Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 12/15 kur. 564-570
  • Kuutazamia Wakati Ujao kwa Matumaini

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuutazamia Wakati Ujao kwa Matumaini
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SABABU GANI MATUMAINI YA WAKATI UJAO YANAHITAJIWA
  • WENYE MATUMAINI KWA SABABU YA ULINZI WA YEHOVA
  • KUJIREKEBISHA SASA TUPATANE NA HALI ZA TARATIBU MPYA
  • MATUMAINI YA KUSISIMUA YA WAKATI UJAO
  • Ongeza Uhakika Sasa Juu ya Wakati Ujao
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kuikabili “Dhiki Kubwa” kwa Uhakika
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Ni Ulinzi Gani kwa Watu wa Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Endelea Kuwa Mwaminifu Wakati wa “Dhiki Kuu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 12/15 kur. 564-570

Kuutazamia Wakati Ujao kwa Matumaini

“Tushikamane sana na matumaini tuliyokuwa nayo mwanzoni yakiwa thabiti mpaka mwisho.”​—Ebr. 3:14, NW.

1. Je! watu wote wana maoni yaliyo sawa juu ya wakati ujao? Eleza.

WATU walio wengi watakataa mara moja wasielezwe juu ya wakati ujao ulio mwangavu kwa sababu ya “taratibu mpya” yenye haki kwa kusema hivi: “Hiyo haitawezekana kamwe!” Kwa kuwa hawana matumaini yo yote katika wakati ujao, si ajabu kwamba walio wengi wanaanza kujifikiria wenyewe tu na kuchagua kuishi kwa ajili ya “leo” tu. Lakini, mashahidi wa Yehova wa Kikristo hawana maoni hayo yenye kuvunja moyo juu ya wakati ujao. Badala yake, mioyo yao inafurika na matumaini wanapotazamia kwa shauku wakati ujao wenye kuongozwa na Mungu aliye hai, Yehova, si na mataifa yenye choyo wala yenye pupa ya utawala. Hata hivyo, maoni ya mtu juu ya wakati ujao yanaweza kuharibiwa. Lakini namna gani?

2. Kuna hatari gani inayoweza kupata mwenye matumaini ya wakati ujao, na mtume Paulo anatuonyaje katika habari hii?

2 Hatari yenyewe ni juu ya kujitia mno katika taratibu iliyopo ya mambo. Lakini pengine umesikia mtu akitetea kujitia kwake kwa kusema hivi, “Lazima tuone mambo inavyofaa wala si kwa kupita kiasi.” Je! wewe ulielekea kukubaliana naye? Kunaweza kutokea nini watu wakiendelea kujitia zaidi? Pengine wewe mwenyewe umeona matokeo. Pengine jamaa nzima​—wazazi na watoto​—inajitia sana katika shughuli za sasa hata hawaoni kama kweli kutakuwa na wakati ujao. Vitu walivyopata “inavyofaa” tu ndivyo wanavyoviona kuwa halisi peke yake. Bila kujua wameacha mioyo yao igeuzwe kuwa isiyo na imani na yenye kutamani maovu. Huo ni usemi mkali? Basi, ndivyo mtume Paulo alivyosema: “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai.” (Ebr. 3:12) Umeona vile maneno ya Paulo yanavyotia ndani watu wote? Anasema hilo linaweza kumpata ‘mmoja wetu,’ naam, hata wale ambao wametumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi! Lakini, ili hilo lisije likatukia acheni tujikumbushe yaliyoko mbele yetu wakati ujao ili tujithibitishie mioyoni mwetu kwamba mambo aliyoahidi Yehova yatatukia kweli. Matumaini yetu katika wakati ujao yakitegemezwa hivyo, ‘tutashikamana sana na matumaini tuliyokuwa nayo mwanzoni yakiwa thabiti mpaka mwisho.’​—Ebr. 3:14, NW.

SABABU GANI MATUMAINI YA WAKATI UJAO YANAHITAJIWA

3. Biblia inaelezaje mpambano wa ulimwengu unaokaribia sana, ukifuatana na tangazo gani lenye majivuno?

3 Ni nini kinachofunuliwa na kiongozi Kile kisichokosea, Biblia, juu ya wakati wetu ujao ulio karibu sana? Kinaonyesha mataifa yaliyodanganywa na mashetani yakivutwa kuingia katika pigano na Mungu. Tunaambiwa hivi: “Pepo za masatani [wanatoka] na kwenda kwa wafalme wa ulimwengu wote, kuwakusanya kwa vita ya siku ile kubwa ya Mungu Mwenyezi,” kwenye mahali panapoitwa “Harmagedoni.” (Ufu. 16:14, 16, Swahili Congo Bible) Mataifa yanadanganywa na kudanganyika kabisa hata wanatangaza kwa kujitumainia kwamba wakati ujao ni wenye usalama, wakipaza sauti, “Kuna amani na salama!” badala ya kuogopa mpambano huo wa mwisho na Mungu. Lakini, mara tu tangazo hilo la majivuno liishapo kutangazwa “ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.” Je! pengine jambo hilo lingali mbali sana? Sivyo kwa maana mataifa sasa yanaelekea kufanya amani. Lakini, matukio yenye kustaajabisha hata zaidi yanakaribia kutukia. Ni nini hayo?

4. (a) “Dhiki kubwa” inaanzaje? (b) Ni shambulio gani juu ya watu wa Yehova linalomfanya Yeye akawaokoe?

4 Serikali za kinyama za kisiasa zitageukia ‘Babeli Mkuu’ kwa mshindo, ambayo ndiyo milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Mwishowe njia zake za ujanja zenye kuchukiza zitawakasirisha mno watawala wa kisiasa hata ibada zake za kikahaba hazitamwokoa na hasira yao kuu. Dharau yao kwa fahari yake inaonyeshwa kwa ukali wanaotumia kufunua uchi wake na kumtafuna-tafuna na kumteketeza kabisa kwa moto. (Ufu. 17:5, 16; 18:8, 21) Hivyo ndivyo “dhiki kubwa” inavyoanza juu ya taratibu ya mambo ionekanayo ya Ibilisi juu ya dunia. Kwa habari ya waabudu wa Yehova, wao wanaelekea kuwa mahali pasipo na ulinzi, “wakikaa pasipo kuta, ambao hawana makomeo wala malango.” (Eze. 38:11) Lakini wao wanamwambia Yehova hivi: ‘Wewe ndiwe kimbilio langu na ngome yangu.’ (Zab. 91:2, NW) Hapo “Gogu, wa nchi ya Magogu” wa kiibilisi anapata nafasi nzuri sana hata asiweze kuiachilia. Akiwa na jeshi kubwa, “kama wingu kuifunika nchi,” anawashambulia watumishi hawa wa Mungu wanaoelekea kutokuwa na ulinzi. (Eze. 38:2, 16) Shambulio hilo la kiwogawoga lisilo na sababu linamfanya Yehova akasirike kwa haki naye anainuka akaokoe watumishi wake kwa kutumia silaha za shambulio zilizo na nguvu kupita zote zilizopata kutumiwa: kumiminwa kwa magonjwa ya kipuku, mvua yenye mafuriko, mawe ya barafu, moto na kiberiti juu ya majeshi ya adui yaonekanayo. (Eze. 38:18, 21, 22) Majeshi ya adui yanashambulia watu wa Yehova kwa bidii kwa sababu yanakana kwamba hakuna miungu iwayo yote. Wakiwa wamechelewa mno, wanatambua kwamba wanapigana na Mungu aliye hai!

5. Ushindi wa Yehova ni wa kadiri gani juu ya wapinzani wake?

5 Ushindi unaopatikana ni mwingi kadiri gani? Je! ni sehemu moja tu ya kumi inayouawa? Mambo yanakuwa mabaya zaidi ya hapo kwa watu hao wachukiao watumishi wa Mungu! Hata sehemu moja ya kumi kati yao hawasalii. Ushindi unakuwa kamili! Yehova amehifadhi waabudu wake waaminifu kupita sehemu ya mwisho ya “dhiki kubwa” nao sasa wanasimama katika dunia iliyoondolewa wapinzani wote. Hata mara moja haikuwapasa wainue mkono wa kujitetea. Yehova amehakikisha wametetewa kupitia kwa ufalme wa Kimasihi na majeshi ya malaika!​—Ufu, 19:11-15, 19-21.

6. Ni hatua gani ya mwisho itakayochukuliwa baada ya hapo juu ya Shetani na mashetani wake, na ni hali gani zitakazoonyesha utawala wa ufalme wa Kimasihi?

6 Jambo moja bado linabaki lifanywe baada ya vita katika Har–​Magedoni, nalo linafanywa kasi kasi! Wale waliotaka kuharibu wengine, Shetani Ibilisi na majeshi yake ya mashetani wasioonekana wanatiwa shimoni; wanatupwa ndani ya shimo kubwa nalo funiko lake linakazwa kikiki na kutiwa muhuri kwa miaka elfu! (Ufu. 20:1-3) Sasa ufalme wa Kimasihi ukiwa chini ya Kristo unaanza kutawala dunia yote ya waokokaji wa uharibifu huo mkubwa, na katika wakati wake Mungu umati mkubwa wa wenye kufufuliwa wanaungana nao kuijaza dunia. Kristo aliyetukuzwa atakamilisha wanadamu wakati wa utawala wa miaka elfu wenye haki kwa kutumia nguvu zile zile za kuponya alizotumia kuponya wagonjwa na kufufua wafu alipokuwa duniani.

7. Sababu gani hatuna haja ya kuona wasiwasi juu ya kupata habari zote za wakati ujao, lakini sisi ni afadhali kuliko nani?

7 Masimulizi ya wakati ujao yanasisimua weee! Ni kweli kwamba hatujapata habari zote, lakini hata hatuzihitaji zote. Tunazo za kutosha kuweza kuona matukio yanayopita kasi kasi hata sasa, yanayoanza kutukia kutuzunguka. Hata hivyo, pengine wengine wanataka kujua kama viongozi wote wa kidini watakufa pamoja na Babeli Mkuu au kama sehemu zote za milki kuu hiyo ya kidini zitaangamia duniani zote kwa pamoja. Lakini, mambo hayo hayapaswi kutuhangaisha, kama kwamba habari hizo ni za lazima ili tuendelee kuziamini ahadi za Mungu za ajabu. Badala yake, imetupasa kufikiria namna tulivyo afadhali kuliko ulimwengu usio na habari hata moja juu ya yatakayotokea kesho, licha ya kuwa na njozi ya miaka elfu ya wakati ujao! Imetupasa tuwe wenye shukrani sana kwamba tunazo sababu za kutazamia yaliyoko mbele, ikiwa tunamtumaini Yehova kwa uhakika. Kama Yeye alivyosema: “Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea [Yehova], ambaye [Yehova] ni tumaini lake.” (Yer. 17:7) Zaidi ya hayo, bado iko sababu nyingine kubwa ya kuwa na matumaini.

WENYE MATUMAINI KWA SABABU YA ULINZI WA YEHOVA

8, 9. (a) Ni sababu gani nyingine ya kutokeza ya kuwa na matumaini katika wakati ujao? (b) Kwa sababu gani tunajua kwamba mambo yatatukia sawa na ambavyo Yehova amesema?

8 Kutokana na yale ambayo tumekwisha zungumza ni wazi kwamba sababu ya kwanza kabisa ya kuwa kwetu na matumaini ni kujua kwamba Yehova anategemeza Wakristo waaminifu. Wakiwa tofauti na wapelelezi walioleta habari za kuvunja moyo juu ya nchi ambayo Yehova alikuwa amewaahidia Waisraeli, Yoshua na Kalebu walikuwa na matumaini Yeye angewaongoza kwenye ushindi, wakitangaza hivi: “Msiwaogope wale wenyeji wa nchi, maana wao ni chakula kwetu; uvuli uliokuwa juu yao umeondolewa, naye [Yehova] yu pamoja nasi; msiwaogope.” (Hes. 14:9) Wakristo leo wamepaswa pia wawe na matumaini ayo hayo, kwa maana imeandikwa, “Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu?” (Rum. 8:31) Kwa kweli, mwandikaji Paulo anasadiki sana kwamba kifungo cha upendo kilicho kati ya Yehova Mungu na waabudu wake waaminifu hakiwezi kuvunjika hata anasema kwamba hakuna cho chote wala ye yote anayeweza kuwatenganisha na upendo wa Mungu. (Rum. 8:35-39) Lo! hiyo ni sababu nzuri namna gani ya kuwa na matumaini!

9 Kwa hiyo watumishi wa Mungu wanazo sababu za kutosha kutazamia wakati ujao ulio mwangavu na wenye kuvutia. Hawana sababu ya kudhani mambo yatakuwa tofauti na vile Yehova amesema katika Neno Lake. Yeye si kama wanadamu wasiotimiza ahadi zao, bali sikuzote amekuwa mwaminifu kwa rafiki zake. Paulo aliamini hivyo, nayo matumaini yake katika Mungu na wakati ujao ulioahidiwa hayakuwa ya upumbavu. Kama angalikuwa duniani leo angalikuwa anatazamia kwa shauku kutimizwa kwa ahadi za Mungu. Imetupasa nasi kuwa hivyo.

10. (a) Je! Zaburi 91 inaunga mkono maoni ya kwamba watu mmoja mmoja watalindwa wakati wa “dhiki kubwa”? (b) Yehova atatoa ulinzi wa namna gani?

10 Je! tutazamie kwamba kwa sababu Yehova yuko upande wetu atajiingiza kwa mwujiza alinde kila mmoja wetu asife au asipate madhara wakati wa “dhiki kubwa”? Wengine wametaja Zaburi 91:7-12 na Mithali 3:25, 26 kwa njia mbaya ili kuunga mkono maoni hayo. Zaburi hiyo inasema hivi: “Ijapo watu elfu waanguka ubavuni pako. Naam, kumi elfu mkono wako wa kuume! Hata hivyo hautakukaribia wewe.”a Ili tusiongeze mambo yasiyosemwa na andiko hilo, lazima tujiulize kama Musa hapa anazungumza juu ya “dhiki kubwa” inayokuja na kama anasema watumishi wote mmoja mmoja wa Mungu watalindwa. Haiwezi kuwa hivyo tukikumbuka kwamba karne nyingi baadaye Paulo alionyesha kufikia wakati wake wafuasi waaminifu wa Yehova walikuwa wamekwisha fanyiwa mizaha, wakapigwa mijeledi, wakafungwa, wakapata dhiki na mateso mengine mengi, hata wakauawa kwa jeuri. Lakini, ‘tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawalinda kama kikundi wasifutiliwe mbali na adui zao wakati wa “dhiki kubwa,” Naye mwenyewe hatawagusa atakapokuwa akifikiliza hukumu kali.​—Ebr. 11:36-38.

11. (a) Je! Mithali 3:25, 26 inahakikisha kwamba hakuna mfuasi mmoja mwaminifu wa Mungu atakayetoroshwa au kukamatwa? (b) Katika habari hii, tuna mifano gani?

11 Je! Sulemani mwandikaji wa mithali iliyokwisha tajwa anatupa sababu ya kutazamia tulindwe na Mungu tusipatwe na madhara yo yote ya kimwili? Yeye alisema hivi: “Usiogope hofu ya ghafula, wala uharibifu wa waovu utakapofika. Kwa kuwa [Yehova] atakuwa tumaini lako, naye akulinda mguu wako usinaswe.” Je! huo unaelekea kuwa ushuhuda wa kwamba Yehova Mungu hataruhusu wafuasi wake waaminifu watoroshwe au wakamatwe wakati wa “dhiki kubwa”? Tusisahau kwamba Sulemani hakuandika akitufikiria sisi leo, bali aliandika hasa kwa faida ya waliokuwa wakiishi chini ya ufalme wake. (Mit.1:1-4; 3:25, 26) Tukiyachukua maneno yake hivyo, tunafahamu kwamba alikuwa akiwapa Waisraeli shauri ambalo lingewasaidia waishi maisha manyofu na kuwafaidi kila siku. Kwa njia hiyo ‘wasingenaswa.’ Ni kunaswa kwa namna gani? Kwa mfano, wasinaswe na utongozi wa kahaba mwenye kutembea barabarani akitafuta mtu wa kunasa. (Mit. 5:3-14) Twaweza kuona maneno yake ni shauri zuri sana kwetu pia. Lakini hayatuhakikishii kwamba hatutakamatwa, kama vile Yeremia mwaminifu asivyoweza kukosa kukamatwa “wakati wa mwisho” wa Yerusalemu. (Yer. 37:15, 21) Wala hatuwezi kutazamia kwamba wakati wa “dhiki kubwa” wengine hawatapoteza maisha zao kwa sababu ya kushikamana na ukamilifu wao wa Kikristo kwa uaminifu, kama vile mtume Yakobo alivyopoteza maisha yake. (Matendo 12:1, 2) Hata hivyo, tunao ulinzi wa kimungu. Namna gani?

12. (a) Twajuaje kwamba tunalindwa kama jamii? (b) Je! Yehova atawasahau watakaopoteza maisha zao, ingawa ni waaminifu? Amefanya mpango gani?

12 Tunao ushuhuda wa kwamba Mungu anatulinda sasa kama jamii. Kwa mfano, kama isingalikuwa hivyo, tungalikuwa tumekwisha futiliwa mbali tutoke katika uso wa dunia zamani za kale na Shetani. Hata hivyo, watu wengine mmoja mmoja huenda wakafa kwa uzee na magonjwa wakati wa “dhiki kubwa” au kwa sababu ya mateso, kama ndugu zetu katika Malawi. Kwa kuwa mambo hayo yanaweza kutupata, je! bado tunaweza kuutazamia wakati ujao kwa matumaini? Bila shaka! Yesu alisema kwamba wafu wataisikia sauti yake nao watatokea katika ufufuo. (Yohana 5:25-29) Hiyo basi inatangua na kufuta matokeo ya kifo. Biblia haiahidi kwamba Shetani ataacha kujaribu kila mmoja wetu wakati wa “dhiki” inayokuja, lakini je! hatufarijiki kujua kwamba Yehova Mungu hatatusahau tukifa kwa sababu ya kumtumikia yeye kwa uaminifu wakati huo?

13. (a) Wakati wa kuharibiwa kwa Babeli Mkuu, je! watu wa Mungu kwa ujumla wataharibiwa pia? (b) Hii inahitaji watumishi wa Mungu wafanye nini?

13 Tutaendelea kulindwa kama kikundi kupita uharibifu wa Babeli Mkuu na vita katika Har–​Magedoni hata tuingie katika Taratibu Mpya. Babeli atakapolala akiwa hoi, uwezo wake wa kuongoza mambo ya ulimwengu ukiwa umeondolewa kabisa, hiyo itakuwa sababu kubwa ya kuweka matumaini katika Yehova Mungu kama mtimizaji wa ahadi zake. Si ajabu watumishi wa Mungu wanaambiwa washangilie kupinduliwa kwake, wakipaziwa sauti hivi: “Furahini juu yake, enyi mbingu, nanyi watakatifu na mitume na manabii; kwa maana Mungu amehukumu hukumu yenu juu yake.” (Ufu. 18:20) Kwa hiyo hawa wanaweza kuwa na matumaini kwamba watapata ulinzi wakati Mungu atakapokuwa akiua waovu na kwamba wataingizwa katika taratibu yake mpya yenye haki.​—Mt. 25:46.

KUJIREKEBISHA SASA TUPATANE NA HALI ZA TARATIBU MPYA

14. Kuna uwezekano gani kwa wale wasiotaka kufanya mabadiliko ya lazima ili kujipatanisha na kanuni za haki sasa?

14 Walakini, ili tuwe na matumaini yenye hakika ya wakati ujao lazima pia tuanze sasa kurekebisha maisha na mawazo yetu yapatane na kanuni anazotufunulia Yehova Mungu kupitia kwa Neno lake na tengenezo lake. Ni kweli, ni vigumu kuondoa tabia na nia mbaya zilizotia mizizi kwa muda mrefu, lakini haitupasi kujipa udhuru kwa kusema: ‘Haya basi, mimi n’tangoja taratibu mpya ifike ndiyo nibadili njia zangu. Itakuwa rahisi wakati huo.’ Dharau hiyo ya kupenda juu ya makusudi ya Mungu inaweza kuwa dhambi machoni pake na huenda ikatupotezea haki yetu yote ya kuingia katika taratibu yake mpya.​—Yak. 4:17.

15. Je! sehemu tunazopaswa kufanyia marekebisho ni zile zinazohusu mafundisho na ufahamu wa unabii? Tunapewa msaada gani tufanye marekebisho katika kuwaza na matendo yetu?

15 Marekebisho hayo si kukubali kwa akili tu mafundisho au ufahamu wa unabii unaoelezwa na “mtumwa mwaminifu.” Huenda yakahusu kubadili moyo, kwa mfano yakitutaka tung’oe maoni mabaya yasiyo na msingi na nia mbaya zinazotuzuia tusipende watu wote kwa moyo wote bila kujali taifa lao wala hali yao ya maisha. (Matendo 10:34) Au huenda yakahusu dalili ya ulimwengu wa zamani iliyoonyeshwa kuwa yenye kuchukiza machoni pa Mungu ambayo lazima uiondoe. Yehova Mungu ametupa waangalizi wa kundi wenye uwezo kutusaidia tufanye marekebisho hayo yanayohitajiwa, kwa sababu ya upendo wake usio na kifani kwetu. Paulo anatutia moyo tukubali msaada wao kwa kupenda, anapoandika hivi: “Mwatambue wale wanaojitaabisha kwa ajili yenu, na kuwasimamia ninyi katika Bwana, na kuwaonyeni; mkawastahi sana katika upendo, kwa ajili ya kazi zao.” (1 The. 5:12, 13) Kuitikia uongozi wao wenye huruma kwa wema kutafanya kazi yao iwe nyepesi zaidi na kugeuza maisha zetu pia zipatane na mpango wa Mungu wa kuishi katika taratibu mpya, kukitufanya tutazamie wakati ujao kwa shauku kwa sababu ya kutambua ukuu wa njia ya Yehova ya kushughulika na watu Wake.

16. Kama ilivyoonyeshwa na Isaya na Kristo Yesu, imetupasa tuonyeshe nia gani juu ya migawo ya kazi?

16 Wala hakuna shaka kwamba katika Taratibu Mpya kutakuwa na kazi za namna zote zitakazopaswa kufanywa. Je! tutakuwa na nia ya kutumikia, kufanya kazi yo yote tutakayogawiwa tufanye? Watumishi wa Mungu zamani walionyesha nia hiyo, bila kujali kama daraka walilopewa lilikuwa la cheo cha juu au cha chini. Isaya alikubali kwa bidii kazi ngumu ya nabii, akisema hivi, “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isa. 6:8) Ingawa Yesu alitambuliwa kuwa “Bwana” na wanafunzi wake, alionyesha nia ya kutumikia hata katika hali ya mtumwa kwa kuosha miguu yao. (Yohana 13:3-17) Lo! alituwekea mfano mzuri kama nini!

17. Ni nini kitakachohitajiwa kwetu ili kutimiza migawo tusiyopendelea? Huenda ikatupasa kufanya marekebisho gani mengine?

17 Ni kweli, pengine kazi tutakayogawiwa ni ile ambayo sisi wenyewe tusingalichagua. Mara ya kwanza, pengine hatutafurahia kazi ngumu iliyo ya lazima kuleta dunia katika hali ya paradiso. Tutapaswa kutokuwa na choyo pia kwa maana jitihada zetu nyingi zitakuwa za kutayarisha mambo kwa ajili ya watakaofufuliwa na kuwaangalia, si za kuangalia mapendezi yetu wenyewe, na wengi wao watakuwa hawamjui Yehova Mungu. Unaweza kuwazia kazi kubwa inayohusika katika kugeuza tu akili na mioyo ya watu hao zipatane na kuwaza kwa taratibu mpya? Wo wote watakaokuwa na maelekeo ya uvivu wakati huo hawataona mazuri, kwa maana mithali inaonya hivi: “Matakwa yake mtu mvivu humfisha, kwa maana mikono yake hukataa kufanya kazi.” (Mit. 21:25) Kwa hiyo huenda ikatupasa kurekebisha kuwaza kwetu sasa, kwa habari ya nia yetu juu ya kazi ambayo Yehova anatupa tufanye sasa na wakati ujao. Hivyo tunaweza kutazamia wakati ujao kwa furaha.

18, 19. (a) Kuna uwezekano gani juu ya mahali ambako mtu ataisha katika dunia ya paradiso? (b) Itatupasa tuoneje mahali tutakapogawiwa katika Taratibu Mpya, na kwa sababu gani hatutaachwa peke yetu humo?

18 Kwa habari ya tutakakoishi katika paradiso ya wakati ujao, inawezekana sana kwamba tutagawiwa mahali pa kuishi badala ya sisi wenyewe kuachwa tujichagulie. Kadiri tutakavyojipatanisha na mpango huo inaweza kuonyeshwa na kama kwa sasa tuna nia ya kwenda kwenye kundi au funzo la kitabu tunaloombwa tuhudhurie. Tukijipatanisha na mahali tutakapogawiwa katika Taratibu Mpya, upesi patakuwa “makao” yetu nasi tutajifunza kupapenda. Ndivyo wamisionari wanavyopata kuona juu ya migawo yao ya kuhubiri hata leo.

19 Inafariji kujua pia kwamba Yehova Mungu atahakikisha “wakuu” wamechaguliwa watutumikie na kutuongoza. Tena, yeye anahakikisha anajua mambo tunayohitaji hasa, yaliyo bora kwetu, na hiyo ni sababu nyingine ya kuwa na matumaini kwa maana tunajua hatutaachwa peke yetu, bali tutakuwa na wanaume waaminifu waliohakikishwa, watakaoangalia faida zetu.

MATUMAINI YA KUSISIMUA YA WAKATI UJAO

20, 21. (a) Kwa sababu gani hatuna haja ya kufikiri-fikiri juu ya wakati ujao? (b) Ni mambo gani yenye kusisimua kati ya yale ambayo Biblia inatueleza juu ya wakati ujao?

20 Tunapotazamia wakati ujao tunayo matumaini ya kuvutia mbele yetu. Kwa hiyo, hatuna haja ya kufikiri-fikiri juu ya habari zisizoonyeshwa na Maandiko, bali imetupasa tuwe na nia ya kumngoja Yehova badala ya kuona wasiwasi au kusumbukia mambo hayo. Kuna haja gani ya kufikiri-fikiri juu ya watakaofufuliwa, namna watoto watakavyoangaliwa, ni nyumba za namna gani zitakazojengwa, kama tutatumia mashine, na maulizo ya namna hiyo. Kama kweli tungalipaswa kuyajua mambo hayo, Yehova angalikuwa ametoa majibu.

21 Badala ya kufikiri-fikiri juu ya yasiyojulikana, ni vizuri zaidi kukaza fikira juu ya mambo ya kusisimua inayosema Biblia. La maana zaidi kati yayo ni tumaini la uzima wenye kibali ya Mungu. Dunia yenye kujawa na uzima ndiyo inayoonyeshwa na Biblia. Itakuwa furaha iliyoje kukaribisha wafu warudi! Machozi ya furaha yatamiminika weee wapendwa watakapokuwa pamoja tena! Na ebu wazia wewe mwenyewe ukikutana na watumishi waaminifu wa Mungu wanaotajwa katika Biblia! Itasisimuaje pia kuona miili yetu ‘ikirudia siku za ujana wake’! (Ayubu 33:25) Itakuwa furaha namna gani kuishi katika paradiso tukiwa na chakula kisicho na kasoro, kazi ya kuridhisha, wenzi tutakaofurahi kushirikiana, na juu ya yote, tukiwa na uhuru kamili wa kumwabudu Mungu wetu, Yehova!

22. Tuna uhakikisho gani kwamba tunaweza kutazamia wakati ujao kwa matumaini?

22 Je! twaweza kweli kuwa na hakika ndivyo wakati ujao utakavyokuwa? Bila shaka twaweza, kwa maana umeahidiwa na Yehova Mungu. Yeye hatakosa kuutimiza, kwa maana “Mungu hawezi kusema uongo.” (Ebr. 6:18) Basi, tunatazamia matukio yaliyoko mbele kwa shauku na matumaini kamili katika Yeye anayetayarisha wakati ujao!

​—Kutoka The Watchtower, June 15, 1975.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama Mnara wa Mlinzi wa Juni 15, 1975, kurasa 271-273.

[Picha katika ukurasa wa 567]

Wakiwa tofauti na waoga, Yoshua na Kalebu walileta habari njema, wakiwa na matumaini kamili kwamba Yehova angewapa Nchi ya Ahadi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki