na ya Pili ambavyo katika hivyo makumi ya mamilioni ya watu walipoteza maisha zao. Naam, ni kubwa zaidi kuliko gharika ya dunia yote iliyotokea siku za Nuhu ikaikumba taratibu nzima ya ulimwengu!

15. Ni jambo gani hasa lenye kuogofya juu ya “dhiki kubwa,” na kwa sababu gani?

15 Basi, “dhiki kubwa” inayokuja itapitaje dhiki nyingine zote za historia ya kibinadamu? Kwanza, itaiharibu milki nzima ya ulimwengu ya dini ya uongo, matengenezo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo na ya waabudu wa miungu ya kishenzi iitwayo katika Biblia Babeli Mkuu wa siri. (Ufu. 17:5) Bila shaka jambo hili litaduwaza wakazi wa dunia ambao wamemwunga mkono huyu “MAMA WA MAKAHABA,” Babeli Mkuu.

16. Ni jambo gani jingine la “dhiki” inayokuja linalotabiriwa katika Ufunuo 19:1921?

16 Lakini Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, itakapotwezwa na kuharibiwa, hiyo itakuwa Sehemu ya Kwanza tu ya “dhiki kubwa.” Watakaoharibiwa katika Sehemu ya Pili ni “wafalme wa nchi, waliozini pamoja naye [Babeli Mkuu] na kufanya anasa pamoja naye.” (Ufu. 18:9; 16:14) Unabii wa Ufunuo sura ya 19, mistari ya 19 mpaka 21, unaendelea kusema hivi: “Mnyama, na wafalme wa nchi, na majeshi yao, wamekutana kufanya vita na yeye [Bwana Yesu Kristo aliyetukuzwa] aketiye juu ya farasi yule, tena na majeshi yake. . . . Wakatupwa wangali hai katika lile ziwa la moto liwakalo kwa kiberiti.” Sura ya 20, mstari wa 14, hueleza kwamba “hii ndiyo mauti ya pili, yaani, hilo ziwa la moto.”

17. Yeremia 25:31-33 inatupaje mawazo machache juu ya yatakayotukia katika dhiki hiyo ipitayo dhiki zote?

17 Naam, itakuwa kubwa zaidi kuliko dhiki ile iliyoelezwa na nabii mwingine wa Yehova, Yeremia, ilipokuwa ikikaribia: “Na waliouawa na [Yehova] siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa; watakuwa samadi juu ya uso wa nchi.”​—Yer. 25:33.

18. Ni nini litakalofuata “dhiki” hiyo, kuifanya itofautiane kabisa na dhiki zote zilizotangulia?

18 Lakini bado kuna jambo jingine litakalofuata hiyo “dhiki kubwa,” jambo ambalo hata halikutukia baada ya ulimwengu wa kwanza kuharibiwa, ‘ulimwengu wa siku za Nuhu.’ Ni kukamatwa na kufungwa kwa Shetani na mashetani wake kwa “mnyororo mkubwa,” na kuvurumishwa katika shimo lisilo na mwisho.​—Ufu. 20:1-3.

19, 20. (a) Wewe unaikabilije dhiki iliyo kubwa kupita zote? (b) Waweza kuonyeshaje una hakika?

19 Basi, sasa, je! wamwamini Yehova na yale ambayo amesema kwa kinywa cha manabii hawa, yaani, kwamba wanadamu wote wanakabili hiyo “dhiki kubwa”? Ikiwa ndivyo, je! waikabili ‘dhiki’ hii isiyoepukika ukiwa na uhakikisho wenye nguvu na tumaini kamili? Ni jambo moja kusema hivyo kwa midomo yako; ni jambo jingine kulionyesha kwa matendo yako.

20 Ebu ifikirie kwa ufupi baadhi ya mifano ya zamani ya wale waliomtumaini kabisa Yehova, na uangalie hasa jinsi walivyoonyesha uhakika wao.

MAONYESHO YA ZAMANI YA UHAKIKA

21. Eleza jinsi Nuhu na jamaa yake walivyoonyesha waliitumaini ahadi ya Yehova.

21 Nuhu alionyesha kwa maisha yake ya kila siku kwamba alitegemea kabisa onyo la Yehova. Hakujitenga kimwili, ijapokuwa alijitenga na taratibu hiyo, kisiasa na kijamii. Wakati uo huo alitimiza kwa bidii mgawo aliopewa na Mungu kujenga safina, kuwahubiri wengine na kuwaonya juu ya uharibifu uliokuwa ukikaribia. Alionyesha wakati wote kwamba alikuwa na tumaini na uhakika kamili kwamba Mungu wake, Yehova, alikuwa na uwezo wa kumlinda na kumwokoa katika wakati huo wataabu iliyokuwa haijatokea mpaka hapo.​—Mwa. 6:9; Ebr. 11:7; 2Pet. 2:5.

22. Twaweza kujifunza masomo gani ya maana kutokana na wale walioondoka katika Sodoma mwovu kabla haujaharibiwa?

22 Alikuwako Lutu pia. Baada ya kuonywa mapema waondoke Sodoma, na kusihiwa na majeshi ya malaika, wanne katika jamaa hiyo waliondoka mjini, lakini watatu peke yao ndio waliookoka wakaweza kusimulia habari hizo. Kwa nini watatu peke yao, si wanne? Yesu alisema: “Mkumbukeni mkewe Lutu.” Alitazama nyuma kinyume cha maagizo wakati wa kuukimbia Sodoma, na ni wazi alifanya hivyo kwa sababu fulani ya kichoyo.​—Mwa. 19: J 1-26; Luka 17:32; 2 Pet. 2:7, 8.

23. Ni jambo gani ambalo Waisraeli na wenzao walilazimika kufanya katika Bahari ya Shamu likawaokoa?

23 Nyakati hizo ni wachache tu waliookoka. Lakini Yehova aweza pia kuokoa kwa wepesi umati wa watu na kuwapeleka mahali salama. Hilo lilionyeshwa katika habari ya taifa la Israeli na wenzao, katika Bahari ya Shamu. “Kwa imani wakapita kati ya Bahari ya Shamu, kama katika nchi kavu,” asema mtume Paulo. Walionyesha imani na uhakika kwa utii wao, kama tusomavyo: “Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli wote; kama [Yehova] alivyowaagiza Musa na Haruni, ndivyo walivyofanya.”​—Ebr. 11:29; Kut. 12:37, 38, 50.

WENGINE WALIOKOKA “DHIKI” ILIYOUPATA YERUSALEMU

24-26. (a) Wakristo waliokuwa wakiishi Yerusalemu miaka ya 60 ya karne ya kwanza W.K. walitakiwa kufanya nini? (b) Eleza matukio yaliyotukia mfululizo kuonyesha kwamba waliotumaini onyo la kimungu hawakukata tamaa.

24 Wakristo waaminifu katika miaka ya 60 ya karne ya kwanza walipaswa wamtumaini Yehova na nabii wake vivyo hivyo, Musa Mkubwa Zaidi, Bwana Yesu Kristo. Iliwapasa pia watende kwa imani na kuonyesha kwamba, kweli walisadiki yale ambayo walikuwa wametangulia kuambiwa juu ya uharibifu wa Yerusalemu uliokuwa ukija. Walionywa kwamba, walionapo “chukizo la uharibifu likisimama pasipolipasa,” wasikawie kutoka Yerusalemu na jimbo la Uyahudi lililokuwa kando.​—Marko 13:14.

25 Baadaye, wenye ufahamu waliiona wazi sana “ishara” hii! Jeshi la Kirumi lililokuwa “chukizo,” lenye kuongozwa na jemadari Sesho Gallo, lilionekana likizunguka mji mtakatifu wa Yerusalemu, “likisimama pasipolipasa,” na hata likaanza kufukua chini ya kuta za eneo halisi la hekalu!​—Mt. 24:15.

26 Basi mara majeshi hayo ya Kirumi yalipoondoa kwa muda mazingiwa yao kwa ghafula, bila kutazamiwa na bila sababu ya wazi ya kijeshi, Wakristo wenye kusadiki walifanya haraka kutoka kabla ya Warumi kurudi. Wasioamini wala kutumaini onyo la unabii la Yesu walikaa mjini mpaka majeshi yenye kushambulia yalipouzuia kabisa mji, yakiongozwa na Jemadari Tito, yakaua umati mkuu wa watu, na kupeleka utumwani wachache waliookoka.

27, 28. Katika hali inayolingana na hiyo, wafuasi wa Mfalme, Kristo Yesu, wanamtumainije Yehova kabisa?

27 Imani kama ile ya Wakristo wa karne ya kwanza yaonyeshwa leo na wale wanaotumaini kabisa Neno la Mungu lililoandikwa. Waliona jinsi makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yalivyoshangilia Ushirika wa Mataifa kama “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani,” na sasa wanauona Umoja wa Mataifa ukiabudiwa kama ‘tumaini la pekee la amani’ ya wanadamu. Wanaona watu wenye kutaka mapinduzi wa Umoja wa Mataifa wakisongamana wakashambulie makao ya utendaji wa Jumuiya ya Wakristo na zinazoitwa haki zake, yaani, “patakatifu” pake. Haya sasa, Umoja wa Mataifa ndio huo, unamkaidi Mfalme wa Amani, Mtawala wa dunia mwenye haki, Bwana Yesu Kristo, na kujitayarisha pia kusimama katika mahali ambapo Jumuiya ya Wakristo hudhani ni “patakatifu.” (Ufu. 11:15; 12:10) Naam, kweli Umoja wa Mataifa ndilo “chukizo la uharibifu” la kisasa litakaloharibu Jumuiya ya Wakristo katika “dhiki kubwa” inayokuja.​—Mt. 24:15, 21.

28 Kwa kuiona “ishara” hii ambayo ingali wazi, wale wanaotumaini Neno la Yehova wametoka katika Babeli Mkuu, ambayo Jumuiya ya Wakristo ndiyo sehemu kuu.​—Ufu. 18:4, 5.

29. Watu zaidi ya 2,000,000 wamechukua hatua gani wakitazamia kuokolewa na uharibifu unaokaribia?

29 Ukiwa wewe ni mmojawapo wale zaidi za 2,000,000 ambao wamekwisha kuikimbia Babeli Mkuu kabla ya uharibifu wake, ukawa mmoja wa waabudu safi wa Yehova, uko katika hali kama ile ya jamaa ya Nuhu iliyoingia katika safina, kama Lutu na binti zake wawili walioukimbia Sodoma, kama Waisraeli waliotoka Misri kwa amri ya Musa. Naam, uko kama Wakristo wa karne ya kwanza walioukimbia Yerusalemu kabla haujaharibiwa.

30. Ni maulizo gani yafaa kujiuliza?

30 Lakini kwa kuwa sasa umo katika hali hiyo yenye pendeleo, utaukabilije wakati ujao? Je! utaendelea kukaa katika paradiso ya kiroho ulimoingia, iliyo mfano wa safina? Kwa kuwa umeiacha milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, je! unatazamia uharibifu wa Babeli Mkuu katika “dhiki kubwa” inayokuja kwa shauku sana na uhakika kamili? Unapofikiria sana maulizo hayo, uangalie makala inayofuata.

[Sanduku katika ukurasa wa 269]

ORODHA YA BIBLIA JUU YA MATUKIO YANAYOKUJA

1. Uharibifu wa ‘Babeli Mkuu,’ milki ya ulimwengu ya dini ya uongo.​—Ufu. 18:4-8.

2. ‘Kuvunjwa vipande vipande kwa falme zote za kibinadamu.’​—Dan. 2:44.

3. Kufungwa kwa Shetani na mashetani wake na kuwatia katika shimo refu sana.​—Ufu. 20:1, 2.

4. Kuingia kwa taratibu mpya ya Mungu, na furaha ya kweli kwa wanadamu.​—Ufu. 21:4, 5.

[Picha katika ukurasa wa 267]

Je! yakupasa uendee mwaguzi ujue ya wakati ujao . . .

. . . au yakupasa ujifunze Biblia, Neno la Mungu?

[Picha katika ukurasa wa 270]

Wakristo walifanya haraka kutoka Yerusalemu, wakiwa na hakika juu ya onyo la Yesu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki